-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, wengi walitendwa kinyama kwa sababu hawakuwa “wazalendo.” Benson Judge, ambaye baadaye alikuwa mwangalizi anayesafiri mwenye bidii, anasema: “Tuliwaona wazee wakirushwa garini kama magunia ya mahindi kwa kuwa walikataa kujiunga na jeshi. Tuliwasikia wakisema, ‘Tidzafera za Mulungu’ (Tutakufa kwa ajili ya Mungu).”
Ingawa Mukosiku Sinaali hakuwa amebatizwa, anakumbuka kwamba wakati huo wa vita, suala la kutounga mkono vita lilizuka mara nyingi. “Kila mtu alipaswa kuchimbua na kukusanya mizizi ya mmea wa mambongo, ambayo hutoa utomvu wenye thamani. Mizizi hiyo ilitolewa maganda kisha ikapondwapondwa na kutumiwa badala ya mpira kutengeneza viatu vya wanajeshi. Mashahidi walikataa kuchimbua mizizi hiyo kwa kuwa kazi hiyo ilihusiana na vita. Ndugu waliadhibiwa kwa kukataa kufanya kazi hiyo. Walionwa kuwa ‘wenye kuchukiza.’”
Joseph Mulemwa alikuwa mmoja wa watu hao “wenye kuchukiza.” Yeye ni mwenyeji wa Rodeshia Kusini aliyehamia Mkoa wa Magharibi wa Rodeshia Kaskazini katika 1932. Watu fulani walidai kwamba aliwahimiza watu waache kulima mashamba yao kwa kuwa ‘Ufalme umekaribia.’ Kasisi wa misheni ya Mavumbo aliyemdharau Joseph alieneza dai hilo la uwongo. Joseph alikamatwa na kufungwa pingu pamoja na mwenda-wazimu fulani. Watu fulani walitarajia kwamba mwenda-wazimu huyo atampiga Joseph. Hata hivyo, Joseph alimtuliza. Alipofunguliwa, Joseph aliendelea kuhubiri na kutembelea makutaniko. Alikufa akiwa mwaminifu katikati ya miaka ya 1980.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Katika miaka yote ya 1960, Mashahidi wa Yehova kotekote nchini Zambia walikabili mateso makali na mali zao zikaharibiwa. Nyumba za akina ndugu na Majumba ya Ufalme yaliteketezwa. Serikali ilifanya vema kuwafunga wengi kati ya wale waliowatesa Mashahidi.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 232, 233]
Ilinibidi Kukimbia ili Niokoe Uhai Wangu
Darlington Sefuka
Alizaliwa: 1945
Alibatizwa: 1963
Maelezo mafupi kumhusu: Alikuwa painia wa pekee, mwangalizi wa mzunguko, na pia alifanya kazi kwenye Betheli nchini Zambia.
Kulikuwa na msukosuko nchini Zambia katika mwaka wa 1963. Mara nyingi tulipohubiri, magenge ya vijana waliounga mkono harakati za kisiasa walitutangulia ili wawaonye watu wasitusikilize na kuwatisha kwamba milango na madirisha ya nyumba zao yangevunjwa kama wangetusikiliza.
Jioni moja, siku mbili tu baada ya kubatizwa, nilipigwa vibaya na genge la vijana 15. Nilitokwa na damu nyingi mdomoni na puani. Jioni nyingine mimi na ndugu mwingine tulishambuliwa na kikundi cha watu 40 hivi waliokuwa wametuandama hadi mahali tulipoishi. Kufikiria mfano wa Bwana Yesu kuliniimarisha. Hotuba iliyotolewa na John Jason wakati wa ubatizo wangu ilionyesha wazi kwamba kila Mkristo atapata matatizo maishani. Basi nilipopatwa na matatizo hayo, sikushtuka bali nilitiwa moyo.
Wakati huo, wanasiasa walitaka watu waunge mkono harakati zao za kupigania uhuru, na kwa sababu sisi hatukujiingiza katika siasa walidhani tunawaunga mkono Wazungu na Wamarekani. Viongozi wa dini waliounga mkono vyama vya kisiasa walieneza habari hizo za uwongo kutuhusu. Mambo yalikuwa magumu kabla na baada ya uhuru. Ndugu wengi walipoteza biashara zao kwa sababu hawakukubali kununua kadi ya chama. Baadhi yao walihama mijini na kurudi vijijini mwao ambako walifanya kazi zisizokuwa na mapato mazuri ili waepuke kuombwa pesa kwa ajili ya harakati za kisiasa.
Nilipokuwa kijana, nilikaa na binamu yangu ambaye hakuwa Shahidi. Familia yake ilitishwa kwa sababu sikuunga mkono siasa. Walikuwa na wasiwasi. Siku moja kabla ya kwenda kazini, binamu yangu aliniambia: “Nitakaporudi jioni, sitaki kukukuta hapa.” Kwanza nilifikiri alikuwa anacheza tu, kwa sababu sikuwa na mtu mwingine wa ukoo mjini humo wala sikuwa na mahali pa kwenda. Baadaye niligundua kwamba hakuwa akicheza. Aliporudi na kunipata nyumbani, alifoka kwa hasira. Aliokota mawe na kuanza kunikimbiza, akisema kwa sauti kubwa: “Nenda kwa mbwa wenzako!” Ilinibidi kukimbia ili niokoe uhai wangu.
Baba yangu alisikia habari hizo na akatuma ujumbe huu: “Ukiendelea kushikilia msimamo wako wa kutounga mkono siasa, usikanyage kwangu tena.” Nilikuwa taabani kwelikweli, kwani nilikuwa na umri wa miaka 18 tu. Ningeenda wapi? Ndugu kutanikoni walinikaribisha. Mara nyingi ninatafakari maneno haya ya Mfalme Daudi: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zab. 27:10) Ninakuambia, Yehova hakosi kutimiza ahadi zake.
-