-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma
Cyrus Nyangu, mmojawapo wa ndugu kwenye Halmashauri ya Tawi ya Zambia anasema hivi: “Katika nchi nyingi, huenda watu wakahofu kwamba kikundi cha vijana 25 hivi kitasababisha ghasia. Hata hivyo, vijana Wakristo wenye nguvu waliojitolea wamezoezwa katika madarasa 31 ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, nao wamewanufaisha watu katika maeneo wanakotumika.” Zaidi ya wahitimu 600 wa shule hiyo ya kimataifa wana mapendeleo mbalimbali ya utumishi wa wakati wote katika nchi sita kusini mwa Afrika. Nchini Zambia, zaidi ya nusu ya waangalizi wanaosafiri ni wahitimu wa shule hiyo. Kwa nini shule hiyo ni muhimu, nayo inatimiza nini?
Tangu 1993, wakati ambapo darasa la kwanza lilihitimu, kumekuwa na ongezeko la asilimia 60 hivi la wahubiri watendaji nchini Zambia. Bado wanaume wanaostahili wanahitajiwa ili kushughulikia makutaniko, hasa kwa sababu jamii husisitiza sana watu wafuate mapokeo na desturi zinazopingana na kanuni za Biblia. Akikazia kwamba wanaume wenye uwezo wanahitajiwa ili kufanya uchungaji na kufundisha, mhitimu mmoja alisema: “Katika eneo letu, kuna tatizo la kuachilia makosa. Nimejifunza kwamba tunapaswa kuwa imara kwa lililo jema na kutopita mambo yaliyoandikwa.”
Wanafunzi huwa hawajazoea kujifunza habari nyingi na kwa undani. Hata hivyo, walimu huwa tayari kuwasaidia. Sarel Hart ambaye ni mmoja wa walimu alisema: “Mimi huona kufundisha kila darasa kama kuongoza kikundi cha watalii katika kijia cha mlimani. Mwanzoni, wote ni wageni, wanaojitahidi kuzoea mazingira mapya ya ajabu. Nyakati nyingine kuna vizuizi njiani. Wanafunzi wanaposhinda vizuizi na kuendelea kupanda mlima, wao hutazama nyuma na kuviona vizuizi walivyodhani hawawezi kuvishinda kuwa si kitu.”
Wengi hulinganisha maendeleo yao ya kiroho baada ya kuhudhuria shule hiyo na jinsi kiwavi anavyobadilika na kuwa kipepeo. Elad, ambaye ni painia wa pekee anasema: “Nilihisi kwamba sistahili kufundisha na kwamba mimi ni mchanga sana nisiweze kukubali majukumu mazito kutanikoni. Shule hiyo ilinisaidia kuona kwamba ninaweza kutumika. Wahubiri 16 katika kutaniko la kwanza nilikotumwa hawakujua jinsi ya kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo. Tulichunguza mapendekezo na kufanya mazoezi kwa ukawaida kabla ya kwenda shambani. Kufikia 2001, kutaniko hilo lilikuwa na wahubiri 60, na kikundi cha mbali chenye wahubiri 20.”
Kukadiria Mafanikio
Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba Shule ya Mazoezi ya Kihuduma imetimiza lengo lake? Richard Frudd, ambaye ni mmoja wa walimu anasema: “Tunakazia sana umuhimu wa mtu kuwa mnyenyekevu na kutojifikiria sana kuliko ilivyo lazima. Tunawasaidia wanafunzi wawe wakomavu, wenye huruma, na uwezo wa kukabiliana na hali ngumu na bado wawe na furaha. Ndugu wakitendeana kwa fadhili na wakiwa na nia ya kutumika badala ya kutumikiwa, basi tunajua kwamba shule imetimiza lengo lake.”
Wanafunzi wanakubaliana na maneno hayo. Emmanuel, ambaye ni mhitimu wa darasa la 14, alisema: “Kutumwa kwenye kutaniko fulani hakumaanishi kwamba tunapaswa kurekebisha kila jambo dogo haraka-haraka. Badala yake, tunapaswa kushirikiana na kutaniko kufanya ile kazi muhimu zaidi, yaani, kuhubiri habari njema.”
Moses ambaye ni painia anasema: “Nimetambua kwamba Yehova anaweza kumtumia mtu yeyote aliye mnyenyekevu na kwamba nyakati nyingine ujuzi na uzoefu si muhimu. Kuwapenda akina ndugu na watu tunaowahubiria na vilevile kufanya kazi kwa umoja ndiyo mambo muhimu kwa Yehova.”
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 204, 205]
Kaptura ya Kaki na Viatu vya Raba
Philemon Kasipoh
Alizaliwa: 1948
Alibatizwa: 1966
Maelezo mafupi kumhusu: Yeye ni mwangalizi wa mzunguko na pia mwalimu na mratibu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Zambia.
Babu yangu alinizoeza kuhubiri. Mara nyingi alinipeleka kwa wanafunzi wenzangu na kuniambia niwahubirie. Babu aliongoza funzo la familia kwa ukawaida, na hakuna mtu aliyeruhusiwa kusinzia! Sikuzote nilitarajia funzo la familia kwa hamu.
Nilibatizwa katika mto karibu na nyumbani kwetu. Mwezi mmoja baadaye nilitoa hotuba yangu ya kwanza kutanikoni. Nakumbuka kwamba nilivaa kaptura mpya ya kaki na viatu vya raba siku hiyo. Lakini nilikuwa nimekaza kamba za viatu kwa nguvu sana hivi kwamba nilisikia uchungu. Mtumishi wa kutaniko alitambua tatizo langu. Kwa fadhili alinijia jukwaani na kuzilegeza huku nikiwa nimenyamaza. Nilifaulu kutoa hotuba, na tendo hilo la fadhili lilinifundisha jambo muhimu. Yehova amenizoeza kwa njia nyingi.
Nimejionea utimizo wa Isaya 60:22. Kwa sababu ya ongezeko la idadi ya makutaniko kuna upungufu wa wazee na watumishi wa huduma ambao wamezoezwa vizuri kushughulikia majukumu makutanikoni. Shule ya Mazoezi ya Kihuduma huwapa ndugu mazoezi hayo. Ninafurahi sana kuwafundisha wanaume hao vijana. Nimejifunza kwamba Yehova anapompa mtu kazi fulani, bila shaka Yeye humpa roho takatifu pia.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 201]
Darasa la kwanza la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Zambia, 1993
[Picha katika ukurasa wa 202]
Richard Frudd na Philemon Kasipoh, ambao ni walimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, wakizungumza na mwanafunzi
-