Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Hivyo, ili wenye kupendezwa wawe na umoja na ujuzi sahihi, ilikuwa lazima vichapo vya kujifunzia Biblia vipatikane kwa ukawaida katika lugha zao wenyewe.

      Vichapo Vyaandaliwa

      Mwanzoni mwa miaka ya 1930, kitabu The Harp of God na vijitabu kadhaa vilitafsiriwa na kuchapwa katika Kichinyanja. Kufikia 1934, wahubiri wachache wenye bidii waligawanya zaidi ya vichapo 11,000. Jambo hilo liliwaudhi wapinzani, ambao hatimaye walitunga “matatizo kwa njia ya amri.” (Zab. 94:20) Hata hivyo, mwishoni mwa 1949, gazeti Mnara wa Mlinzi ambalo halikuwa tena chini ya marufuku, lilikuwa likichapishwa mara moja kwa mwezi katika lugha ya Cibemba na kutumwa kwa njia ya posta kwa watu fulani waliokuwa wameliagiza.

      Jonas Manjoni anakumbuka jinsi alivyoshughulikia magazeti mapema katika miaka ya 1950. Anasema: “Mimi ndiye niliyekuwa mtafsiri pekee wa lugha ya Cibemba. Nilipokea makala ya Kiingereza, nikaitafsiri, na kuisahihisha. Kisha, nikaichapa tena kwenye stensili ambayo niliitumia kutolea nakala nyingi. Ilichukua muda mrefu sana kwa kuwa nyakati nyingine nakala zaidi ya 7,000 zilihitajiwa. Nilitayarisha na kuunganisha kila gazeti kwa mkono. Kisha nikayatuma kwa njia ya posta kwenye makutaniko. Nilitumia muda mrefu kuweka stampu kwenye vifurushi vya magazeti na kuvipeleka kwenye posta vikiwa katika makatoni.”

      Ijapokuwa hawakuwa na mashine nzuri, watafsiri wa wakati huo walifanya kazi kwa bidii kwa kuwa walitambua manufaa ya kazi yao. James Mwango alipokuwa mwangalizi anayesafiri, aliandika kwa mkono habari aliyotafsiri, mara nyingi akitumia mwangaza wa mshumaa. Alisema: “Sikuwahi kuhisi nimechoka sana nisiweze kutafsiri. Nilifurahi kwamba kazi yangu ilisaidia kuwaandalia ndugu zangu chakula cha kiroho ili wakomae.”

      ‘Kubadilishana Mikono’

      Ili kuwasilisha kweli vizuri, mtafsiri anapaswa kujua vizuri lugha yake na pia Kiingereza. Aaron Mapulanga alisema: “Katika tafsiri, maneno yanayotumiwa katika misemo huwa na maana tofauti na ile ya kawaida. Nakumbuka mazungumzo tuliyokuwa nayo kuhusu usemi wa Kiingereza, ‘to change hands’ (‘kubadilisha mikono’), ambao ulitumiwa katika kichapo kimoja kilichozungumzia kisa cha Elisha akichukua majukumu ya Eliya. Ndugu mmoja alitafsiri usemi huo neno kwa neno. Niliuliza ikiwa kwa kweli usemi huo ulimaanisha ‘kubadilishana mikono’ kihalisi. Tulishauriana na ndugu wengine na kupata maana hasa ya usemi huo. Pia ninakumbuka kwamba tulishauriwa tusitafsiri habari neno kwa neno kwa kuwa ingesikika kama Kiingereza. Tulijitahidi kuepuka kutafsiri neno kwa neno na tukaanza kutafsiri kwa njia inayoeleweka vizuri katika lugha zetu.”

      Kompyuta Yaharakisha Kazi

      Tangu 1986, mfumo fulani wa kompyuta (MEPS) umekuwa ukitumiwa katika ofisi za tawi. Mfumo huo umeharakisha sana kazi ya kutafsiri, kuchunguza tafsiri, na kupanga herufi. Hivi karibuni, mfumo mwingine wa kompyuta (Watchtower Translation System) umetumiwa sana. Sasa, vikundi vya watafsiri wa lugha kadhaa zinazotumiwa na Wazambia wengi vinatafsiri vichapo vya kujifunzia Biblia kwa njia inayoeleweka. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na ‘silaha nyingine za uadilifu’ zitaendelea kutumiwa kuwasaidia watu wanyoofu wamjue Yehova.—2 Kor. 6:7.

  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 191, 192]

      “Unajiharibia Maisha!”

      Mukosiku Sinaali

      Alizaliwa: 1928

      Alibatizwa: 1951

      Maelezo mafupi kumhusu: Alihitimu Shule ya Gileadi na akafanya kazi ya kutafsiri. Sasa yeye ni mzee wa kutaniko.

      Siku niliyobatizwa, mmishonari Harry Arnott alizungumza nami. Kulikuwa na uhitaji wa watafsiri wa Kisilozi. Aliniuliza kama ningeweza kusaidia. Muda si mrefu, nilipokea barua iliyosema kwamba nimekubaliwa kuwa mtafsiri. Pia nilipokea nakala ya Mnara wa Mlinzi. Nilianza kufanya kazi kwa bidii jioni hiyo. Kazi ya kutafsiri ilikuwa ngumu. Niliandika kwa kalamu kuukuu ya wino kwa muda wa saa nyingi. Hakukuwa na kamusi yoyote ya Kisilozi. Mchana nilifanya kazi kwenye posta na usiku nikafanya kazi ya kutafsiri. Mara kwa mara ofisi ya tawi iliniandikia hivi: “Tafadhali, itume tafsiri mara moja.” Nilijiuliza mara nyingi, ‘Ni nini kinachonizuia nisiwe mtumishi wa wakati wote?’ Hatimaye niliacha kazi ya posta. Wakuu wangu walikuwa wakiniamini, lakini walinishuku nilipotaka kuacha kazi. Walifikiri nilikuwa nimeiba pesa za posta. Wakuu wa posta waliwatuma wakaguzi wawili Wazungu ili wachunguze kazi yangu. Walifanya ukaguzi kwa makini lakini hawakupata tatizo lolote. Hawakuelewa kwa nini nilitaka kuacha kazi. Waajiri wangu walitaka kunipandisha ngazi ili nisiache kazi, na nilipokataa wakaniambia: “Unajiharibia maisha!”

      Sikujiharibia maisha. Niliitwa Betheli mwaka wa 1960. Muda mfupi baadaye nilialikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Nilikuwa na wasiwasi. Nakumbuka kwamba niliposafiri kwa ndege kwa mara ya kwanza kwenda Paris, Amsterdam, na kisha New York, nilijiuliza: “Hivi ndivyo watiwa mafuta wanavyohisi wanapopaa mbinguni?” Nilifurahi sana wakati ndugu kwenye makao makuu waliponikaribisha kwa upendo. Ndugu hao walikuwa wanyenyekevu sana na hawakuwa na ubaguzi hata kidogo. Baada ya kuhitimu nilirudi Zambia, ambako niliendelea kufanya kazi ya kutafsiri.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki