-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Waangalizi Wanaosafiri
Wahudumu wa Mungu wanahitaji kuwa wavumilivu. (Kol. 1:24, 25) Waangalizi wanaosafiri wameweka mfano mzuri kwa kujitolea kuendeleza kazi ya Ufalme. Wachungaji hao wanaoimarisha makutaniko hufanya kazi ya jasho kwa upendo. Hilo linawafanya wawe “zawadi katika wanadamu.”—Efe. 4:8; 1 The. 1:3.
Kufikia mwisho-mwisho wa miaka ya 1930, ndugu wenye uwezo walikuwa wakizoezwa wawe watumishi wa maeneo na wa mikoa. Leo ndugu hao wanaitwa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya. James Mwango anasema: “Haikuwa rahisi kutembelea makutaniko. Tulipewa baiskeli lakini iliwabidi ndugu waandamane nasi kwa miguu ili watubebee mizigo. Kila safari ilichukua siku kadhaa. Tulikuwa tukikaa majuma mawili katika kila kutaniko.”
‘Alizirai Papo Hapo’
Sawa na ilivyo leo, ilikuwa vigumu nyakati hizo kusafiri katika maeneo ya mashambani. Robinson Shamuluma, ambaye sasa ana umri wa zaidi ya miaka 80, aliandamana na mke wake Juliana katika kazi ya kusafiri. Robinson anakumbuka jinsi alivyonyeshewa katika msimu fulani wa mvua. Mvua ilipoacha kunyesha, barabara iliweza kupitika, lakini walihitaji kutembea katika matope yaliyofika kwenye viti vya baiskeli! Walipofika kwenye kutaniko, Juliana alikuwa amechoka sana hivi kwamba hakuwa hata na nguvu za kunywa maji.
Enock Chirwa, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya katika miaka ya 1960 na 1970, anaeleza: “Jumatatu ilikuwa siku ngumu; ilikuwa siku ya kusafiri. Hata hivyo, tulipofika makutanikoni, tuliisahau safari. Tulifurahi kuwa pamoja na akina ndugu.”
Licha ya safari na hali ngumu, tulikabili matatizo mengine. Alipokuwa akisafiri kwenda kutembelea kutaniko fulani kaskazini mwa nchi, Lamp Chisenga aliandamana na ndugu wawili. Kwa mbali, waliona mnyama fulani kwenye njia ya vumbi. Ndugu Chisenga anasema: “Akina ndugu hawakumwona vizuri. Mnyama huyo aliketi njiani naye alifanana na mbwa. Nikawauliza, ‘Mnamwona? Mnamwona?’ Kisha ndugu mmoja akatambua kuwa ni simba. Alipiga yowe na kuzirai papo hapo. Tuliamua kukaa hapo hadi wakati ambapo simba huyo angetokomea vichakani.”
John Jason aliyekuwa mwangalizi wa wilaya na mke wake Kay, walitumika Zambia kwa miaka zaidi ya 26. Walijifunza kuwa na subira gari lao lilipoharibika kabisa. John alisema: “Nakumbuka pindi moja wakati springi ya gari letu ilipovunjika nasi hatukuwa na spea wala hatukujua mahali pa kupata msaada. Ilitubidi kusafiri umbali wa kilometa 150 gari likiwa katika hali hiyo. Katikati ya safari hiyo gari lilichemka na kuharibika kabisa, nasi tukakwama njiani. Tuliweza tu kufanya jambo moja: Kutumia maji yote tuliyokuwa nayo ili kupoza injini na kupika kikombe cha mwisho cha chai. Hapakuwa na watu karibu na kulikuwa na joto, nasi tulikuwa tumechoka. Hivyo tuliketi garini na kumwomba Yehova atusaidie. Saa tisa alasiri, gari la ujenzi wa barabara lilifika. Hilo lilikuwa gari la kwanza kupita hapo siku hiyo. Wale waliokuwa katika gari hilo waliona tatizo letu na wakakubali kutuvuta. Tulifika kwa ndugu zetu kabla tu usiku haujaingia.”
Kujifunza Kuwategemea Wengine
Chini ya hali kama hizo, waangalizi wanaosafiri hujifunza upesi kumtegemea Yehova Mungu na ndugu Wakristo badala ya kujitegemea au kutegemea mali. (Ebr. 13:5, 6) Geoffrey Wheeler anasema: “Majuma matatu tu baada kuwekwa kuwa mwangalizi wa wilaya tulikabili tatizo. Tulikuwa mahali ambapo tungefanyia kusanyiko na tulikuwa tayari kwa ajili ya programu ya mwisho wa juma. Nilikuwa nimepewa stovu fulani mbovu. Kulikuwa na joto na upepo, na nilipoiwasha, moto ulienea ghafula. Muda si muda, moto huo ukawa mkubwa sana. Gurudumu moja la gari letu lilishika moto na upesi moto ukaenea garini mwote.”
Ilikuwa hasara kubwa kwao kupoteza gari, lakini kulikuwa na matatizo mengine pia. Geoffrey anasema: “Nguo zetu zilikuwa kwenye sanduku la chuma garini. Hazikuteketea lakini ziliharibika. Ndugu walienda upande wa gari ambao haukuwa umeshika moto na kuondoa kitanda chetu, shati, na taipureta yangu. Tuliwashukuru sana kwa kuchukua hatua haraka.” Kwa kuwa vitu vyao viliharibika garini, nao walitazamia kurudi mjini baada ya miezi miwili, walifanyaje? Geoffrey anasema: “Ndugu mmoja alinipa tai na nikatoa hotuba ya watu wote nikiwa nimevalia viatu vikubwa. Tulifaulu kuendelea na kazi yetu na ndugu wakajitahidi sana kumfariji mwangalizi wao wa wilaya ambaye hakuwa na ujuzi.”
Kitanda Kisichoweza Kupandwa na Nyoka
Sifa ya upendo na ya kuwajali wengine zilizoonyeshwa na makutaniko ‘yanayofuata mwendo wa ukaribishaji-wageni,’ ziliwaimarisha waangalizi wanaosafiri pamoja na wake zao na kuwawezesha kuendelea kujitoa katika kazi yao. Kuna masimulizi chungu nzima kuhusu jinsi makutaniko maskini yanavyoandaa kwa upendo msaada unaothaminiwa sana.—Rom. 12:13; Met. 15:17.
Waangalizi wanaosafiri huandaliwa kwa upendo mahali pa kukaa. Fred Kashimoto, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko katika miaka ya 1980, anakumbuka kwamba aliwasili usiku kwenye kijiji fulani katika Mkoa wa Kaskazini wa Zambia. Ndugu walimkaribisha kwa shangwe. Walipoingia kwenye nyumba fulani ndogo, ndugu hao waliweka mifuko yake juu ya meza kubwa iliyotengenezwa kwa magogo na ambayo ilikuwa na kimo cha meta moja na nusu. Baada ya muda, Ndugu Kashimoto akauliza, “Nitalala wapi?”
Ndugu walimwonyesha meza hiyo na kusema: “Kitanda chako ndicho kile pale.” Kwa sababu kulikuwa na nyoka wengi katika eneo hilo, akina ndugu walitengeneza kitanda salama. Ndugu Kashimoto akalala hapo kwenye kitanda chenye godoro la nyasi.
Mashambani watu hupewa zawadi mbalimbali. Geoffrey Wheeler anasema: “Pindi moja tulipewa kuku na akina ndugu. Kabla usiku haujaingia, tulimweka chooni alale hapo. Lakini kiumbe huyo mpumbavu aliruka na kuingia ndani ya shimo la choo. Tulimwokoa kwa kutumia jembe. Kisha mke wangu akamwosha kwa maji ya moto yenye sabuni na dawa nyingi. Tulimpika mwishoni mwa juma naye alikuwa mtamu wee!”
Ndugu na Dada Jason pia walionyeshwa ukarimu. John alisema: “Mara kwa mara ndugu walitupa kuku aliye hai.Tulikuwa na kikapu kidogo cha kubebea kuku tulipokuwa tukisafiri. Alitaga yai kila asubuhi, hivyo hatukumla. Tulipokuwa tukijitayarisha kwenda kwenye eneo lingine, kuku huyo alionyesha wazi kwamba alitaka kuandamana nasi.”
Sinema
Kuanzia 1954, sinema The New World Society in Action na sinema nyingine zilitumiwa katika kampeni yenye kuchochea ya elimu. Ripoti moja ya ofisi ya tawi inasema: “Iliwasukuma wengi waongeze bidii yao katika huduma na kutanikoni.” Wengine walizoea kusema hivi walipokuwa wakibomoa mabanda ya kusanyiko baada ya onyesho la sinema hiyo: “Na tufanye kwa njia ya ‘The New World Society in Action,’” wakimaanisha “kwa bidii na haraka!” Katika kipindi cha mwaka mmoja tangu sinema hiyo itolewe, ilitazamwa na zaidi ya watu 42,000, kutia ndani maofisa wa serikali na wa elimu, ambao waliifurahia sana. Hatimaye, zaidi ya watu milioni moja nchini Zambia wakapata habari kuwahusu Mashahidi wa Yehova na tengenezo lao la Kikristo.
Wayne Johnson anakumbuka jinsi sinema hiyo ilivyokuwa na matokeo mazuri. Anasema: “Watu kutoka mbali walikuja kuiona, nayo ilitumiwa kuwafundisha kuhusu tengenezo la Yehova. Mara kwa mara, watu walishangilia kwa muda mrefu ilipokuwa ikionyeshwa.”
Kwa kipindi fulani, sinema moja kati ya hizo ilionyeshwa Jumamosi jioni katika kusanyiko la mzunguko. Ziliwavutia sana watu wa mashambani. Mpango huo ulifanikiwa, lakini watu ambao hawakufahamu hali za maisha katika nchi nyingine walielewa vibaya baadhi ya picha. Katika sinema moja kulikuwa na picha ya watu wakitoka kwenye kituo cha gari-moshi la chini ya ardhi huko New York City. Wengi walifikiri hiyo ni picha ya ufufuo! Vyovyote vile, sinema hizo ziliwasaidia watu kuwafahamu vizuri Mashahidi wa Yehova. Lakini hali zilikuwa zikibadilika, na tamaa ya Wazambia ya kupata uhuru ingewafanya wengi wawachukie akina ndugu. Makutaniko na waangalizi wanaosafiri wangekabili hali ambazo zingehitaji wawe na uvumilivu hata zaidi.
Siasa Yavuruga Kazi
Mnamo Oktoba 24, 1964, Rodeshia Kaskazini ilipata uhuru kutoka Uingereza na kuwa Jamhuri ya Zambia. Katika kipindi hicho, kulikuwa na uhasama mkubwa wa kisiasa. Kukataa kwa Mashahidi wa Yehova kuunga mkono siasa kulionwa kuwa jitihada ya kuendeleza ukoloni.
Lamp Chisenga anakumbuka safari yake ya kwenda kwenye eneo la Ziwa Bangweulu wakati huo. Alinuia kusafiri kwa mashua hadi visiwani ili kuwatembelea wavuvi waliokuwa Mashahidi. Kwanza alisafiri kwa basi hadi pwani. Aliposhuka, aliitishwa kadi ya chama cha kisiasa. Lakini hakuwa nayo. Wanaharakati fulani wa chama cha kisiasa walichukua mkoba wake na mmoja wao akaona kisanduku kilichoandikwa “Mnara wa Mlinzi.” Alipuliza filimbi yake na kuanza kupiga kelele akisema: “Mnara wa Mlinzi! Mnara wa Mlinzi!”
Akihofia mchafuko, ofisa fulani alimsukuma Lamp na mifuko yake ndani ya basi. Tayari umati ulikuwa umekusanyika na kuanza kulirushia basi mawe na kupiga mlango, magurudumu, na madirisha. Dereva aliliondoa basi mbio, na hakusimama popote njiani hadi walipofika Samfya, umbali wa kilometa 90 hivi. Hali ilitulia usiku. Kesho yake Lamp alipanda mashua, na bila woga akaendelea na safari yake ya kutembelea makutaniko madogo kwenye eneo la ziwa hilo.
“Kwa kuvumilia mengi,” waangalizi wanaosafiri wanaendelea kujipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu. (2 Kor. 6:4) Fanwell Chisenga, aliyetembelea makutaniko kandokando ya Mto Zambezi, anasema: “Mwangalizi wa mzunguko anahitaji kujitoa kwa nafsi yote.” Kutembelea makutaniko kando ya mto huo kulihusisha safari ndefu kwa mitumbwi inayovuja, ambayo ingeweza kuvunjwa kama kijiti kikavu na kiboko mwenye hasira. Ni nini kilichomsaidia Fanwell aendelee kutembelea makutaniko? Anatabasamu anapotazama kwa makini picha ya ndugu na dada wa kutaniko fulani waliomsindikiza hadi mtoni na kusema kwamba ndugu na dada zake ndio waliomchochea. Kisha anauliza: “Ni wapi pengine katika ulimwengu huu wenye hasira unapoweza kupata watu wenye nyuso zenye furaha kama hizi?”
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 221]
Nilikonda Kama Ng’onda
Michael Mukanu
Alizaliwa: 1928
Alibatizwa: 1954
Maelezo mafupi kumhusu: Alikuwa mwangalizi wa mzunguko na sasa anafanya kazi kwenye Betheli nchini Zambia.
Katiwka mzunguko wangu kulikuwa na bonde fulani lenye mwinuko mkali. Nilisumbuliwa na mbung’o mara nyingi. Ili niwaepuke wadudu na jua kali la mchana, nilikuwa nikiamka saa 7:00 usiku na kuanza safari ya kwenda kwenye kutaniko lingine. Safari hizo zilihusisha kupanda milima na vilima. Nilibeba vitu vichache tu kwa sababu mara nyingi nilitembea sana kwa miguu. Sikuwa na chakula cha kutosha, kwa hiyo nilikonda kama ng’onda. Kwa sababu ndugu katika mzunguko huo walifikiri nitakufa hakika, walitaka kuiandikia ofisi ya tawi na kuomba nihamishwe kwenye mzunguko mwingine. Waliponiambia jambo hilo nilisema: “Pendekezo lenu ni la fadhili, lakini kumbukeni kwamba Yehova ndiye aliyenituma huku, naye anaweza kunihamisha. Nikifa, je, nitakuwa mtu wa kwanza kuzikwa huku? Niruhusuni niendelee na utumishi wangu. Nikifa, wajulisheni ndugu kwenye ofisi ya tawi.”
Majuma matatu baadaye nilihamishwa kwenye mzunguko mwingine. Si rahisi sikuzote kumtumikia Yehova, lakini hatuna budi kuendelea. Yehova ni Mungu mwenye furaha na watumishi wake wakikosa furaha, anaweza kubadili hali ili waendelee kumtumikia kwa shangwe.
[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 223, 224]
Hatuamini Ushirikina
Harkins Mukinga
Alizaliwa: 1954
Alibatizwa: 1970
Maelezo mafupi kumhusu: Alikuwa mwangalizi anayesafiri naye aliandamana na mke wake katika kazi hiyo. Sasa yuko Betheli nchini Zambia.
Nilipotembelea makutaniko, niliandamana na mke wangu Idah na mvulana wetu mwenye umri wa miaka miwili. Tulipotembelea kutaniko fulani, ndugu walitukaribisha kwa uchangamfu. Asubuhi siku ya Alhamisi, mtoto wetu alianza kulia mfululizo. Saa 2:00 asubuhi niliondoka ili niende kwenye mkutano wa utumishi, na kumwacha Idah akimtunza mtoto wetu. Muda wa saa moja baadaye nilipokuwa nikiongoza funzo la Biblia, nilipata habari kwamba mtoto wetu amekufa. Tulihuzunika sana kusikia kwamba ndugu kadhaa walifikiri amelogwa. Tulijaribu kuwaonyesha kwamba hatupaswi kuogopa kulogwa kama wengine wanavyoogopa, lakini habari hiyo ilienea kama umeme katika eneo lote. Niliwaeleza ndugu kwamba Shetani ni mwenye nguvu, lakini hawezi kamwe kumshinda Yehova wala watumishi Wake waaminifu. “Wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote, lakini hatupaswi kukata kauli isivyofaa kwa sababu ya woga.—Mhu. 9:11.
Mtoto wetu alizikwa siku iliyofuata na baada ya mazishi tukafanya mkutano. Hata hivyo, tuliufanya baada ya mazishi. Ndugu walijifunza mambo muhimu kutokana na tukio hilo, yaani, hatuwaogopi roho waovu wala hatuamini ushirikina. Ijapokuwa tulihuzunishwa sana na kifo cha mtoto wetu, tuliendelea na utumishi hadi mwisho wa juma letu la pekee, kisha tukaondoka na kwenda kwenye kutaniko lingine. Badala ya ndugu katika makutaniko kutufariji, sisi ndio tuliowafariji na kuwahakikishia kwamba bado kitambo kidogo na kifo hakitakuwapo tena.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 228, 229]
Tulijipa Ujasiri
Lennard Musonda
Alizaliwa: 1955
Alibatizwa: 1974
Maelezo mafupi kumhusu: Amekuwa mtumishi wa wakati wote tangu 1976. Alikuwa mwangalizi anayesafiri kwa miaka sita na sasa anafanya kazi kwenye Betheli nchini Zambia.
Nilikuwa nikitembelea makutaniko katika sehemu ya kaskazini nchini humu, yapata mwaka wa 1985. Katika miaka iliyotangulia kulikuwa na upinzani mkali wa kisiasa katika eneo hilo. Baada ya kuwa mwangalizi wa mzunguko kwa muda mfupi tu nilipata nafasi ya kuonyesha imani na ujasiri. Siku moja baada ya mkutano wa utumishi, tulikuwa tayari kwenda kuhubiri katika kijiji jirani. Ndipo ndugu fulani aliposema amesikia uvumi kwamba watu wote katika kijiji hicho wangewapiga Mashahidi wa Yehova kama wangethubutu kuhubiri kijijini mwao. Ijapokuwa watu wenye ghasia waliwashambulia ndugu mwishoni mwa miaka ya 1960 na mapema katika miaka ya 1970, sikuamini kwamba watu wote kijijini wangetushambulia wakati huu.
Hata hivyo, wahubiri kadhaa waliposikia habari hiyo waliogopa na kukataa kwenda nasi. Wengi wetu tulijipa ujasiri na tukaenda. Tulishangaa tulipofika kijijini humo. Tuligawa magazeti mengi na kuongea kwa urafiki na wale tuliowapata. Lakini baadhi ya watu walitoroka walipotuona tukiingia kijijini. Waliacha nyungu mekoni na hawakufunga milango. Badala ya kutushambulia wanakijiji hao walikimbia.
-