Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Utumishi wa Wamishonari

      Ian (John) Fergusson, aliyetumika kwa miaka mingi huko Zambia anasema: “Mojawapo ya mambo yenye kupendeza sana kuhusu umishonari ni kuona jinsi Yehova anavyowatumia wanaume na wanawake wa aina zote kutimiza kusudi lake. Inafurahisha pia kuona uthamini wa wale wanaopokea msaada wa kiroho.” Wamishonari wa dini nyingine huzingatia zaidi mambo ya kijamii na kiuchumi, hali wamishonari wa Mashahidi wa Yehova huzingatia kazi ya kufanya wanafunzi Wakristo. Kwa kufanya kazi waliyopewa na Mungu, wamishonari wa Mashahidi wamethibitisha kwamba wana “upendo usio na unafiki.”—2 Kor. 6:6.

      Roho ya umishonari ilionyeshwa vizuri na watu kama vile William Johnston ambaye, miaka michache kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, alikuja kusini mwa Afrika na akasafiri katika eneo hilo lote. Mapema katika 1921, Piet de Jager, Parry Williams, na wengine walikuwa wamefika Salisbury (sasa linaitwa Harare), jiji kuu la nchi jirani ya Zambia, yaani, Rodeshia Kusini (sasa inaitwa Zimbabwe). Katikati ya miaka ya 1920, George Phillips, Thomas Walder, na William Dawson, walizingatia eneo la Rodeshia Kaskazini. Watu fulani waliozaliwa Rodeshia Kaskazini lakini wakajifunza na Wanafunzi wa Biblia walipokuwa wakifanya kazi katika maeneo mengine, walirudi Rodeshia Kaskazini ili kueneza “habari njema ya mambo mema.” (Rom. 10:15) Manasse Nkhoma na Oliver Kabungo walieneza sana habari njema wakati huo. Joseph Mulemwa, mwenyeji wa Zambia, alihubiriwa kwenye mgodi huko Wankie (sasa unaitwa Hwange) kaskazini mwa Zimbabwe, na baadaye akatumika kwa uaminifu katika eneo la magharibi la Zambia. Fred Kabombo ndiye aliyekuwa mwangalizi wa kwanza anayesafiri katika eneo hilo. Ndugu hao ndio waliokuwa wa kwanza kufikia maeneo yaliyokuwa yamehubiriwa kidogo na hata yale ambayo hayakuwa yamehubiriwa nao wakaweka msingi mzuri kwa ajili ya ongezeko.

      Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokaribia kwisha, Charles Holliday kutoka Afrika Kusini aliombwa na George Phillips wa ofisi ya tawi ya Cape Town atembelee vikundi vya watu wanaopendezwa katika Wilaya ya Magharibi, naye akakubali. Ndugu Holliday pamoja na ndugu mwenyeji aliyekuwa mfasiri wake walisafiri kwa gari-moshi la kusafirishia mbao, wakasafiri kwa mtumbwi, na kwa kigari cha reli. Walipofika Senanga, ambao ni mji mdogo ulio kilometa 250 kaskazini ya Maporomoko ya Viktoria, walikaribishwa na umati. Baadhi yao walikuwa wamesafiri kwa siku kadhaa, na walikuwa na hamu ya kumsikiliza mgeni huyo akifafanua kweli za Biblia.

      Wamishonari Kutoka Gileadi Wawasili

      Katika 1948, wamishonari wawili, yaani, Harry Arnott na Ian Fergusson, waliwasili Zambia. Waliwahubiria hasa maelfu ya Wazungu waliohamia eneo hilo ili kuchimbua shaba. Walipata matokeo mazuri sana. Mwaka huo idadi ya Mashahidi wa habari njema iliongezeka kwa asilimia 61.

      Katika maeneo mengi ilikuwa kawaida kwa wamishonari kuwa na watu wengi sana waliotaka kujifunza Biblia hivi kwamba walilazimika kuwaomba wengine wasubiri. Ofisi ya tawi ilinunua gari, lililokuwa limetumiwa kwa miaka kumi, ambalo wamishonari wawili waliokuwa waangalizi wanaosafiri walilitumia kusafiri kwenye maeneo yaliyokuwa mbali na maeneo yenye migodi. Ripoti moja ya ofisi ya tawi ilisema kwamba gari hilo “lilisaidia sana, ijapokuwa nyakati nyingine tulirudi kwenye ofisi ya tawi gari likiwa limeharibika sana.”

      Kufikia 1951, kulikuwa na wamishonari sita nchini humo. Katika Desemba 1953, wamishonari wengine sita waliwasili wakiwa tayari kusaidia. Valora na John Miles walikuwa miongoni mwao, nao walitumika Zambia kwa miaka sita, kisha wakatumwa Zimbabwe na hatimaye Lesotho. Katika miaka iliyofuata, Joseph Hawryluk, John na Ian Renton, Eugene Kinaschuk, Paul Ondejko, Peter na Vera Palliser, Avis Morgan, na wamishonari wengine waliwasili. Wote hao walifanya kazi kwa upendo. Bila shaka, ili wafanikiwe katika utumishi wao wa pekee, iliwabidi wajitolee na kufanya marekebisho.

      “Angali Mtoto!”

      Wayne Johnson anasema hivi anapokumbuka jinsi alivyohisi alipotumwa Zambia: “Niliamini kwamba walionituma walikuwa wamekosea.” Wayne, aliyehitimu katika darasa la 36 la Shule ya Gileadi, aliwasili mwanzoni mwa 1962, akiandamana na Earl Archibald. Sasa Wayne ni mwangalizi anayesafiri huko Kanada, naye huandamana na mke wake Grace. Wayne anasema: “Nilikuwa na miaka 24 tu na nilionekana mchanga hata zaidi. Nilipokuwa nikijifunza lugha ya Kichinyanja [pia inaitwa Kichichewa], niliwasikia akina dada walioniona kwa mara ya kwanza wakinong’onezeana: ‘akali mwana,’ yaani, ‘Angali mtoto!’”

      Wayne anasema: “Nilitambua kuwa ningehitaji kumtegemea sana Yehova na tengenezo lake. Nilitaka kila mmoja atambue kwamba kupatana na Matendo 16:4, mwelekezo na ujumbe niliotoa ulitoka kwa Yehova na tengenezo lake. Nilijitahidi kutenda kwa njia ambayo ingekubalika kwa wengine. Ninapokumbuka hayo, bado ninashangaa kwamba nilipewa pendeleo kubwa hivyo.”

      Kufukuzwa Nchini!

      Kulikuwa na mabadiliko katika miaka ya 1960 na 1970. Mara kwa mara mateso yalitokea katika sehemu mbalimbali nchini. Baada ya Zambia kupata uhuru mnamo 1964, ndugu walikabili hali ngumu kuhusiana na kusalimu bendera na kuimba wimbo wa taifa. Mwishoni mwa miaka ya 1960, wanasiasa fulani walifikiri kuwa kazi ya wamishonari ilipingana na malengo ya serikali. Ripoti ya ofisi ya tawi inaeleza kilichotukia: “Alfajiri na mapema Januari 20, 1968, waangalizi wa karibu makutaniko yote ya Kiingereza walipiga simu na kujulisha ofisi ya tawi kwamba walikuwa wamepewa barua ya kufukuzwa nchini. Kwa kushangaza, si Mashahidi wageni tu waliopewa barua hizo bali pia raia wa Zambia, kama vile George Morton na Isaac Chipungu.”

      Serikali ilichukua hatua haraka. Siku hiyohiyo saa nne asubuhi, maofisa wa idara ya uhamiaji walikuja kwenye ofisi ya tawi ili kuwapa wamishonari watano na wake zao barua za kuwafukuza nchini. Mmishonari Frank Lewis anasema: “Walifika upesi kwenye ofisi ya tawi. Iliamuliwa kwamba ndugu wamishonari waliokuwa ofisini waondoke kupitia mlango wa nyuma na kwenda kwa ndugu fulani ili kutekeleza yale ambayo yalikuwa yameamuliwa yafanywe iwapo tungepigwa marufuku. Hata hivyo, tulikawia-kawia kwa sababu dada fulani mmishonari alikuwa na homa kali ya malaria. Lakini ndugu wenyeji walituhimiza tuondoke nao wakasema watamtunza. Tulijua wangefanya hivyo.

      “Tulishangaa sana tuliposoma katika gazeti moja (Times of Zambia) kuwa shirika la Mnara wa Mlinzi, kama walivyokuwa wakituita, limepigwa marufuku na ‘viongozi’ wake wameenda mafichoni. Majina yetu yalikuwa kwenye ukurasa wa kwanza wa gazeti hilo lililosema kwamba serikali ilikuwa ikitutafuta nyumba kwa nyumba mjini! Ndugu wenyeji waliokuwa wamebaki ofisini walifanya kazi yao vizuri. Walihamisha faili na vichapo kwingineko. Siku iliyofuata, baada ya shughuli hiyo kukamilika, tulirudi kwenye ofisi ya tawi na kujisalimisha.”

      Polisi mmoja alishika doria kwenye ofisi ya tawi, na upesi wamishonari kadhaa na pia ndugu wengine ambao hawakuwa Wazambia wakapewa barua za kuwafukuza nchini. “Tulikuwa miongoni mwa watu wa mwisho kuondoka,” akaeleza Ndugu Lewis. “Bado tunawakumbuka kwa majonzi dada tusiowafahamu vizuri, ambao pamoja na watoto wao, walisafiri kilometa 25 kutoka Kalulushi ili kutuaga tu!”

      Wamishonari Wengine Wafukuzwa

      Wakati ulipita. Katika 1975, Albert Musonda, ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Zambia, alikuwa na umri wa miaka 22 naye alikuwa mtumishi wa kujitolea katika Idara ya Hesabu ya Betheli. Siku moja katika 1975, polisi waliwasili ghafula. Musonda anasema: “Waliwapa wamishonari muda usiozidi siku mbili waondoke nchini.”

      John Jason anaongezea: “Mnamo Desemba 1975, barua fupi ya ofisi ya idara ya uhamiaji ilituagiza tuondoke nchi kabla ya saa 36 kupita.” Rufani ilikatwa kupitia kwa wakili mwenyeji, na wamishonari wakaongezewa muda wakusanye baadhi ya vitu vyao. “Baada ya hilo,” anasema Ndugu Jason, “ilitubidi kuwaacha watu tuliowapenda sana.”

      Dailes, mke wa Albert anasema: “Tuliwasindikiza ndugu zetu hadi kwenye Uwanja wa Ndege wa Southdown. John Jason alienda Kenya, naye Ian Fergusson akaenda Hispania.” Kwa nini wamishonari hao walifukuzwa nchini?

      Kwa maoni ya wengi, kusanyiko lililofanywa mnamo 1975 ndilo lililotibua nyongo. John Jason anasema: “Lilikuwa mojawapo ya makusanyiko makubwa zaidi kuwahi kufanywa katika kipindi hicho cha msukosuko, na lilihudhuriwa na watu zaidi ya 40,000.” Kusanyiko hilo lilipokuwa likiendelea, mkutano fulani wa kisiasa ulikuwa ukifanywa hapo karibu. Watu fulani kwenye mkutano huo walitaka Mashahidi wa Yehova wachukuliwe hatua kali kwa kutounga mkono siasa. Ndugu Jason anasema kwamba watu walidai kuwa kusanyiko hilo la Mashahidi wa Yehova ndilo lililofanya mkutano huo wa siasa usihudhuriwe na watu wengi.

      Wamishonari Warudi

      Miaka kumi ilipita kabla wamishonari hawajaruhusiwa tena kuingia Zambia. Katika miaka ya 1980, hali ya kisiasa iliimarika na masharti mengi yakaondolewa. Katika 1986, Edward Finch na mke wake, Linda, kutoka Gambia, waliwasili. Wengine kutia ndani Alfred na Helen Kyhe, na Dietmar na Sabine Schmidt wakaja baadaye.

      Mnamo Septemba 1987, Dayrell na Susanne Sharp walitoka Zaire, ambayo sasa ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, wakapitia Afrika Kusini, na kwenda Zambia. Ndugu Sharp na mke wake walihitimu katika Shule ya Gileadi mnamo 1969 naye aliandamana na mkewe alipokuwa mwangalizi anayesafiri nchini Kongo. Walikuwa wamezoea hali ya maisha katika eneo la katikati ya Afrika. Dayrell, mwanamume mwenye nguvu na afya, amekuwa katika utumishi wa pekee wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 40. Anasema: “Kwa miaka kadhaa tulikuwa tukiishi katika makao ya wamishonari huko Lubumbashi, karibu na mpaka, nasi tulikuwa tukienda Zambia mara kwa mara.”

      Susanne anakumbuka vizuri kipindi hicho. Anasema: “Kwa sababu ya upungufu wa chakula nchini Kongo katika miaka ya 1970, ilitubidi kwenda Zambia kununua chakula baada ya kila miezi michache. Kisha mwanzoni mwa 1987, Baraza Linaloongoza likatuomba tuhame Kongo na kwenda kwenye eneo jipya. Wapi? Zambia!” Kwa kuwa kazi yao ilizuiwa sana huko Kongo, Ndugu na Dada Sharp walifurahia sana kuhamia nchi ambako ndugu walifurahia uhuru wa kidini uliokuwa ukiongezeka.

      Hata hivyo, marekebisho fulani yalihitajiwa katika kazi ya kuhubiri na pia kwenye ofisi ya tawi. Kwa sababu masharti fulani yalikuwa yamewekwa dhidi ya kazi ya kuhubiri habari njema hadharani, ndugu waliongoza tu mafunzo ya Biblia. Mashahidi wa Yehova huhubiri hasa nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, wahubiri wengi hawakujua jinsi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na pia walikosa ujasiri. Hivyo, ndugu walitiwa moyo wawe wajasiri na wahubiri nyumba kwa nyumba, hasa kwa sababu hali nchini ilikuwa imetulia na polisi hawakufuatilia sana shughuli zetu.

      Kusonga Mbele Badala ya Kurudi Nyuma

      Halmashauri ya Tawi ilihangaika kwa kuwa hakukuwa na ongezeko katika miaka ya 1970. Ilikuwa vigumu kwa akina ndugu kujifunza na watoto wao kwa sababu ya mapokeo. Hivyo, kwa kuwa kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ilikuwa imepigwa marufuku, akina baba waliacha wahubiri wengine wajifunze na watoto wao, nao wakajifunza na watoto wa wengine. Wakati wa kufanya maamuzi kwa ujasiri ulikuwa umewadia. Katika miaka iliyofuata, wahubiri walihimizwa waache mapokeo na mazoea yasiyo ya Kimaandiko. Makutaniko yalibarikiwa kwa sababu ya kutii, na ndugu wakajitahidi sana kuishi kupatana na kanuni za Biblia na kwa umoja na akina ndugu ulimwenguni pote.

      Katika kipindi cha miaka mitano tangu wamishonari wafukuzwe mnamo 1975, idadi ya wahubiri ilipungua kwa asilimia 11. Wamishonari walirudi mnamo 1986. Katika miaka mitano iliyofuata, kilele cha wahubiri kilipanda kwa zaidi ya asilimia 50. Tangu mwaka huo, idadi ya wahubiri watendaji imeongezeka zaidi ya mara mbili.

      Silas Chivweka, ambaye zamani alikuwa mwangalizi anayesafiri, anasema hivi katika barua aliyoiandikia ofisi ya tawi: “Tangu miaka ya 1950 na kuendelea, wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wamewasaidia wengine wakomae. Wamishonari walikuwa wenye subira sana, wenye huruma, na wenye fadhili. Kwa kuwa na uhusiano wa karibu na wahubiri, walifaulu kutambua mambo yaliyohitaji kurekebishwa.” Msaada ambao wamishonari hao walitoa kwa upendo na bila unafiki bado unachangia ongezeko.

  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • 1948: Wahitimu wa kwanza wa Shule ya Gileadi wawasili.

  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • 1975: Wamishonari wafukuzwa.

      1986: Wamishonari waruhusiwa tena kuingia nchini.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki