Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kufurahia “Uzima wa Sasa” Kikamili
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 1
    • Muda mfupi baadaye tulipewa mgawo mpya huko Southern Rhodesia (ambayo sasa ni Zimbabwe).

      Tulisafiri kwa gari-moshi nasi tuliona kwa mara ya kwanza Maporomoko ya Victoria kabla ya kufika Bulawayo. Tulikaa kwa kipindi fulani pamoja na familia ya akina McLuckie ambao walikuwa kati ya Mashahidi wa kwanza kuishi huko. Lilikuwa pendeleo kujuana nao vizuri kwa muda wa miaka 16 iliyofuata.

      Kuzoea Mabadiliko

      Baada ya kuzoezwa kwa majuma mawili ili kulifahamu vizuri eneo la Afrika, niliwekwa rasmi kutumika nikiwa mwangalizi wa wilaya. Tulipohubiri mashambani barani Afrika ilitubidi kubeba maji, chakula, malazi, nguo, kifaa na kitambaa kikubwa cha kuonyeshea sinema, jenereta, na vitu vingine vya lazima. Vitu hivyo vyote vilipakiwa katika lori lenye nguvu ambalo lingeweza kupita kwenye barabara mbovu.

      Nilifanya kazi pamoja na waangalizi wa mizunguko Waafrika huku Joyce akiwasaidia kwa furaha wake na watoto wao ambao waliandamana nao. Inachosha kutembea katika maeneo tambarare ya Afrika, hasa wakati wa joto la mchana. Lakini punde si punde, niliona kwamba katika hali hiyo ya hewa, ilikuwa rahisi kwangu kuvumilia udhaifu wangu wa kimwili, nami nilifurahia sana jambo hilo.

      Kwa ujumla watu walikuwa maskini. Wengi walishikilia mila na ushirikina na kuoa zaidi ya mke mmoja, lakini waliiheshimu sana Biblia. Katika maeneo fulani, mikutano ya kutaniko ilifanywa chini ya miti mikubwa yenye kivuli, na wakati wa jioni tulitumia taa za mafuta zilizoning’inizwa. Tulipojifunza Neno la Mungu chini ya anga yenye nyota, sikuzote tulistaajabishwa na sehemu hiyo ya uumbaji mtukufu wa Mungu.

      Kuonyesha sinema za Watch Tower Society katika maeneo ya Kiafrika ni jambo lingine ambalo hatutalisahau. Tulipoonyesha sinema hizo, tulitazamia hudhurio la watu 1,000 au zaidi, ingawa kwa kawaida kutaniko lilikuwa na Mashahidi 30 hivi!

      Bila shaka, katika nchi za joto, inawezekana mtu kuwa mgonjwa mara kwa mara, lakini sikuzote ni muhimu kuwa na mtazamo mzuri. Mimi na Joyce tulikabiliana na hali hiyo vizuri. Nilipatwa mara kwa mara na malaria, naye Joyce alipatwa na ugonjwa unaosababishwa na amiba.

      Baadaye, tuliitwa kwenye ofisi ya tawi huko Salisbury (ambayo sasa ni Harare), ambako tulikuwa na pendeleo la kufanya kazi pamoja na watumishi wengine waaminifu wa Yehova, wakiwemo Lester Davey na George na Ruby Bradley. Serikali iliniweka rasmi kuwa ofisa wa ndoa. Hilo liliniwezesha kuhalalisha ndoa za ndugu Waafrika, na hivyo kuimarisha kifungo cha ndoa ya Kikristo katika makutaniko. Miaka michache baadaye, nilipewa pendeleo lingine, yaani, kutembelea makutaniko yasiyo ya Kibantu nchini. Kwa zaidi ya miaka kumi, mimi na Joyce tulifurahia kujuana na ndugu zetu katika kazi yetu ya kusafiri, nasi tulipendezwa na maendeleo yao ya kiroho. Wakati huo tuliwatembelea pia ndugu zetu huko Botswana na Msumbiji.

  • Kufurahia “Uzima wa Sasa” Kikamili
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 1
    • [Picha katika ukurasa wa 27]

      Kutumikia kikundi cha mbali (juu) na kutaniko (kushoto) huko Southern Rhodesia, ambayo sasa ni Zimbabwe

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki