Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Lazima Wote Watoe Hesabu kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Septemba 15
    • Lazima Wote Watoe Hesabu kwa Mungu

      “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—WARUMI 14:12, NW.

      1. Ni mipaka gani iliyowekewa uhuru wa Adamu na Hawa?

      YEHOVA MUNGU aliwaumba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, wakiwa viumbe walio huru kuchagua. Ingawa walikuwa wa hali ya chini kuliko malaika, walikuwa viumbe wenye akili waliokuwa na uwezo wa kufanya maamuzi yenye hekima. (Zaburi 8:4, 5) Hata hivyo, uhuru huo waliopewa na Mungu haukuwapa wanadamu ruhusa ya kujiamulia kibinafsi mema na mabaya. Walikuwa na wajibu wa kutoa hesabu kwa Muumba wao, na wajibu huo wa kutoa hesabu ulifikia wazao wao wote.

      2. Yehova atafanyiza kutoa hesabu kupi karibuni, na kwa nini?

      2 Sasa kwa sababu tunakaribia upeo wa mfumo huu mwovu wa mambo, Yehova atafanyiza kutoa hesabu duniani. (Linganisha Warumi 9:28.) Karibuni, watu wasiomwogopa Mungu watalazimika kutoa hesabu kwa Yehova Mungu kwa sababu ya uangamizi wa mali za dunia, uharibifu wa uhai wa kibinadamu, na hasa mnyanyaso wa watumishi wake.—Ufunuo 6:10; 11:18.

      3. Ni maswali gani tutakayofikiria?

      3 Kwa sababu tunakabili taraja hilo linalotufanya tufikiri, ni faida kwetu kukumbuka shughuli zenye uadilifu za Yehova pamoja na viumbe wake katika nyakati zilizopita. Maandiko yanaweza kutusaidiaje, kibinafsi, kutoa hesabu yenye kukubalika kwa Muumba wetu? Ni vielelezo vipi ambavyo huenda vikawa vyenye kusaidia, na ni vipi tuepuke kuiga?

      Malaika Wana Wajibu wa Kutoa Hesabu

      4. Twajuaje kwamba Mungu huwapasisha malaika kutoa hesabu kwa ajili ya vitendo vyao?

      4 Viumbe wa kimalaika wa Yehova walio mbinguni wana wajibu uleule tulio nao wa kutoa hesabu kwake. Kabla ya Furiko la siku ya Noa, malaika fulani kwa kutotii walijitwalia miili ya kibinadamu ili wafanye ngono pamoja na wanawake. Wakiwa viumbe hai walio huru kuchagua, viumbe hao wa roho waliweza kufanya uamuzi huo, lakini Mungu aliwatoza hesabu. Wale malaika wasiotii waliporudi kwenye makao ya roho, Yehova hakuwaruhusu warudie cheo chao cha awali. Mwanafunzi Yuda atuambia kwamba “amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu.”—Yuda 6.

      5. Shetani na roho zake waovu wamepatwa na anguko gani, na hesabu ya uasi wao itatozwaje?

      5 Mtawala wa malaika hao wasiotii, au roho waovu, ni Shetani Ibilisi. (Mathayo 12:24-26) Malaika huyo mwovu aliasi dhidi ya Muumba wake akapinga uhaki wa enzi kuu ya Yehova. Shetani aliongoza wazazi wetu wa kwanza kwenye dhambi, na tokeo likawa kufa kwao hatimaye. (Mwanzo 3:1-7, 17-19) Ingawa Yehova alimruhusu Shetani afikie makao ya kimbingu kwa kipindi fulani baada ya tukio hilo, kitabu cha Biblia cha Ufunuo kilitabiri kwamba wakati wa Mungu uwadiapo, mwovu huyo angetupwa chini hadi ujirani wa dunia. Uthibitisho waonyesha kwamba hilo lilitendeka muda mfupi baada ya Yesu Kristo kupokea mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914. Hatimaye, Ibilisi na roho zake waovu wataingia katika uharibifu udumuo milele. Suala la enzi kuu likiwa limesuluhishwa hatimaye, ndipo hesabu ya uasi itakapokuwa imetozwa kwa haki.—Ayubu 1:6-12; 2:1-7; Ufunuo 12:7-9; 20:10.

      Mwana wa Mungu Ana Wajibu wa Kutoa Hesabu

      6. Yesu huonaje wajibu wake mwenyewe wa kutoa hesabu kwa Baba yake?

      6 Ni kielelezo chema kama nini ambacho kimewekwa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo! Akiwa binadamu mkamilifu aliyekuwa sawa na Adamu, Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya kimungu. Aliterema pia kutozwa hesabu kwa ajili ya kufuata sheria ya Yehova. Kumhusu yeye, mtunga-zaburi alitoa unabii huu kwa kufaa: “Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.”—Zaburi 40:8; Waebrania 10:6-9.

      7. Alipokuwa akisali katika siku ya kuamkia kifo chake, kwa nini Yesu aliweza kusema maneno yaliyorekodiwa kwenye Yohana 17:4, 5?

      7 Ujapokuwa upinzani wenye chuki ambao Yesu alipatwa nao, alifanya mapenzi ya Mungu na alidumisha uaminifu-maadili hadi kifo kwenye mti wa mateso. Kwa njia hiyo alilipa bei ya fidia ili kuwakomboa wanadamu kutoka katika matokeo yenye kufisha ya dhambi ya Adamu. (Mathayo 20:28) Kwa sababu hiyo, katika siku ya kuamkia kifo chake, Yesu aliweza kusali hivi kwa uhakika: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye. Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:4, 5) Yesu aliweza kumwambia Baba yake wa kimbingu maneno hayo kwa sababu alikuwa akiupita kwa mafanikio ule mtihani wa kutoa hesabu na alikubalika kwa Mungu.

      8. (a) Paulo alionyeshaje kwamba ni lazima tutoe hesabu kwa Yehova Mungu kujihusu wenyewe? (b) Ni nini kitakachotusaidia kupata kukubaliwa na Mungu?

      8 Tofauti na yule mtu mkamilifu Yesu Kristo, sisi si wakamilifu. Hata hivyo, tuna wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu. Mtume Paulo alisema hivi: “Lakini kwa nini wewe wahukumu ndugu yako? Au kwa nini wewe pia wadharau ndugu yako? Kwa maana sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu; kwa maana imeandikwa: “‘Kama niishivyo,’ asema Yehova, ‘kwangu kila goti litakunjwa, na kila ulimi utakiri waziwazi kwa Mungu.’” Hivyo, basi kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Warumi 14:10-12, NW) Ili tuweze kufanya hivyo na kupata kukubaliwa na Yehova, ametupatia kwa upendo, dhamiri na pia Neno lake lililopuliziwa, Biblia, kutuongoza katika yale tusemayo na tufanyayo. (Warumi 2:14, 15; 2 Timotheo 3:16, 17) Kutumia kwa faida kamili maandalizi ya Yehova ya kiroho na kufuata dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia kutatusaidia kupata kukubaliwa na Mungu. (Mathayo 24:45-47) Roho takatifu, au kani ya utendaji ya Yehova, ni chanzo cha ziada cha kupata nguvu na mwongozo. Tukitenda kwa kupatana na mwelekezo wa roho na miongozo ya dhamiri yetu iliyozoezwa kwa Biblia, twaonyesha kwamba ‘hatumkatai Mungu,’ ambaye ni lazima tutoe hesabu kwake kwa ajili ya vitendo vyetu vyote.—1 Wathesalonike 4:3-8; 1 Petro 3:16, 21.

      Wenye Wajibu wa Kutoa Hesabu Wakiwa Mataifa

      9. Waedomu walikuwa nani, na ni jambo gani lililowapata kwa sababu ya jinsi walivyotenda kuelekea Israeli?

      9 Yehova huyapasisha mataifa kutoa hesabu. (Yeremia 25:12-14; Sefania 3:6, 7) Fikiria ufalme wa kale wa Edomu, uliokuwa kusini mwa Bahari Iliyokufa na kaskazini ya Ghuba ya Akaba. Waedomu walikuwa Wasemiti, wenye ukoo wa karibu sana na Waisraeli. Ingawa babu wa kale wa Waedomu alikuwa Esau, mjukuu wa Abrahamu, Waisraeli hawakuruhusiwa kusafiri kupitia Edomu katika “njia kuu ya mfalme” walipokuwa njiani kwenda Bara Lililoahidiwa. (Hesabu 20:14-21) Karne zilipopita uhasama wa Edomu uliongezeka ukawa chuki isiyo na huruma kwa Israeli. Hatimaye, Waedomu walilazimika kutoa hesabu kwa ajili ya kusihi kwao Wababiloni sana waharibu Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. (Zaburi 137:7) Katika karne ya sita K.W.K., vikosi vya Babiloni chini ya uongozi wa Mfalme Nabonido vilishinda Edomu, nao ukawa ukiwa, sawa na alivyoamuru Yehova.—Yeremia 49:20; Obadia 9-11.

      10. Wamoabi walitendaje kuelekea Waisraeli, na Mungu aliupasishaje Moabu kutoa hesabu?

      10 Moabu ulipatwa na tokeo lilo hilo. Ufalme wa Moabu ulikuwa kaskazini ya Edomu na mashariki ya Bahari Iliyokufa. Kabla ya Waisraeli kuingia Bara Lililoahidiwa, Wamoabi hawakuwatendea kwa ukaribishaji-wageni, ikiwa dhahiri kwamba walikuwa wakiwapa mkate na maji ili tu kufaidika kifedha. (Kumbukumbu la Torati 23:3, 4) Mfalme Balaki wa Moabu alimwajiri nabii Balaamu awalaani Waisraeli, na wanawake Wamoabi walitumiwa ili kuwavuta wanaume Waisraeli katika ukosefu wa adili na ibada ya sanamu. (Hesabu 22:2-8; 25:1-9) Hata hivyo, Yehova hakupuuza chuki ya Moabu kwa Israeli. Kama ilivyotolewa unabii, Moabu ulipatwa na uharibifu mikononi mwa Wababiloni. (Yeremia 9:25, 26; Sefania 2:8-11) Ndiyo, Mungu aliupasisha Moabu kutoa hesabu.

      11. Moabu na Amoni zilipata kuwa kama majiji gani, na unabii mbalimbali wa Biblia huonyesha nini kuhusu mfumo mwovu wa mambo uliopo?

      11 Si Moabu tu bali Amoni pia ililazimika kutoa hesabu kwa Mungu. Yehova alikuwa ametabiri hivi: “Hakika Moabu atakuwa kama Sodoma, na wana wa Amoni kama Gomora, yaani, milki ya upupu, na mashimo ya chumvi, ukiwa wa daima.” (Sefania 2:9) Nchi za Moabu na Amoni ziliangamizwa, sawa na vile Mungu alikuwa ameharibu majiji ya Sodoma na Gomora. Kulingana na Shirika la Kijiolojia la London, watafiti hudai kwamba wamepata mahali pa magofu ya Sodoma na Gomora katika pwani ya mashariki ya Bahari Iliyokufa. Uthibitisho wowote wenye kutegemeka ambao huenda ukavumbuliwa kwa habari hii waweza tu kuunga mkono unabii mbalimbali wa Biblia unaoonyesha kwamba Yehova Mungu ataupasisha mfumo mwovu wa mambo uliopo kutoa hesabu.—2 Petro 3:6-12.

      12. Ingawa Israeli lililazimika kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya dhambi zalo, ni jambo gani lililokuwa limetabiriwa kuhusu mabaki ya Wayahudi?

      12 Ingawa Israeli lilikuwa limependelewa sana na Yehova, lililazimika kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya dhambi zalo. Yesu Kristo alipolijia taifa la Israeli, walio wengi walimkataa. Ni mabaki tu yaliyodhihirisha imani yakawa wafuasi wake. Paulo alitumia unabii fulani-fulani kuhusu mabaki hayo ya Wayahudi alipoandika hivi: “Isaya naye atoa sauti yake juu ya Israeli, kusema, Hesabu ya wana wa Israeli, ijapokuwa ni kama mchanga wa bahari, ni mabaki yao tu watakaookolewa. Kwa maana Bwana atalitekeleza neno lake [“atafanyiza kutoa hesabu,” NW] juu ya nchi, akilimaliza na kulikata. Tena kama Isaya alivyotangulia kunena, Kama Bwana wa majeshi asingalituachia uzao, tungalikuwa kama Sodoma, tungalifananishwa na Gomora.” (Warumi 9:27-29; Isaya 1:9; 10:22, 23) Mtume alitaja kielelezo cha wale 7,000 wakati wa Eliya ambao hawakuwa wameinamia Baali, kisha akasema: “Basi ni vivi hivi wakati huu wa sasa, yako mabaki waliochaguliwa kwa neema.” (Warumi 11:5) Mabaki yalitia ndani watu mmoja-mmoja waliokuwa na wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu.

      Vielelezo vya Wajibu wa Kibinafsi wa Kutoa Hesabu

      13. Ni jambo gani lililompata Kaini wakati Mungu alipompasisha kutoa hesabu kwa ajili ya kumuua kimakusudi ndugu yake Abeli?

      13 Biblia hutaja visa vingi vya watu waliokuwa na wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Yehova Mungu. Fikiria kielelezo cha Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu. Yeye na pia ndugu yake Abeli walimtolea Yehova dhabihu. Dhabihu ya Abeli ilikubalika kwa Mungu, lakini ya Kaini haikukubalika. Alipopasishwa kutoa hesabu kwa ajili ya kumuua kimakusudi ndugu yake, Kaini alimwambia Mungu hivi bila kuona huruma: “Mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” Kwa sababu ya dhambi yake, Kaini alifukuziwa mbali hadi “nchi ya Nodi mbele ya Edeni.” Hakuonyesha toba yoyote yenye weupe wa moyo kwa ajili ya uhalifu wake, akijutia tu adhabu yake aliyostahili.—Mwanzo 4:3-16.

      14. Wajibu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu ulitolewaje kielezi katika kisa cha kuhani wa cheo cha juu Eli na wana wake?

      14 Wajibu wa mtu wa kibinafsi wa kutoa hesabu kwa Mungu unaonyeshwa pia katika kisa cha kuhani wa cheo cha juu wa Israeli Eli. Wana wake, Hofni na Finehasi, walitumikia wakiwa makuhani rasmi lakini “walikuwa na hatia ya udhalimu kuelekea watu, na ya ukosefu wa heshima kuelekea Mungu, na hawakuepuka namna yoyote ya uovu,” asema mwanahistoria Yosefo. “Watu [hao] wasiofaa kitu” hawakumkiri Yehova, walishiriki katika mwenendo wa kukufuru, na walikuwa na hatia ya ukosefu mzito wa adili. (1 Samweli 1:3; 2:12-17, 22-25) Eli, akiwa baba yao na kuhani wa cheo cha juu wa Israeli, alikuwa na wajibu wa kuwatia nidhamu, lakini aliwakaripia kwa upole tu. Eli ‘aliendelea kuwaheshimu wana wake kuliko [“Yehova,” NW].’ (1 Samweli 2:29) Kisasi kikaja juu ya nyumba ya Eli. Wana wote wawili walikufa siku ileile ambayo baba yao alikufa, na nasaba yao ya ukuhani ilikomeshwa kabisa hatimaye. Kwa njia hiyo, ile hesabu ilitozwa.—1 Samweli 3:13, 14; 4:11, 17, 18.

      15. Kwa nini Yonathani mwana wa Mfalme Sauli alithawabishwa?

      15 Kielelezo kilicho tofauti kabisa kiliwekwa na Yonathani mwana wa Mfalme Sauli. Punde si punde baada ya Daudi kumuua Goliathi, “roho ya Yonathani ikaambatana na roho ya Daudi,” nao wakafanya agano la urafiki. (1 Samweli 18:1, 3) Yamkini, Yonathani alitambua kwamba roho ya Mungu ilikuwa imemwacha Sauli, lakini bidii yake mwenyewe kwa ajili ya ibada ya kweli iliendelea bila kupunguka. (1 Samweli 16:14) Uthamini wa Yonathani kwa mamlaka ya Daudi aliyopewa na Mungu haukupunguka kamwe. Yonathani aling’amua wajibu wake wa kutoa hesabu kwa Mungu, na Yehova alimthawabisha kwa sababu ya mwenendo wake wenye kuheshimika kwa kuhakikisha kwamba nasaba ya familia yake iliendelea kwa vizazi kadhaa.—1 Mambo ya Nyakati 8:33-40.

      Wajibu wa Kutoa Hesabu Katika Kutaniko la Kikristo

      16. Tito alikuwa nani, na kwa nini yaweza kusemwa kwamba alitoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe?

      16 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo husema vema juu ya wanaume na wanawake wengi waliotoa hesabu njema kuhusu wao wenyewe. Mathalani, kulikuwa na yule Mkristo Mgiriki aliyeitwa Tito. Imedokezwa kwamba alikuwa Mkristo wakati wa safari ya kwanza ya mishonari ya Paulo hadi Kipro. Kwa kuwa Wayahudi na wageuzwa-imani kutoka Kipro huenda wakawa walikuwa Yerusalemu wakati wa Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., huenda ikawa Ukristo ulifikia hicho kisiwa upesi baada ya tukio hilo. (Matendo 11:19) Hata hivyo, Tito alithibitika kuwa mmoja wa wafanyakazi wenzi waaminifu wa Paulo. Aliandamana na Paulo na Barnaba katika safari ya kwenda Yerusalemu karibu na mwaka wa 49 W.K., suala la tohara liliposuluhishwa. Jambo la kwamba Tito hakuwa ametahiriwa liliongezea umaana hoja ya Paulo ya kwamba wageuzwa-imani Wakristo hawapaswi kuwa chini ya Sheria ya Kimusa. (Wagalatia 2:1-3) Huduma nzuri ya Tito inashuhudiwa katika Maandiko, na hata Paulo alimwandikia barua yenye kupuliziwa kimungu. (2 Wakorintho 7:6; Tito 1:1-4) Ni wazi kwamba kufikia mwisho kabisa wa mwendo wake wa kidunia, Tito aliendelea kutoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe.

      17. Timotheo alitoa hesabu gani, na kielelezo hicho chaweza kutuathirije?

      17 Timotheo alikuwa mtu mwingine mwenye bidii aliyetoa hesabu yenye kukubalika kwa Yehova Mungu kujihusu mwenyewe. Ingawa Timotheo alikuwa na matatizo fulani ya afya, alionyesha ‘imani isiyo na unafiki’ na ‘alitumikia pamoja na Paulo kwa ajili ya habari njema.’ Kwa hiyo mtume aliweza kuwaambia Wakristo wenzake katika Filipi: ‘Sina mtu mwingine ambaye kama Timotheo, anawashughulikieni kwa moyo.’ (2 Timotheo 1:5; Wafilipi 2:20, 22; 1 Timotheo 5:23, Habari Njema kwa Watu Wote) Tukabilipo udhaifu mbalimbali wa kibinadamu na majaribu mengine, sisi pia twaweza kuwa na imani isiyo na unafiki na twaweza kutoa hesabu yenye kukubalika kwa Mungu kuhusu wao wenyewe.

      18. Lidia alikuwa nani, naye alionyesha roho gani?

      18 Lidia alikuwa mwanamke mwenye kumwogopa Mungu ambaye kwa wazi alitoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe. Yeye na watu wa nyumbani mwake walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kukubali Ukristo katika Ulaya kwa sababu ya utendaji wa Paulo katika Filipi yapata mwaka wa 50 W.K. Akiwa mwenyeji wa Thiatira, labda Lidia alikuwa mgeuzwa-imani wa Dini ya Kiyahudi, lakini huenda ikawa kulikuwa na Wayahudi wachache na hakukuwa na sinagogi katika Filipi. Yeye na wanawake wengine wachaji walikuwa wakikutana kando ya mto, Paulo aliposema nao. Likiwa tokeo, Lidia akawa Mkristo na aliwashurutisha Paulo na washiriki wake wakae naye. (Matendo 16:12-15) Ukaribishaji-wageni ambao Lidia alionyesha ungali sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli.

      19. Dorkasi alitoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu mwenyewe kwa matendo gani mema?

      19 Dorkasi alikuwa mwanamke mwingine aliyetoa hesabu nzuri kwa Yehova Mungu kujihusu mwenyewe. Alipokufa, Petro alienda Yafa kwa kuitikia ombi kutoka kwa wanafunzi waliokuwa wakiishi huko. Wale wanaume wawili waliokutana na Petro “wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao.” Dorkasi alirudishwa kwenye uhai. Lakini je, yeye akumbukwe kwa sababu tu ya ukarimu wake wenye upendo? La. Alikuwa “mwanafunzi” na kwa hakika yeye mwenyewe alishiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Leo vilevile wanawake Wakristo ‘wanajaa matendo mema na sadaka.’ Wanafurahia pia kushiriki kwa bidii katika kupiga mbiu ya habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi.—Matendo 9:36-42; Mathayo 24:14; 28:19, 20.

      20. Ni maswali gani ambayo twaweza kujiuliza?

      20 Biblia huonyesha kwa wazi kwamba ni lazima mataifa na watu mmoja-mmoja watoe hesabu kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Jehovah. (Sefania 1:7) Ikiwa tumejiweka wakfu kwa Mungu, twaweza basi kujiuliza, ‘Mimi huonaje mapendeleo na madaraka niliyopewa na Mungu? Ninatoa hesabu ya aina gani kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo kujihusu mwenyewe?’

  • Yehova na Apendezwe na Hesabu Yako
    Mnara wa Mlinzi—1996 | Septemba 15
    • Yehova na Apendezwe na Hesabu Yako

      “Hili . . . ulikumbuke kwenye hesabu yangu, Ee Mungu wangu . . . Unikumbuke, Ee Mungu wangu, kwa ajili ya mema.”—NEHEMIA 13:22, 31, NW.

      1. Ni jambo gani ambalo huwasaidia wale waliojiweka wakfu kwa Mungu kutoa hesabu nzuri kwa Yehova?

      WATUMISHI wa Yehova wana msaada wote unaohitajiwa ili kutoa hesabu nzuri kwake. Kwa nini? Kwa sababu wana uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wakiwa sehemu ya tengenezo lake la kidunia. Amewafunulia makusudi yake, na amewapa msaada na ufahamu wa kiroho wenye kina kupitia roho yake takatifu. (Zaburi 51:11; 119:105; 1 Wakorintho 2:10-13) Kwa kufikiria hali hizo za pekee, Yehova, kwa upendo, huwapasisha watumishi wake wa kidunia kutoa hesabu kwake kuhusu wao wenyewe kwa jinsi walivyo na kwa mambo wanayotimiza katika nguvu zake na kwa msaada wa roho yake takatifu.

      2. (a) Nehemia alitoa hesabu njema kwa Mungu kujihusu mwenyewe katika njia zipi? (b) Nehemia alimalizia kitabu cha Biblia chenye jina lake kwa ombi jipi?

      2 Mtu mmoja aliyetoa hesabu njema kwa Mungu kujihusu mwenyewe, alikuwa Nehemia, mnyweshaji wa Mfalme wa Uajemi Artashasta (Longimano). (Nehemia 2:1) Nehemia alipata kuwa gavana wa Wayahudi, akajenga upya ukuta wa Yerusalemu akikabili maadui na hatari mbalimbali. Akiwa na bidii kwa ajili ya ibada ya kweli, alitekeleza Sheria ya Mungu na kuwaonyesha ufikirio wale walioonewa. (Nehemia 5:14-19) Nehemia aliwasihi sana Walawi wajisafishe kwa ukawaida, walinde malango, na kutakasa siku ya Sabato. Kwa hiyo aliweza kusali hivi: “Hili, nalo, ulikumbuke kwenye hesabu yangu, Ee Mungu wangu, na unisikitikie kulingana na wingi wa fadhili-upendo zako.” Pia, kwa kufaa, Nehemia alimalizia hivi, kitabu chake kilichopuliziwa kimungu: “Unikumbuke, Ee Mungu wangu, kwa ajili ya mema.”—Nehemia 13:22, 31, NW.

      3. (a) Ungemfafanuaje mtu anayefanya mema? (b) Kufikiria mwendo wa Nehemia huenda kukatufanya tujiulize maswali yapi?

      3 Mtu afanyaye mema ni mwenye wema wa adili na hufanya vitendo vya unyoofu vinavyonufaisha wengine. Nehemia alikuwa mtu wa aina hiyo. Alikuwa na hofu yenye staha kwa Mungu na bidii nyingi kwa ajili ya ibada ya kweli. Zaidi ya hayo, alikuwa mwenye shukrani kwa ajili ya mapendeleo yake katika utumishi wa Mungu na alitoa hesabu nzuri kwa Yehova kujihusu mwenyewe. Kufikiria mwendo wake huenda kutatufanya tujiulize, ‘Mimi huyaonaje mapendeleo na madaraka niliyopewa na Mungu? Ninatoa hesabu ya aina gani kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo kujihusu mwenyewe?’

      Ujuzi Hutufanya Tuwe na Wajibu wa Kutoa Hesabu

      4. Yesu aliwapa wafuasi wake utume gani, na wale wenye “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” walipaswa kufanya nini?

      4 Yesu aliwapa wafuasi wake utume huu: “Enendeni . . . mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Wanafunzi wangefanywa kwa kuwafundisha. Wale ambao wangefundishwa kwa njia hiyo na waliokuwa “na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” wangebatizwa, sawa na alivyobatizwa Yesu. (Matendo 13:48; Marko 1:9-11, linganisha NW.) Kutamani kwao kushika mambo yote aliyokuwa ameamuru kungetoka moyoni. Wangefikia hatua ya wakfu kwa kuendelea kutwaa na kutumia ujuzi sahihi juu ya Neno la Mungu.—Yohana 17:3.

      5, 6. Tueleweje Yakobo 4:17? Toa kielezi cha matumizi yalo.

      5 Kadiri ujuzi wetu wa Kimaandiko ulivyo wenye kina zaidi, ndivyo msingi wa imani yetu unavyokuwa bora zaidi. Wakati uo huo, wajibu wetu wa kutoa hesabu kwa Mungu unakuwa mkubwa zaidi. Yakobo 4:17 husema hivi: “Ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi.” Taarifa hiyo yaonekana kuwa mkataa wa yale mwanafunzi Yakobo aliyokuwa ametoka tu kusema juu ya kujivuna badala ya kumtegemea Mungu kikamili. Mtu akijua kwamba hawezi kutimiza jambo lolote lile lenye kudumu bila msaada wa Yehova lakini hatendi kulingana na ujuzi huo, hiyo ni dhambi. Lakini maneno ya Yakobo yaweza pia kutumiwa kuhusu dhambi ya kutokufanya yanayopasa kufanywa. Mathalani, katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, mbuzi wanalaumiwa, si kwa sababu ya matendo mabaya, bali ni kwa sababu ya kutowasaidia ndugu za Kristo.—Mathayo 25:41-46.

      6 Mwanamume mmoja ambaye Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiongoza funzo la Biblia pamoja naye alikuwa akifanya maendeleo machache ya kiroho, yaonekana ni kwa sababu hakuacha kuvuta sigareti, ingawa alijua kwamba alipaswa kufanya hivyo. Mzee mmoja akamwomba asome Yakobo 4:17. Baada ya kueleza juu ya umaana wa andiko hilo, huyo mzee akasema hivi: “Ingawa hujabatizwa, una wajibu wa kutoa hesabu na ni lazima uchukue daraka kamili kwa ajili ya uamuzi wako.” Kwa furaha, mtu huyo aliitikia, akaacha kuvuta sigareti, na upesi akastahili kubatizwa kwa ufananisho wa kujiweka kwake wakfu kwa Yehova Mungu.

      Wenye Wajibu wa Kutoa Hesabu kwa Ajili ya Huduma Yetu

      7. Ni ipi njia moja ya kuonyesha shukrani yetu kwa ajili ya “ujuzi wenyewe juu ya Mungu”?

      7 Tamaa yetu ya kuhisiwa moyoni yapaswa kuwa kumpendeza Muumba wetu. Njia moja ya kuonyesha shukrani yetu kwa ajili ya “ujuzi wenyewe juu ya Mungu” ni kutimiza utume wa kufanya wanafunzi wa Mwana wake, Yesu Kristo. Hiyo ni njia pia ya kuonyesha kumpenda kwetu Mungu na jirani. (Mithali 2:1-5; Mathayo 22:35-40) Ndiyo, ujuzi wetu juu ya Mungu hutufanya tuwe na wajibu wa kutoa hesabu kwake, na twahitaji kuwaona wanadamu wenzetu kuwa watu wawezao kuwa wanafunzi.

      8. Kwa nini twaweza kusema kwamba Paulo alihisi ana wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya huduma yake?

      8 Mtume Paulo alijua kwamba kuikubali kwa moyo wote habari njema na kuitii hutokeza wokovu, hali kuikataa kwaweza kuleta uharibifu. (2 Wathesalonike 1:6-8) Kwa hiyo alihisi ana wajibu wa kutoa hesabu kwa Yehova kwa ajili ya huduma yake. Kwa kweli, Paulo na washiriki wake waliithamini huduma yao sana hivi kwamba waliepuka kwa uangalifu hata kuonyesha watu wazo la kwamba walikuwa wakipata faida ya kifedha kutokana nayo. Zaidi ya hayo, moyo wa Paulo ulimsukuma aseme hivi: “Ijapokuwa naihubiri Injili [“habari njema,” NW], sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!”—1 Wakorintho 9:11-16.

      9. Wakristo wote wana deni gani la maana la kulipa?

      9 Kwa kuwa sisi ni watumishi wa Yehova tuliojiweka wakfu, ‘tumewekewa sharti kuihubiri injili.’ Utume wetu ni kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Tulikubali daraka hilo tulipojiweka wakfu kwa Mungu. (Linganisha Luka 9:23, 24.) Zaidi ya hayo, tuna deni la kulipa. Paulo alisema hivi: “Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani, nawiwa na wenye hekima na wasio na hekima. Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi.” (Warumi 1:14, 15) Paulo alikuwa mdeni kwa sababu alijua kwamba alikuwa na wajibu wa kuhubiri ili watu waweze kusikia habari njema na kuokolewa. (1 Timotheo 1:12-16; 2:3, 4) Kwa hiyo alijitahidi sana kutimiza utume wake na kulipa deni lake kwa wanadamu wenzake. Tukiwa Wakristo, sisi pia tuna deni la jinsi hiyo la kulipa. Kuhubiri Ufalme ni njia kuu pia ya kuonyesha upendo kwa Mungu, kwa Mwana wake, na kwa majirani wetu.—Luka 10:25-28.

      10. Watu fulani wamepanua huduma yao kwa kufanya nini?

      10 Njia moja ya kutoa hesabu yenye kukubalika kwa Mungu ni kutumia uwezo wetu mbalimbali kupanua huduma yetu. Ili kutoa kielezi: Miaka ya juzijuzi kumekuwa na ongezeko katika Uingereza la watu wa kutoka vikundi vingi vya kitaifa. Ili kuwafikia watu hao na habari njema, mapainia (wahubiri wa Ufalme wa wakati wote) zaidi ya 800 na mamia ya Mashahidi wengine wanajifunza lugha tofauti-tofauti. Hilo limetokeza kichocheo kizuri kwa huduma. Painia mmoja anayefundisha Kichina alisema hivi: “Sikufikiri kamwe kwamba ningepata wakati wowote kuwafundisha Mashahidi wengine lugha yangu, ili waweze kushiriki kweli pamoja na wengine katika njia hii. Inaridhisha sana!” Je, ungeweza kuupanua utumishi wako katika njia kama hiyo?

      11. Tokeo lilikuwa nini Mkristo mmoja alipotoa ushahidi kivivihivi?

      11 Yamkini, kila mmoja wetu angefanya lolote lile awezalo kufanya ili kumwokoa mtu anayekufa maji. Vivyo hivyo, watumishi wa Yehova wana hamu ya kutumia uwezo wao mbalimbali ili kutoa ushahidi kwenye kila fursa. Majuzi Shahidi mmoja aliketi karibu na mwanamke fulani katika basi na akaongea naye kuhusu Maandiko. Kwa sababu ya kusisimuliwa na yale aliyoyasikia, huyo mwanamke aliuliza maswali mengi. Shahidi alipokuwa karibu kushuka katika basi, yule mwanamke alimsihi aje nyumbani kwake badala ya kushuka, kwa kuwa alikuwa na maswali mengi bado. Shahidi akakubali. Tokeo likawa nini? Funzo la Biblia lilianzishwa, na miezi sita baadaye huyo mwanamke akawa mtangazaji wa Ufalme asiyebatizwa. Upesi alikuwa akiongoza mafunzo yake mwenyewe sita, ya Biblia nyumbani. Ilikuwa thawabu iliyoje kwa sababu ya kutumia uwezo mbalimbali katika utumishi wa Ufalme!

      12. Uwezo wetu mbalimbali tukiwa wahudumu waweza kutumiwaje kwa matokeo katika utumishi wa shambani?

      12 Uwezo wetu mbalimbali tukiwa wahudumu waweza kutumiwa kwa matokeo shambani kwa kutumia vichapo kama kile kitabu chenye kurasa 192 kiitwacho Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kufikia Aprili 1996, Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova ilikuwa imekubali utangazaji wa kitabu Ujuzi katika lugha zaidi ya 140, na kufikia wakati huo nakala zacho 30,500,000 zilikuwa zimechapwa tayari katika lugha 111. Kitabu hicho kiliandikwa na lengo la kusaidia wanafunzi wa Biblia wajifunze vya kutosha kuhusu Neno na makusudi ya Mungu ili waweze kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Kwa kuwa watangazaji wa Ufalme hawatakuwa wakiongoza funzo la Biblia nyumbani pamoja na mwanafunzi yuleyule kwa miaka mingi, wanaweza kuongoza mafunzo pamoja na watu wengi zaidi au kuongeza kushiriki kwao katika kazi ya kuhubiri nyumba hadi nyumba na namna nyinginezo za huduma. (Matendo 5:42; 20:20, 21) Kwa sababu ya kufahamu wajibu wao wa kutoa hesabu kwa Mungu, wao huelekeza uangalifu kwenye maonyo ya kimungu. (Ezekieli 33:7-9) Lakini kusudi lao kuu ni kumheshimu Yehova na kusaidia wengi iwezekanavyo wajifunze juu ya habari njema katika ule wakati mfupi unaobaki bado wa mfumo huu mwovu wa mambo.

      Kutoa Hesabu Nzuri Tukiwa Familia

      13. Kwa nini familia zinazomwogopa Mungu ziwe na funzo la Biblia la familia la kawaida?

      13 Kila mtu mmoja-mmoja na familia anayekubali Ukristo wa kweli ana wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu na kwa hiyo apaswa “kukaza mwendo [“mbele kwenye ukomavu,” NW]” na kuwa ‘thabiti katika imani.’ (Waebrania 6:1-3; 1 Petro 5:8, 9) Kwa kielelezo, wale ambao wamejifunza kitabu Ujuzi na wamebatizwa wanahitaji kukamilisha ujuzi wao wa Kimaandiko kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na pia kwa kusoma Biblia na vichapo vingine vya Kikristo. Familia zinazomwogopa Mungu zapaswa pia kuwa na funzo la familia la kawaida, kwa maana hiyo ni njia ya maana ya ‘kukesha, kusimama imara katika imani, kufanya kiume, kuwa hodari.’ (1 Wakorintho 16:13) Ikiwa wewe ni kichwa cha nyumba, una wajibu hasa kwa Mungu kuhakikisha kwamba familia yako inalishwa vizuri kiroho. Sawa na vile chakula cha kimwili chenye lishe kinavyochangia afya ya asili, ndivyo chakula cha kiroho kilicho kingi na cha ukawaida kinavyohitajiwa ikiwa wewe na familia yako mtaendelea kuwa “wazima katika imani.”—Tito 1:13.

      14. Ushahidi uliotolewa na msichana Mwisraeli aliyefundishwa vizuri ulikuwa na tokeo jipi?

      14 Ikiwa kuna watoto katika nyumba yako, Mungu atapendezwa na hesabu yako ukiwapa maagizo timamu ya kiroho. Kufundisha huko kutawanufaisha, sawa na vile kulivyomnufaisha msichana mdogo Mwisraeli aliyetekwa na Wasiria katika siku za nabii wa Mungu, Elisha. Alikuwa kijakazi wa mke wa Naamani, mkuu wa jeshi la Siria, aliyekuwa na ukoma. Ingawa msichana huyo alikuwa mchanga, alimwambia bibi-mwenyeji wake hivi: “Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! maana angemponya ukoma wake.” Kwa sababu ya ushuhuda wake, Naamani alienda Israeli, akautii hatimaye mwelekezo wa Elisha wa kuoga mara saba katika Mto Yordani, na akasafishwa ukoma. Zaidi ya hayo, Naamani akawa mwabudu wa Yehova. Hilo bila shaka lilimsisimua kama nini yule msichana mdogo!—2 Wafalme 5:1-3, 13-19.

      15. Kwa nini ni jambo la maana kwa wazazi kuwapa watoto wao mazoezi mazuri ya kiroho? Toa kielezi.

      15 Si rahisi kuwalea watoto wenye kumhofu Mungu katika ulimwengu huu usio na adili unaokaa katika nguvu ya Shetani. (1 Yohana 5:19) Hata hivyo, tangu utoto wa Timotheo, nyanya yake Loisi, na mama yake Eunike, walimfundisha Maandiko kwa mafanikio. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Kujifunza Biblia pamoja na watoto wako, kwenda pamoja nao kwenye mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na hatimaye kuandamana nao katika huduma, yote hayo ni sehemu ya kigezo cha mazoezi ambacho ni lazima utoe hesabu kwa Mungu juu yacho. Mkristo mmoja katika Wales, ambaye sasa yumo katika miaka yake ya 80, akumbuka kwamba katika miaka ya mapema ya 1920, baba yake alienda pamoja naye alipotembea kilometa 10 juu ya mlima (safari ya kwenda na kurudi ya kilometa 20) ili kugawanya trakti za Biblia kwa wana-kijiji katika bonde la karibu. “Baba yangu aliikaza kweli kikiki moyoni mwangu, katika matembezi hayo,” asema kwa shukrani.

      Wazee Hutoa Hesabu—Jinsi Gani?

      16, 17. (a) Wanaume wazee wenye ukomavu katika Israeli la kale walikuwa na mapendeleo yapi? (b) Kwa kulinganisha na hali katika Israeli la kale, kwa nini mengi zaidi yanatakwa kwa wazee Wakristo leo?

      16 “Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki,” akasema Sulemani mwenye hekima. (Mithali 16:31) Lakini si umri wa kimwili tu unaomtayarisha mtu kwa ajili ya daraka katika kutaniko la watu wa Mungu. Wanaume wazee wenye ukomavu kiroho katika Israeli la kale walitumikia wakiwa waamuzi na maofisa wa kusimamia haki na kudumisha amani, utaratibu mzuri, na afya ya kiroho. (Kumbukumbu la Torati 16:18-20) Ingawa ndivyo ilivyo kwa habari ya kutaniko la Kikristo, mengi zaidi yanatakwa kwa wazee kadiri mwisho wa mfumo huu wa mambo ukaribiavyo. Kwa nini?

      17 Waisraeli walikuwa ‘watu wachaguliwa’ waliokombolewa na Mungu kutoka Misri. Kwa kuwa waliipokea Sheria kupitia mpatanishi wao Musa, wazao wao walizaliwa katika taifa lililowekwa wakfu na walifahamu amri za Yehova. (Kumbukumbu la Torati 7:6, 11) Hata hivyo, leo hakuna mtu anayezaliwa katika taifa lililowekwa wakfu, na ni wachache kwa kulinganisha wanaokua katika familia zinazomwogopa Mungu zinazofahamu vizuri kweli ya Kimaandiko. Wale hasa ambao wameanza hivi majuzi ‘kwenda katika kweli’ huenda wakahitaji maagizo juu ya jinsi ya kuishi kulingana na kanuni za Kimaandiko. (3 Yohana 4) Wazee waaminifu wana daraka lililoje basi ‘washikapo kielelezo cha maneno yenye uzima’ na kuwasaidia watu wa Yehova!—2 Timotheo 1:13, 14.

      18. Ni lazima wazee wa kutaniko wawe tayari kutoa msaada wa aina gani, na kwa nini?

      18 Mtoto mchanga anayejifunza kutembea huenda akajikwaa na kuanguka. Hana usalama na anahitaji msaada na uhakikishio wa wazazi. Mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova anaweza vilevile kujikwaa au kuanguka kiroho. Hata mtume Paulo aliona ni lazima kushindana ili kufanya lililo sawa au jema machoni pa Mungu. (Warumi 7:21-25) Wachungaji wa kundi la Mungu wanahitaji kutoa msaada wenye upendo kwa Wakristo ambao wamekosea lakini ni wenye toba kikweli. Wazee walipomtembelea mwanamke mmoja aliyejiweka wakfu aliyekuwa amefanya kosa zito, alisema hivi mbele ya mume wake aliyejiweka wakfu: “Najua mtanitenga na ushirika!” Lakini alianza kulia machozi alipoambiwa kwamba wazee walitaka kujua ni msaada gani uliohitajiwa ili kuirudisha hali ya kiroho ya familia. Kwa sababu ya kufahamu kwamba ni lazima watoe hesabu, wazee walifurahi kusaidia mwamini mwenzao mwenye toba.—Waebrania 13:17.

      Endelea Kutoa Hesabu Nzuri

      19. Twaweza kuendeleaje kutoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu wenyewe?

      19 Wazee wa kutaniko na watumishi wa Mungu wengine wote wanahitaji kuendelea kutoa hesabu nzuri kwa Yehova kuhusu wao wenyewe. Hiyo yawezekana tukishikamana na Neno la Mungu na kufanya mapenzi yake. (Mithali 3:5, 6; Warumi 12:1, 2, 9) Twataka hasa kuwafanyia mema wale ambao katika imani ni jamaa zetu. (Wagalatia 6:10) Hata hivyo, mavuno yangali mengi, na wafanyakazi wangali wachache. (Mathayo 9:37, 38) Kwa hiyo na tuwafanyie wengine mema kwa kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme kwa bidii yenye kuendelea. Yehova atapendezwa na hesabu yetu tukitimiza wakfu wetu, tukifanya mapenzi yake, na kupiga mbiu ya habari njema kwa uaminifu.

      20. Twajifunza nini kutokana na kufikiria mwendo wa Nehemia?

      20 Kwa hiyo na tuendelee kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. (1 Wakorintho 15:58) Na twafanya vema kumfikiria Nehemia, aliyejenga upya ukuta wa Yerusalemu, akatekeleza Sheria ya Mungu, na kuendeleza kwa bidii ibada ya kweli. Alisali kwamba Yehova Mungu amkumbuke kwa ajili ya mema aliyokuwa amefanya. Na uthibitike kuwa mwenye kujitoa vivyo hivyo kwa Yehova, na apendezwe na hesabu yako.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki