Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuhifadhi Hadhi ya Mgonjwa
    Amkeni!—1998 | Septemba 22
    • Kuhifadhi Hadhi ya Mgonjwa

      SIKU mbili kabla ya Sally kumpeleka mume wake kumwona daktari wa ubongo, waziri mkuu mpya alichaguliwa nchini Afrika Kusini. Daktari huyo alipomwuliza Alfie kuhusu matokeo ya uchaguzi, Alfie alimtazama tu na kushindwa kujibu. Kisha, baada ya kumchunguza ubongo, daktari huyo akasema kwa njia isiyo ya fadhili: “Mtu huyu hata hawezi kujua jibu la mbili kuongezea mbili. Ubongo wake umekwisha!” Kisha akamshauri Sally: “Fanya mipango yako ya kifedha. Mtu huyu anaweza kukugeuka na kuwa mjeuri.”

      “Hawezi kamwe!” Sally akajibu, “mume wangu hawezi kufanya hivyo!” Sally alisema kweli; Alfie hakupata kuwa mjeuri kwake, hata ingawa baadhi ya watu ambao wana maradhi ya Alzheimer (AD) huwa wakali. (Mara nyingi hiyo hutukia kwa sababu ya mfadhaiko, ambao nyakati nyingine waweza kupunguzwa kwa kumshughulikia vizuri mgonjwa wa AD.) Ingawa huyo daktari alifaulu kugundua ugonjwa wa Alfie, kwa wazi yeye hakujua kwamba kuna uhitaji wa kuhifadhi hadhi ya mgonjwa. La sivyo, yeye angemweleza Sally kwa fadhili hali ya Alfie faraghani.

      “Uhitaji muhimu zaidi wa watu wenye kasoro za akili ni kuhifadhi hadhi yao, heshima na kujistahi,” chasema kitabu When I Grow Too Old to Dream. Njia muhimu ya kuhifadhi hadhi ya mgonjwa inaelezwa katika kijarida cha mashauri kiitwacho Communication, ambacho kimechapishwa na Shirika la Maradhi ya Alzheimer la London: “Usizungumze kamwe juu ya [wagonjwa wa AD] mbele ya watu wengine kana kwamba hawapo. Hata kama hawaelewi unayosema, wao waweza kuhisi kwamba wanapuuzwa kwa njia fulani na wahisi wameshushiwa hadhi.”

      Kuna uhakika kwamba baadhi ya wagonjwa wa AD huelewa mambo ambayo wengine husema juu yao. Kwa mfano, mgonjwa mmoja kutoka Australia alienda na mke wake kwenye mkutano mmoja wa shirika la kuwasaidia wagonjwa wa Alzheimer. Baadaye alisema hivi: “Walikuwa wakiwafundisha watunzaji mambo ya kufanya na jinsi wapaswavyo kuyafanya. Nilishtuka kwa sababu mimi nilikuwapo na hakuna mtu aliyezungumza juu ya mgonjwa. . . . Nilifadhaika sana. Eti kwa sababu nina Alzheimer, yale niyasemayo hayafai: hakuna mtu atakayesikiliza.”

      Uwe na Maoni Mazuri

      Kuna njia nyingi nzuri za kuwasaidia wagonjwa wahifadhi hadhi yao. Wao waweza kuhitaji msaada wa kuendelea na kazi zao za kila siku ambazo zamani zilikuwa rahisi. Kwa mfano, ikiwa zamani walikuwa wanapenda kuandika barua, basi labda unaweza kuketi nao na kuwasaidia kujibu barua kutoka kwa marafiki wenye kuwahangaikia. Katika kitabu Alzheimer’s—Caring for Your Loved One, Caring for Yourself, Sharon Fish ataja njia nyinginezo za kuwasaidia wagonjwa wa AD: “Tafuta mambo rahisi mnayoweza kufanya pamoja na ambayo ni yenye maana na yenye matokeo: kuosha na kukausha vyombo, kufagia, kukunja nguo na kupika.” Kisha aelezea hivi: “Mgonjwa wa Alzheimer huenda asiweze kusafisha nyumba nzima au kupika mlo wote, lakini polepole yeye hupoteza uwezo wa kufanya hayo. Unaweza kutumia uwezo ambao bado wanao na kuwasaidia kuutumia kwa muda mrefu iwezekanavyo. Ukifanya hivyo, pia unasaidia kuhifadhi kujistahi kwa mpendwa wako.”

      Baadhi ya kazi zinazofanywa na wagonjwa wa AD hazitakuwa bora, basi huenda ukahitajika kufagia tena au kuosha vyombo tena. Lakini, kwa kumfanya mgonjwa aone kwamba anatumika, unamwezesha aridhike maishani. Mpongeze hata kama hajafanya kazi nzuri. Kumbuka kwamba yeye amefanya kadiri awezavyo kwa sababu ya ugonjwa wake. Wagonjwa wa AD huhitaji kukumbushwa nyakati zote kwamba wanathaminiwa na kupongezwa—na hata zaidi wazidipo kudhoofika na kushindwa kutimiza utendaji mbalimbali. “Wakati wowote ule—bila kutarajiwa kabisa wanaweza kulemewa na hisia ya kujiona kuwa wao ni bure tu. Mtunzaji ahitaji kumtuliza mara moja kwa kumliwaza kwamba ‘anaendelea vizuri.’” Asema Kathy, ambaye mume wake mwenye umri wa miaka 84 ana AD. Kitabu Failure-Free Activities for the Alzheimer’s Patient chakubali: “Sisi sote tunahitaji kusikia kwamba tunafanya vizuri, na kwa watu wenye kasoro za akili, uhitaji huo ni wenye nguvu hata zaidi.”

      Jinsi ya Kushughulikia Tabia Zenye Kuaibisha

      Watunzaji wanapaswa kujifunza jinsi ya kushughulikia tabia zenye kuaibisha za mpendwa wao. Mojawapo ya hofu kubwa zaidi ni kwamba mgonjwa hatadhibiti haja mbele ya watu. “Vitendo hivyo havitukii kwa ukawaida navyo vyaweza kuzuiwa ama kupunguzwa. Pia mtu apaswa kufikiria mambo kihalisi, kwa kuwa si tendo lenyewe wala watu wanaotazama wapaswao kuwa hangaiko bali ni kupoteza hadhi kwa mtu mwenye AD.” Aeleza Dakt. Gerry Bennett katika kitabu chake Alzheimer’s Disease and Other Confusional States.

      Kisa kama hicho chenye kuaibisha kikitukia, usimzomee mgonjwa. Badala yake, jaribu kufuata shauri hili: “Tulia na uone mambo kihalisi na ukumbuke kwamba mtu huyo hafanyi hivyo kimakusudi. Isitoshe, wao huelekea zaidi kusikiliza ikiwa wewe ni mpole na mwenye udhibiti kuliko kama umekasirika na kukosa subira. Fanya yote uwezayo ili kufanya kisa hicho kisiharibu uhusiano wako na mgonjwa.”—kijarida cha mashauri cha Incontinence, cha Shirika la Maradhi ya Alzheimer ya London.

      Je, Kweli Wao Wanahitaji Kusahihishwa?

      Mara nyingi wagonjwa wa AD husema mambo yasiyo sahihi. Kwa mfano, wao waweza kusema kwamba wanatarajia ziara kutoka kwa mtu wa ukoo ambaye alikufa zamani. Au wao waweza kuota mambo, wakiona vitu ambavyo viko tu akilini mwao. Je, sikuzote inahitajika kumsahihisha mgonjwa wa AD kwa kukosea katika usemi?

      “Kuna wazazi ambao hawakomi kuwasahihisha watoto wao kila wakati wanapotamka neno vibaya au wanapokosea kisarufi. . . . Mara nyingi mtoto hukasirika au kujitenga kwa sababu anaona jitihada zake za kujieleza zinakandamizwa na hazithawabishwi. Ndivyo inavyotokea kwa mgonjwa wa AD ambaye hukosolewa daima.” Aelezea Robert T. Woods katika kitabu chake Alzheimer’s Disease—Coping With a Living Death. Kwa kupendeza, Biblia inashauri hivi juu ya jinsi ya kuwatendea watoto: “Nyinyi akina baba, msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo.” (Wakolosai 3:21) Ikiwa watoto huchokozeka kwa sababu ya kukosolewa daima, sembuse mtu mzima! “Kumbuka kwamba mgonjwa ni mtu mzima ambaye ana uhuru wake na matimizo yake,” ndivyo inavyotahadharisha ARDA Newsletter ya Afrika Kusini. Kukosoa-kosoa mgonjwa wa AD kunaweza kumkasirisha na vilevile kumfanya ashuke moyo au hata awe mkali.

      Tunaweza kupata somo kutokana na Yesu Kristo litakalosaidia wale wanaoshughulika na wagonjwa wa AD. Yeye hakuwa akisahihisha mara hiyo kila maoni yenye makosa ya mitume wake. Kwa hakika, nyakati nyingine yeye hakuwaambia mambo fulani kwa sababu bado hawangeweza kuyaelewa. (Yohana 16:12, 13) Ikiwa Yesu alifikiria mapungufu ya wanadamu wenye afya, sisi tunapaswa hata zaidi kupatana na maoni ya kiajabu-ajabu lakini ambayo hayadhuru ya mtu mzima ambaye ni mgonjwa sana! Kujaribu kumfanya mgonjwa aone ukweli wa jambo fulani hususa ni kutarajia—au kudai—zaidi ya mtu huyo awezavyo. Badala ya kubishana, mbona usinyamaze au ubadilishe mazungumzo kwa njia ya busara?—Wafilipi 4:5.

      Nyakati nyingine, jambo lenye upendo zaidi laonekana ni kukubaliana na maono ya mgonjwa badala ya kujaribu kumsadikisha kwamba hayo si ya kweli. Kwa mfano, mgonjwa wa AD aweza kufadhaishwa kwa sababu “anaona” mnyama mkali au mtu fulani nyuma ya pazia. Huo si wakati wa kujaribu kusababu naye kiakili. Kumbuka kwamba ‘anachoona’ akilini mwake ni kitu halisi kwake, na basi haifai hofu zake za kweli zipuuzwe. Huenda ukahitaji kuchunguza nyuma ya pazia na kusema, “‘Ukimwona’ tena, niambie ili nikusaidie.” Kwa kutenda kwa kupatana na maoni ya mgonjwa, waeleza Madaktari Oliver na Bock katika kitabu chao Coping With Alzheimer’s: A Caregiver’s Emotional Survival Guide, “unampa hisia ya kushinda vitu vyenye kutisha na kuhofisha ambavyo akili yake inafanyiza. . . . Anajua kwamba anaweza kukutegemea.”

      “Sisi Sote Hujikwaa Mara Nyingi”

      Inaweza kuwa jambo gumu kutumia madokezo hayo yote ambayo yametajwa, hasa kwa wale ambao wana mzigo mzito wa kazi na madaraka mengine ya familia. Pindi kwa pindi, mtunzaji mwenye kufadhaika aweza kukasirika na kushindwa kumtendea mgonjwa wa AD kwa hadhi. Hilo litukiapo, usijiruhusu kamwe ulemewe na hisia ya hatia. Kumbuka kwamba kwa sababu ya hali ya maradhi hayo, labda mgonjwa atasahau kisa hicho haraka sana.

      Pia mwandikaji wa Biblia Yakobo asema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2) Kwa kuwa hakuna mtunzaji wa kibinadamu aliye mkamilifu, mtunzaji aweza kufanya kosa anapofanya kazi hiyo ngumu ya kumtunza mgonjwa wa AD. Katika makala ifuatayo, tutafikiria mambo mengine ambayo yamewasaidia watunzaji wakabiliane na hali ya kumtunza mgonjwa wa AD na hata kufurahia kumtunza.

  • Kuhifadhi Hadhi ya Mgonjwa
    Amkeni!—1998 | Septemba 22
    • Je, Umwambie Mgonjwa?

      WATUNZAJI wengi hujiuliza kama wanapaswa kumwambia mpendwa wao kwamba ana maradhi ya Alzheimer (AD). Ukiamua kumwambia, basi utamwambiaje na wakati gani? Kijarida fulani cha habari cha Shirika la Alzheimer na Matatizo Yanayohusika Nayo cha Afrika Kusini kilikuwa na maelezo haya yenye kupendeza kutoka kwa msomaji mmoja:

      “Mume wangu ameugua Alzheimer kwa miaka saba hivi. Sasa ana umri wa miaka 81, na kwa uzuri hadhoofiki haraka . . . Kwa muda mrefu niliona ni vibaya mno kumwambia kwamba ana Alzheimer na basi tukawa tunakubaliana tu na usemi wake wenye ‘udhuru’: ‘Hutarajii mzee mwenye umri wa miaka 80 afanye mambo sawasawa!’”

      Kisha msomaji huyo akarejezea kitabu kilichopendekeza kwamba mgonjwa aambiwe kwa njia ya fadhili na sahili kuhusu maradhi aliyo nayo. Lakini mke huyo aliogopa kwa sababu alihofu jambo hilo lingemvunja moyo sana mume wake.

      “Kisha siku moja,” akaendelea kusema, “mume wangu alitaja kwamba aliogopa kujiaibisha mbele ya marafiki wake. Nikatwaa fursa hiyo! Basi (huku nikitoka jasho jembamba) nilipiga magoti kando yake na kumwambia kwamba alikuwa na Alzheimer. Bila shaka hakujua Alzheimer ni kitu gani, lakini nikaeleza kwamba hayo ni maradhi ambayo yalikuwa yakifanya iwe vigumu kwake kufanya [mambo] ambayo sikuzote alikuwa akifanya kwa urahisi, na pia yalikuwa yakimfanya asahau mambo upesi. Nikamwonyesha sentensi mbili tu katika broshua yenu Alzheimer’s: We Can’t Ignore It Anymore: ‘Maradhi ya Alzheimer ni tatizo la ubongo linalosababisha kupoteza kumbukumbu na kudhoofika kubaya kwa akili . . . Hayo ni maradhi wala SI HALI YA KAWAIDA YA KUZEEKA.’ Pia nilimhakikishia kwamba marafiki wake walijua ana maradhi hayo na basi wanaelewa hali yake. Akafikiri kidogo, kisha akapaaza sauti: ‘Hayo ni mambo mapya ajabu! Kwa kweli hayo yanasaidia!’ Mnaweza kuwazia jinsi nilivyohisi nilipoona amefarijika sana baada ya kumjulisha hali yake!

      “Na sasa, wakati wowote ambapo anaonekana kukasirikia jambo fulani, naweza kumkumbatia na kumwambia ‘Kumbuka, si kosa lako. Ni hiyo Alzheimer mbovu inayofanya mambo yawe magumu kwako,’ naye hupoa mara moja.”

      Bila shaka, kila kisa cha AD ni tofauti. Pia, mahusiano kati ya watunzaji na wagonjwa hutofautiana. Basi kumwambia au kutomwambia mpendwa wako kwamba ana AD ni uamuzi wa kibinafsi.

  • Kuhifadhi Hadhi ya Mgonjwa
    Amkeni!—1998 | Septemba 22
    • Je, Kweli Haya Ni Maradhi ya Alzheimer?

      MZEE akipatwa na hali mbaya ya kuvurugika akili, usikate kauli mara moja ya kwamba ana maradhi ya Alzheimer (AD). Mambo mengi, kama vile kufiwa, kuhamia kwa ghafula nyumba mpya, au maambukizo, yaweza kumfanya mzee avurugike akili. Mara nyingi kuvurugika akili kwa wazee kwaweza kuponyeshwa.

      Hata kwa wagonjwa wa AD, kuzorota kwa ghafula kwa hali ya mgonjwa, kama vile kushindwa kudhibiti haja, huenda kusisababishwe na tatizo la AD. Maradhi ya AD hudhoofisha polepole. “Kuzorota kwa ghafula,” chaeleza kitabu Alzheimer’s Disease and Other Confusional States, “mara nyingi humaanisha kwamba kuna maambukizo mabaya (kama vile ya kifua au ya mkojo) ambayo yametokea. Kikundi cha wagonjwa wa [AD] huonekana kudhoofika haraka zaidi . . . Lakini, wengi wao hawadhoofiki haraka, hasa kama mtu huyo anatunzwa vizuri na matatizo mengine ya kitiba yanashughulikiwa mapema na kwa njia ifaayo.” Kutodhibiti haja kwa mgonjwa wa AD huenda kukasababishwa na matatizo mengine ya kiafya ambayo yanaweza kutibiwa. “Sikuzote hatua ya kwanza ni kumwona [daktari],” chaeleza kijarida cha kutoa shauri cha Incontinence, ambacho kimechapishwa na Shirika la Maradhi ya Alzheimer la London.

  • Mambo Ambayo Watunzaji Waweza Kufanya
    Amkeni!—1998 | Septemba 22
    • Mambo Ambayo Watunzaji Waweza Kufanya

      “SIKUZOTE nimeshangazwa na jinsi [watu] tofauti-tofauti wanavyoweza kukabiliana na hali,” asema Margaret, mtaalamu wa kitiba kutoka Australia ambaye kwa miaka mingi amewashughulikia wagonjwa wa Alzheimer na wale wanaowatunza. “Familia fulani zinakabiliana vizuri chini ya hali ngumu sana,” aendelea kusema, “huku familia nyinginezo ni kama haziwezi kabisa kukabiliana na hali mara tu mgonjwa adhihirishapo badiliko kidogo tu la utu.”—Nukuu kutoka katika kitabu When I Grow Too Old to Dream.

      Ni nini hutokeza tofauti hiyo? Jambo moja laweza kuwa ubora wa uhusiano uliokuwapo kabla ya maradhi hayo kuanza. Familia zenye uhusiano wa karibu na wenye upendo hupata ikiwa rahisi kukabili hali hiyo. Na mtu ambaye ana maradhi ya Alzheimer (AD) akitunzwa vizuri, inaweza kuwa rahisi zaidi kushughulikia maradhi hayo.

      Japo kudhoofika kwa uwezo wa kiakili, wagonjwa wengi mara nyingi hufanya vizuri mpaka hatua za mwisho kabisa za maradhi hayo iwapo wanatendewa kwa upendo na kwa wororo. “Maneno,” chasema kile kijarida cha mashauri Communication, kilichochapishwa na Shirika la Maradhi ya Alzheimer la London, “si njia pekee ya mawasiliano.” Mawasiliano yasiyohusisha maneno yatia ndani wonyesho mchangamfu na wenye urafiki usoni na sauti ya upole. Jambo muhimu pia ni kumtazama macho na vilevile kusema polepole na kwa wazi—na kutumia jina la mgonjwa mara nyingi.

      “Kudumisha mawasiliano na mpendwa wako kunawezekana,” asema Kathy, aliyetajwa katika makala iliyopita, “na ni muhimu pia. Miguso michangamfu na yenye upendo, sauti ya upole na, kuwapo kwako tu kwenyewe kutampa usalama mpendwa wako na kumfariji.” Shirika la Maradhi ya Alzheimer la London lasema hivi kwa ujumla: “Shauku yaweza kuwafanya mwe karibu, hasa wakati mazungumzo yawapo magumu. Kumshika mgonjwa mikono, kuketi nao kama umewawekea mikono, kuzungumza kwa sauti ya uanana au kuwakumbatia ni njia za kuwaonyesha kwamba bado unajali.”

      Ikiwa kuna uhusiano mchangamfu, mtunzaji na mgonjwa wanaweza kuangua kicheko pamoja hata wakati makosa yanapofanywa. Kwa mfano, mume mmoja akumbuka jinsi ambavyo mke wake aliyevurugika kiakili alitandika kitanda lakini akatandika blanketi kati ya shiti kimakosa. Waligundua kosa hilo walipoenda kulala usiku huo. “Mpenzi!” mke huyo akasema, “nimekuwa mjinga.” Na wote wakaangua kicheko.

      Fanya Maisha Yawe Sahili

      Wagonjwa wa AD hufanya vizuri zaidi katika mazingira wanayoyafahamu. Pia wanahitaji mambo ya kawaida kila siku. Kwa sababu hiyo, kalenda kubwa yenye mambo ya kufanywa kila siku yaweza kuwa yenye msaada sana. “Kumhamisha mtu kutoka mahali ambapo amepazoea,” aeleza Dakt. Gerry Bennett, “kwaweza kudhuru sana. Hali zilezile na mwendelezo ni muhimu sana kwa mtu ambaye amevurugika.”

      Maradhi hayo yasitawipo, wagonjwa wa AD hupata ikiwa vigumu zaidi kuitikia maagizo. Maagizo yatolewe kwa njia rahisi na ya wazi. Kwa mfano, kumwambia mgonjwa avae nguo laweza kuwa jambo gumu sana. Huenda ikahitajika nguo atakazovaa zipangwe kwa utaratibu na mgonjwa kusaidiwa hatua kwa hatua kuvaa kila nguo.

      Uhitaji wa Kuendelea Kuwa Mtendaji

      Baadhi ya wagonjwa wa AD hutembea-tembea ndani ya nyumba au kutembea mbali na nyumbani kwao na kupotea. Kutembea-tembea ndani ya nyumba ni mazoezi mazuri kwa mgonjwa na kwaweza kumsaidia kupunguza mkazo na kuboresha usingizi. Hata hivyo, kuondoka nyumbani kwaweza kuhatarisha. Kitabu Alzheimer’s—Caring for Your Loved One, Caring for Yourself chaeleza: “Mpendwa wako akipotea, unakabili hali ya dharura ambayo ni rahisi iwe msiba. Jambo la kukumbuka ni tulia. . . . Watu wanaomtafuta wanahitaji ufafanuzi mzuri wa mtu ambaye wanamtafuta. Uweke nyumbani picha zake za rangi za karibuni.”a

      Kwa upande mwingine, wagonjwa fulani huwa wachovu sana na huenda wakataka tu kuketi kitako siku nzima. Jaribu kuwafanya wafanye jambo fulani ambalo nyote wawili mtaweza kufurahia. Mwafanye waimbe, wapige mbinja, au kucheza ala fulani ya muziki. Wengine hufurahia kupiga makofi, kutembea, au kucheza dansi za muziki waupendao. Dakt. Carmel Sheridan aeleza: “Utendaji wenye kufanikiwa sana kwa watu wenye A.D. mara nyingi ni ule unaohusisha muziki. Mara nyingi familia hueleza kwamba muda mrefu baada ya maana ya [mambo] mengine kusahauliwa, mtu wao wa ukoo bado hufurahia nyimbo za kale ambazo alizifahamu.”

      “Nilitaka Kufanya Hivyo”

      Mke mmoja aishiye Afrika Kusini ambaye mume wake alikuwa katika hatua za mwisho-mwisho za AD alifurahia kukaa naye kila siku katika makao ya kutunzia wagonjwa. Lakini, washiriki wa familia ambao hawakuwa na nia mbaya walimchambua kwa kufanya hivyo. Ilionekana kwao kwamba labda alikuwa akipoteza wakati wake, kwa kuwa mume wake hakuonekana kama anamtambua na hakuwa akisema kamwe. “Lakini,” mke huyo akaeleza baada ya kifo chake, “nilitaka kuwa naye. Wauguzi walikuwa na shughuli nyingi sana, basi alipojichafua, ningeweza kumwosha na kumbadilishia mavazi. Nilifurahia kufanya hivyo—Nilitaka kufanya hivyo. Pindi moja aliumiza mguu wake nilipokuwa nikimsukuma katika kiti chenye magurudumu. Nikauliza, ‘Umeumia?’ akajibu, ‘Ndiyo!’ Nikatambua kwamba bado angeweza kuhisi na kuzungumza.”

      Hata katika hali ambazo uhusiano mzuri wa familia haukuwapo kabla ya AD kuanza, watunzaji bado wanaweza kukabiliana na hali.b Kujua tu kwamba wanafanya kilicho sawa na kinachompendeza Mungu kwaweza kuwapa uradhi sana. Biblia yasema, “Heshimuni uso wa mtu mzee” na, “Usimdharau mama yako akiwa mzee.” (Mambo ya Walawi 19:32; Mithali 23:22) Isitoshe, Wakristo wanaamriwa: “Ikiwa mjane yeyote ana watoto au wajukuu, acha hawa wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji-kimungu kwa watu wa nyumbani mwao wenyewe na kufuliza kulipa wazazi na babu na nyanya zao fidia ipasayo, kwa maana hili ni lenye kukubalika machoni pa Mungu. Hakika ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:4, 8.

      Kwa msaada wa Mungu, watunzaji wengi wamefaulu kuwatunza vizuri watu wao wa ukoo ambao ni wagonjwa, kutia ndani wale ambao wana maradhi ya Alzheimer.

      [Maelezo ya Chini]

      a Watunzaji fulani wamepata likiwa jambo lenye kunufaisha kumpa mgonjwa aina fulani ya kitambulisho, labda bangili au mkufu.

      b Kwa habari zaidi juu ya utunzaji na jinsi wengine wawezavyo kusaidia, tafadhali ona mfululizo wa makala “Utunzaji—Kukabili Huo Ugumu,” kwenye ukurasa wa 3-13 wa Amkeni! la Februari 8, 1997.

      [Sanduku katika ukurasa wa11]

      Maradhi ya Alzheimer na Tiba

      INGAWA kuna tiba zipatazo 200 ambazo huenda zikatibu Alzheimer (AD) ambazo bado zinachunguzwa kwa wakati huu, bado AD haina tiba. Inaripotiwa kwamba dawa fulani hurekebisha hali ya kupoteza kumbukumbu kwa muda fulani katika hatua za mapema za AD au hupunguza kuendelea kwa maradhi hayo katika wagonjwa fulani. Lakini inahitaji kutahadhari kwa sababu dawa hizo hazifaulu kwa wagonjwa wote, na baadhi ya dawa hizo zaweza kusababisha madhara. Lakini, tiba nyinginezo nyakati nyingine hutumiwa kutibu hali ambazo huandamana na AD, kama vile kushuka moyo, hangaiko, na ukosefu wa usingizi. Kwa kushauriana na daktari wa mgonjwa, kila familia yaweza kupima manufaa na hatari za tiba kabla ya kufanya uamuzi.

      [Sanduku katika ukurasa wa 11]

      Jinsi Wageni Wawezavyo Kusaidia

      KWA sababu ya kudhoofika kwa uwezo wa akili, watu wenye maradhi ya Alzheimer (AD) hawawezi kuzungumzia matukio ya karibuni kindani. Lakini, kuzungumza juu ya mambo yaliyopita ni tofauti. Kumbukumbu za mambo ya zamani zaweza kudumu, hasa katika hatua za mapema za ugonjwa huo. Wagonjwa wengi wa AD hufurahia kukumbuka wakati wao uliopita. Basi uwaombe wasimulie hadithi wazipendazo, hata kama umezisikia mara nyingi awali. Kwa njia hiyo unachangia furaha ya mgonjwa. Wakati uo huo, unaweza kuwa unampa mtunzaji wake wa kawaida pumziko analohitaji sana. Kwa hakika, kujitolea kumtunza mgonjwa kwa kipindi fulani cha wakati, labda kwa siku nzima, kwaweza kumburudisha sana yule ambaye humtunza kwa ukawaida.

      [Sanduku katika ukurasa wa 12]

      Kukabiliana na Hali ya Mgonjwa Kutodhibiti Haja

      INGAWA kutodhibiti haja huenda “kukaonekana kuwa pigo kali la mwisho,” chasema kijarida cha mashauri Incontinence, “kuna mambo ambayo yaweza kufanywa ili kupunguza tatizo hilo au kufanya lisitokeze mkazo mwingi sana.” Kumbuka kwamba huenda tatizo hilo la kutodhibiti haja lisiendelee daima; huenda tu alivurugika akili au huenda ikawa alifanya polepole kwenda msalani. Isitoshe, huenda mgonjwa anaugua ugonjwa mwingine uwezao kutibiwa unaosababisha hali yake ya kutodhibiti haja, na basi huenda akahitaji kumwona daktari.

      Hali ya kutodhibiti haja hata iwe imesababishwa na nini, inaweza kushughulikiwa kwa urahisi ikiwa mgonjwa avalia mavazi ya nje yaliyo rahisi kuvaa na kuvua na suruali zilizoshonwa kufaana na hali yake. Pia litakuwa jambo lenye kunufaisha ikiwa utaweka matandiko yenye kuzuia haja kwenye kitanda na viti. Epuka kuwasha ngozi na kutokeza vidonda kwa kuhakikisha kwamba vitu vya plastiki havigusani na ngozi ya mgonjwa. Pia, osha mgonjwa kwa maji yenye joto na sabuni na kumpangusa kabisa kabla ya kumvalisha nguo. Ondoa vitu ambavyo huenda vikamzuia mgonjwa asiende upesi na kwa usalama msalani. Huenda ikafaa kuacha taa ya usiku ikiwaka ili asipotee. Kwa sababu huenda mgonjwa akawa hana usawaziko mzuri wakati huu, weka kitu cha kushikilia mahali pafaapo ambacho kitamsaidia kwenda msalani bila matatizo mengi.

      “Ikiwa unaweza kuwa mcheshi pia,” ladokeza Shirika la Maradhi ya Alzheimer la London, “huenda hiyo ikaondoa mkazo.” Mtunzaji aweza kukabilije magumu hayo? Mtunzaji mmoja mwenye uzoefu ajibu: “Saburi, uungwana, fadhili, na upole wa hisani zitamsaidia mgonjwa adumishe hadhi yake nyakati zote, bila hofu ya kuaibika au kuona haya.”

      [Sanduku katika ukurasa wa 13]

      Je, Mgonjwa Ahamishwe?

      KWA kusikitisha, kuendelea kudhoofika kwa hali ya watu wenye Alzheimer (AD) kunaweza kuhitaji wahamishwe kutoka nyumbani kwao hadi kwenye nyumba ya mtu wa ukoo au makao ya kutunzia wagonjwa. Lakini, kabla ya kufanya uamuzi wa kumhamisha mgonjwa kutoka kwenye mazingira anayofahamu, ni vizuri kufikiria mambo fulani muhimu.

      Anaweza kuvurugika sana akili kwa sababu ya kuhama. Dakt. Gerry Bennett atoa mfano wa mgonjwa ambaye alikuwa amependa kutembea-tembea nje na nyakati nyingine kupotea. Lakini, bado alifaulu kuishi peke yake. Lakini, familia yake ikaamua kwamba anapaswa kuhamishwa aishi karibu nao ili wamtunze kwa njia bora zaidi.

      “Kwa ubaya,” aeleza Dakt. Bennett, “hakukubali kamwe makao yake mapya. . . . Kwa kusikitisha hakupazoea hapo mahali papya, na kwa kweli walimfanya awategemee zaidi kwa sababu sasa hangeweza kufanya lolote katika mazingira hayo mapya. Hakufahamu jikoni na hakuweza kukumbuka njia mpya ya kuelekea msalani, akawa anajiendea haja. Kutokana na nia nzuri matokeo yakawa msiba na hatimaye ikalazimika atunzwe katika makao fulani.”—Alzheimer’s Disease and Other Confusional States.

      Lakini, namna gani ikionekana kwamba hakuna namna ila tu kumhamisha kwenye makao ya kuwatunza? Huo si uamuzi rahisi kamwe. Kwa hakika, umefafanuliwa kuwa “mojawapo ya [maamuzi] yenye kutokeza hisia ya hatia zaidi” ambazo watunzaji hupata, mara nyingi wakihisi kwamba wamemtamausha na wamemtupa mpendwa wao.

      “Ni jambo la kawaida kuhisi hivyo,” asema muuguzi mmoja mwenye uzoefu sana wa kutibu wagonjwa wa AD, “lakini ni hatia isiyofaa.” Kwa nini? “Kwa sababu” yeye ajibu, “utunzaji na usalama wa [mgonjwa] ungekuwa jambo kuu la kufikiriwa.” Madaktari Oliver na Bock wakubali: “Uamuzi wa kwamba mtu ameshindwa kabisa kihisia-moyo na kwamba maradhi hayo yameenea kufikia hatua ambayo inafanya iwe vigumu sana kumtunza mgonjwa nyumbani ni mojawapo ya uamuzi ulio mgumu zaidi kufanya.” Lakini, baada ya kupima mambo yote yanayohusika katika hali hususa, watunzaji fulani huenda bado wakakata kauli ya kwamba “kumpeleka mgonjwa katika makao ya kuwatunzia wagonjwa ni . . . bora zaidi kwa mgonjwa.”—Coping With Alzheimer’s: A Caregiver’s Emotional Survival Guide.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki