-
Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni PoteMnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 15
-
-
Je, Ni Habari za Kutegemeka au za Uwongo?
Usifikiri kamwe kwamba habari zote zinazopatikana katika Intaneti ni nzuri na ni zenye faida. Vituo vya kutafuta habari katika Intaneti vinaweza kulinganishwa na kikundi kikubwa cha watu wanaovuna kwa bidii uyoga wa kila aina, wanavuna uyoga unaoweza kuliwa na uyoga wenye sumu, na kukusanya uyoga wote katika kikapu kimoja na kutugawia ili tule. Je, ungeanza kula bila kuchunguza kila uyoga kwa uangalifu? Bila shaka huwezi kufanya hivyo! Vituo vya kutafuta habari katika Intaneti vinatumia kompyuta nyingi kuchagua au kukusanya habari kutoka katika mabilioni ya vituo vyenye habari za kila aina, kuanzia habari nzuri sana mpaka habari mbaya zaidi. Tunahitaji utambuzi ili kutenganisha kwa njia ya mfano ngano kutoka katika makapi, ili akili zetu zisitiwe sumu na habari zenye kupotosha.
Mwaka wa 1993, gazeti moja linalojulikana sana lilikuwa na mchoro ambao ulionyesha mbwa wawili wakiwa mbele ya kompyuta. Mbwa mmoja anamwambia hivi yule mwingine: “Katika Intaneti, hakuna mtu anayejua kwamba wewe ni mbwa.” Zamani za kale, Shetani alijificha kwa kumtumia nyoka kuanzisha mazungumzo na Hawa na kumwambia kwamba angekuwa kama Mungu. Leo, mtu yeyote ambaye anaweza kutumia Intaneti anaweza kujifanya kuwa profesa, kana kwamba anajua kila jambo, bila hata kufunua jina lake. Na hakuna sheria zinazomzuia mtu yeyote kuweka mawazo, habari, picha, na mapendekezo katika Intaneti.
Unapotumia Intaneti usiwe mpumbavu kama Hawa. Uwe mwangalifu sana kabla ya kuamini habari unayopata katika Intaneti. Kabla ya kuamini habari, jiulize hivi: (1) Ni nani aliyeandika habari hiyo? Mwandishi huyo ana sifa au mamlaka gani kuhusu habari ambazo anaandika? (2) Kwa nini aliandika habari hiyo? Ni nini kilichomchochea mwandishi huyo kuandika habari hiyo? Je, anapendelea upande fulani? (3) Mwandishi huyo alipata wapi habari hiyo? Je, anataja vyanzo vya habari ambavyo vinaweza kuchunguzwa? (4) Je, habari hiyo ni ya karibuni? Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alimpa Timotheo mashauri ambayo yanafaa kabisa leo. Paulo aliandika hivi: “Linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu na kutoka kwenye maneno yanayopingana ya ule unaoitwa kwa uwongo ‘ujuzi.’”—1 Tim. 6:20.
-
-
Intaneti Kutumia kwa Hekima Kifaa cha Ulimwenguni PoteMnara wa Mlinzi—2011 | Agosti 15
-
-
Je, Ni Habari Zinazofaa au Zisizofaa?
Katika andiko la 1 Wathesalonike 5:21, 22, tunasoma hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri. Jiepusheni na kila namna ya uovu.” Tunahitaji kujua ikiwa habari tunazopata katika Intaneti zinampendeza Mungu, na zinapatana na viwango vyake vya juu. Zinapaswa kuwa habari zenye maadili yanayofaa na zinazomfaa Mkristo. Ponografia (picha au habari za ngono) zimeenea sana hasa katika Intaneti, na tusipokuwa waangalifu, zinaweza kwa urahisi kutushawishi tuanguke katika mtego huo.
Ni jambo la hekima kwetu kujiuliza, ‘Je, ninatazama mambo ambayo nitaficha haraka ikiwa mwenzi wangu wa ndoa, wazazi wangu, au ndugu zangu Wakristo wataingia chumbani?’ Ikiwa jibu ni ndiyo, itakuwa vizuri kutumia Intaneti wakati tu ambapo kuna watu wengine. Kwa kweli, Intaneti imebadili jinsi tunavyopashana habari na kununua vitu. Zaidi ya hayo, imefungua njia mpya kabisa ya ‘kufanya uzinzi moyoni mwetu.’—Mt. 5:27, 28.
-