Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mabomu ya Ardhini—Kuchunguza Athari Zake
    Amkeni!—2000 | Mei 8
    • Vipi Juu ya Kuondoa Mabomu ya Ardhini?

      Katika miaka ya majuzi mataifa yametiwa moyo sana yapige marufuku utumiaji wa mabomu ya ardhini. Pia, serikali fulani zimeanza kazi hatari ya kuondoa mabomu yaliyotegwa ardhini. Lakini kuna vizuizi kadhaa. Kizuizi cha kwanza ni wakati. Kuondoa mabomu ya ardhini ni kazi inayofanywa miaka nenda miaka rudi. Kwa hakika, wateguaji wa mabomu hayo hukadiria kwamba kwa wastani, muda unaohitajiwa kuondoa bomu lililotegwa ardhini ni mara 100 zaidi ya muda unaotumiwa kulitega. Kizuizi kingine ni gharama. Bomu moja hugharimu kati ya dola 3 hadi 15 za Marekani, lakini kuliondoa kwaweza kugharimu dola zipatazo 1,000.

      Kwa hiyo, yaonekana kuondoa mabomu yote yaliyotegwa ni jambo lisilowezekana. Kwa mfano, kuondoa mabomu yote ya ardhini huko Kambodia, kutamaanisha kwamba kila mtu nchini humo atoe mshahara wake wote kwa miaka kadhaa kwa ajili ya kazi hiyo. Inakadiriwa kwamba hata fedha zikiwapo, kuondoa mabomu yote ya ardhini yaliyotegwa huko kungechukua muda wa karne moja. Hali ya ulimwenguni pote ni yenye kusikitisha hata zaidi. Inakadiriwa kwamba kuondoa mabomu yote duniani kwa kutumia tekinolojia ya kisasa, kungegharimu dola bilioni 33 za Marekani na kungechukua muda wa zaidi ya miaka 1,000!

      Ni kweli kwamba mbinu mpya za kuondoa mabomu ya ardhini zimependekezwa—kutoka kutumia nzi-tunda ambao wametiwa chembe za kuwasaidia kugundua mabomu hadi kutumia magari makubwa yenye kuelekezwa kwa mawimbi ya redio ambayo yangeondoa mabomu kwenye eneo la ekari tano kwa kila saa moja. Lakini, itahitaji muda fulani kabla ya mbinu hizo kuweza kutumiwa kila mahali, na yaelekea zitatumiwa katika nchi tajiri tu.

      Hivyo, nchi nyingi hutumia mbinu za kale za kuondoa mabomu yaliyotegwa ardhini. Mtu hujikokota kwa tumbo huku akichimba-chimba mbele kwa kijiti, sentimeta kwa sentimeta, eneo la meta 20 hadi 50 za mraba kwa siku. Ni hatari, sivyo? Ndivyo! Kwa kila mabomu 5,000 yanayoondolewa, mteguaji mmoja hufa na wawili hujeruhiwa.

  • Mabomu ya Ardhini—Kuchunguza Athari Zake
    Amkeni!—2000 | Mei 8
    • [Sanduku katika ukurasa wa 6]

      Je, Wanachuma Fedha Maradufu?

      Kanuni ya msingi ya biashara ni kwamba makampuni yanapasa kushtakiwa bidhaa zao zinapodhuru watu. Hivyo, Lou McGrath, wa shirika la Mines Advisory Group, asema kwamba makampuni ambayo yamefaidika kutokana na utengenezaji wa mabomu ya ardhini yapasa kushurutishwa kulipia hasara. Lakini, jambo la kushangaza ni kwamba watengenezaji wengi ndio wanaochuma fedha kwa kuondoa mabomu hayo. Kwa mfano, imeripotiwa kwamba kampuni moja ya Ujerumani iliyokuwa ikitengeneza mabomu ya ardhini ilipata kandarasi ya dola milioni 100 za Marekani ili kuondoa mabomu ya ardhini huko Kuwait. Na huko Msumbiji, shirika lenye makampuni matatu—mawili kati yake yalikuwa yametengeneza mabomu ya ardhini—lilipata kandarasi ya dola milioni 7.5 ya kuondoa mabomu kwenye barabara zilizoteuliwa.

      Baadhi ya watu wanahisi kwamba ni ukosefu mkubwa wa adili kwa makampuni yanayotengeneza mabomu ya ardhini kuchuma fedha kwa kuondoa mabomu hayo. Wanadai kwamba kwa njia fulani watengenezaji wa mabomu ya ardhini huchuma fedha maradufu. Kwa vyovyote vile, kutengeneza na kuondoa mabomu ya ardhini bado ni biashara zinazositawi.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki