-
Wale Wanaotembea Katika Nuru HushangiliaMnara wa Mlinzi—2001 | Machi 1
-
-
Wale Wanaotembea Katika Nuru Hushangilia
“Njoni twende katika nuru ya BWANA.”—ISAYA 2:5.
1, 2. (a) Nuru ni muhimu kadiri gani? (b) Kwa nini onyo la kwamba giza lingeifunika dunia ni zito sana?
YEHOVA ndiye Chanzo cha nuru. Biblia humtaja kuwa “awapaye watu jua, ili kuwa nuru wakati wa mchana, na amri za mwezi na nyota, ili kuwa nuru wakati wa usiku.” (Yeremia 31:35; Zaburi 8:3) Yeye ndiye aliyeumba jua letu, ambalo kwa kweli ni tanuri kubwa sana ya nyuklia inayotoa nishati nyingi sana, baadhi yake ikiwa nuru na joto. Kiasi kidogo cha nishati hiyo ambayo hutufikia ikiwa nuru ya jua hutegemeza uhai duniani. Hatungeweza kuishi pasipo nuru hiyo ya jua. Dunia ingekuwa sayari isiyo na uhai.
2 Tunapozingatia hilo, tunaweza kuelewa uzito wa hali inayofafanuliwa na nabii Isaya. Alisema hivi: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.” (Isaya 60:2) Ni wazi kwamba giza hilo si giza halisi. Isaya hakumaanisha kwamba siku fulani jua, mwezi, na nyota zitaacha kuangaza. (Zaburi 89:36, 37; 136:7-9) Badala yake, alikuwa akizungumzia giza la kiroho. Lakini giza la kiroho laweza kusababisha kifo. Hatuwezi kuishi bila nuru ya kiroho kwa muda mrefu kama vile tusivyoweza kuishi bila nuru halisi.—Luka 1:79.
3. Kwa kuzingatia maneno ya Isaya, Wakristo wapaswa kufanya nini?
3 Kwa kuzingatia hilo, ni jambo muhimu kutambua kwamba ijapokuwa maneno ya Isaya yalitimizwa katika Yuda la kale, yanatimizwa kwa kiwango kikubwa zaidi leo. Naam, katika wakati wetu ulimwengu umefunikwa na giza la kiroho. Katika hali hiyo hatari, nuru ya kiroho ni muhimu kuliko mambo yote. Ndiyo sababu inafaa Wakristo watii himizo hili la Yesu: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu.” (Mathayo 5:16) Wakristo waaminifu wanaweza kuwaangazia nuru wapole walio katika giza, na hivyo kuwapa fursa ya kupata uhai.—Yohana 8:12.
Nyakati Zenye Giza Katika Israeli
4. Maneno ya kiunabii ya Isaya yalitimizwa lini mara ya kwanza, lakini tayari kulikuwa na hali gani katika siku zake?
4 Maneno ya Isaya kuhusu jinsi ambavyo giza lingeifunika dunia yalitimizwa mara ya kwanza Yuda lilipofanywa ukiwa na watu wake walipokuwa katika utekwa Babiloni. Hata hivyo, hata kabla ya wakati huo, katika siku za Isaya mwenyewe, tayari sehemu kubwa ya taifa hilo ilikuwa imefunikwa na giza la kiroho, jambo lililomchochea awasihi hivi watu wa nchi yake: “Enyi wa nyumba ya Israeli, njoni twende katika nuru ya BWANA”!—Isaya 2:5; 5:20.
5, 6. Ni mambo gani yaliyochangia giza katika siku za Isaya?
5 Isaya alitoa unabii katika Yuda “siku za Uzia, Yothamu, Ahazi na Hezekia, wafalme wa Yuda.” (Isaya 1:1) Zilikuwa nyakati zenye ghasia na misukosuko ya kisiasa, unafiki wa kidini, kupotoshwa kwa haki, na kuonewa kwa maskini. Hata wakati wa wafalme waaminifu, kama vile Yothamu, kulikuwepo madhabahu za miungu isiyo ya kweli kwenye vilele vya milima. Wakati wa watawala wasio waaminifu, hali zilikuwa mbaya hata zaidi. Kwa mfano, Mfalme Ahazi mwovu, hata alimtoa mwana wake kuwa dhabihu katika dhabihu za tambiko kwa mungu aitwaye Moleki. Hilo lilikuwa giza la ajabu!—2 Wafalme 15:32-34; 16:2-4.
6 Hali ya kimataifa ilikuwa yenye kuhuzunisha pia. Moabu, Edomu, na Ufilisti yalizingira mipaka ya Yuda kwa njia yenye kutisha. Ingawa ufalme wa kaskazini wa Israeli ulikuwa na uhusiano wa kijamaa na Yuda, sasa ulionyesha uadui waziwazi. Mbali kaskazini, Siria ilitishia amani ya Yuda. Hatari kubwa hata zaidi ilikuwa ile serikali ya Ashuru yenye ukatili, ambayo ilijitahidi daima kupanua mamlaka yake. Katika kipindi ambacho Isaya alitoa unabii, Ashuru ilishinda Israeli na ikakaribia kuiharibu Yuda. Wakati fulani, Ashuru ilikuwa imeshinda kila mji nchini Yuda isipokuwa Yerusalemu.—Isaya 1:7, 8; 36:1.
7. Israeli na Yuda zilichagua njia gani, naye Yehova alitendaje?
7 Watu wa Mungu waliokuwa wamefanya agano pamoja naye walipatwa na misiba hiyo kwa sababu Israeli na Yuda zilikosa uaminifu-mshikamanifu kwake. Kama wale wanaotajwa katika kitabu cha Mithali, walikuwa ‘wakiacha njia za unyofu, ili kuziendea njia za giza.’ (Mithali 2:13) Hata ingawa Yehova alikasirishwa na watu wake, hakuwaacha kabisa. Badala yake, alimwinua Isaya na manabii wengine ili waangaze nuru ya kiroho kwa yeyote katika taifa hilo aliyetaka bado kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Nuru iliyotolewa kupitia manabii hao ilikuwa yenye thamani kwelikweli. Ilikuwa yenye kuhuisha.
Nyakati za Giza Leo
8, 9. Ni mambo gani yanayochangia giza la ulimwengu leo?
8 Hali katika siku za Isaya yafanana sana na mambo tunayoona leo. Katika kipindi chetu, watawala wa kibinadamu wamemkataa Yehova na Mfalme wake aliyetawazwa, Yesu Kristo. (Zaburi 2:2, 3) Viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wamedanganya makundi yao. Viongozi hao hudai kumtumikia Mungu, lakini kwa kweli wengi wao huunga mkono miungu ya ulimwengu huu—utukuzo wa taifa, utumizi wa nguvu za kijeshi, utajiri, na watu mashuhuri—mbali na kufundisha mafundisho ya kipagani.
9 Dini za Jumuiya ya Wakristo zimejihusisha katika vita na maangamizi ya jamii na matisho mengine mahali mahali. Isitoshe, badala ya kutetea maadili yanayotegemea Biblia, makanisa mengi ama yanapuuza ama kuunga mkono kwa bidii mazoea yasiyo ya adili kama uasherati na ugoni-jinsia-moja. Kwa sababu ya kukataa viwango vya Biblia, makundi ya Jumuiya ya Wakristo ni sawa na watu waliotajwa na mtunga-zaburi wa kale: “Hawajui wala hawafahamu, hutembea gizani.” (Zaburi 82:5) Kwa kweli, Jumuiya ya Wakristo kama vile Yuda la kale, iko katika giza nene.—Ufunuo 8:12.
10. Nuru huangazaje katika giza leo, na wapole hunufaikaje?
10 Katikati ya giza hilo, Yehova anasababisha nuru iangaze kwa ajili ya wapole. Ili kutimiza hilo, anatumia watumishi wake waliotiwa mafuta walioko duniani, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” nao ‘hung’aa wakiwa wamulikaji katika ulimwengu.’ (Mathayo 24:45; Wafilipi 2:15) Jamii hiyo ya mtumwa, ikiungwa mkono na mamilioni ya waandamani wao “kondoo wengine” huangaza nuru ya kiroho inayotegemea Neno la Mungu, Biblia. (Yohana 10:16) Katika ulimwengu huu uliojaa giza, nuru hiyo huwapa wapole tumaini, huwasaidia kuwa na uhusiano na Mungu, na kuepuka mitego ya kiroho. Ni yenye thamani, na huhuisha.
‘Nalihimidi Jina Lako’
11. Yehova alitoa habari gani katika siku za Isaya?
11 Yehova aliandaa mwongozo gani katika siku zenye giza ambazo Isaya aliishi na hata katika siku zilizokuwa na giza zaidi wakati Wababiloni walipoteka taifa la Yehova? Mbali na kutoa mwongozo wa kiadili, alionyesha waziwazi hapo kimbele jinsi ambavyo angetimiza makusudi yake kuhusiana na watu wake. Kwa mfano, fikiria unabii mzuri sana unaopatikana katika Isaya sura ya 25 hadi 27. Sura hizo zaonyesha jinsi Yehova alivyoshughulikia mambo wakati huo na jinsi afanyavyo hivyo leo.
12. Isaya asema maneno gani ya kutoka moyoni?
12 Kwanza, Isaya atangaza hivi: “Ee BWANA [“Yehova,” NW], wewe u Mungu wangu; nitakutukuza na kulihimidi jina lako.” Hayo yalikuwa maneno yenye sifa ya kutoka moyoni kama nini! Mbona nabii huyo alitoa sala ya aina hiyo? Sababu moja kuu yafunuliwa kwenye sehemu iliyobaki ya mstari huo, ambapo twasoma hivi: “Kwa kuwa [wewe Yehova] umetenda mambo ya ajabu, mashauri ya kale, kwa uaminifu na kweli.”—Isaya 25:1.
13. (a) Ni ujuzi gani uliomtia Isaya nguvu amthamini Yehova? (b) Tunawezaje kujifunza kutokana na kielelezo cha Isaya?
13 Kufikia siku za Isaya, Yehova alikuwa amefanya matendo mengi ya ajabu kwa ajili ya Israeli, nayo yakaandikwa. Ni wazi kwamba Isaya aliyafahamu maandiko hayo. Kwa mfano, alijua kwamba Yehova alikuwa amewakomboa watu wake kutoka utumwa wa Misri na kuwaokoa kutoka kwa hasira ya majeshi ya Farao kwenye Bahari Nyekundu. Alijua kwamba Yehova alikuwa amewaongoza watu wake katika nyika na kuwaleta katika Nchi ya Ahadi. (Zaburi 136:1, 10-26) Masimulizi hayo ya kihistoria yalionyesha kwamba Yehova Mungu ni mwaminifu na ni mwenye kutumainika. “Mashauri” yake—mambo yote anayokusudia—hutimia. Ujuzi sahihi uliotolewa na Mungu ulimtia Isaya nguvu aendelee kutembea katika nuru. Hivyo basi, akawa kielelezo kizuri kwetu. Tukijifunza kwa makini Neno la Mungu lililoandikwa na kulitumia maishani, sisi pia tutadumu katika nuru.—Zaburi 119:105; 2 Wakorintho 4:6.
Jiji Laharibiwa
14. Ni nini kilichotabiriwa kuhusu mji fulani, na yaelekea mji huo ni upi?
14 Kielelezo kimoja cha mashauri ya Mungu kipo kwenye Isaya 25:2, ambapo twasoma: “Umefanya mji kuwa ni chungu; mji wenye boma kuwa ni magofu; jumba la wageni kuwa si mji; hautajengwa tena milele.” Ni mji upi huo? Huenda Isaya alikuwa akitabiri juu ya Babiloni. Kwa kweli, wakati ulifika ambapo Babiloni ulikuwa rundo la mawe.
15. Ni “jiji [gani] kubwa” lililopo leo, nalo litapatwa na nini?
15 Je, mji anaoutaja Isaya wafanana na mji wowote leo? Ndiyo. Kitabu cha Ufunuo chasema juu ya “jiji kubwa lililo na ufalme juu ya wafalme wa dunia.” (Ufunuo 17:18) Jiji hilo kuu ni “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 17:5) Sehemu kuu ya Babiloni Mkubwa leo ni Jumuiya ya Wakristo, ambayo makasisi wake huongoza katika kupinga kazi ya kuhubiri Ufalme ya watu wa Yehova. (Mathayo 24:14) Hata hivyo, kama vile Babiloni wa kale, Babiloni Mkubwa litaharibiwa hivi karibuni, halitainuka tena kamwe.
16, 17. Maadui wa Yehova wamemtukuzaje katika nyakati za kale na za leo?
16 Isaya atabiri nini kingine kuhusu “mji wenye boma”? Isaya amwambia Yehova hivi: “Watu walio hodari watakutukuza, mji wa mataifa watishao utakuogopa.” (Isaya 25:3) Mji huo wenye uadui, “mji wa mataifa watishao,” wawezaje kumtukuza Yehova? Kumbuka kilichompata Mfalme Nebukadreza wa Babiloni mwenye nguvu nyingi sana. Baada ya kupatwa na jambo lenye kuamsha fikira lililoonyesha udhaifu wake mwenyewe, alilazimika kukiri ukuu wa Yehova na nguvu za uweza Wake wote. (Danieli 4:34, 35) Yehova anapodhihirisha nguvu zake, hata maadui wake hulazimika kukiri matendo yake yenye nguvu hata ingawa ni kwa kusitasita.
17 Je, Babiloni Mkubwa aliwahi kulazimika kukiri matendo ya Yehova yenye nguvu? Ndiyo. Katika vita ya ulimwengu ya kwanza, watumishi wa Yehova waliotiwa mafuta walihubiri chini ya dhiki. Mwaka wa 1918 waliingia katika utekwa wa kiroho wakati wasimamizi wa Watch Tower Society walipotiwa gerezani. Kazi iliyopangwa ya kuhubiri karibu ikome. Kisha, mwaka wa 1919, Yehova aliwarudisha na kuwatia nguvu upya kwa roho yake, ambapo walitoka ili kutimiza utume wa kuhubiri habari njema katika dunia yote inayokaliwa. (Marko 13:10) Yote hayo yalitabiriwa katika kitabu cha Ufunuo, na pia athari ambazo zingewapata maadui wao. Hawa “wakawa wenye kuogopa na kumpa utukufu Mungu wa mbinguni.” (Ufunuo 11:3, 7, 11-13) Si kwamba wote waligeuzwa imani, lakini walilazimika kutambua matendo ya Yehova yenye nguvu katika pindi hiyo, kama vile Isaya alivyokuwa ametabiri.
“Ngome ya Maskini”
18, 19. (a) Kwa nini wapinzani wameshindwa kuvunja uaminifu-maadili wa watu wa Yehova? (b) “Wimbo wa hao watishao” utashushwa jinsi gani?
18 Akielekeza fikira zake sasa kwa matendo ya fadhili ya Yehova kwa wale wanaotembea katika nuru, Isaya amwambia Yehova hivi: “Umekuwa ngome ya maskini, ngome ya mhitaji katika dhiki yake, mahali pa kukimbilia wakati wa tufani, kivuli wakati wa hari; wakati uvumapo upepo wa watu watishao, kama dhoruba ipigayo ukuta. Kama vile hari katika mahali pakavu utaushusha mshindo wa wageni; kama ilivyo hari kwa kivuli cha wingu, wimbo wa hao watishao utashushwa.”—Isaya 25:4, 5.
19 Tangu mwaka wa 1919, wakatili wamejaribu juu chini kuvunja uaminifu-maadili wa waabudu wa kweli, lakini hawajafaulu. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ni ngome na kimbilio la watu wake. Yeye huandaa kivuli kutoka kwa joto lenye kuchoma la mnyanyaso na husimama kama ukuta imara dhidi ya dhoruba za upinzani. Sisi tunaotembea katika nuru ya Mungu hutazamia kwa uhakika wakati ambapo “wimbo wa hao watishao utashushwa.” Naam, twatazamia kwa hamu siku ambayo maadui wa Yehova watakuwa wametoweka.
20, 21. Ni karamu gani anayoandaa Yehova, na karamu hiyo itatia ndani nini katika ulimwengu mpya?
20 Yehova hufanya mengi kuliko tu kuwalinda watumishi wake. Yeye huwaandalia akiwa Baba yao mpendwa. Baada ya kuwakomboa watu wake kutoka Babiloni Mkubwa mwaka wa 1919, aliwaandalia karamu ya ushindi, chakula kingi cha kiroho. Hayo yalitabiriwa kwenye Isaya 25:6, ambapo twasoma hivi: “Katika mlima huu BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.” Tumebarikiwa kama nini kushiriki katika karamu hiyo! (Mathayo 4:4) Kwa kweli “meza ya Yehova” imejaa vitu vizuri vya kula. (1 Wakorintho 10:21) Kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” tunapewa chochote ambacho tungehitaji kiroho.
21 Karamu hiyo ambayo Mungu ameandaa ina mengi zaidi. Karamu ya kiroho tunayofurahia sasa hutukumbusha wingi wa chakula cha kimwili kitakachokuwepo katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. Kisha, “karamu ya vitu vinono” itatia ndani chakula kingi cha kimwili. Hakuna yeyote atakayelazimika kuona njaa ya kimwili au ya kiroho. Itakuwa faraja iliyoje kwa waamini wenzetu wapendwa ambao sasa huteseka kwa sababu ya “upungufu wa chakula” uliotabiriwa, ambao ni sehemu ya “ishara” ya kuwapo kwa Yesu! (Mathayo 24:3, 7) Maneno ya mtunga-zaburi yanawafariji kwelikweli. Alisema: “Nchi na izae nafaka kwa wingi, vilima vijae mavuno.”—Zaburi 72:16, Biblia Habari Njema.
22, 23. (a) Ni “utaji” au “sitara” gani itakayoondolewa, na jinsi gani? (b) ‘Aibu ya watu wa Yehova’ itaondolewaje?
22 Sasa isikilize ahadi nzuri hata zaidi. Akilinganisha dhambi na kifo na “utaji,” au “sitara,” Isaya asema hivi: “Katika mlima huu [Yehova] atauharibu uso wa sitara iliyowekwa juu ya watu wote, na utaji ule uliotandwa juu ya mataifa yote.” (Isaya 15:7) Hebu wazia! Dhambi na kifo, ambazo zimewalemea wanadamu kama blanketi inayomzuia mtu kupumua, hazitakuwapo tena. Twatazamia kwa hamu kama nini siku ambayo wanadamu watiifu na waaminifu watanufaishwa kikamili na dhabihu ya fidia ya Yesu!—Ufunuo 21:3, 4.
23 Akirejezea wakati huo mzuri ajabu, nabii aliyepuliziwa atuhakikishia hivi: “[Mungu] amemeza mauti hata milele; na BWANA Mungu atafuta machozi katika nyuso zote; na aibu ya watu wake ataiondoa katika ulimwengu wote; maana BWANA amenena hayo.” (Isaya 25:8) Hakuna atakayekufa kutokana na sababu za kiasili wala kulia kwa sababu ya kifo cha mpendwa. Ni mabadiliko yenye baraka kama nini! Isitoshe, suto na propaganda ya uwongo, mambo ambayo Mungu na watumishi wake wamevumilia kwa muda mrefu hayatasikika popote duniani. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ataondoa mwenye kuyasababisha—baba ya uwongo, Shetani Ibilisi, pamoja na mbegu yote ya Shetani.—Yohana 8:44.
24. Wale wanaotembea katika nuru huitikiaje matendo ya Yehova yenye nguvu anayowafanyia?
24 Baada ya kutafakari udhihirisho huo wa nguvu za Yehova, wale wanaotembea katika nuru wanachochewa kutangaza hivi: “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, ndiye tuliyemngoja atusaidie; huyu ndiye BWANA tuliyemngoja, na tushangilie na kufurahia wokovu wake.” (Isaya 25:9) Karibuni, wanadamu waadilifu watafurahi kwelikweli. Giza litaondoshwa kabisa, nao waaminifu watafurahia nuru ya Yehova kwa umilele. Je, kuna tumaini lingine tukufu kuliko hilo? Kwa kweli hakuna!
-
-
Wokovu kwa Wanaochagua NuruMnara wa Mlinzi—2001 | Machi 1
-
-
Wokovu kwa Wanaochagua Nuru
“BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani?”—ZABURI 27:1.
1. Yehova huandaa mambo gani yenye kuhuisha?
YEHOVA ndiye Chanzo cha nuru ya jua ambayo hutegemeza uhai duniani. (Mwanzo 1:2, 14) Yeye pia ndiye Muumba wa nuru ya kiroho, ambayo huondoa giza linaloweza kuua la ulimwengu wa Shetani. (Isaya 60:2; 2 Wakorintho 4:6; Waefeso 5:8-11; 6:12) Wale wanaochagua nuru wanaweza kujiunga na mtunga-zaburi kusema: “BWANA ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani?” (Zaburi 27:1a) Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Yesu wale wanaopendelea giza wanaweza tu kutarajia hukumu isiyopendeza.—Yohana 1:9-11; 3:19-21, 36.
2. Ni nini kilichowapata watu waliokataa nuru ya Yehova na wale waliosikiliza neno lake katika nyakati za kale?
2 Katika siku za Isaya, watu wengi wa Yehova waliokuwa wamefanya agano naye walikataa nuru. Kwa sababu hiyo, Isaya aliona uharibifu wa ufalme wa kaskazini wa taifa la Israeli. Na katika mwaka wa 607 K.W.K., Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa na wakazi wa Yuda wakapelekwa katika utekwa. Hata hivyo, wale waliosikiliza neno la Yehova waliimarishwa kukinza uasi-imani wa siku hizo. Kuhusu mwaka wa 607 K.W.K., Yehova aliahidi kwamba wale ambao wangemsikiliza wangeokoka. (Yeremia 21:8, 9) Leo, sisi ambao tunapenda nuru twaweza kujifunza mengi kutokana na mambo yaliyotukia wakati huo.—Waefeso 5:5.
Furaha ya Wale Walio Katika Nuru
3. Leo twaweza kuwa na uhakika gani, twapenda ‘taifa gani lenye haki’ na ni ‘mji gani ulio na nguvu’ ambao “taifa” hilo linao?
3 “Sisi tunao mji ulio na nguvu; [Mungu] ataamuru wokovu kuwa kuta na maboma. Wekeni wazi malango yake, taifa lenye haki, lishikalo kweli liingie.” (Isaya 26:1, 2) Hayo ni maneno yenye shangwe ya watu waliomtumaini Yehova. Wayahudi waaminifu katika siku za Isaya walimtegemea Yehova kuwa Chanzo pekee cha usalama wa kweli, wala si miungu isiyo ya kweli ya watu wa nchi yao. Leo, tuna uhakika kama huo. Isitoshe, tunalipenda “taifa lenye haki” la Yehova—“Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Mathayo 21:43) Yehova hulipenda pia taifa hili kwa sababu ya mwenendo wake wa uaminifu. Kwa sababu ya baraka zake, Israeli wa Mungu ana “mji ulio na nguvu,” tengenezo lililo kama mji ambalo hutegemeza na kulinda taifa hilo.
4. Yafaa tusitawishe mtazamo gani wa akili?
4 Wale walio ndani ya “mji” huu wanatambua kwamba ‘Yehova atamlinda yeye ambaye moyo wake umemtegemea katika amani kamilifu, kwa kuwa anamtumaini.’ Yehova hutegemeza wale ambao humtumaini na kutii kanuni zake za uadilifu. Hivyo, wale waliokuwa waaminifu huko Yuda walitii himizo hili la Isaya: “Mtumainini BWANA siku zote maana BWANA [“Yah,” NW] YEHOVA ni mwamba wa milele.” (Isaya 26:3, 4; Zaburi 9:10; 37:3; Mithali 3:5) Wale walio na mtazamo huo wa akili humtegemea “BWANA YEHOVA” akiwa ndiye Mwamba pekee ulio salama. Wao hufurahia “amani kamilifu” pamoja naye.—Wafilipi 1:2; 4:6, 7.
Kuaibishwa kwa Maadui wa Mungu
5, 6. (a) Babiloni la kale liliaibishwaje? (b) “Babiloni Mkubwa” aliaibishwa katika njia gani?
5 Namna gani wale wanaomtumaini Yehova wakipatwa na dhiki? Hawahitaji kuogopa. Yehova huruhusu mambo hayo kwa muda, lakini hatimaye huleta kitulizo, naye anawahukumu wale wanaosababisha dhiki hiyo. (2 Wathesalonike 1:4-7; 2 Timotheo 1:8-10) Fikiria hali ya ‘mji fulani ulioinuka.’ Isaya asema: “[Yehova] amewashusha wakaao juu, mji ule ulioinuka, aushusha, aushusha hata nchi, auleta hata mavumbini. Mguu utaukanyaga chini, naam, miguu yao walio maskini, na hatua zao walio wahitaji.” (Isaya 26:5, 6) Labda mji ulioinuka ambao unatajwa hapa ni Babiloni. Bila shaka mji huo ulitaabisha watu wa Mungu. Lakini ni nini kilichoupata Babiloni? Katika mwaka wa 539 K.W.K. ulishindwa na Wamedi na Waajemi. Kulikuwa kutwezwa kulikoje!
6 Katika siku zetu maneno ya kiunabii ya Isaya yafafanua vizuri kile ambacho kimetukia kwa “Babiloni Mkubwa” tangu mwaka wa 1919. Mji huo ulioinuka ulianguka kwa aibu mwaka huo wakati ulipolazimishwa kuwaachilia watu wa Yehova kutoka utekwa wa kiroho. (Ufunuo 14:8) Jambo lililofuatia liliaibisha hata zaidi. Kikundi hicho kidogo cha Wakristo nacho kikaanza kumkanyagia chini mtekaji wao wa awali. Mwaka wa 1922 walianza kutangaza mwisho unaokuja wa Jumuiya ya Wakristo, wakitangaza hadharani ile mipigo ya tarumbeta ya malaika wanne wa Ufunuo 8:7-12 na zile ole tatu zilizotabiriwa katika Ufunuo 9:1–11:15.
“Njia Yake Mwenye Haki Ni Unyofu”
7. Wale wanaogeukia nuru ya Yehova hupata mwongozo gani, nao humtumaini nani na kuthamini nini?
7 Yehova huwaokoa wale wanaogeukia nuru yake, naye huelekeza njia yao, kama Isaya aendeleavyo kuonyesha: “Njia yake mwenye haki ni unyofu; wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki. Naam, katika njia ya hukumu zako sisi tumekungoja, Ee BWANA; shauku ya nafsi zetu inaelekea jina lako na ukumbusho wako.” (Isaya 26:7, 8) Yehova ni Mungu mwenye haki, na wale wanaomwabudu lazima watii viwango vyake vya uadilifu. Wanapofanya hivyo, Yehova huwaongoza, na kunyoosha njia yao. Kwa kutii mwelekezo wake, wapole hao huonyesha kwamba wanamtumaini Yehova na kuthamini jina lake—“ukumbusho” wake—kwa moyo wote.—Kutoka 3:15.
8. Isaya alionyesha kielelezo gani cha kuigwa kuhusu mtazamo?
8 Isaya alilipenda jina la Yehova. Hilo laonyeshwa waziwazi na maneno yake yafuatayo: “Kwa nafsi yangu nimekutamani wakati wa usiku; naam, kwa nafsi yangu ndani yangu nitakutafuta mapema; maana hukumu zako zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki [“uadilifu,” NW].” (Isaya 26:9) Isaya alimtamani Yehova ‘kwa nafsi yake’ yote. Wazia nabii huyo akitumia wakati wa usiku wenye utulivu kusali kwa Yehova, akimweleza mawazo yake ya ndani zaidi na kutafuta kwa bidii mwongozo wake. Ni kielelezo kizuri kama nini! Isitoshe, Isaya alijifunza uadilifu kutokana na hukumu za Yehova. Kwa njia hiyo, atukumbusha uhitaji wa kuwa macho daima, kuendelea kuwa chonjo ili kufahamu mapenzi ya Yehova.
Wengine Huchagua Giza
9, 10. Yehova alifanya matendo gani ya fadhili kwa taifa lake lisilo na uaminifu, lakini walitendaje?
9 Yehova alionyesha fadhili-upendo kubwa sana kwa Yuda, lakini kwa kusikitisha si wote waliozikubali. Mara nyingi, wengi walichagua uasi-imani badala ya nuru ya kweli ya Yehova. Isaya alisema: “Mtu mbaya ajapofadhiliwa, hata hivyo, hatajifunza haki; katika nchi ya unyofu atatenda udhalimu. Wala hatauona utukufu wa BWANA.”—Isaya 26:10.
10 Katika siku za Isaya Yehova alipolinda Yuda dhidi ya maadui wake, wengi walikataa kutambua jambo hilo. Alipowabariki kwa amani yake, taifa hilo halikuonyesha shukrani. Kwa hiyo, Yehova akawaacha watumikie “mabwana wengine,” hatimaye akaruhusu Wayahudi wapelekwe katika utekwa huko Babiloni mwaka wa 607 K.W.K. (Isaya 26:11-13) Hata hivyo, hatimaye mabaki ya taifa hilo walirudi katika nchi yao wakiwa wametiwa nidhamu.
11, 12. (a) Watekaji wa Yuda walikuwa na tumaini gani? (b) Mwaka wa 1919 watekaji wa awali wa watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walikuwa na tumaini gani?
11 Namna gani watekaji wa Yuda? Isaya ajibu kwa kutoa unabii huu: “Wao wamekufa, hawataishi; wamekwisha [“kufa,” NW], hawatafufuka; kwa sababu hiyo umewajilia, na kuwaangamiza, na kuupoteza ukumbusho wao.” (Isaya 26:14) Ndiyo, baada ya anguko lake mwaka wa 539 K.W.K., Babiloni haukuwa na tumaini lolote. Baada ya muda, mji huo haungekuwapo tena. Ungekuwa ‘umekwisha kufa’ nayo milki yake kubwa ingekuwa imetoweka kabisa. Ni onyo lililoje kwa wale wanaotumaini watu wenye nguvu wa ulimwengu huu!
12 Mambo mbalimbali yanayohusu unabii huo yalitimizwa Mungu alipowaruhusu watumishi wake watiwa-mafuta wapelekwe katika utekwa wa kiroho mwaka wa 1918 kisha akawakomboa mwaka wa 1919. Kuanzia wakati huo na kuendelea, mtekaji wao wa awali hasa Jumuiya ya Wakristo, hakuwa na tumaini lolote. Lakini watu wa Yehova wangepata baraka nyingi kwelikweli.
“Umeliongeza Hilo Taifa”
13, 14. Watumishi watiwa-mafuta wa Yehova wamefurahia baraka gani nyingi tangu 1919?
13 Mungu alibariki mtazamo huo wa toba wa watumishi wake watiwa-mafuta katika mwaka wa 1919 na kuwapa ongezeko. Kwanza, walizingatia kukusanywa kwa washiriki wa mwisho wa Israeli wa Mungu, kisha “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ukaanza kukusanywa. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Baraka hizo zilitabiriwa katika unabii huu wa Isaya: “Umeliongeza hilo taifa, BWANA umeliongeza taifa; wewe umetukuzwa, umeipanua mipaka yote ya nchi hii. BWANA katika taabu zao walikwenda kwako; waliomba maombi mengi wakati adhabu yako ilipokuwa juu yao.”—Isaya 26:15, 16.
14 Leo, mipaka ya Israeli wa Mungu imepanuka na kuenea duniani pote, na umati mkubwa ambao umeongezwa sasa umefikia watu milioni sita wanaoshiriki kwa shangwe kazi ya kuhubiri habari njema. (Mathayo 24:14) Ni baraka iliyoje kutoka kwa Yehova! Hilo huleta utukufu ulioje kwa jina lake! Jina hilo husikiwa leo katika nchi 235—utimizo wa ajabu wa ahadi yake.
15. Ni ufufuo gani wa ufananisho uliotukia mwaka wa 1919?
15 Yuda ilihitaji msaada wa Yehova ili kuponyoka kutoka utekwa wa Babiloni. Hawangeweza kufanya hivyo bila msaada. (Isaya 26:17, 18) Vivyo hivyo, kukombolewa kwa Israeli wa Mungu mwaka wa 1919 kulikuwa ithibati ya utegemezo wa Yehova. Haingeweza kutukia hivyo pasipo msaada wake. Hali yao ilibadilika kwa njia ya kushtusha sana hivi kwamba Isaya aliilinganisha na ufufuo: “Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, nyinyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea, nayo ardhi itawatoa waliokufa.” (Isaya 26:19; Ufunuo 11:7-11) Naam, wale waliokufa ni kana kwamba watazaliwa tena kwa ajili ya utendaji mpya!
Kulindwa Nyakati za Hatari
16, 17. (a) Katika mwaka wa 539 K.W.K., Wayahudi walihitaji kufanya nini ili kuokoka anguko la Babiloni? (b) Huenda “vyumba vya ndani” vyafananisha nini leo, navyo hutunufaishaje?
16 Watumishi wa Yehova wanahitaji ulinzi wake sikuzote. Hata hivyo, hivi karibuni atanyoosha mkono wake mara ya mwisho dhidi ya ulimwengu wa Shetani, nao waabudu wake watahitaji msaada wake kuliko wakati mwingine wowote. (1 Yohana 5:19) Kuhusu wakati huo wa hatari, Yehova atuonya hivi: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako [“vyumba vya ndani,” NW], ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, BWANA anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.” (Isaya 26:20, 21; Sefania 1:14) Onyo hili lilionyesha Wayahudi jinsi ya kuokoka anguko la Babiloni mwaka wa 539 K.W.K. Wale waliotii onyo hilo wangekaa katika nyumba zao, wakiwa salama bila kusumbuliwa na majeshi yenye kushinda yaliyokuwa barabarani.
17 Leo, “vyumba vya ndani” vinavyotajwa katika unabii huo huenda vyafananisha makumi ya maelfu ya makutaniko ya watu wa Yehova ulimwenguni pote. Makutaniko hayo ni ulinzi hata sasa, ni mahali ambapo Wakristo hupata usalama miongoni mwa ndugu zao, chini ya uangalizi wenye upendo wa wazee. (Isaya 32:1, 2; Waebrania 10:24, 25) Ni kweli hasa tunapozingatia jinsi ambavyo mwisho wa mfumo huu wa mambo umekaribia wakati ambapo wokovu utategemea utii.—Sefania 2:3.
18. Yehova ‘atamwuaje yule joka aliye baharini’ hivi karibuni?
18 Kuhusu wakati huo, Isaya atabiri hivi: “Katika siku hiyo BWANA, kwa upanga wake ulio mkali, ulio mkubwa, ulio na nguvu, atamwadhibu lewiathani, nyoka yule mwepesi, na lewiathani, nyoka yule mwenye kuzonga-zonga; naye atamwua yule joka aliye baharini.” (Isaya 27:1) “Lewiathani” wa siku hizi ni nani? Yaonekana, ni “nyoka wa awali,” Shetani mwenyewe, pamoja na mfumo wake mwovu wa mambo, anaotumia kupiga vita dhidi ya Israeli wa Mungu. (Ufunuo 12:9, 10, 17; 13:14, 16, 17) Mwaka wa 1919, Lewiathani alishindwa kuzuia watu wa Mungu. Baada ya muda, atatoweka kabisa. (Ufunuo 19:19-21; 20:1-3, 10) Hivyo, Yehova “atamwua yule joka aliye baharini.” Kwa sasa, chochote ambacho Lewiathani anafanya dhidi ya watu wa Yehova hakitakuwa na mafanikio ya kudumu. (Isaya 54:17) Inafariji kama nini kuhakikishiwa hivyo!
“Shamba la Mizabibu la Mvinyo”
19. Hali ya mabaki ikoje leo?
19 Kwa kuzingatia nuru hii yote kutoka kwa Yehova, je, hatuna kila sababu ya kushangilia? Kwa kweli, ndiyo! Isaya afafanua vizuri shangwe ya watu wa Yehova aandikapo hivi: “Katika siku hiyo; shamba la mizabibu la mvinyo, liimbieni. Mimi, BWANA nalilinda, nitalitia maji kila dakika, asije mtu akaliharibu; usiku na mchana nitalilinda.” (Isaya 27:2, 3) Yehova amelitunza “shamba [lake] la mizabibu” mabaki ya Israeli wa Mungu, na waandamani wao wanaofanya kazi kwa bidii. (Yohana 15:1-8) Matokeo yamekuwa kwamba kumekuwa na matunda yaletayo utukufu kwa jina lake na kufanya watumishi wake duniani washangilie sana.
20. Yehova hulindaje kutaniko la Wakristo?
20 Twaweza kufurahi kwamba hasira ambayo Yehova alikuwa nayo hapo awali dhidi ya watumishi wake watiwa-mafuta—iliyomfanya aruhusu wapelekwe katika utekwa wa kiroho mwaka wa 1918—imekoma. Yehova mwenyewe asema hivi: “Hasira sinayo ndani yangu; kama mibigili na miiba [“magugu,” NW] ingekuwa mbele zangu, ningepanga vita juu yake, ningeiteketeza yote pamoja. Au azishike nguvu zangu, afanye amani nami; naam, afanye amani nami.” (Isaya 27:4, 5) Ili kuhakikisha kwamba shamba lake la mizabibu litaendelea kutoa “mvinyo” kwa wingi, Yehova huvunja-vunja na kuharibu uvutano wowote ulio kama magugu unaoweza kuwapotosha. Kwa hiyo, mtu yeyote asihatarishe hali njema ya kutaniko la Kikristo! Acheni wote ‘wazishike nguvu za Yehova,’ wakitafuta kibali na ulinzi wake. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa na amani na Mungu—jambo lililo muhimu sana hivi kwamba Isaya analitaja mara mbili.—Zaburi 85:1, 2, 8; Waroma 5:1.
21. Ni katika njia gani uso wa ulimwengu umejazwa “matunda”?
21 Baraka zaendelea: “Siku zijazo Yakobo atatia mizizi; Israeli atatoa maua na kuchipuka; nao watajaza uso wa ulimwengu matunda.” (Isaya 27:6) Mstari huo umetimizwa tangu 1919, ukionyesha uthibitisho wa ajabu wa nguvu za Yehova. Wakristo watiwa-mafuta wameijaza dunia “matunda,” chakula cha kiroho chenye lishe. Katikati ya ulimwengu mpotovu, wanategemeza kwa shangwe viwango vya Mungu. Naye Yehova anaendelea kuwabariki kwa ongezeko. Kwa sababu hiyo, mamilioni ya waandamani wao, kondoo wengine, “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku.” (Ufunuo 7:15) Acheni tusipuuze kamwe pendeleo kubwa tulilo nalo la kula “matunda” na kuwapa wengine!
22. Wale wanaokubali nuru hupata baraka gani?
22 Katika nyakati hizi zenye hatari, wakati ambapo giza linaifunika dunia na giza kuu kufunika kabila za watu, je, hatushukuru kwamba Yehova anaangazia watu wake nuru ya kiroho? (Isaya 60:2; Waroma 2:19; 13:12) Kwa wote wanaoikubali, nuru hiyo yamaanisha amani ya akili na shangwe sasa na hata uhai udumuo milele wakati ujao. Basi, ni kwa sababu nzuri kwamba sisi ambao tunapenda nuru twainua mioyo yetu kumsifu Yehova na kujiunga na mtunga-zaburi kusema: “BWANA ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani? Umngoje BWANA, uwe hodari, upige moyo konde, naam, umngoje BWANA.”—Zaburi 27:1b, 14.
-