Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tsunami ya 2011 Nchini Japani—Masimulizi Kutoka kwa Waokokaji
    Amkeni!—2011 | Desemba
    • Mashirika kadhaa yaliwasaidia watu wao. Mashahidi wa Yehova walifanya hivyo pia. Punde baada ya tetemeko la nchi na tsunami kutokea Ijumaa alasiri, Mashahidi walianza kuwatafuta wale ambao wanakutana pamoja nao kwa ajili ya ibada. Hata hivyo, katika sehemu nyingi barabara hazingeweza kupitika, na huduma za umeme na za simu zilikuwa zimekatwa. Ilikuwa vigumu sana kuwapata watu katika eneo hilo kubwa lililoathiriwa.

      Takayuki, mmoja wa wazee katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova huko Soma, Wilaya ya Fukushima, angeweza kuwasiliana na familia chache tu alasiri hiyo ya Ijumaa. “Niliamua kuwatafuta wengine siku iliyofuata,” akasema. “Alfajiri, nilienda kwa gari kisha nikaenda kwa miguu ili kuwatafuta na nikaendelea hadi jioni. Nilienda kwenye maeneo 20, kutia ndani vituo mbalimbali, ili kuwatafuta washiriki wa kutaniko. Nilipowapata, nilisoma maandiko na kusali pamoja nao.”

      Shunji, huko Ishinomaki, anaeleza: “Tulianzisha vikundi mbalimbali vya kuwatafuta waumini wenzetu. Tulipofika kwenye eneo lililokumbwa na msiba tulibaki mdomo wazi. Magari yalikuwa yakining’inia juu ya milingoti ya umeme, nyumba zilikuwa zimelaliana, na marundo ya maporomoko yalikuwa makubwa kuliko nyumba zenyewe. Juu ya gari moja, tuliona mwili wa mtu, ambaye huenda alishindwa kustahimili baridi ya usiku. Gari lingine lilikuwa likining’inia juu chini katikati ya nyumba mbili. Kulikuwa na mwili wa mtu ndani yake.”

      Shunji alifurahi kuwapata waumini wenzake katika vituo mbalimbali. “Nilipowaona,” anasema, “nilitambua jinsi ninavyowapenda sana.”

      “Mmekuja Haraka Sana!”

      Wasichana wawili Mashahidi, Yui na Mizuki, walikuwa majirani huko Minamisanriku, Miyagi. Tetemeko la kwanza lilipokwisha, walikimbia nje na wakakutana. Walikimbilia eneo lililoinuka. Hazikupita dakika kumi walipoona mji wote, kutia ndani nyumba zao, ukifagiliwa na wimbi moja baada ya lingine.

      Yui na Mizuki waliwapata marafiki ambao ni Mashahidi katika kituo fulani na wakasali pamoja. Siku iliyofuata, washiriki wa kutaniko lao na wengine wa kutaniko jirani walisafiri kuvuka mlima ili kuwaletea chakula na vitu vingine. Yui na Mizuki wakasema, “Tulijua mtakuja, lakini mmekuja haraka sana!”

      Hideharu, mmoja wa waangalizi wa Mashahidi katika Kutaniko la Tome alitembelea kituo hicho. Anaeleza hivi: “Usiku mzima nilijaribu kuwatafuta ndugu zetu wanaoishi ufuoni. Mwishowe, saa 10 usiku nikapata habari kuhusu shule fulani ambako watu walikuwa wamekimbilia. Saa moja asubuhi, tukiwa kikundi cha watu kumi tulikutana ili kupika wali na mimi pamoja na wengine wawili tuliondoka kwa gari ili kupeleka chakula hicho. Barabara nyingi hazingeweza kupitika. Baada ya jitihada nyingi, tulifika kwenye shule hiyo. Hata wale waliokuwa wamepoteza nyumba zao waliungana nasi kuwasaidia wengine.”

      Kutosheleza Uhitaji wa Kiroho

      Mashahidi wa Yehova hukutana kwa ukawaida ili kujifunza Biblia, na makutaniko mengine hukutana Ijumaa usiku ili kufanya hivyo. Huko Rikuzentakata wao hukutana jioni hiyo; hata hivyo, Jumba la Ufalme—jengo ambalo Mashahidi hutumia kwa ajili ya mikutano yao—lilikuwa limefagiliwa na tsunami. “Si tufanye mkutano,” akasema Shahidi mmoja. Kwa hiyo, nyumba moja ambayo haikuwa imeharibiwa sana ikachaguliwa, na washiriki wa kutaniko wakajulishwa.

      Ingawa umeme ulikuwa umekatwa, jenereta ilitumiwa kutokeza mwangaza. Watu kumi na sita walihudhuria. “Tulilia kwa shangwe,” anakumbuka kijana anayeitwa Yasuyuki, ambaye nyumba yake ilisombwa na tsunami hiyo. “Hilo ndilo lililokuwa kimbilio bora zaidi kwetu.” Hideko anasema: “Matetemeko mengine madogo yaliyotukia baadaye yalitusumbua mkutano ulipokuwa ukiendelea, lakini tulipokuwa pamoja, nilisahau hofu na wasiwasi niliokuwa nao.”

      Tangu wakati huo, kutaniko hilo halijakosa kamwe kufanya hata mkutano mmoja. Siku mbili baadaye, Jumapili, kichwa cha hotuba ya watu wote iliyochaguliwa kwa ajili ya siku hiyo kilikuwa “Udugu wa Ulimwenguni Pote Waokolewa Kutoka Afa.”

      Kazi ya Kutoa Msaada kwa Utaratibu

      Mashirika kadhaa ya serikali yalianza kazi ya kutoa msaada, na pia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ambayo inapatikana huko Ebina, karibu na Tokyo, ilianza kufanya hivyo. Kufikia Jumamosi, siku iliyofuata tetemeko la nchi, ofisi ya tawi ilikuwa imegawanya eneo kubwa lililokumbwa na tetemeko hilo katika sehemu tatu. Jumatatu, siku tatu baada ya tetemeko hilo la nchi, wawakilishi kutoka kwenye ofisi ya tawi walitembelea maeneo hayo.

      Jitihada za kutoa msaada ziliendelea kwa majuma na miezi kadhaa iliyofuata. Tani nyingi za msaada zilizotolewa na Mashahidi zimegawanywa. Wakati mmoja kulikuwa na vituo 3 vya kutoa msaada, mabohari 21 na vituo vingine vilikuwa vikitoa msaada uliohitajika. Katika miezi miwili ya kwanza, mamia ya wajitoleaji waligawa zaidi ya tani 250 za chakula, mavazi, na vitu vingine vilivyohitajika. Mashahidi wengi waliwagawia majirani wao vitu walivyopata.

      Washiriki wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Rikuzentakata na kutaniko jirani la Ofunato wanatumia Jumba lao la Ufalme lililojengwa upya ili kuwaimarisha watu kiroho. Hilo litawasaidia watu kukabiliana na magumu wanayopata wakijaribu kuanza upya maisha yao na kupona kutokana na huzuni waliyopata kutokana na tetemeko la nchi na tsunami hiyo. Kati ya Mashahidi zaidi ya 14,000 wanaoishi katika eneo lililokumbwa na msiba, 12 walikufa na 2 hawajawahi kupatikana.

      Wengi kati ya Mashahidi wa Yehova walioathiriwa na msiba huo mkubwa walisema maneno kama haya yaliyosemwa na familia moja: “Tulipokimbia, kila mmoja wetu alikuwa na mfuko mmoja tu. Lakini mahitaji yetu yote yalishughulikiwa na waumini wenzetu.” Inafurahisha kama nini kwamba watumishi wa Mungu wa kweli, Yehova, wanaweza kufurahia undugu wa ulimwenguni pote ambao Yesu na mitume wake walizungumzia! Undugu huo hauwezi kuvunjwa na tsunami au msiba mwingine wowote wa asili.—Yohana 13:34, 35; Waebrania 10:24, 25; 1 Petro 5:9.

  • Tsunami ya 2011 Nchini Japani—Masimulizi Kutoka kwa Waokokaji
    Amkeni!—2011 | Desemba
    • [Picha katika ukurasa wa 19]

      Wafanyakazi wakitoa msaada

      [Picha katika ukurasa wa 20]

      Jumba la Ufalme la Rikuzentakata baada ya “tsunami”

      [Picha katika ukurasa wa 20]

      Kazi ya ujenzi miezi mitatu baadaye

      [Picha katika ukurasa wa 20]

      Jumba la Ufalme lililokamilishwa

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki