Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unapotishwa
    Amkeni!—2001 | Agosti 22
    • Unapotishwa

      “Nina kisu! Nyamaza, au nikuue!”

      ILIKUWA alasiri nzuri ya kiangazi. Jane,a mwenye umri wa miaka 17 ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alikuwa anacheza kwa kuteleza kwa viatu vya magurudumu katika bustani moja ya umma kule Virginia, Marekani. Ghafula ilionekana kana kwamba yeye pekee ndiye alibaki bustanini, akaamua kuondoka. Alipokuwa ameketi karibu na gari dogo la familia yao na kutoa viatu vya magurudumu, mtu fulani alimkaribia. Kwa maneno yenye kutisha yaliyo juu, huyo mtu alionyesha kwamba alitaka kufanya ngono na Jane, akajaribu kumsukuma ndani ya gari. Jane alipiga mayowe, lakini hakuacha kumshambulia.

      ‘Nilijisikia mdogo sana, kana kwamba nilikuwa mdudu na yeye alikuwa jitu,’ Jane alisema baadaye. “Lakini niliendelea kupiga mayowe na kupambana naye. Mwishowe nilimlilia Mungu kwa kusema, ‘Yehova, usimruhusu anitende hivyo!’” Inaonekana kwamba maneno hayo yalimshtua mtu huyo, kwa kuwa alimwachilia ghafula na kukimbia.

      Mtu huyo aliyejaribu kumbaka Jane aliingia katika gari lake, naye Jane alijifungia katika gari lake akitetemeka. Alijilazimisha kutulia, akachukua simu ya mkononi. Akapigia polisi simu, na mshukiwa akakamatwa baada ya dakika chache tu kwa kuwa Jane aliweza kufafanua vizuri gari lake na namba yake.

      Je, Mwisho Ulikuwa Mzuri?

      Ndiyo, lakini si mara moja. Mateso ya Jane yalikuwa yameanza tu. Jane alisifiwa na polisi na katika magazeti kwa sababu ya kutenda bila kuchelewa na bila kuvurugika akili. Hata hivyo, baada ya mshtuko kwisha, Jane alihisi kwamba amevurugika akili kwelikweli. Anasema hivi: ‘Baada ya majuma machache nilianza kuwa na mfadhaiko. Nilikuwa na hofu ya daima iliyonizuia nisipate usingizi. Hata baada ya majuma kadhaa nilishindwa kujifunza au kuwa makini. Nilishikwa pia na hofu ya ghafula. Siku moja nilishtuka sana shuleni, mwanafunzi mwenzangu, anayefanana kidogo na yule mtu aliyenishambulia, aliponishika begani ili aniulize ni saa ngapi.’

      Anasema hivi: ‘Nilishuka moyo sana. Niliacha kushirikiana na marafiki wangu, na upweke ulifanya nishuke moyo hata zaidi. Nilijilaumu kwa kuruhusu shambulio hilo, na nilihuzunika sana kwa kuwa sikuweza tena kuwa mwenye furaha na tumaini vile nilivyokuwa kabla ya shambulio hilo. Nilihisi kana kwamba nilikuwa mtu tofauti.’

      Jane aliathiriwa na dalili za kawaida za mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha. Mfadhaiko huo ni nini, na wale wanaougua wanaweza kusaidiwaje? Sehemu inayofuata itajibu maswali hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Jina limebadilishwa.

  • Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha Ni Nini?
    Amkeni!—2001 | Agosti 22
    • Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha Ni Nini?

      MIAKA MINGI ILIYOPITA, mfadhaiko huo ulichunguzwa hasa ulipowaathiri maaskari waliostaafu vitani waliopatwa na ugonjwa wa akili kwa sababu ya mshtuko wakati wa vita.a Leo hali imebadilika. Si lazima uwe askari ili utambuliwe kuwa na hali hiyo. Ikiwa tu umenusurika kwenye tukio lenye kutisha waweza kupatwa na hali hiyo.

      Matukio kama vita, shambulio la mbakaji, au aksidenti ya gari, na kadhalika yanaweza kusababisha hali hiyo. Hati inayotaarifu juu ya hali hiyo kutoka kwa Kitovu cha Taifa cha Mfadhaiko wa Tukio Lenye Kutisha, huko Marekani, yasema hivi: “Mtu aliye na tatizo hilo lazima awe amepatwa na tukio lenye kutisha.” Na lazima awe “amejeruhiwa au kutishwa kujeruhiwa KIMWILI.”

      Jane, aliyetajwa katika sehemu iliyotangulia asema hivi: “Nimejifunza kwamba tisho la ghafula hufanya homoni fulani ziongezeke ghafula, na homoni hizo hufanya mtu awe macho kutambua hatari. Kwa kawaida homoni hizo hurudia kiwango cha kawaida baada ya hatari kupita, lakini kiwango cha homoni hizo huendelea kuwa juu katika wale walio na mfadhaiko huo.” Tukio hilo lilikuwa limepita, lakini hofu kubwa ya kipindi hicho ilidumu katika akili ya Jane kama vile mpangaji asiyetakikana anavyokataa kuondoka katika nyumba, japo ameambiwa aondoke.

      Ikiwa umenusurika kwenye tukio lenye kutisha na unahisi mifadhaiko hiyo, ni muhimu kukumbuka kwamba wengine pia wana hisia kama hizo. Katika kitabu ambacho aliandika kuhusu ubakaji mwandishi Linda E. Ledray alisema kwamba mfadhaiko huo, “ni hali ya kawaida katika watu wa kawaida ambao wamepatwa na tukio lenye kutisha ambalo walishindwa kulizuia.”

      Hata hivyo, ijapokuwa hisia hizo ni za kawaida haimaanishi kwamba kila mtu anayenusurika kwenye tukio lenye kutisha atakuwa nazo. Ledray anasema hivi: “Uchunguzi mmoja wa mwaka wa 1992 unaonyesha kwamba, asilimia 94 ya wale waliobakwa walikuwa na mfadhaiko huo juma moja baada ya tukio hilo, na asilimia 12 waliendelea kuwa nao baada ya majuma 47. Asilimia 50 ya wanawake waliotibiwa kwenye kituo cha Kuhudumia Walioshambuliwa Kingono cha Minneapolis mwaka wa 1993 walikuwa na mfadhaiko huo mwaka mmoja baada ya kubakwa.”

      Si watu wengi wanaotambua kwamba hali hiyo ni ya kawaida sana kama vile taarifa hiyo inavyoonyesha. Na watu wa aina zote wanaweza kukumbwa na mfadhaiko huo, na unaweza kusababishwa na matukio ya aina mbalimbali. Waandishi Alexander C. McFarlane na Lars Weisaeth wanasema hivi: “Uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba matukio yenye kutisha yanaathiri watu wakati wa amani, na vilevile maaskari wa vita, na huonyesha vilevile kwamba wale wanaoathiriwa na vita, na wengi wanaonusurika kwenye matukio hayo ya kawaida hupatwa na mfadhaiko huo.” Mara nyingine hali hiyo imesababishwa na tiba mbalimbali na mshtuko wa moyo.

      Waandishi walionukuliwa hapo juu wanaeleza kwamba “mfadhaiko huo ni wa kawaida sana siku hizi.” Na wanaongeza kusema hivi: “Uchunguzi wa vijana Wamarekani 1,245 ulionyesha kwamba asilimia 23 ya vijana hao walikuwa wametendwa vibaya kimwili au kingono, na pia walikuwa wameshuhudia wengine wakitendwa kwa ukatili. Mmoja kati ya vijana watano alishikwa na mfadhaiko. Hiyo inadokeza kwamba vijana Wamarekani milioni 1.07 hivi wanapatwa na hali hiyo.”

      Kwa hiyo, ikiwa taarifa hiyo ni sahihi, inamaanisha kwamba kuna vijana wengi wanaoteseka katika nchi hiyo moja tu! Vijana hao na vilevile mamilioni wengine wanaoteseka kotekote duniani wanaweza kusaidiwaje?

      Suluhisho Ni Nini?

      Ikiwa unafikiri kwamba wewe au mtu fulani unayemjua ana mfadhaiko huo, madokezo yanayofuata huenda yakasaidia.

      Jitahidi kuwa na mpango wa kiroho wa kila siku. Jane anasema hivi: “Sikuzote nilihudhuria mikutano kwenye Jumba letu la Ufalme. Nilijua kwamba Yehova Mungu alitaka niwe mkutanoni hata niliposhindwa kuelekeza fikira kwenye habari iliyozungumziwa. Ndugu na dada kutanikoni walionyesha upendo na kunitia moyo sana. Na nilithamini sana upendo wao na jinsi walivyonijali muda wote nilipoteseka. Jane anaongeza kusema: “Kusoma zaburi mbalimbali kulinisaidia pia. Ni kana kwamba sala katika zaburi hizo za wale walioteseka zilisema kwa niaba yangu. Niliposhindwa kusema kile nilichotaka kusema katika sala niliweza kusema tu ‘Ameni.’”

      Mtie moyo yule anayeteseka. Ikiwa mpendwa wako anafadhaika kupita kiasi kwa sababu ya kumbukumbu mbaya ya tukio lenye kutisha, fahamu kwamba yeye hana hisia hizo kwa sababu anataka kusumbua. Huenda hataweza kuonyesha uthamini unapojitahidi kumsaidia kwa sababu hisia zake zimekufa ganzi, au kwa sababu ya wasiwasi au hasira. Lakini usife moyo! Biblia yasema hivi: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.”—Mithali 17:17.

      Mwenye kuteseka apaswa kuwa macho na kuepuka mazoea yote yasiyo ya hekima yanayoweza kumdhuru anapojitahidi kuvumilia hali yake. Mazoea hayo yatia ndani utumizi wa dawa za kulevya au kutumia vileo kupita kiasi. Ijapokuwa matumizi ya dawa za kulevya na vileo yanaweza kutuliza kwa muda, punde si punde hufanya tatizo lizidi. Kwa kawaida hufanya mtu ajitenge na wengine, akataliwe na watu wanaotaka kusaidia; huchangia pia mtu kufanya kazi kupita kiasi; hasira isiyothibitiwa; kula kupita kiasi au kutokula, au tabia nyingine za kujiumiza au hata kujiua.

      Omba ushauri kutoka kwa mtaalamu stadi wa tiba. Huenda ikawa mwenye kuteseka hana mfadhaiko wa aina hiyo, lakini ikiwa anao, kuna matibabu yanayofanya kazi.b Ikiwa unatibiwa na daktari mwombe msaada ili kushinda tabia zozote zilizotajwa juu.

      Kumbuka: Mara nyingi majeraha ya mwili hupona kwanza, lakini watu wanaougua mfadhaiko huo, huenda wamejeruhiwa kwa njia nyingi kimwili, kiakili na kihisia. Sehemu inayofuata itazungumzia yale ambayo mwenye mfadhaiko anaweza kufanya, na jinsi wengine wanavyoweza kumsaidia kupona, na itazungumzia vilevile tumaini kwa wote walio na mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha.

      [Maelezo ya Chini]

      a Soma “Do They Come Back the Same?” (Je, Wanaporudi Watakuwa Wamebadilika?), na “He Came Back a Stranger” (Alirudi Akiwa Amebadilika Sana), katika toleo la Kiingereza la Amkeni! la Agosti 8, 1982.

      b Mashahidi wa Yehova hawapendekezi matibabu yoyote ya kimwili wala ya akili.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

      Dalili za Mfadhaiko Unaosababishwa na Tukio Lenye Kutisha

      Wengi walionusurika tukio lenye kutisha wanarudia-rudia tukio hilo akilini. Kwa kawaida hawawezi kujizuia wasifanye hivyo. Huenda matokeo yakawa:

      • Kumbukumbu za ghafula za tukio hilo—kuhisi kana kwamba linatukia tena

      • Ndoto zenye kuhofisha

      • Tabia ya kushtuka sana kwa sababu ya kelele au mtu anapowakaribia ghafula kutoka nyuma

      • Kutetemeka na kutoa jasho

      • Moyo kupiga-piga na tatizo la kupumua

      • Kuvurugika akili wakati wanapokumbushwa tukio hilo kwa kuona, kusikia, kuhisi, kunusa, au kuonja kitu fulani

      • Wasiwasi au hofu—kuhisi kwamba wamo hatarini tena

      • Kushindwa kujizuia kwa kuwa kumbukumbu zinasababisha wasiwasi, mvurugo, au hasira za ghafula

      • Kushindwa kuwa makini au kufikiri vizuri

      • Kushindwa kupata usingizi au kulala vizuri

      • Wasiwasi na hali ya kuwa macho daima

      • Hisia za moyoni zilizo kufa ganzi

      • Ugumu wa kupenda wengine au kuwa na hisia za moyoni zenye nguvu

      • Kuhisi kwamba mahali wanapoishi pamebadilika au si halisi

      • Kutopendezwa na mambo waliyopenda mbeleni

      • Kushindwa kukumbuka mambo muhimu ya tukio hilo

      • Kuhisi kwamba hawahusiki na maisha wala na mambo yanayowapata

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Matukio mbalimbali yenye kutisha yanaweza kusababisha mfadhaiko

  • Mfadhaiko Utakoma
    Amkeni!—2001 | Agosti 22
    • Mfadhaiko Utakoma

      HUENDA wewe ni mwanajeshi aliyestaafu na husumbuliwa na ndoto zinazotisha na kumbukumbu za ghafula, ambazo hufanya uhisi kana kwamba vita inaendelea hata leo. Huenda umetendwa kwa ukatili kama vile kubakwa na unahisi kana kwamba sehemu fulani ndani yako imekufa kwa sababu ya tisho hilo. Au huenda mpendwa wako alikufa katika msiba wa asili au aksidenti na maisha bila huyo mpendwa ni magumu sana.

      Je, unajiuliza ikiwa hisia hizo zinaweza kwisha? Tunaweza kujibu kwa uhakika kwamba: Ndiyo, zinaweza kwisha! Kwa sasa, wote wanaoathiriwa na tukio lenye kutisha wanaweza kupata faraja kutokana na Neno la Mungu, Biblia.

      Tunaweza Kusaidiwa Kuvumilia Mfadhaiko Huo

      Karibu miaka elfu mbili iliyopita, mtume Paulo alipitia matukio yenye kutisha yaliyohatarisha maisha yake. Maelezo yake ya baadhi ya matukio hayo yamo katika Biblia. Aliandika hivi: “Hatutaki nyinyi mwe wasio na ujuzi, akina ndugu, juu ya dhiki iliyotupata katika wilaya ya Asia, kwamba tulikuwa chini ya mkazo mkali mno upitao nguvu yetu, hivi kwamba tulikuwa bila hakika kabisa hata juu ya uhai wetu. Kwa kweli, tulihisi ndani yetu wenyewe kwamba tulikuwa tumeipokea hukumu ya kifo.”—2 Wakorintho 1:8, 9.

      Ijapokuwa hatujui yote yaliyotukia, bila shaka pindi hiyo ilikuwa yenye kutisha. (2 Wakorintho 11:23-27) Paulo alivumiliaje hali hiyo?

      Anapotafakari tukio hilo lenye kutisha alilopitia huko Asia, Paulo aliandika hivi: “Mbarikiwa na awe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo kwayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

      Naam, “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote,” atawasaidia wote wanaonusurika kwenye tukio lenye kutisha. Unawezaje kupata msaada huo?

      Jinsi ya Kupata Msaada

      Kwanza—omba msaada. Ikiwa hisia zako zote zimekufa ganzi kumbuka kwamba wengine wamepatwa na hali hiyo pia. Wale ambao wameshinda hali hiyo kwa kawaida hufurahia kuwasaidia wengine. Mara nyingi hao huhisi jinsi mtume Paulo alivyohisi kwamba inawabidi kushiriki faraja waliyokuwa wamepokea kutoka kwa Mungu wakati wa majaribu yao pamoja na “wale walio katika namna yoyote ya dhiki.” Usikawie kuzungumza na mmoja wa Mashahidi wa Yehova—yeyote ambaye unaweza kuongea naye kwa uhuru—na kuomba akusaidie kupata msaada kutoka kwa Yehova, “Mungu wa faraja yote.”

      Dumu katika sala. Ikiwa unaona ugumu kutoa sala kwa sababu ya hasira, omba mtu aliyekomaa kiroho atoe sala pamoja nawe. (Yakobo 5:14-16) Unaposema na Yehova Mungu katika sala, usisahau ‘kutupa hangaiko lako lote juu yake, kwa sababu anakujali.’ (1 Petro 5:7) Mara nyingi Maandiko huonyesha kwamba Mungu anajali kila mmoja wa watumishi wake.

      Yamkini mwandishi wa Zaburi ya 94 alikuwa amepitia tukio lenye kutisha kwa kuwa aliandika hivi: “Kama BWANA asingalikuwa msaada wangu, nafsi yangu kwa upesi ingalikaa penye kimya. Niliposema, Mguu wangu unateleza; Ee BWANA, fadhili zako zilinitegemeza. Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.”—Zaburi 94:17-19.

      Baadhi ya watu walio na mfadhaiko uliosababishwa na tukio lenye kutisha wanasumbuliwa hasa na “wingi wa mawazo,” ambayo nyakati nyingine yanaweza kusababisha hofu au hasira kubwa zenye kulemea. Hata hivyo, sala kutoka moyoni inaweza ‘kukutegemeza’ hadi hisia hizo zipite. Mwone Yehova kuwa mzazi mwenye upendo na ujione mwenyewe kuwa mtoto mchanga ambaye Yehova anamlinda kwa upendo. Kumbuka ahadi hii ya Biblia: “Amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:7.

      Mtu hupona hatua kwa hatua iwe ni kimwili, kiakili, au kiroho. Kwa hiyo, wale wenye mfadhaiko mbaya kwa sababu ya matukio yenye kutisha hawapaswi kutarajia kupata amani ya akili mara moja tu wanaposali. Hata hivyo, kudumu katika sala ni muhimu. Kutamsaidia anayeteseka asilemewe kabisa na kukata tamaa.

      Soma na utafakari Neno la Mungu. Ikiwa huwezi kuelekeza fikira, omba mtu mwingine asome pamoja nawe masimulizi ya Biblia yanayofariji. Unaweza kuchagua masimulizi yanayoonyesha jinsi Yehova anavyowahurumia waaminifu wake, haidhuru wameshuka moyo au kukata tamaa kadiri gani.

      Jane, aliyetajwa mapema, alifarijika aliposoma sehemu nyingi za Biblia za kitabu cha Zaburi. Hizo zinatia ndani Zaburi 3:1-8; 6:6-8; 9:9, 10; 11:1-7; 18:5, 6; 23:1-6; 27:7-9; 30:11, 12; 31:12, 19-22; 32:7, 8; 34:18, 19; 36:7-10; 55:5-9, 22; 56:8-11; 63:6-8; 84:8-10; 130:1-6. Usisome sehemu nyingi za Biblia kwa wakati mmoja. Badala yake, chukua muda kuzitafakari na kusali.

      Mfadhaiko Usio na Kifani wa Siku Hizi

      Kwa kusikitisha, haipasi kutushangaza kwamba ubakaji, mauaji, vita, na ujeuri usio wa lazima, zinazidi leo. Kwa nini? Kwa sababu Yesu Kristo alisema kwamba katika wakati wetu kungekuwa na ‘ongezeko la uasi-sheria.’ Aliongeza kusema hivi: “Upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.”—Mathayo 24:7, 12.

      Mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha umekuwa jambo la kawaida sana katika miaka ya majuzi, na mara nyingi unasababishwa na matukio yale ambayo Yesu alitabiri. Kama vile Biblia inavyoonyesha katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21, Yesu alisema kwamba katika siku za mwisho za ulimwengu huu, kungekuwapo vita vya kimataifa, misiba ya asili, ongezeko la uhalifu, na ukosefu wa upendo. Hata hivyo, Yesu alionyesha pia kwamba faraja iko karibu.

      Baada ya kuonyesha ongezeko la duniani pote la matukio yenye kutisha na mwanzo wa “dhiki kubwa” ambayo ingefuata, sikiliza kile ambacho Yesu aliwaambia watu wafanye: “Jisimamisheni wenyewe wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.” (Mathayo 24:21-31; Luka 21:28) Ndiyo, hali ya ulimwengu inapozidi kuwa ngumu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba dhiki kubwa itakayokuja juu ya mfumo huu wenye kusababisha mfadhaiko itamaliza uovu wote ili mfumo mpya wenye uadilifu uanze.—1 Yohana 2:17; Ufunuo 21:3, 4.

      Hatupaswi kushangaa kwamba wokovu wetu utakuja tu baada ya uovu na ujeuri kufikia upeo wake. Hivyo ndivyo ilivyokuwa wakati Mungu alipohukumu ulimwengu wa siku za Noa na wakazi waovu wa Sodoma na Gomora. Hukumu hizo za kale za Mungu zaonyesha jinsi atakavyotekeleza hukumu wakati ujao.—2 Petro 2:5, 6.

      Mwisho wa Mfadhaiko

      Ikiwa unaugua mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha, huenda ukajiuliza ikiwa kumbukumbu zako zenye kuumiza zitakwisha kamwe. Jibu la hakika ni: Ndiyo, zitakwisha! Katika andiko la Isaya 65:17, Yehova Mungu anasema hivi: “Maana, tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Italiki ni zetu.) Ijapokuwa mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha unaonekana kuwa wa kudumu, andiko hili latuonyesha kwamba siku moja hautakuwapo tena.

      Leo, mwaka mmoja baada ya kushambuliwa na mbakaji, Jane anatumikia kama mhudumu painia (mweneza-Injili wa wakati wote) wa Mashahidi wa Yehova. ‘Nilirudia hali yangu ya kawaida baada ya kesi tu na baada ya yule aliyenishambulia kupatikana na hatia—zaidi ya miezi minane baada ya shambulio hilo. Mwaka mmoja uliopita sikuweza kuwazia amani na furaha niliyo nayo sasa. Ninamshukuru Yehova kwa tumaini la ajabu la kuishi milele na fursa ya kushiriki tumaini hilo na wengine,’ alisema hivi majuzi.—Zaburi 27:14.

      Ikiwa wewe unapambana na majonzi na mfadhaiko unaotokana na tukio lenye kutisha, tumaini hilo linaweza kukuimarisha vilevile.

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kunaweza kukusaidia kuvumilia hali

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      Kusoma Neno la Mungu na kutoa sala kunaweza kukuimarisha

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      Mfadhaiko wote utaondolewa hivi karibuni

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki