-
Yehova Awaremba Watu Wake kwa Kuwapa NuruMnara wa Mlinzi—2002 | Julai 1
-
-
Yehova Awaremba Watu Wake kwa Kuwapa Nuru
“Ondoka [“inuka,” “NW”], uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa BWANA umekuzukia.”—ISAYA 60:1.
1, 2. (a) Hali ya wanadamu ikoje? (b) Ni nani wanaosababisha giza la wanadamu?
“LAITI tungekuwa na mtu kama Isaya au Mtakatifu Paulo!” Hivyo ndivyo Rais Harry Truman wa Marekani alivyoomboleza kule nyuma katika miaka ya 1940. Kwa nini alisema hivyo? Ni kwa sababu aliona uhitaji wa kuwa na viongozi wenye maadili bora ulimwenguni katika siku zake. Wanadamu walikuwa wamepitia kipindi cha giza zito lisilo na kifani katika karne ya 20, yaani, vita ya pili ya ulimwengu. Lakini, ingawa vita hiyo ilikuwa imekwisha, ulimwengu haukuwa na amani, giza liliendelea. Naam, hata sasa, miaka 57 baada ya vita hiyo, bado ulimwengu umo gizani. Kama Rais Truman angekuwa hai leo, bila shaka bado angeona uhitaji wa kuwa na viongozi wenye maadili kama Isaya au mtume Paulo.
2 Iwe Rais Truman alijua au hakujua, mtume Paulo alizungumzia giza linalowakumba wanadamu, naye alitoa onyo kulihusu katika maandiko yake. Kwa mfano, aliwaonya waamini wenzake hivi: “Tuna kushindana mwereka, si dhidi ya damu na mwili, bali dhidi ya serikali, dhidi ya mamlaka, dhidi ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Waefeso 6:12) Kwa maneno hayo Paulo alionyesha kwamba mbali na kutambua giza la kiroho linalofunika ulimwengu, alijua pia chanzo chake, yaani, mashetani wenye nguvu wanaofafanuliwa kuwa “watawala wa ulimwengu.” Basi, ikiwa viumbe wa roho wenye nguvu ndio chanzo cha giza hili, wanadamu wanaweza kufanya nini ili kuliondoa?
3. Licha ya giza linalokumba wanadamu, Isaya alitabiri nini kuhusu waaminifu?
3 Isaya pia alitaja giza linalowakumba wanadamu. (Isaya 8:22; 59:9) Hata hivyo, Isaya alipotabiri kuhusu siku zetu, Mungu alimwongoza kuandika kwamba hata katika siku hizi zenye giza, Yehova angewapa tumaini wale wanaopenda nuru. Ndiyo, ijapokuwa Paulo na Isaya hawako leo, maandishi yao yanaweza kutuongoza. Ili tuone jinsi Maandiko hayo ni baraka kwa wale wanaompenda Yehova, na tuchunguze maneno ya kiunabii ya Isaya katika sura ya 60 ya kitabu chake.
Mwanamke wa Kiunabii Aangaza Nuru
4, 5. (a) Yehova anamwamuru mwanamke afanye nini, naye anatoa ahadi gani? (b) Sura ya 60 ya Isaya ina habari gani yenye kusisimua?
4 Mwanamke aliye katika hali mbaya sana ndiye anayeambiwa maneno ya kwanza ya sura ya 60 ya Isaya. Amelala chini kifudifudi katika giza tititi. Ghafula, nuru inalipenya lile giza, naye Yehova anaita kwa sauti kubwa: “Ondoka [“inuka,” NW], uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, na utukufu wa BWANA umekuzukia.” (Isaya 60:1) Wakati umewadia kwa mwanamke huyo kusimama ili aangaze nuru ya Mungu, yaani, utukufu wake. Kwa nini? Tunapata jibu katika mstari unaofuata: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu; bali BWANA atakuzukia wewe, na utukufu wake utaonekana juu yako.” (Isaya 60:2) Mwanamke huyo anapotii agizo la Yehova anahakikishiwa kwamba kutakuwa na matokeo mazuri ajabu. Yehova anasema hivi: “Mataifa wataijilia nuru yako, na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako.”—Isaya 60:3.
5 Maneno yenye kusisimua yaliyo katika mistari hii mitatu ni utangulizi wa Isaya sura ya 60 na vilevile muhtasari wa mambo makuu ya sura hiyo. Sura hiyo inatabiri yale yatakayompata yule mwanamke wa kiunabii, na inaeleza jinsi tunavyoweza kukaa katika nuru ya Yehova licha ya giza linalofunika wanadamu. Lakini mifano inayotajwa katika mistari hiyo mitatu ya utangulizi inamaanisha nini?
6. Mwanamke anayetajwa katika sura ya 60 ya Isaya ni nani, naye anawakilishwa na nani duniani?
6 Mwanamke anayetajwa katika Isaya 60:1-3 ni Sayuni, tengenezo la kimbingu la Yehova la viumbe wa roho. Leo, Sayuni anawakilishwa duniani na mabaki ya “Israeli wa Mungu,” lile kutaniko la kimataifa la Wakristo ambao wametiwa mafuta kwa roho. Wao wana tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (Wagalatia 6:16) Taifa hilo la kiroho lina washiriki 144,000, na utimizo wa kisasa wa Isaya sura ya 60 unahusu hasa wale walio hai duniani katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1; Ufunuo 14:1) Unabii huo una maelezo mengi pia kuhusu ule “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” waandamani wa hao Wakristo watiwa-mafuta.—Ufunuo 7:9; Yohana 10:16.
7. Hali ya Sayuni ilikuwaje mwaka wa 1918, na hali hiyo ilikuwa imetabiriwa jinsi gani?
7 Je, “Israeli wa Mungu” alikuwa amelala gizani wakati fulani, kama yule mwanamke wa kiunabii? Ndiyo, jambo hilo lilitukia zaidi ya miaka 80 iliyopita. Wakati wa vita ya kwanza ya ulimwengu, Wakristo watiwa-mafuta walijitahidi sana kuendeleza kazi ya kutoa ushahidi. Lakini mwaka wa 1918, mwaka wa mwisho wa vita, kazi ya kuhubiri karibu ikomeshwe kabisa. Joseph F. Rutherford, aliyesimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na Wakristo wengine mashuhuri walihukumiwa vifungo virefu gerezani kwa mashtaka bandia. Katika kitabu cha Ufunuo, Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa duniani wakati huo walitajwa katika unabii huo kuwa maiti zilizolala “juu ya njia pana ya jiji kubwa ambalo katika maana ya kiroho laitwa Sodoma na Misri.” (Ufunuo 11:8) Kwa kweli huo ulikuwa wakati wenye giza kwa Sayuni aliyewakilishwa na watoto wake watiwa-mafuta duniani.
8. Ni badiliko gani kubwa lililotukia mwaka wa 1919, na matokeo yalikuwa nini?
8 Hata hivyo, mwaka wa 1919 kukawa na badiliko kubwa. Yehova aliangaza nuru juu ya Sayuni! Washiriki wa Israeli wa Mungu waliokuwa duniani walianza kuangaza nuru ya Mungu, wakaanza tena kuzitangaza habari njema kwa ujasiri. (Mathayo 5:14-16) Kwa sababu ya bidii hiyo mpya ya Wakristo hao, wengine walivutwa kwenye nuru ya Yehova. Mwanzoni, wapya waliokuja walitiwa mafuta ili wawe washiriki wa Israeli wa Mungu. Katika Isaya 60:3 wanaitwa wafalme, kwa kuwa wataurithi Ufalme wa kimbingu wa Mungu pamoja na Kristo. (Ufunuo 20:6) Baadaye, umati mkubwa wa kondoo wengine walivutwa kwenye nuru ya Yehova. Hao ndio “mataifa” yanayotajwa katika unabii huo.
Watoto wa Mwanamke Wanakuja Nyumbani!
9, 10. (a) Mwanamke huyo aliona jambo gani la kustaajabisha, na hilo lilikuwa ishara ya matukio gani ya wakati ujao? (b) Sayuni amekuwa na sababu gani ya kuwa na shangwe?
9 Sasa, Yehova anaanza kutoa maelezo zaidi kuhusu Isaya 60:1-3. Anampa yule mwanamke amri nyingine. Sikiliza maneno yake: “Inua macho yako, utazame pande zote!” Mwanamke huyo anatii, na lo, anaona jambo la kuchangamsha moyo kama nini! Watoto wake wanakuja nyumbani. Andiko linaendelea kusema hivi: “Wote wanakusanyana; wanakujia wewe; wana wako watakuja kutoka mbali. Na binti zako watabebwa nyongani.” (Isaya 60:4) Kazi ya kuutangaza Ufalme ulimwenguni pote, iliyoanza mwaka wa 1919, iliwavuta maelfu ya watu wapya kwenye utumishi wa Yehova. Hao pia wakawa “wana” na “binti” za Sayuni, washiriki waliotiwa mafuta wa Israeli wa Mungu. Hivyo, Yehova ameremba Sayuni kwa kuwapa nuru washiriki wa mwisho wa wale 144,000.
10 Je, unaweza kuwazia furaha ya Sayuni watoto wake wanapomjia? Na bado Yehova anampa Sayuni sababu nyingine za kushangilia. Tunasoma hivi: “Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, na moyo wako utatetemeka na kukunjuka; kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, utajiri wa mataifa utakuwasilia.” (Isaya 60:5) Kwa kupatana na maneno hayo ya unabii, tangu miaka ya 1930, Wakristo wengi wenye tumaini la kuishi duniani, wamemwendea Sayuni. Wametoka katika “bahari” ya wanadamu wasio na kibali cha Mungu, nao ndio utajiri wa mataifa. Wao ni “vitu vinavyotamaniwa na mataifa [“vya mataifa,” NW].” (Hagai 2:7; Isaya 57:20) Ona pia, kwamba “vitu [hivyo] vinavyotamaniwa” hawaendi zao wakamtumikie Yehova kila mtu kivyake. Bali wao huongeza uzuri wa Sayuni wanapokuja kuabudu pamoja na ndugu zao waliotiwa mafuta, na hivyo kuwa “kundi moja” lenye “mchungaji mmoja.”—Yohana 10:16.
Wafanyabiashara na Wachungaji Waja Sayuni
11, 12. Fafanua makundi yanayomwendea Sayuni.
11 Kule kukusanywa kulikotabiriwa kumetokeza ongezeko kubwa la watu wanaomsifu Yehova. Maneno yanayofuata ya unabii huo yanaonyesha jambo hilo. Wazia kwamba umesimama pamoja na mwanamke huyo wa kiunabii kwenye Mlima Sayuni. Unaona nini unapotazama upande wa mashariki? “Wingi wa ngamia utakufunika, ngamia vijana wa Midiani na Efa; wote watakuja kutoka Sheba; wataleta dhahabu na uvumba; na kuzitangaza sifa za BWANA.” (Isaya 60:6) Wafanyabiashara wengi wanaongoza misafara ya ngamia kwenye njia zinazoelekea Yerusalemu. Ngamia hao ni wengi hivi kwamba ni kama wanaifunika nchi! Wafanyabiashara hao wamebeba zawadi zenye thamani, “dhahabu na uvumba.” Nao wanakuja kwenye nuru ya Mungu ili “kuzitangaza sifa za BWANA,” yaani, kumtukuza mbele za watu.
12 Si wafanyabiashara peke yao walio safarini. Wachungaji wengi wanamwendea Sayuni pia. Unabii unasema hivi: “Makundi yote ya Kedari yatakusanyika kwako, kondoo waume wa Nebayothi watakutumikia.” (Isaya 60:7a) Makabila yanayofuga mifugo yanakuja hadi jiji takatifu ili kumtolea Yehova wanyama bora kutoka katika makundi yao. Hata wanajitoa kumtumikia Sayuni! Yehova anawakaribishaje wageni hao? Mungu mwenyewe anajibu hivi: “Watapanda juu ya madhabahu yangu kwa kibali, nami nitaitukuza [“nitairemba,” NW] nyumba ya utukufu wangu.” (Isaya 60:7b) Yehova anakubali kwa fadhili matoleo na utumishi wa wageni hao. Wanaliremba hekalu lake.
13, 14. Ni nini kinachoonekana kikija kutoka upande wa magharibi?
13 Sasa geuka utazame upande wa magharibi. Unaona nini? Kule mbali kuna wingu jeupe linaloonekana kana kwamba linafunika uso wa bahari. Yehova anauliza swali ambalo unataka kuuliza: “Ni nani hawa warukao kama wingu, na kama njiwa waendao madirishani kwao?” (Isaya 60:8) Yehova anajibu swali lake mwenyewe: “Visiwa vitaningojea, na merikebu za Tarshishi kwanza, ili kuleta wana wako kutoka mbali, na fedha yao na dhahabu yao pamoja nao, kwa ajili ya jina la BWANA, Mungu wako, kwa ajili yake Mtakatifu wa Israeli, kwa kuwa amekutukuza wewe.”—Isaya 60:9.
14 Je, unaweza kuwazia jambo hilo? Lile wingu jeupe limekaribia zaidi na sasa linaonekana kama madoa mengi kule mbali upande wa magharibi. Madoa hayo yanaonekana kama ndege wanaoruka juu tu ya mawimbi ya bahari. Lakini yanapokaribia zaidi, unaona kwamba kumbe ni merikebu zenye matanga yaliyofunguliwa. Merikebu zinazosafiri kuelekea Yerusalemu ni nyingi sana hivi kwamba zinaonekana kama kundi la njiwa. Kundi hilo la merikebu limetoka bandari za mbali na linasafiri kwa kasi kuwapeleka waamini hadi Yerusalemu ili wamwabudu Yehova.
Tengenezo la Yehova Lapanuka
15. (a) Maneno ya Isaya 60:4-9 yanatabiri ongezeko gani? (b) Wakristo wa kweli wana moyo gani?
15 Mstari wa 4 hadi 9 unatabiri waziwazi mpanuko ambao umeendelea ulimwenguni pote tangu mwaka wa 1919. Kwa nini Yehova alimbariki Sayuni kwa ongezeko hilo? Kwa sababu tangu mwaka wa 1919, Israeli wa Mungu ameonyesha utii na kuangaza nuru ya Yehova bila kuacha. Hata hivyo, je, uliona kwamba mstari wa 7 unasema kwamba wapya hao wanaowasili ‘hupanda juu ya madhabahu ya Mungu’? Madhabahu ni mahali pa kutolea dhabihu, na maneno hayo ya unabii yanatukumbusha kwamba kumtumikia Yehova kunahusisha kujidhabihu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Nawasihi sana . . . mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri kuzuri.” (Waroma 12:1) Kwa kupatana na maneno ya Paulo, Wakristo wa kweli hawatosheki tu kwenda kumwabudu Mungu mara moja kwa juma. Wanatumia wakati wao, nguvu na mali zao ili kuendeleza ibada safi. Je, waabudu hao wanaojitoa, wanairemba nyumba ya Yehova? Unabii wa Isaya unajibu, ndiyo. Na tunaweza kuwa na uhakika kwamba waabudu hao wenye bidii pia wamerembwa vizuri machoni pa Yehova.
16. Ni nani waliojitolea kusaidia katika ujenzi siku za kale, na ni nani ambao wamefanya hivyo katika siku zetu?
16 Wapya hao wanaokuja wanataka kufanya kazi. Unabii unaendelea kusema hivi: “Wageni watajenga kuta zako, na wafalme wao watakuhudumu.” (Isaya 60:10) Maneno hayo yalitimizwa mara ya kwanza wakati Wayahudi waliporudi kutoka uhamishoni huko Babiloni. Wafalme na watu wengine wa mataifa walisaidia kujenga upya hekalu na jiji la Yerusalemu. (Ezra 3:7; Nehemia 3:26) Katika utimizo wa siku zetu, umati mkubwa umewaunga mkono mabaki ya watiwa-mafuta ili kuendeleza ibada ya kweli. Wamesaidia kuanzisha na kuimarisha makutaniko ya Kikristo, na hivyo kuzitia nguvu “kuta” za tengenezo la Yehova lililo kama jiji. Wanashiriki pia katika ujenzi halisi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya Betheli. Kwa njia hizi zote, wanawaunga mkono ndugu zao waliotiwa mafuta ili kuyatimiza mahitaji ya tengenezo la Yehova linalopanuka!
17. Taja njia moja ambayo Yehova anawaremba watu wake.
17 Maneno ya kumalizia ya Isaya 60:10 yanatia moyo sana. Yehova anasema hivi: “Katika ghadhabu yangu nalikupiga, lakini katika upendeleo wangu nimekurehemu.” Ndiyo, huko nyuma, mwaka wa 1918 na 1919, Yehova aliwatia watu wake nidhamu. Lakini jambo hilo limekwisha pita. Sasa, wakati umewadia kwa Yehova kuwarehemu watumishi wake waliotiwa mafuta na waandamani wao wa kondoo wengine. Na ongezeko kubwa ajabu ambalo wamepata linaonyesha kwamba anawabariki, yaani ‘anawaremba.’
18, 19. (a) Yehova anaahidi nini kuwahusu wapya wanaoingia katika tengenezo lake? (b) Mistari inayobaki ya sura ya 60 ya Isaya inatueleza nini?
18 Kila mwaka, mamia ya maelfu ya “wageni” huja kwenye tengenezo la Yehova, na njia itabaki wazi ili wengine wengi waje. Yehova anamwambia Sayuni hivi: “Malango yako nayo yatakuwa wazi daima; hayatafungwa mchana wala usiku; ili watu wapate kukuletea utajiri wa mataifa, na wafalme wao wakiongozwa pamoja nao.” (Isaya 60:11) Wapinzani fulani wanajaribu kufunga “malango” hayo, lakini tunajua kwamba hawatafanikiwa. Yehova mwenyewe amesema kwamba kwa njia moja au nyingine malango hayo yatabaki wazi. Ongezeko litaendelea.
19 Yehova amewabariki, au amewaremba, watu wake kwa njia nyingine pia katika siku hizi za mwisho. Mistari inayobaki ya sura ya 60 ya Isaya inatabiri njia hizo.
-
-
Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu WakeMnara wa Mlinzi—2002 | Julai 1
-
-
Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu Wake
“BWANA mwenyewe atakuwa nuru yako ya milele.”—ISAYA 60:20.
1. Yehova anawabariki watu wake waaminifu jinsi gani?
“BWANA awaridhia watu wake, huwapamba [“huwaremba,” NW] wenye upole kwa wokovu.” (Zaburi 149:4) Hivyo ndivyo alivyosema mtunga-zaburi wa kale, na maneno yake yamethibitishwa kuwa ya kweli. Yehova huwatunza, kuwafanikisha, na kuwalinda watu wake walio waaminifu. Nyakati za kale aliwapa ushindi juu ya adui zao. Leo, anawasaidia kuwa wenye nguvu kiroho na kuwahakikishia kwamba watapata wokovu kupitia dhabihu ya Yesu. (Waroma 5:9) Anafanya hivyo kwa kuwa wanapendeza machoni pake.
2. Ijapokuwa watu wa Mungu hupata upinzani, wana uhakika gani?
2 Bila shaka, wale ‘wanaoishi kwa ujitoaji-kimungu’ katika ulimwengu wenye giza watapata upinzani. (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, Yehova anawaona wapinzani, naye anawaonya hivi: “Kila taifa na ufalme wa watu wasiotaka kukutumikia wataangamia; naam, mataifa hayo wataharibiwa kabisa.” (Isaya 60:12) Leo, Wakristo hupingwa kwa njia nyingi. Katika nchi fulani, wapinzani hujaribu kuzuia au kupiga marufuku ibada ambayo Wakristo wa kweli humtolea Yehova. Katika nchi nyingine, watu washupavu hushambulia waabudu wa Yehova na kuteketeza mali zao. Hata hivyo, kumbukeni kwamba tayari Yehova ameamua kile kitakachowapata wote wanaopinga mapenzi yake. Wapinzani watashindwa. Wale wanaopigana na Sayuni, kwa kuwapinga watoto wake duniani, hawatafanikiwa. Je, huo si uhakikishio wenye kutia moyo kutoka kwa Mungu wetu mkuu, Yehova?
Baraka Nyingi Zisizotarajiwa
3. Uzuri na mafanikio ya waabudu wa Yehova yalifananishwa na nini?
3 Katika siku za mwisho za ulimwengu huu, Yehova amewapa watu wake baraka nyingi zisizotarajiwa. Ameremba hasa mahali pake pa ibada na wale waliomo wanaoitwa kwa jina lake. Kulingana na unabii wa Isaya, anamwambia Sayuni hivi: “Utukufu wa Lebanoni utakujia wewe, mberoshi na mtidhari na mteashuri pamoja; ili kupapamba [“kuparemba,” NW] mahali pangu patakatifu, nami nitapatukuza mahali pa miguu yangu.” (Isaya 60:13) Milima iliyofunikwa kwa misitu inayositawi inavutia sana. Kwa hiyo, miti inayositawi ni mfano unaofaa wa uzuri na ufanisi wa waabudu wa Yehova.—Isaya 41:19; 55:13.
4. “Patakatifu” na “mahali pa miguu [ya Yehova]” panamaanisha nini, na pamerembwa kwa njia gani?
4 Mahali “patakatifu” na “mahali pa miguu [ya Yehova]” panapotajwa katika Isaya 60:13 panamaanisha nini? Panamaanisha nyua za lile hekalu kuu la kiroho la Yehova, yaani, mpango wa kumkaribia Yehova katika ibada kupitia Yesu Kristo. (Waebrania 8:1-5; 9:2-10, 23) Yehova ameamua kutukuza hekalu hilo la kiroho kwa kuwakusanya watu wa mataifa yote waje wakaabudu humo. (Hagai 2:7) Hapo awali, Isaya mwenyewe aliona halaiki ya watu kutoka mataifa yote wakiuendea mlima ulioinuliwa wa ibada ya Yehova. (Isaya 2:1-4) Mamia ya miaka baadaye, mtume Yohana aliona katika njozi “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” Hao walisimama ‘mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu wakimtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.’ (Ufunuo 7:9, 15) Unabii huo mbalimbali umetimizwa katika siku zetu. Kwa hiyo, tumejionea kwamba nyumba ya Yehova imerembwa.
5. Hali ya watoto wa Sayuni ilibadilika kuwa nzuri jinsi gani?
5 Hayo yote yamemletea Sayuni hali nzuri iliyoje! Yehova anasema hivi: “Kwa kuwa [uliachwa] na kuchukiwa, hata ikawa hapana mtu aliyepita ndani yako, nitakufanya kuwa fahari ya milele, furaha ya vizazi vingi.” (Isaya 60:15) Mwishoni mwa vita ya kwanza ya ulimwengu, “Israeli wa Mungu” alipatwa na kipindi cha ukiwa. (Wagalatia 6:16) Alihisi akiwa ‘ameachwa,’ kwa kuwa watoto wake duniani hawakutambua waziwazi mapenzi ya Mungu kwao. Halafu, mwaka wa 1919, Yehova aliwapa watumishi wake watiwa-mafuta nguvu mpya, na tangu wakati huo amewabariki kwa ufanisi mzuri ajabu wa kiroho. Isitoshe, mstari huo una ahadi yenye kusisimua sana. Ndiyo, Yehova mwenyewe na watoto wa Sayuni watamwonea Sayuni “fahari.” Sayuni atakuwa “furaha” tele. Na si kwa muda mfupi tu. Hali ya kupendelewa ya Sayuni, inayoonekana katika watoto wake duniani, itadumu kwa “vizazi vingi.” Haitakoma kamwe.
6. Wakristo wa kweli hutumiaje mali za thamani kutoka kwa mataifa?
6 Sikiliza sasa Mungu anapotoa ahadi nyingine. Yehova anamwambia Sayuni hivi: “Utanyonya maziwa ya mataifa, utanyonya matiti ya wafalme; nawe utajua ya kuwa mimi, BWANA, ni mwokozi wako, na mkombozi wako, Mwenye enzi wa Yakobo.” (Isaya 60:16) Sayuni hunyonya “maziwa ya mataifa” na “matiti ya wafalme” jinsi gani? Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao ambao ni “kondoo wengine” wanafanya hivyo kwa kutumia mali za thamani kutoka kwa mataifa ili kuendeleza ibada safi. (Yohana 10:16) Michango ya hiari inatumiwa kutimiza kazi kubwa ya kuhubiri na kufundisha ulimwenguni pote. Wao hutumia kwa hekima vifaa vya kisasa vya uchapishaji. Hivyo, Biblia na vitabu vya Biblia huchapishwa katika mamia ya lugha. Leo, watu wengi zaidi wana nafasi ya kujifunza kweli ya Biblia kuliko wakati mwingine wowote. Watu wa mataifa mengi sana wanajifunza kwamba Yehova ndiye Mwokozi aliyewakomboa watumishi wake watiwa-mafuta waliokuwa mateka wa kiroho.
Maendeleo ya Kitengenezo
7. Watoto wa Sayuni wamekuwa na maendeleo gani makubwa?
7 Yehova amewaremba watu wake kwa njia nyingine. Amewabariki kwa maendeleo ya kitengenezo. Tunasoma hivi kwenye Isaya 60:17: ‘Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.’ Kubadilisha shaba kwa dhahabu ni maendeleo, na ndivyo ilivyo na vitu vinginevyo vinavyotajwa. Kwa kupatana na andiko hilo, Israeli wa Mungu amefanya maendeleo ya kitengenezo muda wote wa siku hizi za mwisho. Fikiria mifano michache.
8-10. Taja maendeleo mbalimbali ya kitengenezo ambayo yamefanywa tangu mwaka wa 1919.
8 Kabla ya mwaka wa 1919, makutaniko ya watu wa Mungu yalisimamiwa na wazee na mashemasi waliochaguliwa na washiriki wa kutaniko kupitia kura. Kuanzia mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliweka mkurugenzi wa utumishi katika kila kutaniko ili kusimamia utumishi wa shambani. (Mathayo 24:45-47) Hata hivyo, mpango huo haukufanikiwa sana katika makutaniko mengi kwa kuwa baadhi ya wazee waliochaguliwa kwa kura hawakuunga mkono kazi ya kuhubiri habari njema. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1932, makutaniko yaliagizwa yaache kuchagua kwa kura wazee na mashemasi. Badala yake, walipaswa kuchagua wanaume ambao wangetumikia katika halmashauri ya utumishi pamoja na mkurugenzi wa utumishi. Jambo hilo lilikuwa kama “shaba” badala ya “mti,” na yakawa maendeleo makubwa!
9 Katika mwaka wa 1938, makutaniko ulimwenguni pote yalikubali mpango bora uliopatana zaidi na Maandiko. Usimamizi wa kutaniko ukakabidhiwa mtumishi wa shirika na watumishi wengine, ambao waliteuliwa chini ya usimamizi wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Tangu wakati huo mambo ya kura yakaisha! Kwa hiyo, watumishi wote katika kutaniko waliwekwa kulingana na kanuni za Mungu. Hiyo ilikuwa kama “chuma” badala ya “mawe” au “dhahabu” badala ya “shaba.”
10 Tangu wakati huo, kumekuwa na maendeleo. Kwa mfano, katika mwaka wa 1972 ilieleweka kwamba makutaniko yalipaswa kusimamiwa na baraza la wazee waliowekwa kulingana na kanuni za Mungu, na hakuna mzee aliyepaswa kuwa na mamlaka juu ya wale wengine. Utaratibu huo ulipatana hata zaidi na jinsi makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza yalivyosimamiwa. Isitoshe, yapata miaka miwili iliyopita, hatua nyingine ilichukuliwa. Rekebisho lilifanywa katika usimamizi wa mashirika fulani ya kisheria, na hivyo kuwezesha Baraza Linaloongoza kukaza fikira kwa ukamili juu ya masilahi ya kiroho ya watu wa Mungu badala ya kukengeushwa na mambo ya kisheria.
11. Ni nani ambaye ameleta maendeleo ya kitengenezo miongoni mwa watu wa Yehova, na matokeo yamekuwa nini?
11 Ni nani anayeleta maendeleo hayo? Ni Yehova Mungu. Yeye ndiye anayesema hivi: “Nitaleta dhahabu.” (Italiki ni zetu.) Na anaongeza hivi: “Nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” (Italiki ni zetu.) Ndiyo, Yehova ndiye anayeongoza usimamizi juu ya watu wake. Yehova anawaremba watu wake kwa maendeleo hayo ya kitengenezo ambayo yalitabiriwa. Na kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova wamebarikiwa katika njia nyingi. Tunasoma hivi kwenye Isaya 60:18: “Jeuri haitasikiwa tena katika nchi yako, ukiwa na uharibifu hazitakuwa mipakani mwako; bali utaziita kuta zako, Wokovu, na malango yako, Sifa.” Maneno hayo yanapendeza sana. Lakini yametimizwaje?
12. Wakristo wa kweli wamepata amani nyingi jinsi gani?
12 Wakristo wa kweli wanamtegemea Yehova kabisa ili awape maagizo na mwongozo, na matokeo yalitabiriwa na Isaya: “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Isitoshe, roho ya Yehova i juu ya watu wake na mojawapo ya matunda ya roho hiyo ni amani. (Wagalatia 5:22, 23) Amani ya watu wa Yehova inawafanya wawe kimbilio katika ulimwengu huu wenye jeuri. Hali yao yenye amani inayotokana na upendo ambao Wakristo wa kweli huonyeshana, inaonyesha jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya. (Yohana 15:17; Wakolosai 3:14) Bila shaka sisi sote tunafurahia sana kuwa na amani hiyo na kuiendeleza, kwa kuwa inaleta sifa na utukufu kwa Mungu wetu, nayo ni muhimu sana katika paradiso yetu ya kiroho.—Isaya 11:9.
Nuru ya Yehova Itazidi Kuangaza
13. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatakoma kamwe kuwaangazia watu wake nuru?
13 Je, Yehova ataendelea kuwaangazia watu wake nuru? Ndiyo! Tunasoma hivi kwenye Isaya 60:19, 20: “Jua halitakuwa nuru yako tena wakati wa mchana, wala mwezi hautakupa nuru kwa mwangaza wake; bali BWANA atakuwa nuru ya milele kwako, na Mungu wako atakuwa utukufu wako. Jua lako halitashuka tena, wala mwezi wako hautajitenga [‘hautafifia,’ Biblia Habari Njema]; kwa kuwa BWANA mwenyewe atakuwa nuru yako ya milele; na siku za kuomboleza kwako zitakoma.” Nuru ya Yehova ilianza kuwaangazia watu hao mwaka wa 1919, baada ya ‘maombolezo’ yao kukoma walipotoka katika uhamisho wa kiroho. Zaidi ya miaka 80 baadaye, bado wana kibali cha Yehova huku nuru yake ikiendelea kuwaangazia. Na nuru hiyo itaendelea kuwaangazia daima. Kuhusiana na waabudu wake, Mungu wetu ‘hatashuka’ kama jua wala “kufifia” kama mwezi. Badala yake, ataendelea kuwaangazia watu wake nuru kwa umilele wote. Huo ni uhakikisho mzuri kama nini kwetu sisi tunaoishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu wenye giza!
14, 15. (a) Watu wote wa Mungu ni “waadilifu” kwa njia gani? (b) Kondoo wengine wanatazamia kuona utimizo gani muhimu wa Isaya 60:21?
14 Sikia sasa ahadi nyingine ambayo Yehova anatoa kuhusu mwakilishi wa kidunia wa Sayuni, Israeli wa Mungu. Andiko la Isaya 60:21 linasema hivi: “Watu wako nao watakuwa wenye haki wote, nao watairithi nchi milele; chipukizi nililolipanda mimi mwenyewe, kazi ya mikono yangu mwenyewe, ili mimi nitukuzwe.” Mwaka wa 1919, wakati Wakristo watiwa-mafuta walipoanza kutenda tena, walikuwa tofauti na watu wengine. Katika ulimwengu wenye dhambi, wao walikuwa ‘wametangazwa kuwa waadilifu’ kwa sababu ya imani yao thabiti katika dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu. (Waroma 3:24; 5:1) Halafu, kama vile Waisraeli walioachwa huru kutoka katika Babiloni, walianza kumiliki “nchi” ya kiroho, au utendaji wa kiroho, ambamo wangefurahia paradiso ya kiroho. (Isaya 66:8) Hali ya kiparadiso ya nchi hiyo haitafifia kamwe, kwa sababu, tofauti na Israeli la kale, taifa la Israeli wa Mungu halitamwasi Yehova. Imani yao, uvumilivu wao, na bidii yao zitaleta sifa kwa jina la Mungu daima.
15 Washiriki wote wa taifa hilo la kiroho wamo katika agano jipya. Wote wana sheria ya Yehova mioyoni mwao, na Yehova amewasamehe dhambi zao kupitia dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yeremia 31:31-34) Amewatangaza kuwa waadilifu wakiwa “wana” na kuwashughulikia kana kwamba wao ni wakamilifu. (Waroma 8:15, 16, 29, 30) Waandamani wao ambao ni kondoo wengine, pia wamesamehewa dhambi zao kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, na kama vile Abrahamu, wametangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu kwa sababu ya imani yao. “Wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Na waandamani hao wa kondoo wengine wanatazamia kwa hamu baraka nyingine ya ajabu. Baada ya kuokoka “dhiki kubwa” au baada ya kufufuliwa, wataona utimizo halisi wa maneno ya Isaya 60:21 wakati dunia yote itakapokuwa paradiso. (Ufunuo 7:14; Waroma 4:1-3) Wakati huo, “wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11, 29.
Ongezeko Linazidi
16. Yehova alitoa ahadi gani ya pekee, na imetimizwa kwa njia gani?
16 Katika mstari wa mwisho wa Isaya sura ya 60, tunasoma kuhusu ahadi ya mwisho ya Yehova katika sura hiyo. Anamwambia Sayuni hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” (Isaya 60:22) Yehova ametimiza ahadi yake katika wakati wetu. Wakati watiwa-mafuta walipoanza kutenda tena mwaka wa 1919, walikuwa wachache, yaani “mdogo.” Idadi yao iliongezeka wakati Waisraeli wengine wa kiroho walipokusanywa. Halafu wale kondoo wengine wakaanza kujiunga nao, na idadi yao inaongezeka daima. Hali ya amani ya watu wa Mungu, paradiso ya kiroho iliyo katika “nchi” yao, imewavuta watu wengi sana wenye mioyo minyofu hivi kwamba yule “mnyonge” kwa kweli amekuwa “taifa hodari.” Wakati huu “taifa” hili, ambalo ni Israeli wa Mungu pamoja na “wageni” zaidi ya milioni sita waliojiweka wakfu, lina watu wengi kuliko mataifa mengi duniani. (Isaya 60:10) Raia wake wote hushiriki pia kuangaza nuru inayotoka kwa Yehova, na kwa hiyo wanapendeza machoni pake.
17. Mazungumzo haya kuhusu Isaya sura ya 60 yamekutia moyo jinsi gani?
17 Ndiyo, imani yetu inaimarishwa tunapochunguza mambo makuu ya Isaya sura ya 60. Inatia moyo kuona kwamba Yehova alijua zamani sana kwamba watu wake wangepelekwa kwenye uhamisho wa kiroho kisha kurudishwa. Tunashangazwa kuona kwamba zamani sana Yehova alitabiri ongezeko kubwa la idadi ya waabudu wa kweli ambalo tunaona katika siku hizi zetu. Isitoshe, inatia moyo sana kujua kwamba Yehova hatatuacha kamwe! Kwa upendo mwingi anahakikisha kwamba malango ya “jiji” yatakuwa wazi daima ili wale walio na “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” waweze kukaribishwa kwa ukarimu. (Matendo 13:48) Yehova ataendelea kuwaangazia watu wake nuru. Sayuni ataendelea kuwa mwenye fahari watoto wake wanapozidi kuangaza nuru yao. (Mathayo 5:16) Bila shaka tumetiwa moyo hata zaidi kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Israeli wa Mungu na kuthamini pendeleo letu la kuangaza nuru ya Yehova!
-
-
Utukufu wa Yehova Unaangazia Watu WakeMnara wa Mlinzi—2002 | Julai 1
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]
UNABII WA ISAYA—Nuru kwa Wanadamu Wote
Mambo makuu ya makala hizi yalizungumziwa katika hotuba kwenye Kusanyiko la Wilaya la mwaka wa 2001/2002 lenye kichwa “Walimu wa Neno la Mungu.” Katika makusanyiko mengi, msemaji alipomalizia hotuba yake, alitangaza kutolewa kwa kitabu kipya chenye kichwa Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la Pili. Mwaka uliotangulia, kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote, Buku la Kwanza, kilitolewa. Vitabu hivyo viwili vina maelezo kuhusu karibu kila mstari katika kitabu cha Isaya. Vitabu hivyo vinatusaidia sana kuelewa na kuthamini kitabu cha unabii cha Isaya kinachoimarisha imani.
-