Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Tazama, Huyu Ndiye Mungu Wetu”
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Julai 1
    • “Tazama, Huyu Ndiye Mungu Wetu”

      Habari inayozungumziwa katika makala hizi mbili inapatikana katika kitabu Mkaribie Yehova, kilichotolewa kwenye makusanyiko ya wilaya yaliyofanywa ulimwenguni kote katika mwaka wa 2002/2003.—Ona makala “Kilijaza Pengo Fulani Moyoni Mwangu,” ukurasa wa 20.

      “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu, tumemungoja, naye atatuokoa; huyu ndiye BWANA.” —ISAYA 25:9, Zaire Swahili Bible.

      1, 2. (a) Yehova alimwitaje mzee wa ukoo Abrahamu, na jambo hilo linaweza kufanya tujiulize swali gani? (b) Biblia hutuhakikishiaje kwamba tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu?

      “RAFIKI yangu.” Hivyo ndivyo Yehova, Muumba wa mbingu na dunia, alivyomwita mzee wa ukoo Abrahamu. (Isaya 41:8) Hebu wazia, mwanadamu wa kawaida tu akiwa rafiki ya Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu! Huenda ukajiuliza, ‘Je, mimi ninaweza kuwa na uhusiano wa karibu kama huo na Mungu?’

      2 Biblia inatuhakikishia kwamba tunaweza kuwa rafiki za Mungu. Abrahamu alikuwa na uhusiano wa karibu na Mungu kwa sababu “aliweka imani katika Yehova.” (Yakobo 2:23) Leo pia Yehova “huwafanya marafiki zake wale walio wanyofu.” (Mithali 3:32, Biblia Habari Njema) Kwenye Yakobo 4:8 Biblia hutuhimiza hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” Ni wazi kwamba tukichukua hatua za kumkaribia Yehova, yeye atafanya vivyo hivyo. Naam, atatukaribia. Lakini je, maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanamaanisha kwamba sisi wanadamu wasio wakamilifu, ndio tunapaswa kuchukua hatua ya kwanza? Hapana. Urafiki pamoja na Yehova unawezekana tu kwa sababu Mungu wetu mwenye upendo amechukua hatua mbili muhimu.—Zaburi 25:14.

      3. Yehova amechukua hatua gani mbili ili kutuwezesha kuwa rafiki zake?

      3 Kwanza, Yehova alifanya mpango ili Yesu ‘atoe nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Dhabihu hiyo ya fidia hutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu. Andiko la 1 Yohana 4:19 linasema: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” Naam, kwa kuwa Mungu “alitupenda sisi kwanza,” aliweka msingi ili tuwe rafiki zake. Pili, Yehova ametueleza jinsi alivyo. Ili kuwa na urafiki na mtu yeyote, ni lazima tumjue mtu huyo, tuvutiwe na sifa zake za pekee na kuzithamini. Ona jambo hilo linamaanisha nini. Hatungeweza kamwe kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova kama angekuwa Mungu aliyejificha na asiyeeleweka. Badala ya kujificha, Yehova hutaka tumjue. (Isaya 45:19) Katika Neno lake, Biblia, Yehova hujifunua kwa kutumia lugha tunayoweza kufahamu, na jambo hilo linathibitisha kwamba anatupenda na anataka tumjue na kumpenda akiwa Baba yetu wa mbinguni.

      4. Tutahisije kumhusu Yehova tunapopata kuzijua sifa zake vizuri zaidi?

      4 Je, umewahi kumwona mtoto mdogo akiwaonyesha rafiki zake baba yake na kusema hivi kwa furaha na fahari, “Huyu ndiye baba yangu”? Waabudu wa Mungu wana sababu nzuri sana za kuhisi vivyo hivyo kumhusu Yehova. Biblia inatabiri kuhusu wakati ambapo watu waaminifu watasema hivi kwa shauku: “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu.” (Isaya 25:8, 9) Kadiri tunavyojua sifa za Yehova vizuri zaidi, ndivyo tutakavyohisi kwamba tuna Rafiki bora zaidi. Naam, tukifahamu sifa za Yehova, tutamkaribia zaidi. Hivyo, na tuone jinsi Biblia inavyoeleza sifa kuu za Yehova—nguvu, haki, hekima, na upendo. Katika makala hii tutazungumzia sifa za kwanza tatu kati ya sifa hizo.

      “Mkuu Mwenye Uweza”

      5. Kwa nini inafaa kwamba Yehova peke yake aitwe “Mweza-Yote,” na ni katika njia gani mbalimbali yeye hutumia nguvu zake nyingi?

      5 Yehova ni “mkuu mwenye uweza.” (Ayubu 37:23) Andiko la Yeremia 10:6 linasema: “Hapana hata mmoja aliye kama wewe, Ee BWANA; wewe ndiwe uliye mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza.” Yehova ana nguvu zisizo na mipaka, hawezi kulinganishwa na kiumbe yeyote. Hiyo ndiyo sababu yeye peke yake ndiye anayeitwa “Mweza-Yote.” (Ufunuo 15:3) Yehova hutumia nguvu zake nyingi kuumba, kuharibu, kulinda, na kurudisha hali upya. Fikiria mifano miwili tu—nguvu zake za kuumba na nguvu zake za kulinda.

      6, 7. Jua lina nguvu nyingi kadiri gani, nalo linathibitisha jambo gani muhimu?

      6 Unapokuwa nje wakati wa jua kali, unahisi joto la jua, sivyo? Yehova aliumba joto hilo kwa nguvu zake za kuumba. Jua lina nguvu nyingi kadiri gani? Kipimo cha joto kwenye kiini cha jua ni nyuzi Selsiasi milioni 15 hivi. Kama ungeweza kuchukua kipande cha kiini cha jua kinachotoshana na kichwa cha pini ndogo na kukiweka duniani, ungeteketea hata kama ungekuwa umbali wa kilometa 140 kutoka kwenye chanzo hicho kidogo sana cha joto! Kila sekunde, jua hutoa nishati inayolingana na mlipuko wa mamia ya mamilioni ya mabomu ya nyuklia. Lakini, dunia huizunguka tanuru hiyo kubwa yenye joto kwa umbali barabara. Kama dunia ingekaribia jua, maji yote duniani yangekuwa mvuke; na kama dunia ingesonga mbali zaidi, maji yote yangekuwa barafu. Joto au baridi kali ingeangamiza kila kiumbe duniani.

      7 Watu wengi huona jua kuwa kitu cha kawaida tu, ingawa uhai wao unalitegemea. Hivyo basi, hawajifunzi lolote kutokana na jua. Zaburi 74:16 inasema hivi kumhusu Yehova: “Ndiwe uliyeufanya mwanga na jua.” Naam, jua humletea Yehova sifa, “aliyezifanya mbingu na nchi.” (Zaburi 146:6) Hata hivyo, jua ni mojawapo tu ya nyota nyingi sana zilizo angani ambazo zinatufundisha kuhusu nguvu nyingi za Yehova. Kadiri tunavyojifunza mengi kuhusu nguvu za Yehova za kuumba, ndivyo tunavyokuwa na heshima zaidi.

      8, 9. (a) Ni mfano gani wa wororo ambao unaonyesha utayari wa Yehova wa kuwalinda na kuwatunza waabudu wake? (b) Mchungaji wa nyakati za Biblia aliwatunzaje kondoo zake, na jambo hilo linatufunza nini kumhusu Mchungaji wetu Mkuu?

      8 Yehova pia huwalinda na kuwatunza watumishi wake kwa nguvu zake nyingi. Biblia inatumia mifano kadhaa iliyo wazi yenye kugusa moyo ili kuonyesha jinsi Yehova anavyoahidi kuwalinda. Kwa mfano, ona andiko la Isaya 40:11. Katika andiko hilo, Yehova anajilinganisha na mchungaji na anawalinganisha watu wake na kondoo. Tunasoma hivi: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake, nao wanyonyeshao atawaongoza polepole.” Je, waweza kuwazia jambo linaloelezwa katika mstari huo?

      9 Si wanyama wengi walio dhaifu kama kondoo anayefugwa. Mchungaji katika nyakati za Biblia alihitaji kuwa jasiri ili kuwalinda kondoo zake kutoka kwa mbwa-mwitu, dubu, na simba. (1 Samweli 17:34-36; Yohana 10:10-13) Lakini nyakati nyingine alihitaji kuwalinda kondoo kwa wororo. Kwa mfano, kondoo alipozalia mbali na zizi, mchungaji angewezaje kumlinda mwana-kondoo huyo asiye na ulinzi? Angembeba mwana-kondoo huyo “kifuani” mwake—katika mapindo ya vazi lake la juu, labda hata kwa siku kadhaa. Lakini mwana-kondoo mchanga angefikaje “kifuani” mwa mchungaji? Labda mwana-kondoo huyo angemkaribia mchungaji na hata kuugusa mguu wake kwa upole. Hata hivyo, ingembidi mchungaji ainame, amchukue mwana-kondoo huyo, na kumweka kifuani penye usalama. Mfano huo wenye kugusa moyo unaonyesha vyema jinsi Mchungaji wetu Mkuu alivyo tayari kuwalinda na kuwatunza watumishi wake.

      10. Yehova hutoa ulinzi gani leo, na kwa nini ulinzi huo ni muhimu sana?

      10 Yehova amefanya mengi mbali na kuahidi ulinzi. Katika nyakati za Biblia, alionyesha kwa miujiza kwamba anaweza “kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” (2 Petro 2:9) Namna gani leo? Tunajua kwamba yeye hatumii nguvu zake kutulinda tusipatwe na misiba sasa. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kwamba Yehova hutulinda kiroho. Mungu wetu mwenye upendo hutulinda kutokana na madhara ya kiroho kwa kutupatia tunachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wetu naye. Kwa mfano andiko la Luka 11:13 linasema: “Ikiwa nyinyi, mjapokuwa waovu, mwajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, si zaidi sana yule Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba!” Nguvu hizo nyingi zinaweza kutusaidia kukabiliana na jaribu au tatizo lolote. (2 Wakorintho 4:7) Kwa hiyo, Yehova huhifadhi uhai wetu, si kwa miaka michache tu bali kwa umilele. Tukikumbuka tumaini hilo, kwa kweli tunaweza kuona mateso yoyote yanayotupata katika mfumo huu kuwa ‘ya dakika na mepesi.’ (2 Wakorintho 4:17) Je, hatuvutiwi kumkaribia Mungu ambaye anatumia nguvu zake kwa upendo kwa faida yetu?

      “Bwana Hupenda Haki”

      11, 12. (a) Kwa nini haki ya Yehova hutuvuta kwake? (b) Daudi alifikia mkataa gani kuhusu haki ya Yehova, na maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaweza kutufariji jinsi gani?

      11 Sikuzote Yehova hutenda yaliyo sawa na yaliyo haki bila kupendelea. Haki ya Yehova si sifa inayochukiza, bali ni sifa ya kupendeza inayotuvuta kwake. Biblia inaeleza waziwazi kuhusu sifa hiyo yenye kuchangamsha moyo. Hebu tuchunguze njia tatu ambazo Yehova anaonyesha haki.

      12 Kwanza, haki ya Yehova humchochea awe mwaminifu na mshikamanifu kwa watumishi wake. Mtunga-zaburi Daudi alipata kuelewa na kuthamini wonyesho huo wa haki ya Yehova maishani mwake. Daudi alifikia mkataa gani kutokana na mambo yaliyompata na yale aliyojifunza kuhusu njia za Mungu? Alisema hivi: “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake. Wao hulindwa milele.” (Zaburi 37:28) Ahadi hiyo inatia moyo kama nini! Mungu wetu hatawaacha kamwe wale walio waaminifu kwake. Kwa hiyo, tunaweza kumtegemea atulinde akiwa rafiki yetu anayetupenda na kutujali. Jambo hilo ni hakika kwa sababu yeye ni mwenye haki!—Mithali 2:7, 8.

      13. Yehova alionyeshaje kwamba anawajali watu wa hali ya chini katika Sheria aliyowapa Waisraeli?

      13 Pili, Mungu hujali mahitaji ya wale wanaotaabika kwa sababu yeye ni mwenye haki. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyesha kwamba anawajali wanaotaabika. Kwa mfano, Sheria ilitaja mipango ya pekee ya kuhakikisha kwamba mayatima na wajane walitunzwa. (Kumbukumbu la Torati 24:17-21) Kwa kutambua magumu ambayo yangezipata familia hizo, Yehova mwenyewe alizijali akiwa Hakimu na Mlinzi wao. (Kumbukumbu la Torati 10:17, 18) Aliwaonya Waisraeli kwamba ikiwa wangewatesa wanawake na watoto hao wasio na msaidizi, angesikia kilio chao. Alisema hivi katika andiko la Kutoka 22:22-24: “Hasira yangu itawaka moto.” Ijapokuwa hasira si mojawapo ya sifa kuu za Mungu, hasira yake adilifu huwaka anapoona watu wa hali ya chini na wanyonge wakionewa kimakusudi.—Zaburi 103:6.

      14. Kuna uthibitisho gani wa pekee unaoonyesha kwamba Yehova hana upendeleo?

      14 Tatu, kwenye Kumbukumbu la Torati 10:17, Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova ‘hapendelei nyuso za watu, wala hakubali rushwa.’ Yehova si kama wanadamu wengi mashuhuri au wenye mamlaka ambao huangalia utajiri au sura ya mtu. Hana ubaguzi wala upendeleo wowote. Uthibitisho wa pekee unaoonyesha kwamba Yehova hana upendeleo ni: Hakuwapa watu wachache tu walioteuliwa nafasi ya kuwa waabudu wake wa kweli wenye tumaini la kuishi milele. Badala yake, andiko la Matendo 10:34, 35 linasema: “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” Watu wote wanaweza kuwa na tumaini hilo bila kujali cheo chao katika jamii, rangi yao, au nchi wanamoishi. Je, huo si uthibitisho bora kabisa wa haki ya kweli? Kwa kweli, tunavutiwa kumkaribia Yehova zaidi tunapofahamu vyema haki yake.

      ‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’

      15. Hekima ni nini, naye Yehova huionyeshaje?

      15 Mtume Paulo alichochewa kusema hivi kwenye Waroma 11:33: ‘Lo! kina cha hekima ya Mungu!’ Naam, tunamheshimu Yehova sana tunapotafakari wonyesho mbalimbali wa hekima yake nyingi. Lakini tunaweza kuifafanuaje sifa hiyo? Hekima ni kutumia ujuzi, utambuzi, na ufahamu ili kutekeleza jambo fulani. Sikuzote Yehova hufanya maamuzi bora kabisa kwa kutumia hekima na ufahamu wake usio na mipaka, na anatekeleza maamuzi hayo kwa njia bora kabisa.

      16, 17. Uumbaji wa Yehova unathibitishaje kwamba ana hekima nyingi? Toa mfano.

      16 Ni mambo gani hasa yanayothibitisha kwamba Yehova ana hekima nyingi? Zaburi 104:24 inasema: “Ee BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” Kwa kweli, kadiri tunavyojifunza kuhusu vitu ambavyo Yehova ameumba, ndivyo hekima yake inavyozidi kutufanya tumheshimu. Wanasayansi wamejifunza mambo mengi sana kwa kuchunguza uumbaji wa Yehova. Hata kuna elimu fulani ya uhandisi inayojaribu kuiga ubuni wa maumbile inayoitwa biomimetics.

      17 Kwa mfano, labda umewahi kustaajabia umaridadi wa utando wa buibui. Huo ni ubuni wa ajabu kweli. Tando fulani nyembamba ni ngumu kuliko chuma, ni ngumu kushinda nyuzi za mavazi yasiyopenywa na risasi. Hiyo inamaanisha nini? Hebu wazia utando wa buibui uliofanywa kuwa mkubwa ukafikia ukubwa wa nyuzi za wavu unaovutwa na mashua ya uvuvi. Utando wa aina hiyo ungekuwa mgumu hivi kwamba ungeweza kusimamisha ndege ya abiria inayosafiri kwa kasi angani! Naam, Yehova amefanya vitu hivyo vyote “kwa hekima.”

      18. Yehova alionyeshaje hekima kwa kutumia wanadamu waandike Neno lake, Biblia?

      18 Tunaweza kupata uthibitisho bora kabisa wa hekima ya Yehova katika Neno lake, Biblia. Shauri la hekima lililo katika Biblia linatuonyesha njia bora kabisa ya maisha. (Isaya 48:17) Biblia imeandikwa kwa njia inayoonyesha hekima ya Yehova isiyo na kifani. Jinsi gani? Yehova alionyesha hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake. Ikiwa Yehova angalitumia malaika kuandika Biblia, je, ingalivutia kwa njia ileile? Kwa kweli, malaika wangeeleza jinsi Yehova alivyo kulingana na maoni yao yaliyotukuka, wangeeleza jinsi wanavyojitoa kwake. Lakini je, tungeweza kweli kuelewa maoni ya viumbe wakamilifu wa roho, ambao wana ujuzi, ufahamu, na uwezo wa hali ya juu kutushinda?—Waebrania 2:6, 7.

      19. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba kutumia wanadamu kuiandika Biblia huifanya Biblia ipendeze na kuvutia sana?

      19 Biblia inapendeza na kuvutia sana kwa sababu Mungu alitumia wanadamu kuiandika. Waandishi wa Biblia walikuwa wanadamu wenye hisia kama zetu. Wakiwa wanadamu wasiokamilika, walipata majaribu na mikazo kama yetu. Nyakati nyingine, waliandika kuhusu hisia zao na matatizo yaliyowapata. (2 Wakorintho 12:7-10) Kwa hiyo, waliandika maneno ambayo hakuna malaika angeweza kuandika. Kwa mfano, fikiria maneno ya Daudi katika Zaburi sura ya 51. Maneno ya utangulizi yanaonyesha kwamba Daudi alitunga zaburi hiyo baada ya kufanya dhambi nzito sana. Alifunua mambo yaliyokuwa moyoni mwake na kumwomba Mungu msamaha. Tunasoma hivi kwenye mstari wa 2 na 3: ‘Unioshe kabisa uovu wangu, unitakase dhambi zangu. Maana nimejua mimi makosa yangu na dhambi yangu i mbele yangu daima.’ Ona mstari wa 5: “Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani.” Nao mstari wa 17 unaongezea: “Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.” Je, huguswi moyo na uchungu wa mwandishi huyo? Mwanadamu asiye mkamilifu tu ndiye angeweza kuandika maneno hayo yenye kugusa moyo.

      20, 21. (a) Kwa nini tunaweza kusema Biblia ina hekima ya Yehova ingawa iliandikwa na wanadamu? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      20 Kwa kuwatumia wanadamu wasio wakamilifu kuandika Neno lake, Yehova alitupatia kile tunachohitaji—kitabu ambacho ‘kimepuliziwa na Mungu’ lakini kinachozingatia hali ya binadamu. (2 Timotheo 3:16) Ndiyo, waandishi hao waliongozwa na roho takatifu. Kwa hiyo, wakaandika hekima ya Yehova si yao wenyewe. Hekima hiyo ni amini kabisa na ni bora kuliko hekima yetu hivi kwamba Mungu anatusihi hivi kwa upendo: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Tunamkaribia zaidi Mungu wetu mwenye hekima yote tunapotii shauri hilo la hekima.

      21 Upendo ndiyo sifa ya Yehova inayovutia zaidi. Katika makala inayofuata tutazungumzia jinsi ambavyo Yehova ameonyesha upendo.

  • “Mungu Ni Upendo”
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Julai 1
    • “Mungu Ni Upendo”

      “Yeye ambaye hapendi hajaja kujua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.”—1 YOHANA 4:8.

      1-3. (a) Biblia inasema nini kuhusu sifa ya Yehova ya upendo, na ni katika njia gani usemi huo ni wa pekee? (b) Kwa nini Biblia husema kwamba “Mungu ni upendo?”

      SIFA zote za Yehova ni bora sana, ni kamilifu, na zinavutia. Lakini upendo unavutia kuliko sifa nyingine zote. Hakuna kitu kingine chochote kinachotuvutia tumkaribie Yehova zaidi kama upendo wake. Inafurahisha kwamba upendo ndiyo sifa yake kuu. Tunajuaje?

      2 Kuhusiana na upendo, Biblia inasema jambo fulani la pekee ambalo haisemi kuhusu zile sifa nyingine kuu za Yehova. Maandiko hayasemi kwamba Mungu ni nguvu wala hayasemi kwamba Mungu ni haki au hata Mungu ni hekima, bali yanasema kwamba ana sifa hizo, naye ndiye chanzo cha zote tatu. Hata hivyo, andiko la 1 Yohana 4:8 linasema jambo fulani la pekee sana kuhusu upendo: “Mungu ni upendo.” Naam, Yehova ana upendo mwingi sana. Upendo ni utu au sifa ya Mungu ya asili. Kwa ujumla, tunaweza kulifikiria jambo hilo kwa njia hii: Nguvu za Yehova humwezesha kutenda. Haki na hekima yake humwongoza katika utendaji wake. Lakini upendo wa Yehova humchochea kutenda. Naye sikuzote hutumia sifa nyingine zote kupatana na upendo wake.

      3 Mara nyingi imesemwa kwamba Yehova ni wonyesho halisi wa upendo. Kwa hiyo, tukitaka kujifunza kuhusu upendo, ni lazima tujifunze kumhusu Yehova. Basi, na tuchunguze sehemu mbalimbali za upendo wa Yehova usio na kifani.

      Tendo Kuu Zaidi la Upendo

      4, 5. (a) Ni nini lililo tendo kuu zaidi la upendo katika historia yote? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova na Mwana wake wameunganishwa na kifungo cha upendo chenye nguvu kuliko kifungo chochote kile?

      4 Yehova ameonyesha upendo kwa njia nyingi sana, lakini kuna njia moja ya pekee. Ni njia gani hiyo? Ni kumtuma Mwana wake ateseke na kufa kwa ajili yetu. Tunaweza kusema kwa hakika kwamba hilo ndilo tendo kuu zaidi la upendo katika historia yote. Kwa nini tuseme hivyo?

      5 Biblia humwita Yesu “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Hebu fikiria—Mwana wa Yehova alikuwapo kabla ya ulimwengu kuumbwa. Basi, Mwana huyo alikaa na Baba yake kwa muda gani? Wanasayansi fulani wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo kwa muda wa miaka bilioni 13. Lakini, hata kama makisio hayo ni sahihi, urefu wake hauwezi kamwe kuwakilisha umri wa Mwana mzaliwa wa kwanza wa Yehova! Alikuwa akifanya kazi gani wakati huo wote? Mwana huyo alifurahi kutumiwa na Baba yake akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:30; Yohana 1:3) Yehova na Mwana wake walishirikiana kuumba vitu vingine vyote. Walifurahia kama nini kufanya kazi pamoja! Basi, ni nani kati yetu anayeweza kuelewa kwa ukamili nguvu za kifungo ambacho kimekuwapo kwa muda mrefu hivyo? Ni wazi kwamba Yehova Mungu na Mwana wake wameunganishwa na kifungo cha upendo chenye nguvu kuliko kifungo chochote kile.

      6. Yesu alipobatizwa, Yehova alionyeshaje hisia zake kumwelekea?

      6 Hata hivyo, Yehova alimtuma Mwana wake duniani ili azaliwe akiwa mwanadamu. Kwa hiyo, kwa miaka kadhaa Yehova alikosa ushirikiano wa karibu na Mwana wake mpendwa huko mbinguni. Akiwa mbinguni, alipendezwa sana kumtazama Yesu akikua hadi akawa mwanamume mkamilifu. Yesu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi. Pindi hiyo, Baba yake alisema moja kwa moja kutoka mbinguni: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Bila shaka Baba ya Yesu alifurahi sana kumwona akifanya kwa uaminifu yote yaliyotabiriwa, mambo yote ambayo alipaswa kufanya!—Yohana 5:36; 17:4.

      7, 8. (a) Yesu alitendewaje Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., naye Baba yake wa mbinguni alihisije? (b) Kwa nini Yehova aliruhusu Mwana wake ateseke na kufa?

      7 Lakini Yehova alihisije Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu aliposalitiwa na kukamatwa na umati wenye hasira? Alihisije Yesu alipodhihakiwa, kutemewa mate, na kupigwa ngumi? Alihisije alipopigwa mijeledi iliyochanachana mgongo wake? Alihisije mikono na miguu yake ilipopigiliwa misumari kwenye mti, kisha akaachwa akining’inia huku watu wakimtukana? Baba alihisije Mwana wake mpendwa alipokuwa akimlilia kwa maumivu makali? Yehova alihisije Yesu alipokata pumzi, na kwa mara ya kwanza kabisa tangu mwanzo wa uumbaji wote, Mwana wake mpendwa akakoma kuwapo?—Mathayo 26:14-16, 46, 47, 56, 59, 67; 27:26, 38-44, 46; Yohana 19:1.

      8 Kwa kuwa Yehova ana hisia, uchungu ambao alihisi kwa sababu ya kifo cha Mwana wake ni usioweza kuelezeka. Lakini tunaweza kueleza kusudi la Yehova la kuruhusu jambo hilo litukie. Kwa nini Baba ya Yesu alijiruhusu apatwe na uchungu huo? Yehova anafunua jambo la kupendeza katika Yohana 3:16—mstari wa Biblia ambao ni muhimu sana hivi kwamba umeitwa Injili ndogo. Mstari huo unasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” Kwa hiyo, Mungu alifanya hivyo kwa sababu ya upendo. Hilo ndilo tendo kuu zaidi la upendo ambalo limewahi kutendwa na yeyote.

      Jinsi Yehova Anavyotuhakikishia Upendo Wake

      9. Shetani anataka tuamini nini kuhusu jinsi Yehova anavyotuona, lakini Yehova anatuhakikishia nini?

      9 Hata hivyo, swali muhimu linazuka: Je, Mungu anampenda kila mmoja wetu? Baadhi ya watu wanakubali kwamba Mungu anawapenda wanadamu kwa ujumla kama andiko la Yohana 3:16 linavyosema. Lakini wanahisi hivi: ‘Mungu hawezi kamwe kunipenda mimi.’ Shetani Ibilisi anataka sana tuamini kwamba Yehova hatupendi wala hatuthamini. Kwa upande mwingine, Yehova anatuhakikishia kuwa anamthamini kila mmoja wa watumishi wake waaminifu hata kama tunafikiri hatupendwi au hatuthaminiwi.

      10, 11. Mfano wa Yesu wa shore unaonyeshaje kwamba tuna thamani machoni pa Yehova?

      10 Kwa mfano, fikiria maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:29-31. Yesu alitoa mfano huu ili kuonyesha kwamba wanafunzi wake wana thamani: “Je, shore wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na hofu: nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” Hebu fikiria jinsi wasikilizaji wa Yesu katika karne ya kwanza walivyoyaelewa maneno hayo.

      11 Katika siku za Yesu, shore alikuwa ndege wa bei rahisi sana aliyenunuliwa ili kuliwa. Mtu aliyelipa sarafu moja ya thamani ndogo sana, alipewa shore wawili. Lakini kulingana na andiko la Luka 12:6, 7, baadaye Yesu alisema kwamba mtu aliyelipa sarafu mbili, alipewa shore watano badala ya shore wanne. Shore mmoja aliongezwa kana kwamba hakuwa na thamani yoyote. Huenda ndege hao hawakuwa na thamani machoni pa wanadamu, lakini Muumba aliwaonaje? Yesu alisema: “Hakuna hata mmoja wao [hata yule aliyeongezwa] hupata kusahaulika mbele ya Mungu.” Sasa huenda tumeanza kuelewa alilomaanisha Yesu. Ikiwa Yehova anamthamini sana shore mmoja, namna gani mwanadamu! Kama Yesu alivyosema, Yehova anatujua vizuri sana. Kwani, hata nywele za kichwa chetu zimehesabiwa zote!

      12. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu hakutia chumvi aliposema kwamba nywele za kichwa chetu zimehesabiwa?

      12 Huenda wengine wakafikiri kwamba Yesu alitia chumvi. Hata hivyo, hebu fikiria ufufuo. Ni lazima Yehova awe anatujua vizuri sana ili aweze kutuumba upya! Anatuthamini sana hivi kwamba anakumbuka kila jambo, hata chembe zetu za urithi, kumbukumbu, na ujuzi wetu wote. Kichwa cha mtu huwa na nywele 100,000 hivi, kwa hiyo kuhesabu nywele za vichwa vyetu ni jambo rahisi sana ikilinganishwa na kukumbuka mambo hayo yote. Bila shaka, maneno hayo ya Yesu yanatuhakikishia kabisa kwamba Yehova anamjali kila mmoja wetu.

      13. Kisa cha Mfalme Yehoshafati kinaonyeshaje kwamba Yehova hutafuta mema ndani yetu ingawa sisi si wakamilifu?

      13 Biblia hufunua jambo lingine linalotuhakikishia kwamba Yehova anatupenda. Yeye hutafuta na huthamini mema yaliyo ndani yetu. Kwa mfano, fikiria Mfalme Yehoshafati aliyekuwa mwema. Mfalme huyo alipotenda jambo la kipumbavu, nabii wa Yehova alimwambia hivi: “Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa BWANA.” Ulikuwa ujumbe wenye kuogofya kama nini! Lakini ujumbe wa Yehova haukukomea hapo. Uliendelea kusema hivi: “Walakini yameonekana mema ndani yako.” (2 Mambo ya Nyakati 19:1-3) Kwa hiyo, hasira adilifu ya Yehova haikumzuia asione “mema” yaliyokuwa ndani ya Yehoshafati. Inatia moyo sana kujua kwamba Mungu wetu hutafuta mema ndani yetu hata ingawa sisi si wakamilifu.

      Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”

      14. Tunapofanya dhambi tunakuwa na hisia gani zenye kulemea, lakini tunaweza kunufaikaje na msamaha wa Yehova?

      14 Tunapofanya dhambi, sisi huona aibu, hukata tamaa, na kuhisi hatia na huenda hali hiyo ikafanya tufikiri kwamba hatustahili kabisa kumtumikia Yehova. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova ‘amekuwa tayari kusamehe.’ (Zaburi 86:5) Naam, Yehova anaweza kutusamehe dhambi zetu tunapotubu na kujitahidi kabisa kutozirudia. Ona jinsi Biblia inavyofafanua sehemu hiyo yenye kuvutia ya upendo wa Yehova.

      15. Yehova huweka dhambi zetu mbali nasi kadiri gani?

      15 Mtunga-zaburi Daudi alitumia usemi mwingine ulio wazi zaidi kufafanua msamaha wa Yehova: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi.” (Zaburi 103:12, italiki ni zetu.) Mashariki ni mbali kadiri gani kutoka magharibi? Katika maana fulani, sikuzote mashariki huwa mbali kabisa na magharibi; pande hizo mbili haziwezi kamwe kukutana. Msomi mmoja anasema kwamba usemi huo unamaanisha “mbali iwezekanavyo; mbali kabisa.” Maneno ya Daudi yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanatuambia kwamba Yehova anapotusamehe, anaweka dhambi zetu mbali kabisa nasi.

      16. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hutuona kuwa safi baada ya kutusamehe dhambi zetu?

      16 Je, umewahi kujaribu kuondoa doa katika nguo nyeupe? Huenda hukufaulu kuondoa doa hilo ingawa ulijitahidi kadiri unavyoweza. Ona jinsi Yehova anavyoeleza msamaha wake: “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isaya 1:18, italiki ni zetu.) Usemi “nyekundu sana” unaonyesha kwamba rangi hiyo ni nyangavu.a Rangi “nyekundu” ilikuwa mojawapo ya rangi zilizotiwa kwenye nguo. Hatuwezi kamwe kuondoa doa la dhambi kwa jitihada zetu. Lakini Yehova anaweza kuondoa dhambi ambazo ni nyekundu sana na kuzifanya kuwa nyeupe kama theluji au sufu isiyotiwa rangi. Kwa hiyo, Yehova anapotusamehe dhambi zetu, hatupaswi kuhisi kwamba tuna hatia ya dhambi hizo maisha yetu yote.

      17. Ni katika maana gani Yehova hutupa dhambi zetu nyuma yake?

      17 Hezekia alimwambia Yehova hivi katika wimbo wa shukrani wenye kugusa moyo ambao alitunga baada ya kuponywa ugonjwa wa kufisha: “Umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako.” (Isaya 38:17, italiki ni zetu.) Ni kana kwamba Yehova anachukua dhambi za mtenda-dhambi mwenye kutubu na kuzitupa nyuma Yake ambako Hawezi tena kuziona wala kuzikazia fikira. Kichapo kimoja cha kitaalamu kinasema kwamba andiko hilo linaweza kuelezwa hivi: ‘Umefanya iwe ni kana kwamba sikufanya dhambi.’ Je, hilo si jambo lenye kufariji?

      18. Nabii Mika anaonyeshaje kwamba Yehova anapotusamehe Anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu?

      18 Katika ahadi ya urudisho, nabii Mika alieleza usadikisho wake kwamba Yehova angewasamehe watu wake wenye kutubu: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye . . . kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? . . . Nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.” (Mika 7:18, 19, italiki ni zetu.) Hebu fikiria maana ya maneno hayo kwa watu walioishi nyakati za Biblia. Haingewezekana kupata tena kitu kilichotupwa “katika vilindi vya bahari.” Kwa hiyo maneno ya Mika yanamaanisha kwamba Yehova anapotusamehe, anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu.

      “Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”

      19, 20. (a) Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa “onyesha rehema” au “sikitikia” kinamaanisha nini? (b) Biblia hutumiaje hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha kuhusu huruma ya Yehova?

      19 Huruma ni sehemu nyingine ya upendo wa Yehova. Huruma ni nini? Katika Biblia, huruma na rehema zinahusiana sana. Maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanadokeza sifa ya huruma yenye upendo. Kwa mfano, mara nyingi kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ hutafsiriwa “onyesha rehema” au “sikitikia.” Neno hilo la Kiebrania, ambalo Yehova anatumia kujihusu, linahusiana na neno linalomaanisha “tumbo la uzazi” linaloweza kufasiriwa kuwa “huruma ya mama.”

      20 Biblia inatumia hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha kuhusu huruma ya Yehova. Andiko la Isaya 49:15 linasema: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie [ra·chamʹ] mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.” Ni vigumu kuwazia kwamba mama anaweza kusahau kumnyonyesha na kumtunza mtoto wake mchanga. Kwa kweli, mtoto mchanga ni dhaifu; anahitaji kupendwa na kutunzwa na mama yake usiku na mchana. Ingawa hivyo, inasikitisha kupata habari kuhusu akina mama wanaowatupa watoto wao, hasa katika ‘nyakati hizi za hatari.’ (2 Timotheo 3:1, 3) “Lakini mimi sitakusahau wewe,” atangaza Yehova. Huruma nyororo ya Yehova ni yenye nguvu zaidi ya hisia yenye nguvu tunayoweza kuwazia, yaani, huruma ambayo kwa kawaida mama humwonyesha mtoto wake mchanga.

      21, 22. Waisraeli walipatwa na nini katika nchi ya Misri ya kale, naye Yehova aliitikiaje kilio chao?

      21 Yehova huonyeshaje sifa ya huruma akiwa kama mzazi mwenye upendo? Sifa hiyo ya huruma inaonekana wazi kutokana na jinsi alivyolitendea taifa la Israeli la kale. Kufikia mwisho wa karne ya 16 K.W.K., mamilioni ya Waisraeli waliteswa sana walipokuwa watumwa huko Misri. (Kutoka 1:11, 14) Waisraeli walimlilia Yehova awasaidie walipokuwa wakiteseka. Mungu mwenye huruma nyororo aliitikiaje?

      22 Yehova aliwahurumia. Akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao . . . maana nayajua maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Yehova hangeweza kuwatazama watu wake wakiteseka au kusikia vilio vyao na asiwahurumie. Yehova ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Nayo hisia-mwenzi, yaani, sifa ya kuguswa moyo na uchungu wa wengine, inahusiana sana na huruma. Lakini Yehova hakuwahurumia tu watu wake; alichochewa kuwasaidia. Andiko la Isaya 63:9 linasema: “Kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe.” Yehova aliwaokoa Waisraeli kutoka Misri kwa “mkono hodari.” (Kumbukumbu la Torati 4:34) Baadaye, aliwalisha kimuujiza na kuwapa nchi yenye rutuba.

      23. (a) Maneno ya mtunga-zaburi yanatuhakikishiaje kwamba Yehova anamjali sana kila mmoja wetu? (b) Yehova hutusaidia katika njia gani mbalimbali?

      23 Yehova hawahurumii watumishi wake tu wakiwa kikundi. Mungu wetu mwenye upendo anamjali sana kila mmoja wetu. Anajua kabisa mateso yoyote yanayoweza kutupata. Mtunga-zaburi alisema: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:15, 18) Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu? Si lazima aondoe jambo linalofanya tuteseke. Lakini yeye amewapa maandalizi tele wale wanaomwomba msaada. Neno lake lina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kutusaidia sana. Katika kutaniko, Yehova ameweka waangalizi wanaostahili kiroho, ambao hujitahidi kuwa na huruma kama yeye wanapowasaidia waabudu wenzao. (Yakobo 5:14, 15) Akiwa “Msikiaji wa sala,” Yehova huwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Zaburi 65:2, NW; Luka 11:13) Maandalizi hayo yote ni uthibitisho wa “huruma nyororo ya Mungu wetu.”—Luka 1:78.

      24. Utaitikiaje upendo wa Yehova?

      24 Je, si jambo lenye kusisimua kutafakari juu ya upendo wa Baba yetu wa mbinguni? Katika makala iliyotangulia, tulikumbushwa kwamba Yehova ameonyesha nguvu, haki, na hekima yake kwa njia ya upendo ili kutunufaisha. Na katika makala hii tumeona kwamba kwa njia ya pekee, Yehova ameonyesha upendo wake moja kwa moja kwa kila mmoja wetu na kwa wanadamu kwa ujumla. Sasa kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Nitaitikiaje upendo wa Yehova?’ Na uitikie kwa kumpenda kwa moyo wako wote, kwa nafsi yako yote, kwa akili yako yote, na kwa nguvu zako zote. (Marko 12:29, 30) Maisha yako ya kila siku na yaonyeshe kwamba una tamaa ya kutoka moyoni ya kumkaribia Yehova hata zaidi. Na Yehova, Mungu ambaye ni upendo, na akukaribie hata zaidi—milele!—Yakobo 4:8.

      [Maelezo ya Chini]

      a Msomi mmoja anasema kwamba rangi nyekundu “ilikuwa rangi isiyofifia, rangi ya kudumu. Haingeweza kuondolewa na umande, wala mvua, wala kufuliwa, wala kutumiwa kwa muda mrefu.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki