-
Ujumbe wa Yehova wa Wakati Uliopita na LeoIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
6 Hata hivyo, kuna sehemu ya Biblia ambayo kwa wengi ni kama eneo lenye hazina ambalo halijavumbuliwa bado. Sehemu hiyo ni vile vitabu 12 ambavyo mara nyingi huitwa Manabii Wadogo. Kwa kawaida vitabu hivyo hufuata vile vitabu vikubwa zaidi vya Biblia kama vile Ezekieli na Danieli lakini vinatangulia Injili ya Mathayo. (Katika Biblia nyingi, vitabu hivyo 12 vinafuatana hivi: Hosea, Yoeli, Amosi, Obadia, Yona, Mika, Nahumu, Habakuki, Sefania, Hagai, Zekaria, na Malaki.) Kama tulivyoona, Biblia imeongozwa na roho ya Mungu, nayo inafaa kwa kufundisha na kuwaonyesha watu jinsi ya kuishi. Je, hilo linatia ndani vitabu hivyo?
7 Bila shaka! Kwa kweli, vile vitabu vinavyoitwa Manabii Wadogo vina hazina zinazoweza kutuonyesha jinsi ya kuishi leo. Ili kuelewa ni kwa nini watu fulani hupuuza vitabu hivyo, hebu fikiria jina la vitabu hivyo 12 katika lugha nyingi: vinaitwa Manabii Wadogo. Je, jina hilo laweza kuathiri maoni ya watu kuhusu vitabu hivyo? Je, huenda maoni yako kuhusu vitabu hivyo yakawa yameathiriwa kwa kiasi fulani?
JE, WALE “MANABII WADOGO” NI WADOGO KWELI?
8. (a) Mungu hutumia njia gani muhimu kutoa mwongozo? (b) Vile vitabu 12 vinavyozungumziwa huitwaje mara nyingi, hata hivyo, jina hilo linamaanisha nini?
8 Katika barua aliyowaandikia Waebrania, mtume Paulo alianza kwa kusema hivi: “Mungu, ambaye zamani za kale alisema katika pindi nyingi na katika njia nyingi na mababu zetu kupitia manabii, mwishoni mwa siku hizi amesema nasi kupitia Mwana.” (Waebrania 1:1, 2) Kwa kuwa Mungu alitumia manabii wa kibinadamu kuwasilisha ujumbe wake, hatupaswi kamwe kumwona yeyote kati yao au ujumbe wao kuwa “mdogo.” Hata hivyo, jina “Manabii Wadogo” limewafanya watu fulani wazione habari zilizo katika vitabu hivyo kuwa zenye maana ndogo. Wengine wamekata kauli kwamba ujumbe ulio katika vitabu hivyo si muhimu sana kama ule ulio katika vitabu vingine vya Biblia. Hata hivyo, ukweli ni kwamba katika lugha nyingi jina “Manabii Wadogo”a humaanisha tu kwamba vitabu hivyo 12 ni vifupi kuliko vitabu vingine.
9. Kwa nini umuhimu wa kitabu fulani cha Biblia hautegemei urefu wake?
9 Kwa kuwa tu kitabu fulani ni kifupi, haimaanishi kwamba hakina umuhimu wowote kwako. Kitabu cha Ruthu ni kifupi kuliko vitabu vinavyotangulia na vinavyofuata, hata hivyo, habari zilizomo ni zenye kuchochea kwelikweli! Kitabu hicho kifupi hukazia jinsi tunavyopaswa kushikamana na ibada ya kweli, huonyesha jinsi Mungu anavyowathamini sana wanawake, nacho huandaa habari muhimu kuhusu ukoo wa Yesu. (Ruthu 4:17-22) Mfano mwingine ni ule wa kitabu cha Yuda kilicho karibu na mwisho wa Biblia. Ni kifupi sana hivi kwamba katika Biblia fulani zilizochapishwa, hakijazi hata ukurasa mmoja. Hata hivyo, habari na mwongozo uliomo ni wenye thamani sana. Kinaonyesha jinsi Mungu alivyoshughulika na malaika waovu, maonyo kuhusu watu wafisadi waliojipenyeza kutanikoni, na mahimizo ya kuipigania vikali imani! Kwa hiyo basi, unaweza kuwa na uhakika kwamba ingawa vitabu vya wale wanaoitwa Manabii Wadogo ni vifupi, habari zilizomo na faida unayoweza kupata si ndogo.
VYA KINABII—JINSI GANI?
10, 11. (a) Watu fulani hufikiri nini wanaposikia neno “manabii”? (b) Kulingana na Biblia, manabii walikuwa nani, nao walifanya nini?
10 Jambo lingine la kuzingatia ni yale maneno “manabii” na “kinabii.” Huenda maneno hayo yakaleta wazo la kutabiri kuhusu wakati ujao. Watu wengi hufikiri kwamba kazi ya nabii ni kutabiri matukio ya wakati ujao, na kwamba huenda yeye hufanya hivyo kwa kutumia maneno ya kifumbo yanayoweza kufasiriwa katika njia mbalimbali. Mawazo hayo huathiri jinsi watu fulani huviona vitabu hivyo 12.
11 Ni kweli kwamba unaposoma vitabu hivyo 12, muda si muda utaona vina matabiri mengi, na mengi ya matabiri hayo yanahusu kuja kwa ile siku kuu ya Yehova. Hilo linapatana na maana ya msingi ya neno “nabii.” Nabii ni mtu aliyekuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu na mara nyingi alitumiwa kufunua mambo ambayo yangetokea. Kuanzia Enoko, manabii wengi wa Biblia walitabiri kuhusu wakati ujao.—1 Samweli 3:1, 11-14; 1 Wafalme 17:1; Yeremia 23:18; Matendo 3:18; Yuda 14, 15.
12. Unaweza kuonyeshaje kwamba neno nabii linatia ndani mengi zaidi ya kutabiri mambo?
12 Hata hivyo, twahitaji kukumbuka kwamba kazi ya manabii wa Yehova haikuwa tu kutabiri ujumbe wa Mungu. Mara nyingi Mungu aliwatumia manabii wakiwa wasemaji ili kuwaambia wengine mapenzi yake. Kwa mfano, huenda tusiwaone Abrahamu, Isaka, na Yakobo kama watu waliotabiri kuhusu wakati ujao, hata hivyo, andiko la Zaburi 105:9-15 huwaita manabii. Nyakati nyingine, Mungu aliwatumia kufunua jambo fulani la wakati ujao, kama wakati ambapo Yakobo aliwabariki wanawe. Lakini wazee hao wa ukoo walikuwa manabii pia kwa kuwa waliziambia familia zao mambo ambayo Yehova alisema kuhusu jukumu lao katika kutimiza kusudi la Mungu. (Mwanzo 20:7; 49:1-28) Jambo lingine linaloweza kutusaidia kuelewa jinsi Biblia hutumia neno “nabii” ni kwamba Haruni alikuwa nabii wa Musa. Haruni alitimiza jukumu la nabii kwa kuwa msemaji wa, au “kinywa” cha Musa.—Kutoka 4:16; 7:1, 2; Luka 1:17, 76.
13, 14. (a) Mbali na kutabiri, manabii walifanya mambo gani mengine? (b) Unaweza kufaidikaje kwa kujua kwamba kazi ya manabii haikuwa tu kutabiri?
13 Pia, wafikirie manabii Samweli na Nathani. (2 Samweli 12:25; Matendo 3:24; 13:20) Yehova aliwatumia kutangaza mambo ambayo yangetokea wakati ujao, hata hivyo, aliwatumia kama manabii katika njia nyinginezo. Akiwa nabii, Samweli aliwahimiza Waisraeli waache ibada ya sanamu na kurudia ibada safi. Naye alitangaza hukumu ya Mungu dhidi ya Mfalme Sauli, jambo linalotufundisha kwamba Yehova huthamini utii kuliko dhabihu za kimwili. Ndiyo, kazi ya unabii ya Samweli ilitia ndani kutangaza maoni ya Mungu kuhusu njia bora ya kuishi. (1 Samweli 7:3, 4; 15:22) Nabii Nathani alitabiri kwamba Sulemani angejenga hekalu na kwamba ufalme wake ungekuwa imara. (2 Samweli 7:2, 11-16) Hata hivyo, Nathani alikuwa pia akifanya kazi ya nabii alipotaja dhambi ya Daudi na Bath-sheba na dhambi ya Daudi dhidi ya Uria. Ni nani anayeweza kusahau jinsi Nathani alivyoufunua uzinzi wa Daudi kwa kutumia mfano wa tajiri mmoja aliyemchukua mwana-kondoo mpendwa na wa pekee wa maskini mmoja? Nathani pia alikuwa na jukumu la kupanga ibada ya kweli katika patakatifu pa Mungu.—2 Samweli 12:1-7; 2 Mambo ya Nyakati 29:25.
14 Jambo kuu ni kwamba hatupaswi kuona ujumbe ulio katika vitabu hivyo vya kinabii kana kwamba ni matabiri tu ya wakati ujao. Vitabu hivyo vina ujumbe wa Mungu kuhusu mambo mengine mengi, kutia ndani habari nyingi kuhusu jinsi watu wa Mungu wa wakati uliopita walivyopaswa kuishi na jinsi sisi leo tunavyopaswa kuishi. Kwa hiyo, tuna hakika kwamba habari zilizo katika Biblia, kutia ndani vitabu hivyo 12, ni muhimu sana na zenye faida, na huwasaidia watu kuona jinsi ya kuishi maisha bora. Vitabu hivyo vilivyoongozwa kwa roho ya Mungu hutupa mwongozo muhimu sana unaoweza kutusaidia “tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.”—Tito 2:12.
-
-
Ujumbe wa Yehova wa Wakati Uliopita na LeoIzingatie Siku ya Yehova Maishani
-
-
a Kichapo Encyclopaedia Judaica chataja kwamba jina hilo “yaonekana latokana na jina la Kilatini lililo katika Vulgate (Prophetae Minores). Kivumishi ‘-dogo’ katika jina ‘Manabii Wadogo’ hakimaanishi kwamba wale manabii 12 hawakuwa muhimu kwa kuwalinganisha na Isaya, Yeremia, na Ezekieli, badala yake charejelea ufupi wa vitabu hivyo.”—Buku la 12, ukurasa wa 49.
-