-
Kudumisha Msimamo Wetu Tukiwa “Wakaaji wa Muda”Mnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 15
-
-
Kudumisha Msimamo Wetu Tukiwa “Wakaaji wa Muda”
“Nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za kimwili.”—1 PET. 2:11.
1, 2. Petro alikuwa akiwarejelea nani alipotumia maneno “wale waliochaguliwa,” na kwa nini aliwaita “wakaaji wa muda”?
MIAKA 30 hivi baada ya Yesu kwenda mbinguni, mtume Petro aliwaandikia barua “wakaaji wa muda waliotawanyika huku na huku katika Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia, kwa wale waliochaguliwa.” (1 Pet. 1:1) Ni wazi kwamba Petro alitumia maneno “wale waliochaguliwa,” kuwarejelea Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho takatifu na ‘kuzaliwa upya kwenye tumaini lililo hai’ kama yeye ili watawale pamoja na Kristo mbinguni. (Soma 1 Petro 1:3, 4.) Lakini kwa nini baadaye alisema kwamba watu hao waliochaguliwa ni “wageni na wakaaji wa muda”? (1 Pet. 2:11) Na maneno hayo yana maana gani kwetu leo ilhali Mashahidi watendaji wanaodai kuwa watiwa-mafuta waliochaguliwa ni wachache sana, yaani, uwiano wao ni karibu tu mtiwa-mafuta 1 kwa kila Mashahidi 650?
2 Maneno “wakaaji wa muda” yaliwafaa watiwa-mafuta katika karne ya kwanza. Wakristo hao hawakuwa wakaaji wa kudumu duniani sawa na Wakristo watiwa-mafuta walio duniani leo. Mtume Paulo, aliyekuwa mshiriki wa “kundi dogo” lililotiwa mafuta alieleza hivi: “Lakini sisi, uraia wetu uko mbinguni, ambako kutoka huko pia tunamngojea mwokozi kwa hamu, Bwana Yesu Kristo.” (Luka 12:32; Flp. 3:20) Kwa kuwa ‘uraia wao uko mbinguni,’ watiwa-mafuta wanapokufa wanaondoka duniani na kupata kitu bora zaidi, uhai usioweza kufa mbinguni. (Soma Wafilipi 1:21-23.) Kwa hiyo, kihalisi wanaweza kuitwa “wakaaji wa muda” katika dunia iliyo chini ya utawala wa Shetani.
3. Ni swali gani linalozuka kuhusu “kondoo wengine”?
3 Lakini namna gani “kondoo wengine”? (Yoh. 10:16) Je, si ni kweli kwamba wana tumaini thabiti linalotegemea Maandiko la kuwa wakaaji wa kudumu duniani? Bila shaka, wataishi humo milele! Hata hivyo, kwa sasa tunaweza kusema kwamba kwa njia fulani wao ni wakaaji wa muda. Kwa njia gani?
“UUMBAJI WOTE UNAENDELEA KUUGUA”
4. Viongozi wa ulimwengu hawawezi kuzuia nini?
4 Maadamu Yehova anauruhusu mfumo mwovu wa Shetani uendelee kuwapo, kila mtu, kutia ndani Wakristo, wataendelea kuteseka kwa sababu ya uasi wa Shetani dhidi ya Yehova. Tunasoma hivi katika Waroma 8:22: “Tunajua kwamba uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.” Viongozi wa ulimwengu, wanasayansi, na watetezi wa haki za kibinadamu hawawezi kuzuia jambo hilo hata kama wana nia nzuri kadiri gani.
5. Tangu mwaka wa 1914, mamilioni ya watu wamechukua hatua gani, na kwa nini?
5 Kwa hiyo, tangu mwaka wa 1914, mamilioni ya watu wamechagua kwa hiari kuwa raia wa Kristo Yesu, Mfalme aliyetawazwa na Mungu. Hawatamani kuwa sehemu ya mfumo wa ulimwengu wa Shetani. Wanakataa kuunga mkono ulimwengu wa Shetani. Badala yake, wanatumia maisha yao na mali zao kuunga mkono Ufalme wa Mungu, na kuendeleza masilahi yake.—Rom. 14:7, 8.
6. Mashahidi wa Yehova wanaweza kuitwa wakaaji wageni katika maana gani?
6 Naam, Mashahidi wa Yehova ni raia wanaotii sheria katika nchi zaidi ya 200, lakini wao ni kama wakaaji wageni popote wanapoishi. Wanadumisha msimamo wa kutounga mkono kamwe upande wowote ule katika mambo ya kisiasa na ya kijamii. Hata sasa wanajiona kuwa raia wa ulimwengu mpya wa Mungu. Wanashangilia kuona siku zao za kuwa wakaaji wa muda katika mfumo huu wa mambo wa ulimwengu usio mkamilifu zikikaribia haraka kwisha.
7. Watumishi wa Mungu watakuwaje wakaaji wa kudumu, na wataishi wapi?
7 Hivi karibuni Kristo atatumia mamlaka yake kuuharibu mfumo mwovu wa Shetani. Serikali kamilifu ya Kristo itaondoa dhambi na huzuni duniani. Itaondoa kabisa madhara yote yanayoonekana na yasiyoonekana ya uasi dhidi ya enzi kuu halali ya Yehova. Watumishi washikamanifu wa Mungu watapata fursa ya kuwa wakaaji wa kudumu katika Paradiso duniani. (Soma Ufunuo 21:1-5.) Wakati huo, uumbaji utakuwa ‘umewekwa huru kikamili kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Rom. 8:21.
WAKRISTO WA KWELI WANATARAJIWA KUTIMIZA MATAKWA GANI?
8, 9. Eleza alichomaanisha Petro alipotumia maneno “kujiepusha na tamaa za kimwili.”
8 Petro anaeleza matakwa ambayo Wakristo wanatarajiwa kutimiza anaposema hivi: “Wapendwa, nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za kimwili, ambazo ndizo huendelea kupambana na nafsi.” (1 Pet. 2:11) Shauri hilo lilielekezwa kwanza kwa Wakristo watiwa-mafuta, lakini linawahusu pia kondoo wengine wa Yesu.
9 Tamaa fulani si mbaya ikiwa zinatoshelezwa kulingana na maagizo ya Muumba. Kwa kweli, zinaongeza furaha maishani. Kwa mfano, kuna tamaa za kawaida kama vile tamaa ya kufurahia kinywaji na chakula kizuri, kushiriki katika tafrija yenye kuburudisha, na kufurahia urafiki mzuri. Hata tamaa ya kufurahia ngono na mwenzi wa ndoa inafaa na ina wakati wake. (1 Kor. 7:3-5) Hata hivyo, kwa kufaa Petro alizungumzia hasa “tamaa za kimwili” ambazo “huendelea kupambana na nafsi.” Tafsiri fulani za Biblia zinaonyesha waziwazi ni tamaa gani hizo zinapotaja “uchu wa kimwili” (King James Version) au “tamaa zenye dhambi” (New International Version). Kwa wazi, ni lazima mtu adhibiti tamaa yoyote ya kibinadamu inayopingana na kusudi la Yehova lililofunuliwa na inayoweza kuathiri uhusiano wake mzuri pamoja na Mungu. Mkristo asipofanya hivyo anaweza kuhatarisha kabisa tumaini lake la kuendelea kuwa hai.
10. Ni baadhi ya njia gani anazotumia Shetani kuwafanya Wakristo wawe sehemu ya ulimwengu wake?
10 Lengo la Shetani ni kudhoofisha azimio la Wakristo wa kweli la kuwa “wakaaji wa muda” katika mfumo wa sasa. Ni lazima tutambue kwamba Shetani anatumia mitego kama vile fahari ya kuwa na vitu vya kimwili, maadili mapotovu yenye kushawishi, tamaa yenye nguvu ya kuwa maarufu, roho inayovutia ya “mimi kwanza,” na roho ya utaifa yenye uvutano mkubwa. Tukiazimia kabisa kuepuka tamaa hizo za kimwili zisizofaa, tunaonyesha waziwazi kwamba hatutaki kuwa sehemu ya ulimwengu mwovu wa Shetani. Tunathibitisha kwamba sisi ni wakaaji wa muda tu katika ulimwengu huu. Kwa kweli tunachotaka na tunachojitahidi kabisa kupata ni fursa ya kuwa wakaaji wa kudumu katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.
MWENENDO MZURI
11, 12. Nyakati nyingine wageni wanaonwaje, na tunaweza kusema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova?
11 Petro anaendelea kueleza matakwa ambayo Wakristo wanatarajiwa kutimiza wakiwa “wakaaji wa muda.” Anasema hivi katika mstari wa 12: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” Nyakati nyingine, wageni, yaani, wakaaji wa muda katika nchi ya kigeni hushutumiwa. Huenda hata wakaonwa kama watenda-maovu kwa sababu tu ya kuwa tofauti na wenyeji. Usemi wao, matendo yao, na mavazi yao yako tofauti, na labda hata wanaonekana kuwa tofauti kwa njia fulani. Lakini wanapotenda mema, yaani, wanapojiendesha kwa njia nzuri, mambo mabaya ambayo watu wanawasingizia eti kwa sababu wako tofauti, yanathibitika kuwa yasiyo na msingi.
12 Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli wako tofauti na jirani zao wengi katika mambo fulani, kama vile usemi wao au burudani wanayochagua. Mara nyingi, mavazi na mapambo yao yanawatofautisha na watu wengi katika jamii. Nyakati nyingine tofauti hizo zimewafanya watu waliopotoshwa wadai kwamba Wakristo wa kweli ni watenda-maovu. Hata hivyo, huenda watu wengine wakawasifu kwa sababu ya mtindo wao wa maisha.
13, 14. Hekima ‘huonyeshwaje kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake’? Toa mfano.
13 Naam, mwenendo mzuri unaweza kuonyesha kwamba madai ya uwongo hayana msingi. Hata Yesu, mwanadamu pekee aliyewahi kuishi na kudumisha uaminifu mkamilifu kwa Mungu, alishtakiwa kwa uwongo. Watu fulani walimwita “mtu mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya-kodi na watenda-dhambi.” Hata hivyo, ukweli ni kwamba mwenendo wake wa hekima katika utumishi wa Mungu ulithibitisha kwamba madai hayo yalikuwa ya uwongo. Yesu alisema hivi: “Hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mt. 11:19) Ndivyo ilivyo leo pia. Kwa mfano, baadhi ya watu wanaoishi karibu na Betheli ya Selters, Ujerumani, wanaona kwamba ndugu na dada wanaotumika katika Betheli hiyo ni watu wa ajabu. Hata hivyo, meya wa mji huo aliwatetea Wakristo hao kwa kusema hivi: “Ni kweli kwamba Mashahidi wanaotumikia katika majengo hayo wana njia yao ya maisha, lakini hawawasumbui kamwe watu wengine katika jamii.”
14 Maoni kama hayo yalitolewa hivi karibuni kuhusu Mashahidi wa Yehova wanaoishi Moscow, Urusi. Walikuwa wameshtakiwa kwa uwongo kwamba walitenda mambo fulani mabaya. Kisha mnamo Juni 2010, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, Ufaransa, ikatoa uamuzi huu: “Mahakama hii imeona kwamba wenye mamlaka jijini [Moscow] waliingilia bila sababu halali haki ya washtakiwa ya kuwa na uhuru wa kidini na ushirika. Mahakama za Urusi hazikutoa sababu ‘za kutosha na zinazofaa’ kuthibitisha kwamba walalamishi” walikuwa na hatia ya kufanya mambo kama vile kuvunja familia, kuwachochea watu wajiue, au kukataa matibabu. Kwa hiyo, “vizuizi vilivyotangazwa na mahakama za nchi hiyo vilipita mipaka kwa sababu sheria za nchi hazikuzingatia kila jambo na hivyo zilikiuka lengo la kisheria ambalo zilipaswa kutimiza.”
KUJITIISHA IFAAVYO
15. Wakristo wa kweli ulimwenguni pote wanafuata kanuni gani ya Biblia?
15 Mashahidi wa Yehova jijini Moscow, na hata ulimwenguni pote, wanatimiza takwa lingine ambalo Petro anasema linapaswa kutimizwa na Wakristo. Aliandika hivi: “Kwa ajili ya Bwana jitiisheni wenyewe kwa kila kitu kilichofanywa na binadamu: iwe ni kwa mfalme akiwa mkubwa au ni kwa magavana.” (1 Pet. 2:13, 14) Ingawa Wakristo wa kweli si sehemu ya ulimwengu huu mwovu, wanajitiisha kwa hiari kwa wenye mamlaka za kiserikali walio “katika vyeo vyao vya kadiri,” kama Paulo alivyowaagiza.—Soma Waroma 13:1, 5-7.
16, 17. (a) Ni nini kinachothibitisha kwamba hatupingi serikali? (b) Viongozi fulani wa kisiasa wamekiri nini?
16 Mashahidi wa Yehova wanapojiendesha kama “wakaaji wa muda” katika mfumo huu, hawafanyi hivyo kama njia ya kutetea haki zao kimya-kimya; wala hawapingi au kuingilia maamuzi ambayo wengine wanafanya katika masuala ya kisiasa au ya kijamii. Tofauti na vikundi vingine vya kidini, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa. Hawajaribu kamwe kuwashurutisha wenye mamlaka ya kiserikali wafuate sera fulani. Wazo la kwamba wanaweza kuvuruga amani au kuchochea uasi dhidi ya serikali halina msingi kamwe!
17 Wakristo wanafuata shauri la Petro la ‘kumheshimu mfalme’ kwa kuwatii maofisa wa umma na kuwaonyesha heshima na staha wanayostahili kulingana na vyeo vyao. (1 Pet. 2:17) Nyakati nyingine, maofisa wa umma wamekiri kwamba hawana sababu halali ya kuwa na wasiwasi kuhusu Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, Steffen Reiche, mwanasiasa Mjerumani aliyekuwa waziri katika jimbo la Brandenburg na mbunge wa Ujerumani, alisema hivi: “Mwenendo wa Mashahidi wa Yehova walipokuwa kambini na gerezani unaonyesha sifa nzuri ambazo ni muhimu leo na ambazo zilikuwa muhimu zamani ili kuendeleza serikali ya kidemokrasia: hasa msimamo wao imara walipoteswa na askari wa SS na huruma waliyowaonyesha wafungwa wenzao. Tukifikiria jinsi matendo ya kinyama yanavyoongezeka dhidi ya wageni na dhidi ya watu wenye msimamo au maoni tofauti ya kisiasa, kila raia wa nchi yetu anapaswa kuwa na sifa hizo nzuri.”
KUONYESHA UPENDO
18. (a) Kwa nini tunafurahia kuupenda ushirika mzima wa akina ndugu? (b) Watu fulani ambao si Mashahidi wamesema nini kuwahusu?
18 Mtume Petro aliandika hivi: “Upendeni ushirika mzima wa akina ndugu, mwogopeni Mungu.” (1 Pet. 2:17) Mashahidi wa Yehova wana woga unaofaa wa kutompendeza Mungu, nao unawachochea zaidi kufanya mapenzi yake. Wanafurahia kumtumikia Yehova wakiwa sehemu ya ushirika wa ulimwenguni pote wa akina ndugu na dada wanaotamani kufanya vivyo hivyo. Kwa hiyo, wanafurahia ‘kuupenda ushirika mzima wa akina ndugu.’ Upendo huo wa kindugu, usiopatikana kwa urahisi katika ulimwengu wa leo wenye uchoyo, unawashangaza watu ambao si Mashahidi. Kwa mfano, mfanyakazi mmoja wa shirika la Marekani la kupanga safari za watalii alishangaa kuona jinsi Mashahidi walivyowasaidia na kuwaonyesha upendo wajumbe wa nchi nyingine waliohudhuria kusanyiko la kimataifa nchini Ujerumani mwaka wa 2009. Mwanamke huyo alisema kwamba katika miaka yote ambayo amekuwa akiwatembeza watalii, hajawahi kamwe kuona jambo kama hilo. Baadaye, Shahidi mmoja alisema hivi: “Kila jambo alilosema kutuhusu alilisema kwa mshangao na msisimko.” Je, umewahi kusikia watu wakisema vivyo hivyo walipowatazama Mashahidi katika kusanyiko ambalo ulihudhuria?
19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini, na kwa nini?
19 Mashahidi wa Yehova wanaonyesha katika njia hizo zote na nyingine nyingi kwamba kwa kweli wao ni “wakaaji wa muda” katika mfumo huu wa Shetani. Na wameazimia kwa shangwe kuendelea kuwa wakaaji wa muda. Wana tumaini thabiti na lenye kutegemeka kwamba hivi karibuni watakuwa wakaaji wa kudumu katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. Je, hutazamii kwa hamu wakati huo?
-
-
“Wakaaji wa Muda” Waungana Katika Ibada ya KweliMnara wa Mlinzi—2012 | Desemba 15
-
-
“Wakaaji wa Muda” Waungana Katika Ibada ya Kweli
“Watu wa nchi nyingine watakuwa wakulima wenu na watunza-mizabibu wenu. Nanyi mtaitwa makuhani wa Yehova.”—ISA. 61:5, 6.
1. Baadhi ya watu wana maoni gani kuhusu watu wa nchi nyingine, lakini kwa nini maoni hayo hayafai?
KAMA makala iliyotangulia ilivyoonyesha, watu hutumia maneno “mtu wa nchi nyingine” au mgeni ili kumdharau mtu, kumdhihaki, au hata kuonyesha waziwazi kwamba wanamchukia. Si jambo la heshima kuwadharau watu wa taifa lingine. Isitoshe, mtazamo kama huo unaonyesha kwamba hatukubali ukweli wa mambo. Kitabu kimoja (The Races of Mankind) kinasema hivi: “Wanadamu wa jamii zote ni ndugu, kama Biblia inavyosema.” Kwa kawaida, ndugu wanakuwa tofauti sana, lakini vyovyote vile, wao ni ndugu.
2, 3. Yehova ana maoni gani kuhusu watu wa nchi nyingine?
2 Bila shaka, watu wa nchi nyingine wanaishi miongoni mwetu popote tulipo. Ndivyo ilivyokuwa pia kwa Waisraeli wa kale, ambao walikuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova Mungu kwa msingi wa agano la Sheria. Watu hao ambao hawakuwa Waisraeli walikuwa na haki kwa kiasi fulani, hata hivyo, Waisraeli walipaswa kuwatendea kwa heshima na bila ubaguzi. Huo ni mfano mzuri kama nini wa kuiga! Wakristo wa kweli hawapaswi kamwe kuwa na ubaguzi au upendeleo. Kwa nini? Mtume Petro alisema hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Mdo. 10:34, 35.
3 Wageni walioishi katika taifa la kale la Israeli walinufaika kwa kushirikiana kwa ukaribu na Waisraeli. Hilo lilionyesha maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo, maoni ambayo yaliandikwa miaka mingi baadaye na mtume Paulo alipouliza hivi kumhusu Yehova: “Je, yeye ni Mungu wa Wayahudi peke yao? Je, yeye si wa watu wa mataifa pia? Ndiyo, wa watu wa mataifa pia.”—Rom. 3:29; Yoe. 2:32.
4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba hakuna wageni katika taifa la “Israeli wa Mungu”?
4 Kwa msingi wa agano jipya, kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilichukua mahali pa taifa la asili la Israeli na kuwa na uhusiano wa pekee na Mungu. Kwa hiyo, kutaniko hilo linaitwa “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Na kama Paulo alivyoeleza, katika taifa hilo jipya, “hakuna Mgiriki wala Myahudi, tohara wala kutotahiriwa, mgeni, Msikithe, mtumwa, mtu huru, bali Kristo ni kila kitu na katika vitu vyote.” (Kol. 3:11) Basi, ni katika maana hiyo kwamba hakungekuwa na wageni katika kutaniko la Kikristo.
5, 6. (a) Andiko la Isaya 61:5, 6 linaweza kutokeza swali gani? (b) “Makuhani wa Yehova” na “wageni” wanaotajwa na Isaya ni nani? (c) Vikundi hivyo viwili vinashirikiana kufanya kazi gani?
5 Kwa upande mwingine, huenda mtu akarejelea sura ya 61 ya kitabu cha Isaya, ambayo ina unabii unaotimizwa katika kutaniko la Kikristo. Mstari wa 6 wa sura hiyo unawataja wale ambao watatumikia wakiwa “makuhani wa Yehova.” Hata hivyo, mstari wa 5 unawataja “wageni” ambao watashirikiana na kufanya kazi na “makuhani” hao. Tunapaswa kuuelewaje unabii huo?
6 Tunaelewa kwamba hao “makuhani wa Yehova” ni Wakristo watiwa-mafuta walio na sehemu “katika ufufuo wa kwanza” na ambao ‘watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na kutawala wakiwa wafalme pamoja naye ile miaka elfu.’ (Ufu. 20:6) Kwa kuongezea, kuna Wakristo wengi washikamanifu wenye tumaini la kuishi duniani. Wakristo hao ni wageni kwa njia ya mfano, ingawa wanafanya kazi na kushirikiana kwa ukaribu na wale watakaotumika mbinguni. Wanafurahia kuwaunga mkono na kufanya kazi pamoja na “makuhani wa Yehova,” wakitumikia kama “wakulima” na “watunza-mizabibu” wao kwa njia ya mfano. Naam, wanawasaidia watu kusitawisha matunda ya kiroho na kumletea Mungu utukufu, wakiwatunza na kuwavuna watu kwa njia ya mfano. Kwa kweli, watiwa-mafuta na “kondoo-wengine” wanawatafuta na kuwachunga kwa upendo watu wanyoofu wanaotamani kumtumikia Mungu milele.—Yoh. 10:16.
“WAKAAJI WA MUDA” KAMA ABRAHAMU
7. Wakristo leo wako kama Abrahamu na wanaume wengine waaminifu wa kale katika njia gani?
7 Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Wakristo wa kweli ni kama wageni, au wakaaji wa muda, katika ulimwengu mwovu wa Shetani. Kwa hiyo, wanaweza kulinganishwa na wanaume waaminifu wa kale, kama Abrahamu, ambao Biblia inasema kwamba walikuwa “wageni na wakaaji wa muda katika nchi.” (Ebr. 11:13) Hata iwe tuna tumaini gani la wakati ujao, tuna pendeleo la kufurahia uhusiano kama ule ambao Abrahamu alikuwa nao pamoja na Yehova. Yakobo anasema kwamba “‘Abrahamu alikuwa na imani katika Yehova, na ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu,’ naye akaitwa ‘rafiki ya Yehova.’”—Yak. 2:23.
8. Abrahamu alipewa ahadi gani, naye alihisije kuhusu kutimizwa kwa ahadi hiyo?
8 Mungu aliahidi kwamba familia zote duniani—si taifa moja tu—zingebarikiwa kupitia Abrahamu na wazao wake. (Soma Mwanzo 22:15-18.) Ingawa ahadi hiyo ya Mungu ingetimizwa wakati ujao, Abrahamu aliendelea kuwa na hakika kwamba ingetimizwa. Abrahamu alihama-hama pamoja na familia yake kwa zaidi ya miaka tisini. Kwa muda huo wote, Abrahamu alidumisha urafiki wake pamoja na Yehova.
9, 10. (a) Tunaweza kuiga mfano wa Abrahamu katika njia zipi? (b) Tunaweza kuwapa wengine mwaliko gani?
9 Ingawa hakujua angengoja kwa muda mrefu kadiri gani ili aone tumaini lake likitimia, Abrahamu hakuyumbayumba kamwe katika upendo na ujitoaji wake kwa Yehova. Alikazia macho tumaini lake, hakuishi maisha ya kawaida na kuwa mkaaji wa kudumu katika taifa fulani. (Ebr. 11:14, 15) Ni jambo la hekima kama nini kwetu kuiga mfano wa Abrahamu kwa kuishi maisha rahisi na kutohangaikia kupita kiasi vitu vya kimwili, vyeo katika jamii, au kutafuta kazi zenye mshahara mnono! Kwa nini tung’ang’ane kuwa na yale yanayoitwa eti maisha ya kawaida katika mfumo ambao utaangamia hivi karibuni? Kwa nini ushikamane sana na kitu ambacho ni cha muda mfupi tu? Kama Abrahamu, tunatazamia kupata kitu bora zaidi. Tuko tayari kuonyesha mtazamo wa kungojea kwa subira hadi tumaini letu litimie.—Soma Waroma 8:25.
10 Yehova bado anawaalika watu wa mataifa yote ili wapate baraka kupitia uzao wa Abrahamu. Na “makuhani wa Yehova” waliotiwa mafuta, na vilevile “wageni,” yaani, kondoo wengine, wanawatolea watu ulimwenguni pote mwaliko huo katika lugha zaidi ya 600.
USIWABAGUE WATU WA MATAIFA MENGINE
11. Sulemani alisema jambo gani ambalo liliwahusu watu wengine wasio Waisraeli?
11 Wakati wa uzinduzi wa hekalu mwaka wa 1026 K.W.K., na kupatana na ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu, Sulemani alisema kwamba watu wa mataifa yote wangeshiriki katika kumsifu Yehova. Alisali hivi kutoka moyoni: “Pia kwa mgeni, ambaye si sehemu ya watu wako Israeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako (kwa maana watasikia habari za jina lako kuu na za mkono wako wenye nguvu na za mkono wako ulionyooshwa), naye kwa kweli aje na kusali kuelekea nyumba hii, basi na usikilize ukiwa mbinguni, makao yako yaliyofanywa imara, nawe ufanye kulingana na yote ambayo mgeni huyo anakuomba; kusudi watu wote wa dunia wajue jina lako ili wakuogope kama vile watu wako Israeli wanavyokuogopa.”—1 Fal. 8:41-43.
12. Kwa nini huenda watu fulani wanawaona Mashahidi wa Yehova kuwa watu wa ajabu au kama “wageni”?
12 Mgeni ni mtu anayeishi katika nchi ya kigeni au mtu anayejiunga na jamii au kikundi fulani. Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova walivyo. Wanawajibika kwanza kwa serikali ya kimbingu, yaani, Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo. Hivyo, hawajihusishi kamwe na mambo ya kisiasa, hata ikiwa wengine wanawaona kuwa watu wa ajabu wasiofaa katika jamii ya leo.
13. (a) Kwa nini mara nyingi maana ya neno “mgeni” inategemea maoni ya mtu binafsi? (b) Je, kusudi la Yehova la mwanzoni lilitia ndani wazo la wageni? Eleza.
13 Kwa kawaida wageni wanatambuliwa kwa sababu ya mambo fulani yanayowafanya waonekane kuwa tofauti na wengine. Wanaweza kutambuliwa kwa lugha yao, desturi zao, mwonekano au sura yao, au mavazi yao. Hata hivyo, mambo yanayowatofautisha na wengine ni machache yakilinganishwa na mambo yanayofanya wafanane na wanadamu wengine wote bila kujali ni wa taifa gani. Basi, kwa kweli mtu huonwa kuwa mgeni kwa sababu yuko tofauti katika njia fulani. Tunapojifunza kutokazia fikira mambo hayo yanayofanya mtu aonekane kuwa tofauti, inaelekea kwamba hatutamwona yeyote kuwa “mgeni” katika maana hiyo. Ikiwa watu wote duniani wangeishi chini ya serikali au chama kimoja cha kisiasa, hakungekuwa na mgeni katika maana ya kisiasa. Kwa kweli, Yehova alikusudia mwanzoni wanadamu wote waungane wakiwa familia moja chini ya utawala mmoja—utawala wake. Je, watu wa mataifa yote duniani wanaweza kuwa kama familia moja chini ya utawala mmoja leo?
14, 15. Mashahidi wa Yehova wamethamini nini wakiwa kikundi?
14 Katika ulimwengu wenye roho ya uchoyo na utaifa, inaburudisha kuona watu wasiowabagua watu wa mataifa mengine. Kwa kweli, si rahisi kuishinda roho ya ubaguzi. Mwanzilishi wa kituo cha televisheni cha CNN, Ted Turner, anaeleza jinsi alivyohisi alipofanya kazi na watu wenye vipawa kutoka katika mataifa mbalimbali: “Nilifurahi sana kukutana na watu hao. Nilijifunza kuwaona watu kutoka nchi nyingine kuwa raia wenzangu badala ya kuwaona kuwa ‘wageni.’ Nilianza kuona neno ‘mgeni’ kuwa neno la dharau na nikaweka sheria katika kituo cha CNN ya kwamba neno hilo lisitumiwe katika vipindi vya televisheni au katika mazungumzo ofisini. Badala yake, niliwaamuru watumie neno ‘kimataifa.’”
15 Katika nchi zote duniani, ni Mashahidi wa Yehova peke yao wakiwa kikundi wanaoiga njia ya Mungu ya kufikiri. Kwa sababu wamejifunza kuona mambo kama Yehova anavyoyaona, wamefanikiwa kushinda mawazo na hisia za ubaguzi kuelekea watu wa mataifa mengine. Badala ya kuwatilia shaka, kutowaamini, au hata kuwachukia watu wa mataifa mengine, wamejifunza kuthamini uwezo na sifa mbalimbali za watu hao nao wanaziona kuwa zenye kuvutia. Je, umetafakari kuhusu jambo hilo la pekee na kuona jinsi ambavyo limekunufaisha unaposhughulika na wengine?
ULIMWENGU USIO NA WAGENI
16, 17. Utimizo wa Ufunuo 16:16 na Danieli 2:44 utamaanisha nini kwako?
16 Hivi karibuni mataifa yote yatakabiliana na Yesu Kristo na majeshi yake ya kimbingu katika vita vya mwisho dhidi ya utawala wa Mungu, vita ambavyo ‘vinaitwa katika Kiebrania Har–Magedoni.’ (Ufu. 16:14, 16; 19:11-16) Miaka zaidi ya 2,500 iliyopita, nabii Danieli aliongozwa na roho ya Mungu kutabiri mambo yatakayozipata serikali za wanadamu zinazopinga kusudi la Mungu. Aliandika hivi: “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Dan. 2:44.
17 Je, waweza kuwazia manufaa utakayopata wakati unabii huo utakapotimizwa? Hakutakuwa tena na mipaka ya kitaifa iliyowekwa na wanadamu inayomfanya kila mtu awe mgeni kwa njia fulani leo. Tofauti zozote zilizopo za kimaumbile au sifa nyingine za kawaida za kimwili zitaonyesha tu kwamba Mungu aliumba vitu vingi vya aina mbalimbali vyenye kustaajabisha. Tumaini hilo lenye kusisimua linapaswa kutuchochea sote tuendelee kadiri tunavyoweza kumsifu na kumheshimu Muumba wetu, Yehova Mungu.
Je, unatazamia wakati ambapo hakutakuwa tena na mipaka ya kitaifa iliyowekwa na wanadamu, wala hakutakuwa na “mgeni”?
18. Ni matukio gani ya hivi karibuni yanayoonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hawawaoni wengine kuwa “wageni”?
18 Je, ni ndoto tu kuamini kwamba kutakuwa na mabadiliko hayo duniani? Hapana, kwa kweli si ndoto. Kinyume chake, ni jambo linalopatana kabisa na akili kuamini kwamba dunia itabadilika. Hata sasa, Mashahidi wa Yehova hawawaoni wengine kuwa “wageni” kwa sababu hawatilii maanani mataifa ya wale wanaoshirikiana nao. Kwa mfano, hivi karibuni ofisi kadhaa ndogo za Mashahidi wa Yehova ziliunganishwa ili kurahisisha usimamizi katika maeneo hayo na kuwasaidia kutimiza kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa njia bora zaidi. (Mt. 24:14) Kwa kadiri ambavyo matakwa ya kisheria yaliruhusu, hawakuzingatia mipaka ya kitaifa walipounganisha ofisi hizo. Huo pia ni uthibitisho unaoonyesha wazi kwamba Yesu Kristo, Mtawala aliyetawazwa kihalali na Yehova, anavunja mipaka iliyowekwa na wanadamu, na hivi karibuni ‘atakamilisha ushindi wake’!—Ufu. 6:2.
19. Lugha safi ya kweli imewawezesha watu wa Yehova kuwa na hali gani?
19 Mashahidi wa Yehova wanatoka katika mataifa mengi nao wanazungumza lugha nyingi mbalimbali, lakini wanajitahidi kudumisha lugha safi ya kweli. Lugha hiyo inawawezesha kuwa na kifungo cha umoja ambacho hakiwezi kuvunjwa. (Soma Sefania 3:9.) Mashahidi wa Yehova si sehemu ya mfumo huu mwovu licha ya kwamba wanaishi ndani yake, badala yake wao ni familia moja ya kimataifa. Familia hiyo yenye umoja inaonyesha kwa kadiri ndogo tu jinsi mambo yatakavyokuwa katika ulimwengu utakaokuja ambao hautakuwa na wageni. Kila mtu atakayeishi wakati huo atafurahi kuona ukweli wa maneno haya yaliyosemwa na kitabu kilichonukuliwa awali: “Wanadamu wa jamii zote ni ndugu, kama Biblia inavyosema.”—The Races of Mankind.
-