Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Mtu Anaweza Kufanya Mambo Mema Siku ya Sabato?
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
    • Yesu akizungumza na mgonjwa katika dimbwi la Bethzatha

      SURA YA 29

      Je, Mtu Anaweza Kufanya Mambo Mema Siku ya Sabato?

      YOHANA 5:1-16

      • YESU AHUBIRI HUKO YUDEA

      • AMPONYA MTU MGONJWA KWENYE DIMBWI

      Yesu amefanya mambo mengi wakati wa huduma yake kuu huko Galilaya. Hata hivyo, anaposema, “Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika majiji mengine,” Yesu anafikiria maeneo mengine zaidi ya Galilaya. Hivyo, anaenda “kuhubiri katika masinagogi ya Yudea.” (Luka 4:43, 44) Hilo linapatana na akili kwa sababu ni majira ya kuchipua na hivi karibuni kutakuwa na sherehe huko Yerusalemu.

      Katika Injili tunapata mambo machache sana kuhusu utendaji wa Yesu huko Yudea, kwa kulinganisha na mambo tunayosoma kuhusu huduma yake huko Galilaya. Hata kama watu hawapendezwi huko Yudea, hilo halimzuii Yesu kuhubiri kwa bidii na kufanya mambo mema popote alipo.

      Baada ya muda mfupi Yesu anaelekea Yerusalemu, jiji kuu la Yudea, kwa ajili ya Pasaka ya mwaka 31 W.K. Katika eneo lenye shughuli nyingi lililo karibu na Lango la Kondoo, kuna dimbwi kubwa lenye safu ya nguzo liitwalo Bethzatha. Watu wengi wagonjwa, vipofu, na vilema wanakuja kwenye dimbwi hilo. Kwa nini? Kwa sababu inaaminiwa kwamba watu wanaweza kuponywa wakiingia kwenye dimbwi hilo maji yanapotibuliwa.

      Ni siku ya Sabato, naye Yesu anamwona mwanamume fulani kando ya dimbwi hilo ambaye amekuwa mgonjwa kwa miaka 38. Yesu anamuuliza: “Je, unataka kupona?” Mtu huyo anajibu: “Bwana, sina mtu wa kuniweka ndani ya dimbwi maji yanapotibuliwa, lakini ninapotaka kuingia, mtu mwingine huingia kabla yangu.”—Yohana 5:6, 7.

      Yesu anasema jambo ambalo lazima linamshangaza mwanamume huyo na wengine wanaosikia: “Simama! Chukua mkeka wako, utembee.” (Yohana 5:8) Na hivyo ndivyo anavyofanya. Papo hapo anapona, anachukua mkeka wake na kuanza kutembea!

      Wayahudi wakizungumza na mtu aliyeponywa

      Badala ya kushangilia kwa sababu ya jambo la kustaajabisha lililotokea, Wayahudi wanamwona mtu huyo na kumhukumu wakisema: “Ni Sabato, hupaswi kubeba mkeka.” Mtu huyo anawajibu: “Yule aliyeniponya aliniambia, ‘Beba mkeka wako utembee.’” (Yohana 5:10, 11) Wayahudi hao wanamshutumu mtu anayeponya siku ya Sabato.

      “Ni nani huyo aliyekuambia, ‘Beba mkeka wako utembee’?” wanauliza. Kwa nini wanamuuliza mtu huyo hivyo? Kwa sababu Yesu “ameingia katika umati,” na mtu huyo aliyeponywa hajui jina la Yesu. (Yohana 5:12, 13) Lakini mtu huyo atakutana tena na Yesu. Baadaye, mtu huyo anakutana na Yesu hekaluni na kumtambua mtu aliyemponya kwenye dimbwi.

      Mtu huyo aliyeponywa anawatafuta Wayahudi waliomuuliza kuhusu kuponywa kwake. Anawaambia kwamba Yesu ndiye aliyemponya. Wanapojua hivyo, Wayahudi hao wanamwendea Yesu. Je, wanamwendea ili kujua Yesu anafanya miujiza hiyo kwa uwezo wa nani? Hapana. Badala yake, wanaenda kumshutumu Yesu kwa kufanya mambo mema siku ya Sabato. Hata wanaanza kumtesa!

      • Kwa nini Yesu anaenda Yudea, na bado anaendelea kufanya nini?

      • Kwa nini watu wengi wanaenda kwenye dimbwi liitwalo Bethzatha?

      • Yesu anafanya muujiza gani kwenye dimbwi, na baadhi ya Wayahudi wanatendaje kuhusu jambo lililotokea?

  • Uhusiano Kati ya Yesu na Baba Yake
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
    • Wayahudi wakimshutumu Yesu kwamba anavunja Sabato

      SURA YA 30

      Uhusiano Kati ya Yesu na Baba Yake

      YOHANA 5:17-47

      • MUNGU NI BABA YA YESU

      • AHADI YA UFUFUO

      Wayahudi fulani wanapomshutumu Yesu kwamba anavunja Sabato kwa kumponya mtu, Yesu anawajibu: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, nami ninaendelea kufanya kazi.”—Yohana 5:17.

      Jambo ambalo Yesu anafanya halijakatazwa na Sheria ya Mungu kuhusu Sabato. Kwa kuhubiri na kuponya, Yesu anaiga kazi njema za Mungu. Basi Yesu anaendelea kufanya mambo mema kila siku. Anapowajibu wale wanaomshutumu, wanakasirika hata zaidi, nao wanataka kumwua Yesu. Kwa nini?

      Zaidi ya kuwa na maoni yenye makosa kwamba Yesu anavunja Sabato kwa kuwaponya watu, wanakasirika sana anaposema kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Wanaona kwamba anakufuru kwa kusema Mungu ni Baba yake, kana kwamba Yesu anaposema Yehova ni Baba yake anamaanisha kwamba analingana na Mungu. Hata hivyo, Yesu haogopi na anaendelea kuwaeleza kuhusu uhusiano wake wa pekee pamoja na Mungu. Anasema: “Baba anampenda Mwana na humwonyesha mambo yote anayofanya.”—Yohana 5:20.

      Baba ndiye Mpaji-Uhai, na ameonyesha hivyo nyakati zilizopita kwa kuwawezesha wanadamu kuwafufua wafu. Yesu anaendelea kusema: “Kama vile Baba anavyowafufua wafu na kuwafanya kuwa hai, ndivyo Mwana pia anavyowafanya kuwa hai wale anaotaka.” (Yohana 5:21) Maneno hayo muhimu yanatoa tumaini zuri ajabu kwa ajili ya wakati ujao! Hata sasa, Mwana anawafufua watu waliokufa kiroho. Basi Yesu anasema: “Yeyote ambaye husikia neno langu na kumwamini Yule aliyenituma ana uzima wa milele, naye hahukumiwi bali amevuka kutoka katika kifo na kuingia kwenye uzima.”—Yohana 5:24.

      Kufikia sasa Yesu hajamfufua mtu yeyote aliyekufa, lakini anawaeleza wale wanaomshtumu kwamba atawafufua watu kihalisi. Anasema: “Saa inakuja ambayo wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

      Ingawa Yesu ana jukumu la pekee, anaonyesha waziwazi kwamba yuko chini ya Mungu anaposema: “Siwezi kufanya jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe. . . . Sitafuti mapenzi yangu mwenyewe, bali mapenzi ya yule aliyenituma.” (Yohana 5:30) Hata hivyo, Yesu anafafanua jukumu lake muhimu katika kusudi la Mungu, anafanya hivyo hadharani, jambo ambalo hakuwa amefanya kufikia wakati huo. Lakini wale wanaomshutumu Yesu wana ushahidi mwingine mbali na ushahidi wa Yesu. Yesu anawakumbusha: “Mmewatuma watu kwa Yohana [Mbatizaji], naye ametoa ushahidi kuhusu kweli.”—Yohana 5:33.

      Huenda wale wanaomshutumu Yesu walisikia kwamba miaka miwili iliyopita, Yohana alikuwa amewaambia viongozi wa dini ya Kiyahudi kuhusu Yule anayekuja baada yake—aliyeitwa “Nabii” na “Kristo.” (Yohana 1:20-25) Akiwakumbusha wale wanaomshutumu jinsi wakati fulani walivyomheshimu Yohana ambaye sasa amefungwa gerezani, Yesu anasema: “Kwa wakati mfupi mlikuwa tayari kufurahia sana mwangaza wake.” (Yohana 5:35) Lakini Yesu anatoa ushahidi mkubwa hata kuliko Yohana.

      “Kazi hizi ninazofanya [kutia ndani uponyaji ambao amefanya hivi punde] zinatoa ushahidi kwamba Baba alinituma.” Zaidi ya hilo, Yesu anasema: “Baba aliyenituma ametoa ushahidi kunihusu.” (Yohana 5:36, 37) Kwa mfano, Yesu alipobatizwa Mungu alitoa ushahidi kumhusu.—Mathayo 3:17.

      Kwa kweli wale wanaomshutumu Yesu hawana sababu ya kumkataa. Maandiko wanayodai kwamba wanayachunguza yanatoa ushahidi kumhusu Yesu. Yesu anamalizia kwa kusema: “Ikiwa mngemwamini Musa mngeniamini pia, kwa sababu aliandika kunihusu. Lakini ikiwa hamwamini mambo aliyoandika, mnawezaje kuamini mambo ninayosema?”—Yohana 5:46, 47.

      • Kwa nini Yesu havunji Sabato anapofanya mambo mema siku hiyo?

      • Yesu anafafanuaje jukumu lake muhimu katika kusudi la Mungu?

      • Ni ushahidi gani unaothibitisha kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu?

  • Wakata Masuke ya Nafaka Siku ya Sabato
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
    • Wanafunzi wa Yesu wakata masuke na kula nafaka siku ya Sabato

      SURA YA 31

      Wakata Masuke ya Nafaka Siku ya Sabato

      MATHAYO 12:1-8 MARKO 2:23-28 LUKA 6:1-5

      • WANAFUNZI WAKATA MASUKE YA NAFAKA SIKU YA SABATO

      • YESU NDIYE “BWANA WA SABATO”

      Sasa Yesu na wanafunzi wake wanasafiri kuelekea kaskazini huko Galilaya. Ni majira ya kuchipua na katika mashamba, mimea imezaa nafaka. Kwa kuwa wanafunzi wana njaa wanakata masuke ya nafaka na kula. Lakini ni siku ya Sabato na Mafarisayo wanaona kile ambacho wanafunzi wanafanya.

      Kumbuka kwamba hivi karibuni Wayahudi fulani huko Yerusalemu walitaka kumuua Yesu, wakimshtumu kwamba anavunja Sabato. Sasa Mafarisayo wanaleta mashtaka kuhusu jambo wanalofanya wanafunzi. “Tazama! Wanafunzi wako wanafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato.”—Mathayo 12:2.

      Mafarisayo wanadai kwamba kukata masuke ya nafaka na kuyapukusa mikononi ili kula, ni kuvuna na kupura. (Kutoka 34:21) Ufafanuzi wao usio na usawaziko kuhusu kazi unafanya Sabato iwe yenye kuchosha, ingawa ilipoanzishwa ilipaswa kuwa siku yenye shangwe na inayojenga kiroho. Yesu anapinga maoni yao yenye makosa kwa kutoa mifano inayoonyesha kwamba Yehova Mungu hakukusudia sheria Yake kuhusu Sabato itekelezwe kwa njia hiyo.

      Mfano mmoja ambao Yesu anatoa unahusu Daudi na wanaume waliokuwa pamoja naye. Walipohisi njaa, walisimama kwenye hema la ibada na kula mikate ya wonyesho. Mikate hiyo ambayo ilikuwa tayari imeondolewa mbele za Yehova na badala yake mikate mingine ikawekwa, kwa kawaida ilipaswa kuliwa na makuhani. Hata hivyo, chini ya hali walizokuwa nazo, Daudi na wanaume hao hawakushutumiwa kwa kula mikate hiyo.—Mambo ya Walawi 24:5-9; 1 Samweli 21:1-6.

      Yesu anatoa mfano wa pili, anasema: “Je, hamjasoma katika Sheria kwamba siku ya Sabato makuhani huvunja Sabato na wanabaki bila hatia?” Anamaanisha kwamba hata katika siku ya Sabato, makuhani huchinja wanyama kwa ajili ya dhabihu na kufanya kazi nyingine hekaluni. Yesu anasema: “Lakini ninawaambia, hapa pana mtu mkuu kuliko hekalu.”—Mathayo 12:5, 6; Hesabu 28:9.

      Tena Yesu anatumia Maandiko kufafanua hoja yake: “Kama mngeelewa maana ya maneno haya, ‘Ninataka rehema si dhabihu,’ hamngewalaumu watu wasio na hatia.” Anamalizia kwa kusema: “Kwa maana Mwana wa binadamu ndiye Bwana wa Sabato.” Yesu anarejezea utawala wake unaokuja wa Ufalme wenye amani wa miaka elfu moja.—Mathayo 12:7, 8; Hosea 6:6.

      Kwa muda mrefu, wanadamu wameteseka chini ya utumwa mgumu wa Shetani, uliojaa ukatili na vita. Hali zitakuwa tofauti sana chini ya Sabato kuu ya utawala wa Kristo, ambaye ataandaa muda wa kupumzika tunaotamani na kuhitaji sana!

      • Mafarisayo wanaleta mashtaka gani dhidi ya wanafunzi wa Yesu, na kwa nini?

      • Yesu anarekebishaje maoni ya Mafarisayo?

      • Yesu ni “Bwana wa Sabato” katika njia gani?

  • Ni Mambo Gani Yaliyo Halali Siku ya Sabato?
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
    • Yesu akiwa karibu kumponya mwanamume aliyepooza mkono

      SURA YA 32

      Ni Mambo Gani Yaliyo Halali Siku ya Sabato?

      MATHAYO 12:9-14 MARKO 3:1-6 LUKA 6:6-11

      • KUMPONYA MTU MKONO SIKU YA SABATO

      Ni siku nyingine ya Sabato, Yesu anaenda kwenye sinagogi, huenda ni huko Galilaya. Humo anampata mtu aliyepooza mkono wa kulia. (Luka 6:6) Waandishi na Mafarisayo wanamtazama Yesu kwa makini. Kwa nini? Wanafunua nia yao wanapouliza: “Je, ni halali kumponya mtu siku ya Sabato?”—Mathayo 12:10.

      Viongozi wa dini ya Kiyahudi wanaamini kwamba ni halali kuponya katika siku ya Sabato iwapo tu uhai umo hatarini. Kwa hiyo, siku ya Sabato si halali kutibu mfupa uliovunjika au kufunga kiungo kilichoteguka, kwa sababu hali hizo hazihatarishi uhai. Ni wazi kwamba Mafarisayo wanapomuuliza Yesu maswali si kwa sababu wanamhangaikia kikweli mtu huyu anayeteseka. Wanajaribu kupata sababu ya kumshutumu Yesu.

      Hata hivyo, Yesu anajua maoni yao yaliyopotoka. Anatambua kwamba wana maoni yasiyo na usawaziko na yasiyopatana na maandiko kuhusu kuvunja amri ya kutofanya kazi siku ya Sabato. (Kutoka 20:8-10) Tayari amekabiliana na shutuma kama hizo zisizo na msingi kwa sababu ya kufanya mambo mema. Sasa Yesu anaanzisha makabiliano anapomwambia hivi mwanamume aliyepooza mkono: “Simama uje hapa katikati.”—Marko 3:3.

      Yesu anawageukia waandishi na Mafarisayo na kuwaambia: “Ukiwa na kondoo mmoja, naye kondoo huyo atumbukie shimoni siku ya Sabato, je, kuna yeyote kati yenu ambaye hatamshika na kumtoa humo?” (Mathayo 12:11) Kondoo anaweza kuwaletea pesa, hivyo hawawezi kumwacha shimoni hadi siku inayofuata; anaweza kufia humo na kuwaletea hasara. Isitoshe, Maandiko yanasema: “Mwadilifu huwatunza wanyama anaowafuga.”—Methali 12:10.

      Akionyesha jinsi mambo hayo yanavyohusiana, Yesu anaendelea kusema: “Kwa kweli, mwanadamu ni mwenye thamani sana kuliko kondoo! Basi ni halali kutenda mema siku ya Sabato.” (Mathayo 12:12) Kwa hiyo, Yesu hatavunja Sabato ikiwa atamponya mtu huyo. Viongozi hao wa kidini wanashindwa kupinga hoja hizo zinazopatana na akili na zenye huruma. Wanakaa kimya tu.

      Akiwa na hasira na huzuni kwa sababu ya maoni yao yenye makosa, Yesu anatazama huku na huku. Kisha anamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” (Mathayo 12:13) Yule mtu anapounyoosha mkono wake uliopooza, unapona. Mtu huyo anafurahi sana, lakini vipi kuhusu wale wanaojaribu kumtega Yesu?

      Viongozi wa Kiyahudi wapanga njama ya kumuua Yesu

      Badala ya kufurahi kwamba yule mtu ameponywa mkono, Mafarisayo wanaenda nje na mara moja wanapanga njama “na wafuasi wa chama cha Herode ili wamuue Yesu.” (Marko 3:6) Inaelekea chama hiki cha kisiasa kinatia ndani washiriki wa kikundi cha kidini cha Masadukayo. Kwa kawaida, Masadukayo na Mafarisayo hawaelewani, lakini sasa wameungana kabisa ili kumpinga Yesu.

      • Ni nini kinachosababisha makabiliano kati ya Yesu na viongozi wa dini ya Kiyahudi?

      • Viongozi wa dini ya Kiyahudi wana maoni gani yenye makosa kuhusu sheria ya Sabato?

      • Yesu anapingaje kwa hekima maoni yasiyofaa kuhusu Sabato?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki