-
Mungu Alimwita “Binti ya Mfalme”Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 5
-
-
Miaka kumi imepita tangu Abrahamu na familia yake kubwa walipovuka Mto Efrati na kuingia Kanaani. Sara alimuunga mkono mume wake kwa hiari kwenye safari hii bila kujua walipokuwa wakienda. Alijua kwamba Abrahamu angetimiza jukumu muhimu katika kusudi la Yehova la kutokeza taifa na uzao wa pekee sana. Lakini, Sara angetimiza jukumu gani? Alikuwa na umri wa miaka 75 na hakuwa na mtoto. Huenda alijiuliza hivi, ‘Kwa kuwa mimi ni tasa, ahadi ya Yehova itatimizwaje?’ Kwa hakika tunaweza kuelewa vizuri jinsi alivyohangaika au hata kukosa subira.
-
-
Mungu Alimwita “Binti ya Mfalme”Mnara wa Mlinzi (Toleo la Watu wote)—2017 | Na. 5
-
-
Badala ya kuzingatia mambo aliyoacha, Sara alikazia fikira wakati ujao. Aliendelea kumuunga mkono mume wake walipohama-hama katika nchi hiyo, akimsaidia kukunja mahema, kusafiri na mifugo, na kupiga kambi tena. Alivumilia changamoto na mabadiliko mengine pia. Kwa mara nyingine, Yehova alimwambia Abrahamu kuhusu ahadi yake, lakini hakumtaja Sara kwenye mazungumzo hayo!—Mwanzo 13:14-17; 15:5-7.
Mwishowe, Sara aliamua kumpendekezea Abrahamu jambo lililokuwa akilini mwake. Hebu wazia jinsi uso wake ulivyokuwa na hisia nyingi alipomwambia: “Tafadhali sasa! Yehova amenifunga nisizae watoto.” Kisha akamwomba mume wake, Abrahamu, amchukue kijakazi wake, Hagari, ili wapate watoto. Je, unaweza kuwazia jinsi Sara alivyohangaika kumwambia mume wake jambo hilo? Huenda tukashangazwa na ombi hilo leo, lakini nyakati hizo, lilikuwa jambo la kawaida kwa mwanamume kuchukua mke wa pili au suria ili kupata mrithi.b Je, huenda Sara alifikiri kwamba kusudi la Mungu la kutokeza uzao kupitia Abrahamu lingetimia kwa njia hiyo? Vyovyote vile, alikuwa tayari kujidhabihu kwa njia kubwa. Abrahamu aliitikiaje? Biblia inasema, Abrahamu “akaisikiliza sauti ya [Sara].”—Mwanzo 16:1-3.
Je, simulizi hilo linadokeza kwamba Yehova alimwongoza Sara kumweleza Abrahamu jambo hilo? Hapana. Badala yake, pendekezo la Sara linafunua njia ya mwanadamu ya kuona mambo. Alifikiri kwamba Mungu ndiye aliyesababisha matatizo yake, na hakuwazia ikiwa Mungu alikuwa na njia nyingine ya kuyasuluhisha. Uamuzi wa Sara ungemletea taabu na uchungu yeye mwenyewe. Kwa kupendeza, ombi lake lilionyesha hakuwa mbinafsi. Je, haipendezi kuona jinsi ambavyo Sara alikuwa mfano bora kwa kutokuwa na ubinafsi licha ya kuzungukwa na wanadamu wanaofuatilia tamaa zao wenyewe? Tutakuwa tunaiga imani ya Sara ikiwa tuko tayari kutanguliza mapenzi ya Mungu na si yetu.
-