-
Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 1
-
-
Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?
Kumbukumbu la Torati 10:12, 13
JE, NITII au nisitii? Si rahisi sikuzote kufanya uamuzi huo. Mtu anapokuwa mkali au mwenye kudai mengi kupita kiasi huenda watu walio chini yake wakatii kwa kulazimishwa. Hata hivyo, Yehova Mungu hupewa utii wa hiari na waabudu wake. Kwa nini? Ili kujibu swali hilo acheni tuchunguze maneno ya Musa yanayopatikana kwenye Kumbukumbu la Torati 10:12, 13.a
Akijumlisha matakwa ya Mungu, Musa aliuliza swali hili lenye kuamsha fikira: “Yehova Mungu wako anataka nini kutoka kwako?” (Mstari wa 12) Mungu ana haki ya kudai chochote anachotaka kutoka kwetu. Kwa kweli, yeye ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu na ndiye Chanzo na Mtegemezaji wa uhai. (Zaburi 36:9; Isaya 33:22) Hiyo ni sababu yenye nguvu ya kudai utii kutoka kwetu. Hata hivyo, hataki tumtii kwa kulazimishwa. Anataka nini kutoka kwetu? Kwamba ‘tutii kutoka moyoni.’—Waroma 6:17.
Ni nini kinachoweza kutuchochea tumtii Mungu kwa hiari? Musa anataja sababu moja: “Kumwogopa Yehova Mungu wako.”b (Mstari wa 12) Huo si woga wa kupata matokeo mabaya bali ni woga unaotokana na kumheshimu Mungu na njia zake. Ikiwa tunamwogopa Mungu kwa njia inayofaa, tutaepuka kumkasirisha.
Lakini nia yetu kuu ya kumtii Mungu inapaswa kuwa nini? Musa alisema hivi: “Kumpenda [Yehova] na kumtumikia Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote.” (Mstari wa 12) Kumpenda Mungu kunahusisha mengi kuliko hisia. Kitabu kimoja kinaeleza: “Vitenzi vya Kiebrania vinavyorejelea hisia nyakati nyingine hurejelea matokeo ya hisia hizo.” Kitabu hichohicho kinasema kwamba kumpenda Mungu kunamaanisha “kutenda kwa upendo” kumwelekea Mungu. Kwa maneno mengine, ikiwa kwa kweli tunampenda Mungu, tutatenda kwa njia ambazo tunajua zitamfurahisha.—Methali 27:11.
Tumtii Mungu kadiri gani? Musa anasema: ‘Tembea katika njia zote za Mungu.’ (Mstari wa 12) Yehova anataka tufanye yote anayotuomba tufanye. Je, utii kamili kama huo unaweza kutuletea madhara? Hilo haliwezekani.
-
-
Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?Mnara wa Mlinzi—2009 | Oktoba 1
-
-
a Ingawa maneno ya Musa yaliwahusu Waisraeli wa kale, yanawahusu pia watu wote wanaotaka kumpendeza Mungu leo.—Waroma 15:4.
-