Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Paradiso Yarudishwa!
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • Kuzaliwa kwa Taifa Jipya

      19. Kwa nini twaweza kusema kwamba unabii wa Isaya una utimizo wa kiasi tu katika karne ya sita K.W.K.?

      19 Hapana budi utimizo wa unabii wa Isaya sura ya 35 ni wa kiasi tu katika karne ya sita K.W.K. Hali za kiparadiso wanazofurahia Wayahudi waliorudishwa ni za muda tu. Baadaye, mafundisho ya kidini yasiyo ya kweli na uzalendo zachafua ibada safi. Wayahudi wapata tena huzuni na majonzi ya kiroho. Hatimaye Yehova awakataa wasiwe watu wake. (Mathayo 21:43) Furaha yao haidumu kwa sababu ya kutotii ambako kumetokea tena. Hayo yote yaonyesha kuwepo kwa utimizo mwingine ulio mkubwa zaidi wa Isaya sura ya 35.

      20. Kulitokea Israeli gani jipya katika karne ya kwanza W.K.?

      20 Kwa wakati wa Yehova uliowekwa, Israeli nyingine ya kiroho ilitokea. (Wagalatia 6:16) Yesu alitayarisha msingi wa kuzaliwa kwa hilo Israeli jipya wakati wa huduma yake duniani. Aliirudisha ibada safi, na maji ya ile kweli yakaanza kutiririka tena kupitia mafundisho yake. Aliwaponya wagonjwa, kimwili na kiroho vilevile. Sauti ya furaha ilisikika huku habari njema za Ufalme wa Mungu zikihubiriwa. Majuma saba baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu aliyetukuzwa alianzisha kutaniko la Kikristo, Israeli la kiroho linalojumlisha Wayahudi na watu wengine waliokombolewa na damu ya Yesu iliyomwagwa, wakazaliwa kuwa wana wa kiroho wa Mungu na ndugu za Yesu, na kutiwa-mafuta kwa roho takatifu.—Matendo 2:1-4; Waroma 8:16, 17; 1 Petro 1:18, 19.

  • Paradiso Yarudishwa!
    Unabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
    • 21. Kuhusiana na kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, ni matukio gani yawezayo kuonwa kuwa utimizo wa mambo fulani ya unabii wa Isaya?

      21 Akiandikia washiriki wa Israeli la kiroho, mtume Paulo alirejezea maneno ya Isaya 35:3, akisema: “Inyoosheni mikono ining’iniayo na magoti yaliyodhoofishwa.” (Waebrania 12:12) Basi, yaonekana kwamba maneno ya Isaya sura ya 35 yalitimizwa katika karne ya kwanza W.K. Yesu na wanafunzi wake waliwawezesha vipofu kuona tena kihalisi na viziwi kusikia tena kwa njia ya mwujiza. Waliwawezesha “vilema” kutembea na mabubu kusema tena. (Mathayo 9:32; 11:5; Luka 10:9) Jambo la maana zaidi ni kwamba wenye mioyo minyofu waliponyoka kutoka dini isiyo ya kweli nao wakaanza kufurahia paradiso ya kiroho katika kutaniko la Kikristo. (Isaya 52:11; 2 Wakorintho 6:17) Kama ilivyokuwa kwa Wayahudi waliokuwa wakirudi kutoka Babiloni, hao walioponyoka walitambua uhitaji wa roho nzuri na yenye ujasiri.—Waroma 12:11.

      22. Wakristo waaminifu, waliotafuta kweli katika nyakati za kisasa waliingiaje kwenye utekwa wa Kibabiloni?

      22 Namna gani leo? Je, unabii wa Isaya una utimizo mwingine, ulio kamili zaidi uhusuo kutaniko la Kikristo leo? Ndiyo. Baada ya mitume kufa, idadi ya Wakristo wa kweli ilipungua sana, na “magugu,” yaani Wakristo wasio wa kweli, yakasitawi duniani. (Mathayo 13:36-43; Matendo 20:30; 2 Petro 2:1-3) Hata wakati watu walio waaminifu katika karne ya 19 walipoanza kujitenga na Jumuiya ya Wakristo na kutafuta ibada safi, uelewevu wao bado ulichafuliwa na mafundisho yasiyopatana na Maandiko. Yesu alitawazwa kuwa Mfalme wa Kimesiya mwaka wa 1914, lakini muda mfupi baadaye, hali ya watu hao wenye kutafuta kweli kwa uaminifu ilionekana kuwa mbaya. Kama ilivyotabiriwa, mataifa ‘yalifanya vita pamoja nao na kuwashinda,’ na majaribio ya Wakristo hao waaminifu ya kuhubiri habari njema yakazimwa. Babiloni ikawateka.—Ufunuo 11:7, 8.

      23, 24. Maneno ya Isaya yametimia kwa njia zipi miongoni mwa watu wa Mungu tangu mwaka wa 1919?

      23 Hata hivyo, mambo yalibadilika mwaka wa 1919. Yehova aliwatoa watu wake utekwani. Walianza kuyakataa mafundisho yasiyo ya kweli yaliyochafua ibada yao hapo awali. Basi wakaponywa. Wakaingia katika paradiso ya kiroho, ambayo yaendelea kusambaa duniani kote hata sasa. Vipofu wanajifunza kuona na viziwi kusikia kwa njia ya kiroho—wakitambua waziwazi utendaji wa roho takatifu ya Mungu, daima wakitambua uhitaji wa kukaa karibu na Yehova. (1 Wathesalonike 5:6; 2 Timotheo 4:5) Huku ububu wao ukiwa umeondolewa, Wakristo wa kweli wana hamu ya ‘kuimba,’ wakiwatangazia wengine kweli za Biblia. (Waroma 1:15) Wale waliokuwa dhaifu kiroho, au “vilema,” sasa waonyesha bidii na furaha. Wao waweza ‘kuruka-ruka kama kulungu’ kitamathali.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki