-
Unaweza Kuwa Rafiki ya YehovaFurahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
5. Mambo ambayo Yehova anatarajia kutoka kwa rafiki zake
Kwa kawaida sisi hutazamia mambo fulani kutoka kwa rafiki zetu.
Ni mambo gani ambayo ungependa rafiki zako wakufanyie?
Soma 1 Yohana 5:3, kisha mzungumzie swali hili:
Yehova anatarajia nini kutoka kwa rafiki zake?
Ili kumtii Yehova, tunapaswa kubadili mwenendo na tabia zetu. Soma Isaya 48:17, 18, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini Yehova anataka rafiki zake wabadili mwenendo na tabia zao?
Rafiki mzuri hutukumbusha kufanya mambo yanayoweza kutulinda na kutunufaisha. Yehova hufanya vivyo hivyo pia kwa rafiki zake
-
-
Tunaweza Kuonyeshaje Kwamba Tunampenda Yehova?Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 34
Tunaweza Kuonyeshaje Kwamba Tunampenda Yehova?
Tangu ulipoanza kujifunza Biblia, je, upendo wako kwa Mungu umeongezeka? Je, ungependa kuendelea kuimarisha urafiki wako na Mungu? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba Yehova anapoona upendo wako kwake ukizidi kuongezeka, ndivyo atakavyoendelea kukupenda na kukujali zaidi. Unawezaje kumwonyesha kwamba unampenda?
1. Tunawezaje kumwonyesha Yehova kwamba tunampenda?
Tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova kwa kumtii. (Soma 1 Yohana 5:3.) Yehova hamlazimishi mtu yeyote amtii. Badala yake, amempa kila mmoja wetu nafasi ya kuamua ikiwa tutamtii au la. Kwa nini? Yehova anataka tuwe “watiifu kutoka moyoni.” (Waroma 6:17) Hilo linamaanisha kwamba anataka tumtii si kwa kulazimishwa, bali kwa sababu tunampenda. Sehemu ya 3 na ya 4 ya kitabu hiki imekusudiwa kukusaidia kuonyesha kwamba unampenda Yehova kwa kufanya mambo yanayomfurahisha na kuepuka mambo anayochukia.
2. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwetu kumpenda Yehova?
“Mwadilifu ana matatizo mengi.” (Zaburi 34:19) Sote tunapambana na hali yetu ya kutokamilika. Huenda pia tukakabili matatizo ya kiuchumi, ukosefu wa haki, na matatizo mengine. Tunapokabili matatizo, huenda isiwe rahisi kwetu kumtii Yehova. Kwa sababu matatizo yanaweza kufanya iwe vigumu kumtii Yehova. Lakini ikiwa utakuwa mwaminifu na kumtii Yehova, utaonyesha kwamba unampenda kuliko kitu kingine chochote. Na utathibitisha kwamba wewe ni mshikamanifu kwake. Naye atakuwa mshikamanifu kwako. Hatakuacha kamwe.—Soma Zaburi 4:3.
CHIMBA ZAIDI
Chunguza kwa nini Yehova anafurahi unapomtii, na ujifunze jinsi unavyoweza kuendelea kuwa mwaminifu kwake.
3. Suala linalokuhusu
Katika kitabu cha Biblia cha Ayubu, Shetani alitokeza madai si dhidi ya Ayubu tu, bali pia dhidi ya kila mtu anayetaka kumtumikia Yehova. Soma Ayubu 1:1, 6–2:10, kisha mzungumzie maswali haya:
Kulingana na madai ya Shetani, kwa nini Ayubu alimtii Yehova?—Ona Ayubu 1:9-11.
Shetani anadai nini kuhusu wanadamu wote, kutia ndani wewe?—Ona Ayubu 2:4.
Soma Ayubu 27:5b, kisha mzungumzie swali hili:
Ayubu alithibitishaje kwamba alimpenda sana Yehova?
Ayubu alithibitisha kwamba anampenda Yehova kwa kuendelea kuwa mshikamanifu kwake
Tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova tunapoendelea kuwa washikamanifu kwake
4. Fanya moyo wa Yehova ushangilie
Soma Methali 27:11, kisha mzungumzie maswali haya:
Yehova anahisije unapotenda kwa hekima na kumtii? Kwa nini?
5. Unaweza kuwa mshikamanifu kwa Yehova
Upendo wetu kwa Yehova hutuchochea kuwaambia wengine kumhusu. Ushikamanifu wetu kwake hutuchochea kufanya hivyo hata inapokuwa vigumu. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.
Je, wakati mwingine ni vigumu kwako kuwaambia wengine kumhusu Yehova?
Katika video hiyo, ni nini kilichomsaidia Grayson ashinde woga wake?
Ni rahisi kuwa washikamanifu kwa Yehova ikiwa tunapenda mambo anayopenda na kuchukia mambo anayochukia. Soma Zaburi 97:10, kisha mzungumzie maswali haya:
Kutokana na mambo uliyojifunza, ni baadhi ya mambo gani ambayo Yehova anapenda? Na anachukia mambo gani?
Unawezaje kujifunza kupenda mambo mazuri na kuchukia mambo mabaya?
6. Tunanufaika tunapomtii Yehova
Sikuzote kumtii Yehova ndilo jambo bora. Soma Isaya 48:17, 18, kisha mzungumzie maswali haya:
Je, tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova anajua jambo linalotufaa kabisa? Kwa nini?
Kufikia sasa, umenufaikaje kwa kujifunza Biblia na kumhusu Mungu wa kweli, Yehova?
WATU FULANI HUSEMA: “Mungu hajali ninachofanya.”
Unaweza kutumia andiko gani kuthibitisha kwamba matendo yetu yanaweza kumfurahisha au kumhuzunisha Yehova?
MUHTASARI
Unaweza kuonyesha kwamba unampenda Yehova kwa kumtii na kuendelea kuwa mshikamanifu kwake hata unapokabili changamoto.
Ungejibuje?
Mfano wa Ayubu umekufundisha nini?
Utathibitishaje kwamba unampenda Yehova?
Ni nini ambacho kitakusaidia uendelee kuwa mshikamanifu kwa Yehova?
CHUNGUZA ZAIDI
Ona jinsi unavyoweza kuwa mshikamanifu kwa Yehova na kutaniko?
Jifunze kuhusu madai ya Shetani dhidi ya wanadamu.
“Ayubu Adumisha Utimilifu” (Biblia—Ina Ujumbe Gani? sehemu ya 6)
Ona jinsi vijana na watoto wanavyoweza kuonyesha kwamba wanampenda Yehova.
Vijana wanawezaje kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu hata wanaposhinikizwa na vijana wenzao?
-
-
Jinsi ya Kufanya Maamuzi MazuriFurahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 35
Jinsi ya Kufanya Maamuzi Mazuri
Kila mtu hufanya maamuzi. Maamuzi tunayofanya yanaweza kuwa na matokeo mazuri au mabaya na yanaweza kuathiri urafiki wetu na Yehova. Kwa mfano, huenda tukahitaji kuamua mahali tutakapoishi, kazi tutakayofanya, au ikiwa tutafunga ndoa. Tunapofanya maamuzi mazuri, tunakuwa na maisha yenye furaha na tunamfurahisha Yehova.
1. Biblia inaweza kukusaidiaje kufanya maamuzi mazuri?
Kabla ya kufanya uamuzi, sali kwa Yehova umwombe akusaidie kisha uchunguze maoni yake katika Biblia kuhusu jambo hilo. (Soma Methali 2:3-6.) Wakati fulani, Yehova hutuambia jambo hususa la kufanya. Ikiwa kuna amri hususa, jambo la busara ni kutii mwongozo huo.
Namna gani ikiwa hakuna amri hususa katika Biblia kuhusu jambo unalopaswa kufanya? Bado Yehova atakuongoza “katika njia unayopaswa kutembea.” (Isaya 48:17) Jinsi gani? Unaweza kupata kanuni ambazo zitakuongoza. Kanuni za Biblia ni kweli za msingi zinazofunua mawazo na hisia za Mungu. Kwa kawaida tunaelewa maoni ya Mungu kuhusu jambo fulani tunaposoma simulizi la Biblia. Tunapoelewa jinsi Yehova anavyohisi, tunaweza kufanya maamuzi yanayomfurahisha.
2. Unapaswa kufikiria mambo gani kabla ya kufanya uamuzi?
Biblia inasema: “Mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Hilo linamaanisha kwamba kabla ya kufanya uamuzi tunapaswa kufikiria kwa makini mambo yote yanayohusika. Unapochunguza kila jambo, jiulize hivi: ‘Ni kanuni gani za Biblia zinazohusika? Ni uamuzi gani ambao utaniletea amani ya akili? Uamuzi wangu utakuwa na matokeo gani kwa watu wengine? Jambo muhimu zaidi, je, uamuzi huu utamfurahisha Yehova?’—Kumbukumbu la Torati 32:29.
Yehova ana haki ya kutuamulia mambo mema na mabaya. Tunapoelewa vizuri sheria na kanuni zake na kuazimia kuzifuata, tunazoeza dhamiri yetu. Dhamiri ni uwezo ulio ndani yetu wa kutambua mambo yanayofaa na yasiyofaa. (Waroma 2:14, 15) Tukizoeza dhamiri yetu, itatusaidia kufanya maamuzi mazuri.
CHIMBA ZAIDI
Jifunze jinsi dhamiri na kanuni za Biblia zinavyoweza kutusaidia kufanya maamuzi.
3. Fuata mwongozo wa Biblia
Kanuni za Biblia zinaweza kutusaidiaje kufanya maamuzi? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.
Yehova ametupatia zawadi gani ya pekee?
Kwa nini Yehova alitupatia uhuru wa kujiamulia?
Ametupatia nini ili kutusaidia kufanya maamuzi bora?
Ili uone mfano wa kanuni ya Biblia, soma Waefeso 5:15, 16. Kisha mzungumzie jinsi unavyoweza ‘kutumia vizuri kabisa wakati wako’ ili . . .
kusoma Biblia kwa ukawaida.
kuwa mume, mke, mzazi, mwana, au binti bora.
kuhudhuria mikutano ya kutaniko.
4. Zoeza dhamiri yako kufanya maamuzi mazuri
Kunapokuwa na amri hususa ya Maandiko kuhusu jambo, ni rahisi kufanya uamuzi unaofaa. Lakini vipi ikiwa hakuna amri hususa? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Dada katika video hiyo alichukua hatua gani ili kuzoeza dhamiri yake na kufanya uamuzi uliomfurahisha Yehova?
Kwa nini hatupaswi kuwaomba watu wengine watufanyie maamuzi? Soma Waebrania 5:14, kisha mzungumzie maswali haya:
Ingawa huenda ikawa rahisi kuwaomba wengine watufanyie maamuzi, tunapaswa kuwa na uwezo wa kutofautisha nini?
Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuzoeza dhamiri yetu na kufanya maamuzi mazuri?
Dhamiri ni kama ramani inayotuongoza kufanya maamuzi maishani
5. Heshimu dhamiri za watu wengine
Maamuzi yetu hutofautiana na maamuzi ya watu wengine. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaheshimu dhamiri za watu wengine? Fikiria hali mbili zinazofuata:
Hali ya 1: Dada anayependa kujipamba anahamia kutaniko ambalo dada wengi wanakwazika wanapoona watu wakijipamba.
Soma Waroma 15:1 na 1 Wakorintho 10:23, 24, kisha mzungumzie maswali haya:
Kulingana na maandiko haya, dada huyo anaweza kuamua kufanya nini? Utafanya nini unaposhughulika na mtu ambaye dhamiri yake inamkataza kufanya jambo ambalo dhamiri yako inakubali?
Hali ya 2: Ndugu ambaye anajua kwamba Biblia haikatazi kunywa kileo kwa kiasi, lakini anaamua kutokunywa kileo. Anakaribishwa kwenye tafrija ambapo anaona akina ndugu wakinywa kileo.
Soma Mhubiri 7:16 na Waroma 14:1, 10, kisha mzungumzie maswali haya:
Kulingana na maandiko haya, ndugu huyo anaweza kuamua kufanya nini? Utafanya nini ukimwona mtu anafanya jambo ambalo dhamiri yako inakuzuia kufanya?
Hatua zinazotusaidia kufanya maamuzi mazuri.
1. Mwombe Yehova akusaidie kuamua jambo la kufanya.—Yakobo 1:5.
2. Fanya utafiti katika Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia ili upate kanuni zinazohusika. Unaweza pia kuzungumza na Wakristo wenye uzoefu.
3. Fikiria matokeo ya uamuzi utakaofanya, yaani, jinsi utakavyoathiri dhamiri yako na dhamiri za watu wengine.
WATU FULANI HUSEMA: “Una haki ya kufanya chochote unachopenda, bila kujali maoni ya watu wengine.”
Kwa nini tunapaswa kufikiria maoni ya Mungu, na maoni ya watu wengine?
MUHTASARI
Tunafanya maamuzi mazuri tunapochunguza maoni ya Yehova kuhusu jambo fulani na kufikiria ikiwa maamuzi yetu yatawasaidia watu wengine au kuwasababishia madhara.
Ungejibuje?
Unawezaje kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova?
Unawezaje kuizoeza dhamiri yako?
Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unaheshimu dhamiri za watu wengine?
CHUNGUZA ZAIDI
Unawezaje kufanya maamuzi yatakayoimarisha urafiki wako na Mungu?
“Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima” (Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 2011)
Jifunze jinsi Yehova anavyotupatia ushauri.
Ona mambo yaliyomsaidia mwanamume fulani kufanya uamuzi mgumu.
Jifunze kufanya mambo yanayomfurahisha Yehova hata kama hakuna sheria hususa.
“Je, Sikuzote Unahitaji Amri ya Biblia?” (Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 2003)
-