-
Kitabu Cha Biblia Namba 27—Danieli“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
-
-
4, 5. Akiolojia imeondoleaje mbali madai ya wachambuzi wa Biblia kuhusiana na Danieli?
4 Ingawa wachambuzi wa Biblia wametilia shaka ukweli wa kihistoria wa kitabu cha Danieli, mavumbuzi ya kiakiolojia kwa miaka iliyopita yameyamaliza nguvu kabisa maoni wanayoshikilia. Kwa kielelezo, wachambuzi hao walifanyia mzaha wenye dharau taarifa ya Danieli kwamba Belshaza alikuwa mfalme katika Babuloni wakati ambapo Nabonido alikuwa akisemwa kuwa ndiye mtawala. (Dan. 5:1) Sasa akiolojia imethibitisha kwa kadiri isiyoweza kutiliwa shaka kwamba Belshaza alikuwa mtu halisi na kwamba alikuwa mfalme-mwenzi wa Nabonido katika miaka ya mwisho ya Milki ya Kibabuloni. Kwa kielelezo, maandishi-kabari ya kale yanayoelezwa kuwa “Simulizi la Aya la Nabonido” yathibitisha waziwazi kwamba Belshaza alikuwa na mamlaka ya kifalme kule Babuloni na yaeleza namna alivyokuwa mtawala-mwenzi wa Nabonido.b Uthibitisho mwingine wa maandishi-kabari waunga mkono maoni ya kwamba Belshaza alitimiza madaraka ya kifalme. Bamba moja, la tarehe ya mwaka wa 12 wa Nabonido, lina kiapo kilichofanywa katika jina la Nabonido, mfalme, na Belshaza, mwana wa mfalme, hivyo kuonyesha kwamba Belshaza alikuwa na daraja moja na babake.c Hilo pia ni jambo la kupendeza katika kueleza kwa nini Belshaza alijitolea kumfanya Danieli “mtu wa tatu katika ufalme” ikiwa angeweza kufasiri ule mwandiko ukutani. Nabonido angeonwa kuwa ndiye wa kwanza, Belshaza angekuwa wa pili, na Danieli angetangazwa kuwa ndiye mtawala wa tatu. (Dan. 5:16, 29) Mtafiti mmoja asema hivi: “Marejezo ya maandishi-kabari yanayogusia habari za Belshaza yametokeza nuru nyingi sana juu ya jukumu alilotimiza hivi kwamba mahali pake katika historia panafunuka wazi. Kuna maandishi mengi yanayoonyesha kwamba Belshaza alikaribia kuwa na cheo na fahari inayolingana na ya Nabonido. Imethibitishwa hakika kwamba kulikuwa na utawala wenye sehemu mbili katika muda mwingi wa umaliki wa mwisho wa Babuloni Mpya. Nabonido alitumia mamlaka iliyo kubwa zaidi akiwa katika ua wake katika Tema katika Uarabu, hali Belshaza alitenda akiwa mfalme-mwenzi katika bara la maskani ya kwao, huku Babuloni ikiwa ndicho kitovu cha maongozi. Kuna uthibitisho wa kwamba Belshaza hakuwa naibu-mfalme aliye mnyonge; yeye aliaminishwa ‘ule umaliki.’”d
-
-
Kitabu Cha Biblia Namba 27—Danieli“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
-
-
11. Ni wakati wa anasa gani isiyo ya adili ambapo Belshaza aona ule mwandiko wa mkono unaomaanisha msiba, Danieli aufasirije, nao watimizwaje?
11 Karamu ya Belshaza: mwandiko wa mkono wafasiriwa (5:1-31). Sasa ni ule usiku wenye msiba wa Oktoba 5, 539 K.W.K. Mfalme Belshaza, mwana wa Nabonido, akiwa mfalme-mwenzi wa Babuloni, afanya karamu kubwa kwa ajili ya waheshimiwa wake elfu moja. Mfalme huyo, akiwa chini ya uvutano wa divai, aitisha vile vyombo vitakatifu vya dhahabu na fedha kutoka kwenye hekalu la Yehova, na Belshaza na wageni wake wavinywea, katika anasa yao isiyo ya adili, huku wakisifu miungu yao ya kipagani. Mara hiyo mkono watokea na kuandika ukutani ujumbe uliofichika maana. Mfalme atetemeka kwa woga. Wanaume wake wenye hekima washindwa kufasiri mwandiko huo. Mwishowe Danieli aletwa ndani. Mfalme afanya toleo la kumfanya awe wa tatu katika ufalme ikiwa aweza kusoma na kufasiri mwandiko ule, lakini Danieli amwambia ajiwekee mwenyewe zawadi zake. Ndipo aendelea kujulisha mwandiko ule na maana yao: “MENE, MENE, TEKELI, NA PERESI. . . . Mungu ameuhesabu ufalme wako na kuukomesha. . . . Umepimwa katika mizani nawe umeonekana kuwa umepunguka. . . . Ufalme wako umegawanyika, nao wamepewa Wamedi na Waajemi.” (5:25-28) Usiku uo huo Belshaza auawa, na Dario Mmedi apokea ufalme ule.
-