-
Alijifunza Kutokana na Makosa YakeIgeni Imani Yao
-
-
18, 19. Ni nini kilichompata Yona alipozama baharini, ni kiumbe gani aliyehusika, na ni nani aliyekuwa akiongoza mambo? (Ona pia maelezo ya chini.)
18 Lakini hebu ngoja! Aliona kitu fulani kikimkaribia, kilikuwa kikubwa, cheusi, na kilicho hai. Kilizidi kumkaribia zaidi na zaidi. Kikafungua mdomo mkubwa, na kummeza!
Yehova ‘alimweka samaki mkubwa ammeze Yona’
19 Yona akadhani amefikia mwisho wake. Hata hivyo, alishangazwa na jambo fulani. Bado alikuwa hai! Hakuwa amevunjwa-vunjwa, kumeng’enywa, wala hakushindwa kupumua. Bado alikuwa hai, hata ingawa ilionekana alikuwa katika kaburi lake. Pole kwa pole, Yona akajawa na hofu. Bila shaka, ni Mungu wake, Yehova, ‘aliyemweka samaki mkubwa ammeze Yona.’c—Yona 1: 17.
20. Tunajifunza nini kumhusu Yona kutokana na sala aliyotoa alipokuwa ndani ya yule samaki mkubwa?
20 Muda ulizidi kusonga. Akiwa katika giza kubwa zaidi, Yona alipata nafasi ya kutafakari na kusali kwa Yehova Mungu. Sala yake, ambayo imerekodiwa katika sura ya pili ya kitabu cha Yona, inafunua mengi. Inaonyesha kwamba Yona alikuwa na ujuzi mwingi wa Maandiko, kwa sababu mara nyingi inarejelea Zaburi. Pia, inaonyesha sifa fulani nzuri ya Yona: alikuwa mwenye shukrani. Alimalizia hivi: “Lakini mimi, kwa sauti ya kutoa shukrani nitakutolea dhabihu. Nilichoweka nadhiri, nitakitimiza. Wokovu ni wa Yehova.”—Yona 2:9.
21. Yona alijifunza nini kuhusu wokovu, na tunajifunza mambo gani muhimu?
21 Yona alijifunza kwamba Yehova anaweza kumwokoa mtu yeyote, wakati wowote, mahali popote, hata “ndani ya tumbo la samaki.” Yehova alimpata humo na kumwokoa mtumishi wake aliyekuwa taabani. (Yona 1:17) Ni Yehova peke yake ambaye angemhifadhi mtu hai kwa siku tatu mchana na usiku ndani ya tumbo la samaki mkubwa. Leo, tunapaswa kukumbuka kwamba ‘pumzi yetu imo mkononi mwa’ Yehova Mungu. (Dan. 5:23) Tuko hai kwa sababu ya mapenzi yake. Je, tunaonyesha shukrani? Hivyo basi, tunapaswa kumtii Yehova.
22, 23. (a) Baada ya muda roho ya shukrani ya Yona ilijaribiwaje? (b) Tunajifunza nini kutokana na Yona kuhusu makosa tunayofanya?
22 Namna gani Yona? Je, alijifunza kumwonyesha Yehova shukrani kwa kumtii? Ndiyo. Baada ya siku tatu mchana na usiku, samaki huyo alimpeleka hadi ufuoni na “akamtapika Yona kwenye nchi kavu.” (Yona 2:10) Hebu fikiria—baada ya mambo hayo yote, Yona hakuhitaji kuogelea hadi ufuoni! Bila shaka, alipaswa kutafuta njia ya kutoka ufuoni. Hata hivyo, baada ya muda roho yake ya kuonyesha shukrani ilijaribiwa. Andiko la Yona 3:1, 2 linasema: “Ndipo neno la Yehova likamjia Yona mara ya pili, na kusema: ‘Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie neno ninalokuambia.’” Yona angefanya nini?
-
-
Alijifunza Kutokana na Makosa YakeIgeni Imani Yao
-
-
c Katika Kigiriki, neno la Kiebrania “samaki,” lilitafsiriwa “kiumbe mkubwa wa baharini,” au “samaki mkubwa.” Ingawa hatuwezi kuthibitisha ni kiumbe gani wa baharini aliyehusika, imegunduliwa kwamba katika Bahari ya Mediterania kuna papa wakubwa wanaoweza kummeza mtu mzima. Kuna papa wakubwa zaidi katika maeneo mengine, kwa mfano, papa-nyangumi anaweza kukua kufikia urefu wa mita 15 au zaidi!
-