Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Baraka ya Yehova Hutajirisha
    Mnara wa Mlinzi—1992 | Desemba 1
    • Kuhukumiwa na “Bwana wa Kweli”

      18. (a) Yehova aonya kuhusu kuja kwa nani? (b) Kuja kwenye hekalu kulitukia wakati gani, ni nani aliyehusika, na tokeo lilikuwa nini kwa Israeli?

      18 Yehova kupitia Malaki alionya pia kwamba angekuja kuwahukumu watu wake. “Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana [wa kweli, NW] mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam, yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, [kwa hakika, NW] anakuja.” (Malaki 3:1) Kule kuja kwenye hekalu kulikoahidiwa kulitukia wakati gani? Kwenye Mathayo 11:10, Yesu alinukuu unabii wa Malaki wa mjumbe ambaye angetayarisha njia na akautumia kumhusu Yohana Mbatizaji. (Malaki 4:5; Mathayo 11:14) Kwa hiyo katika 29 W.K., wakati wa hukumu ulikuwa umewasili! Ni nani aliyekuwa mjumbe wa pili, mjumbe wa agano ambaye angeandamana na Yehova, yule “Bwana wa kweli,” kwenye hekalu? Yesu mwenyewe, na kwenye pindi mbili alikuja kwenye hekalu katika Yerusalemu na kulisafisha kwa njia yenye kutokeza, akiwaondosha wale wabadili pesa wasiofuatia haki. (Marko 11:15-17; Yohana 2:14-17) Yehova auliza hivi kiunabii kuhusu wakati huo wa hukumu wa karne ya kwanza: “Ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye?” (Malaki 3:2) Kwa kweli, Israeli hawakusimama. Walichunguzwa, wakapatikana kupungukiwa, na katika 33 W.K., waliondoshwa mbali kuwa taifa teule la Yehova.—Mathayo 23:37-39.

      19. Katika karne ya kwanza baki lilimrudia Yehova katika njia gani, nalo lilipokea baraka gani?

      19 Hata hivyo, Malaki aliandika hivi pia: “[Yehova] ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa, naye atawatakasa wana wa Lawi, atawasafisha kama dhahabu na fedha; nao watamtolea BWANA [Yehova, NW] dhabihu katika haki [toleo la zawadi katika uadilifu, NW].” (Malaki 3:3) Kupatana na hayo, ingawa wengi kati ya wale waliodai kumtumikia Yehova katika karne ya kwanza waliondoshwa mbali, baadhi yao walisafishwa wakamjia Yehova, wakitoa dhabihu zenye kukubalika. Ni nani hao? Wale waliokuwa wamemwitikia Yesu, yule mjumbe wa agano. Kwenye Pentekoste 33 W.K., 120 kati ya wale walioitikia walikusanyika pamoja katika chumba cha juu katika Yerusalemu. Wakiwa wameimarishwa na roho takatifu, walianza kutoa toleo la zawadi katika uadilifu, na upesi hesabu zao zikaongezeka. Upesi, walienea kotekote katika Milki ya Roma. (Matendo 2:41; 4:4; 5:14) Hivyo, baki likamrudia Yehova.—Malaki 3:7.

      20. Yerusalemu na hekalu vilipoharibiwa, ni nini kilichopata Israeli wa Mungu jipya?

      20 Baki hilo la Israeli, lililokuja kutia ndani Wasio Wayahudi waliokuwa kana kwamba wamepandikizwa, katika shina la Israeli, lilikuwa “Israeli wa Mungu” jipya, taifa lililojumuika kuwa la Wakristo wapakwa-mafuta kwa roho. (Wagalatia 6:16; Warumi 11:17) Katika 70 W.K., ‘siku yenye kuwaka kama tanuru’ iliwajia Israeli wa kimnofu wakati Yerusalemu na hekalu lalo vilipoharibiwa na majeshi ya Waroma. (Malaki 4:1; Luka 19:41-44) Ni nini kilichowapata Israeli wa Mungu wa kiroho? Yehova aliwaonyesha ‘huruma, jinsi ambavyo mtu humwonyesha huruma mwana wake anayemtumikia.’ (Malaki 3:17, NW) Kundi la Kikristo la wapakwa-mafuta lilitii onyo la Yesu la kiunabii. (Mathayo 24:15, 16) Liliokoka, na baraka ya Yehova iliendelea kulitajirisha kiroho.

      21. Ni maswali gani yanayobaki kuhusu Malaki 3:1 na 10?

      21 Huo ulikuwa utetezi ulioje wa Yehova! Lakini, Malaki 3:1 linatimizwaje leo? Na Mkristo apaswa aitikieje kile kitia-moyo kwenye Malaki 3:10 cha kuleta sehemu ya kumi yote ghalani? Hayo yatachunguzwa katika makala inayofuata.

  • ‘Leteni Sehemu ya Kumi Yote Ghalani’
    Mnara wa Mlinzi—1992 | Desemba 1
    • 1. (a) Katika karne ya tano K.W.K., Yehova aliwatolea watu wake mwaliko gani? (b) Katika karne ya kwanza W.K., tokeo lilikuwa nini la kuja kwa Yehova kwenye hekalu kwa ajili ya hukumu?

      KATIKA karne ya tano K.W.K., Waisraeli walikuwa wamekosa uaminifu kwa Yehova. Walikuwa wamezuia sehemu ya kumi na walileta wanyama wasiofaa kwenye hekalu wakiwa matoleo. Hata hivyo, Yehova aliwaahidi kwamba ikiwa wangeleta sehemu ya kumi nzima ghalani, yeye angemwaga baraka mpaka kuwe hakuna upungukio zaidi. (Malaki 3:8-10) Miaka 500 hivi baadaye, Yehova, akiwakilishwa na Yesu akiwa mjumbe Wake wa agano, alikuja kwenye hekalu la Yerusalemu kwa ajili ya hukumu. (Malaki 3:1) Israeli likiwa taifa lilipatikana kupungukiwa, lakini wale watu mmoja mmoja waliomrudia Yehova walibarikiwa sana. (Malaki 3:7) Walipakwa mafuta kuwa wana wa kiroho wa Yehova, uumbaji mpya, “Israeli wa Mungu.”—Wagalatia 6:16; Warumi 3:25, 26.

      2. Malaki 3:1-10 lingekuwa na utimizo wa pili wakati gani, nasi tunaalikwa kufanya nini kuhusiana na hilo?

      2 Karibu miaka 1,900 baada ya hayo, katika 1914, Yesu alitawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu, na maneno ya Malaki 3:1-10 yenye kupuliziwa kimungu yakawa karibu kupata utimizo wa pili. Kuhusiana na tukio hilo lenye kusisimua, Wakristo wa leo wanaalikwa waleta sehemu ya kumi nzima ghalani. Tukifanya hivyo, sisi pia tutafurahia baraka mpaka kuwe hakuna upungukio zaidi.

      3. Ni nani aliyekuwa mjumbe aliyetayarisha njia mbele za Yehova (a) katika karne ya kwanza? (b) kabla ya vita ya ulimwengu ya kwanza?

      3 Kuhusu kuja kwake kwenye hekalu, Yehova alisema hivi: “Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu.” (Malaki 3:1) Ukiwa utumizo wa karne ya kwanza wa hilo, Yohana Mbatizaji alikuja Israeli akihubiri toba ya dhambi. (Marko 1:2, 3) Je! kulikuwako kazi ya utayarisho kwa habari ya kuja kwa pili kwa Yehova kwenye hekalu lake? Ndiyo. Katika ile miongo kabla ya vita ya ulimwengu ya kwanza, Wanafunzi wa Biblia walitokea kwenye mandhari ya ulimwengu wakifundisha mafundisho safi ya Biblia na kufunua uwongo mbalimbali wenye kutomheshimu Mungu, kama vile mafundisho ya Utatu na moto wa helo. Walionya pia juu ya kuja kwa Nyakati za Wasio Wayahudi katika 1914. Wengi waliitikia wachukuaji nuru hao wa ukweli.—Zaburi 43:3; Mathayo 5:14, 16.

      4. Ni swali gani lililohitaji kujibiwa katika siku ya Bwana?

      4 Mwaka 1914 ulianza kile ambacho Biblia huita “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Mambo ya maana yangetukia katika siku hiyo, kutia na kutambulishwa kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na kuwekwa rasmi kwa huyo “juu ya vitu [vya Bwana-Mkubwa] vyote.” (Mathayo 24:45-47) Huko nyuma katika 1914, maelfu ya makanisa yalidai kuwa ya Kikristo. Ni kikundi gani ambacho kingekubaliwa na Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo, kuwa mtumwa wake mwaminifu mwenye akili? Swali hilo lingejibiwa wakati Yehova angekuja kwenye hekalu.

      Kuja Kwenye Hekalu la Kiroho

      5, 6. (a) Yehova alikuja kwenye hekalu jipi kwa ajili ya hukumu? (b) Jumuiya ya Wakristo ilipokea hukumu gani kutoka kwa Yehova?

      5 Lakini, yeye alikuja kwenye hekalu jipi? Kwa wazi si kwenye hekalu halisi katika Yerusalemu. La mwisho kati ya mahekalu hayo liliharibiwa huko nyuma katika 70 W.K. Hata hivyo, Yehova ana hekalu kubwa zaidi lililofananishwa na lile katika Yerusalemu. Paulo alisema juu ya hekalu hilo kubwa zaidi na kuonyesha jinsi lilivyo tukufu kwelikweli, likiwa na patakatifu mbinguni na ua hapa duniani. (Waebrania 9:11, 12, 24; 10:19, 20) Yehova alikuja kwenye hekalu hilo kubwa la kiroho ili kufanya kazi ya hukumu.”—Linganisha Ufunuo 11:1; 15:8.

      6 Hilo lilitukia wakati gani? Kulingana na uthibitisho wenye nguvu unaopatikana, ni katika 1918.a Tokeo lilikuwa nini? Kwa habari ya Jumuiya ya Wakristo, Yehova aliona tengenezo ambalo mikono yalo ilitiririka damu, mfumo wa kidini wenye ufisadi uliokuwa umefanya ukahaba na ulimwengu huu, ukijifanya rafiki na matajiri na kuonea maskini, ukifundisha mafundisho ya kipagani badala ya kuzoea ibada safi. (Yakobo 1:27; 4:4) Kupitia Malaki, Yehova alikuwa ameonya hivi: “Nami nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi, na juu ya wazinzi, na juu yao waapao kwa uongo; na juu yao wamwoneao mwenye kuajiriwa, kwa ajili ya mshahara wake, wamwoneao mjane na yatima.” (Malaki 3:5) Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imefanya yote hayo na hata mabaya zaidi. Kufikia 1919 ilionekana kwa wazi kwamba Yehova alikuwa ameilaani kuharibiwa pamoja na ile sehemu nyingine ya Babuloni Mkubwa, ule muundo wa dini bandia wa ulimwenguni pote. Tangu wakati huo na kuendelea, mwito ulitolewa kwa wale wenye mioyo ifaayo: “Tokeni kwake, enyi watu wangu.”—Ufunuo 18:1, 4.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki