“Ishara Itokayo Mbinguni”
SHAIRI la zamani lasema hivi: “Anga jekundu usiku, ni furaha ya mabaharia,/Anga jekundu asubuhi, enyi mabaharia jihadharini.” Leo, satelaiti, masomo ya halijoto yenye kuendelezwa na kompyuta, rada ya Dopla, na njia nyinginezo za kisayansi hutumiwa ili kutabiri halihewa. Mara nyingi matabiri hupatana na shairi lililotoka kunukuliwa.
Wakati mmoja maadui wa kidini wa Yesu Kristo walidai kwake “ishara itokayo mbinguni,” yaani wonyesho usio wa kawaida wa kuthibitisha kwamba yeye alikuwa ndiye Mesiya. “Kukiwa jioni,” akasema, “mwasema, Kutakuwa na kianga; kwa maana mbingu ni nyekundu. Na asubuhi, mwasema, Leo kutakuwa na dhoruba; kwa maana mbingu ni nyekundu, tena kumetanda. Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa mbingu; lakini, je! ishara za zamani hizi hamwezi kuzitambua? Kizazi kibaya na cha zinaa chataka ishara; wala hakitapewa ishara, isipokuwa ishara ya Yona.”—Mathayo 16:1-4.
Maadui wa Yesu waliweza kutabiri halihewa lakini hawakuweza kuelewa mambo ya kiroho. Kwa mfano, namna gani ile “ishara ya Yona”? Baada ya kutumia karibu siku tatu akiwa katika tumbo la samaki mkubwa, Yona, nabii wa Mungu alihubiri katika Ninawi na hivyo akawa ishara kwa jiji hilo kuu la Ashuru. Kizazi cha Yesu kilikuwa na “ishara ya Yona” wakati Kristo alipotumia sehemu za siku tatu katika kaburi akafufuliwa. Wanafunzi wake walipiga mbiu ya uthibitisho wa tukio hilo, na hivyo Yesu akawa ishara kwa kizazi hicho.—Mathayo 12:39-41.
Kwenye pindi nyingine, wanafunzi wa Yesu walimwomba “ishara” ya “kuwapo” kwake kwa wakati ujao katika mamlaka ya Ufalme. Kwa kujibu, alitoa ishara ya mambo mengi yenye sehemu-sehemu, kutia na vita visivyo na kifani, matetemeko makubwa ya dunia, upungufu wa chakula, na kuhubiriwa duniani pote kwa Ufalme wa Mungu wa kimbingu uliosimamishwa.—Mathayo 24:3-14, NW.
Je! wewe waitambua ishara ya kuwapo kwa Kristo akiwa Mfalme wa kimbingu asiyeonekana? Sehemu-sehemu zayo zinatimizwa juu ya kizazi hiki. (Mathayo 24:34) Na namna gani wakati ujao? Biblia haifunui tu kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu bali pia hutabiri juu ya ile siku mpya ya Mungu iliyoahidiwa ambayo hivi karibuni itapambazukia ainabinadamu kwa utakato na uangavu mwingi.—2 Petro 3:13.