-
Baraka ya Yehova InatajirishaMnara wa Mlinzi—1986 | Juni 15
-
-
5. Yesu alikuwa na maoni gani juu ya mali?
5 Mara nyingi Yesu aliitaja hatari ya mali, kwa sababu inamwelekea kila mtu, wale walio na wale wasio matajiri. (Mathayo 6:24-32; Luka 6:24; 12:15-21) Ili uone msingi wa kila mtu kujichunguza binafsi, fikiria aliyoyasema Yesu katika pindi moja, kama yanavyosimuliwa katika Mathayo 19:16-24; Marko 10:17-30; na Luka 18:18-30. Kwa kweli, kwa sababu gani usitue sasa ili usome moja au yote ya masimulizi hayo?
6, 7. (a) Kulitukia nini kati ya Yesu na kijana mwanamume? (b) Baadaye, Yesu alitoa shauri gani?
6 Mtawala kijana alimjia Yesu na kumuuliza: “Nifanye nini ili nipate kuurithi uzima wa milele?” Yesu alimwelekeza kwenye Torati, hivyo akaonyesha kwamba Yehova hakuwa ameshindwa kuonyesha mambo yanayohitajiwa. Mtu huyo akajibu kwamba yeye alikuwa ameshika amri za Mungu “tangu utoto wake.” Ilikuwa kama kwamba alikuwa amekaribia kuingia mlangoni, lakini akahisi kwamba bado alikuwa na ukosefu wa jambo fulani. Labda yeye aliwaza kwamba kulikuwa na wema fulani wa ziada, kitendo fulani cha kishujaa, ambacho kingekuwa ndicho hatua ya mwisho ya kupitia mlango huo na kuingia katika uzima wa milele. Jibu la Yesu lina maana pana: “Viuze ulivyo navyo vyote, ukawagawanyie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate.” Ikawaje? “Aliposikia hayo alihuzunika sana, maana alikuwa na mali nyingi.” Kwa hiyo mtu huyo akaenda zake.—Luka 18:18, 21-23; Marko 10:22.
-
-
Baraka ya Yehova InatajirishaMnara wa Mlinzi—1986 | Juni 15
-
-
8. (a) Mtawala huyo kijana Myahudi alikuwaje? (b) Yeye alikuwa na kasoro gani, na kwa sababu gani jambo hilo lituhangaishe sisi?
8 Unaweza kusaidiwa uifahamu hali ya mtawala huyo kijana ukiwazia hali nyingine ya kisasa inayofanana nayo—Mkristo kijana aliye safi, mwenye maarifa mazuri ya Biblia, maadili bora, na mwenye kutoka katika jamaa yenye utajiri. Huenda ukaonea wivu mtu wa namna hiyo leo. Lakini Yesu alipata ukosefu mkubwa katika kijana yule Myahudi: Utajiri au mali zake zilikuwa za maana mno katika maisha yake. Ndiyo sababu Yesu alishauri hivyo. Unaweza kuona ni kwa nini usimulizi huo wa Biblia ni kwa ajili yetu, kama sisi ni matajiri au maskini. Pesa na mali zingeweza kuwa za maana mno kwa ye yote kati yetu, tuwe tunazo tayari au tunatamani tu kuwa nazo.
-