-
Jifunze Kutokana na Mfano wa TalantaMnara wa Mlinzi—2015 | Machi 15
-
-
MTUMWA MWOVU NA GOIGOI
14, 15. Je, Yesu alimaanisha kwamba idadi kubwa ya ndugu zake watiwa-mafuta wangekuwa waovu na goigoi? Fafanua.
14 Katika mfano huo, mtumwa wa mwisho aliificha talanta yake kwenye udongo badala ya kuitumia kufanya biashara au hata kuiweka kwa watunza-akiba. Mtumwa huyo alikuwa na mtazamo mbaya, kwa kuwa aliamua kimakusudi kutoitumia talanta yake kumwongezea faida bwana wake. Kwa hiyo, haishangazi kwamba bwana akasema mtumwa huyo ni “mwovu na goigoi.” Bwana aliichukua talanta hiyo na kumpa yule aliyekuwa na talanta kumi. Kisha, mtumwa huyo mwovu akatupwa ‘nje katika giza, na huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’—Mt. 25:24-30; Luka 19:22, 23.
15 Kwa kuwa mtumwa mmoja kati ya wale watatu alificha talanta yake, je, Yesu alimaanisha kwamba theluthi moja ya wafuasi wake watiwa-mafuta wangekuwa waovu na goigoi? Hapana. Fikiria muktadha. Katika mfano wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yesu alieleza kuhusu mtumwa mwovu anayewapiga watumwa wenzake. Yesu hakuwa akitabiri kwamba kungekuwa na jamii ya mtumwa mwovu. Badala yake, alikuwa akimwonya mtumwa mwaminifu asiwe na tabia kama za mtumwa mwovu. Vivyo hivyo, katika mfano wa mabikira kumi, Yesu hakumaanisha kwamba nusu ya wafuasi wake watiwa-mafuta wangekuwa kama wale mabikira watano wapumbavu. Badala yake, alikuwa akiwaonya ndugu zake wa kiroho kuhusu mambo ambayo yangetokea ikiwa hawangeendelea kukesha na kuwa tayari.f Katika muktadha huo, inaonekana kwamba inafaa kufikia mkataa kuwa katika mfano wa talanta, Yesu hakumaanisha kwamba idadi kubwa ya ndugu zake watiwa-mafuta wangekuwa waovu na goigoi katika siku za mwisho. Badala yake, alikuwa akiwaonya wafuasi wake watiwa-mafuta kwamba wanahitaji kuendelea kuwa na bidii, yaani, “kufanya biashara” kwa kutumia talanta yao, na kuepuka mitazamo na matendo ya mtumwa mwovu.—Mt. 25:16.
-