-
Jinsi Habari Njema InavyohubiriwaFurahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 21
Jinsi Habari Njema Inavyohubiriwa
Hivi karibuni, Yehova atatumia Ufalme wake kuondoa matatizo yetu yote. Hizo ni habari njema ambazo kila mtu anapaswa kusikia. Yesu aliwaagiza wafuasi wake wawahubirie watu wote ujumbe huo! (Mathayo 28:19, 20) Mashahidi wa Yehova wametii jinsi gani amri hiyo ya Yesu?
1. Andiko la Mathayo 24:14 linatimizwaje leo?
Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanafurahia kufanya kazi hiyo muhimu. Tunahubiri habari njema ulimwenguni pote katika lugha zaidi ya elfu moja! Kazi hiyo kubwa inahitaji jitihada nyingi na mipango mizuri. Kazi hiyo haiwezi kufanikiwa bila msaada wa Yehova.
2. Tunafanya jitihada gani ili kuwahubiria watu?
Tunahubiri mahali popote ambapo tunaweza kuwapata watu. Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunahubiri “nyumba kwa nyumba.” (Matendo 5:42) Kupitia njia hiyo, tunahubiri kikamili na kuwafikia mamilioni ya watu kila mwaka. Kwa kuwa wakati mwingine si rahisi kuwapata watu nyumbani, tunahubiri pia katika maeneo mengi ya hadharani. Sikuzote tunatafuta fursa za kuwaambia wengine kumhusu Yehova na makusudi yake.
3. Ni nani walio na jukumu la kuhubiri habari njema?
Wakristo wote wa kweli wanapaswa kuwahubiria wengine habari njema. Tunachukua jukumu hilo kwa uzito. Tunahubiri kwa bidii kwa sababu tunajua kwamba uhai wa watu uko hatarini. (Soma 1 Timotheo 4:16.) Hatulipwi mshahara tunapofanya kazi hii kwa sababu Biblia inasema hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:7, 8) Si kila mtu ambaye atakubali ujumbe wetu. Lakini tunaendelea kuhubiri kwa sababu hiyo ni sehemu ya ibada yetu, na tunamfurahisha Yehova.
CHIMBA ZAIDI
Jifunze kuhusu jitihada za Mashahidi wa Yehova za kuhubiri ulimwenguni pote na uone jinsi Yehova anavyotusaidia.
Kuhubiri ulimwenguni pote: (A) Kosta Rika, (B) Marekani, (C) Benin, (D) Thailand, (E) Yap, (F) Sweden
4. Tunajitahidi sana ili kuwafikia watu wote
Mashahidi wa Yehova hufanya jitihada za pekee ili kuwahubiria watu habari njema kila mahali. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Ni nini kinachokuvutia kuhusu jitihada za Mashahidi wa Yehova za kuhubiri?
Soma Mathayo 22:39 na Waroma 10:13-15, kisha mzungumzie maswali haya:
Kazi yetu ya kuhubiri inaonyeshaje kwamba tunawapenda jirani zetu?
Yehova anahisije kuhusu wale wanaohubiri habari njema?—Ona mstari wa 15.
5. Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu
Mambo mengi yaliyoonwa yanathibitisha kwamba Yehova anaongoza kazi yetu. Kwa mfano, nchini New Zealand, ndugu anayeitwa Paul alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, alikutana na mwanamke fulani alasiri moja. Siku hiyohiyo asubuhi, mwanamke huyo alikuwa amesali kwa Mungu akitumia jina la Mungu, Yehova, na akamwomba amtume mtu amtembelee. Paul anasema: “Saa tatu baadaye, nilibisha mlango wake.”
Soma 1 Wakorintho 3:9, kisha mzungumzie swali hili:
Mambo yaliyoonwa, kama hilo lililotokea huko New Zealand, yanathibitishaje kwamba Yehova anaongoza kazi ya kuhubiri?
Soma Matendo 1:8, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini tunahitaji msaada wa Yehova ili tutimize huduma yetu?
Je, wajua?
Katika kila mkutano wetu wa katikati ya juma, tunapata mazoezi ya jinsi ya kuhubiri. Ikiwa umewahi kuhudhuria mkutano huo, una maoni gani kuhusu mazoezi yanayotolewa?
6. Tunatii amri ya Mungu ya kuhubiri
Katika karne ya kwanza, wapinzani walijaribu kuwazuia wanafunzi wa Yesu ili wasihubiri. Wakristo wa mapema walitetea haki yao ya kuhubiri kwa “kuithibitisha kisheria habari njema.” (Wafilipi 1:7) Mashahidi wa Yehova wanafanya vivyo hivyo leo.a
Soma Matendo 5:27-42, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini hatutaacha kuhubiri?—Ona mstari wa 29, 38, na 39.
HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanahubiri nyumba kwa nyumba?”
Wewe ungejibuje swali hilo?
MUHTASARI
Yesu aliwaagiza wafuasi wake wahubiri habari njema katika mataifa yote. Yehova anawasaidia watu wake kufanya kazi hiyo.
Ungejibuje?
Kazi ya kuhubiri habari njema inafanywaje ulimwenguni pote?
Kazi yetu ya kuhubiri inaonyeshaje kwamba tunawapenda jirani zetu?
Je, unafikiri kazi ya kuhubiri inaweza kutuletea furaha? Kwa nini?
CHUNGUZA ZAIDI
Ona jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyowahubiria watu katika majiji makubwa.
Mashahidi wa Yehova wamewasaidiaje wakimbizi?
Sikiliza maelezo ya dada fulani aliyefurahia kutumia maisha yake katika utumishi wa wakati wote.
Jifunze kuhusu ushindi wa kesi mahakamani ambao umesaidia kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema.
“Wahubiri wa Ufalme Wanapeleka Kesi Mahakamani” (Ufalme wa Mungu Unatawala!, sura ya 13)
a Mungu ndiye ametupatia amri ya kuhubiri. Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawahitaji kibali cha serikali za wanadamu ili kuhubiri habari njema.
-
-
Ubatizo—Lengo Muhimu!Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 23
Ubatizo—Lengo Muhimu!
Yesu alifundisha kwamba ni lazima Wakristo wabatizwe. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Lakini ubatizo ni nini? Na mtu anapaswa kufanya nini ili afikie lengo hilo?
1. Ubatizo ni nini?
Neno “batiza” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “zamisha” ndani ya maji. Yesu alipobatizwa, alizamishwa ndani ya Mto Yordani na kisha ‘akatoka katika maji.’ (Marko 1:9, 10) Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli hubatizwa kwa kuzamishwa kabisa ndani ya maji.
2. Ubatizo unamaanisha nini?
Mtu anapobatizwa, anaonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Mtu anajiweka wakfu jinsi gani? Kabla ya kubatizwa, anatoa sala faraghani na kumwambia Yehova kwamba anataka kumtumikia milele. Anaahidi kwamba atamwabudu Yehova peke yake, na jambo muhimu zaidi maishani mwake litakuwa kufanya mapenzi ya Mungu. Anaamua ‘kujikana mwenyewe na kuendelea kufuata’ mafundisho na mfano wa Yesu. (Mathayo 16:24) Kujiweka wakfu na kubatizwa humwezesha mtu kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova na watu wengine wanaomwabudu Yehova.
3. Mtu anapaswa kuchukua hatua gani kabla ya kubatizwa?
Kabla ya kubatizwa, unapaswa kujifunza kumhusu Yehova na kujenga imani yenye nguvu kwake. (Soma Waebrania 11:6.) Kadiri ujuzi na imani yako inavyozidi kuongezeka, ndivyo utakavyompenda Yehova zaidi. Bila shaka, utatamani kuwaambia wengine kumhusu na kuishi kulingana na viwango vyake. (2 Timotheo 4:2; 1 Yohana 5:3) Mtu anapoanza kuishi “kwa kumstahili Yehova ili kumpendeza kikamili,” inawezekana kwamba ataamua kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.—Wakolosai 1:9, 10.a
CHIMBA ZAIDI
Ona mambo tunayojifunza kutokana na ubatizo wa Yesu na jinsi mtu anavyoweza kujitayarisha ili kuchukua hatua hiyo muhimu.
4. Mambo tunayojifunza kutokana na ubatizo wa Yesu
Soma Mathayo 3:13-17 ili ujifunze mengi kuhusu ubatizo wa Yesu. Kisha mzungumzie maswali haya:
Je, Yesu alikuwa mtoto mchanga alipobatizwa?
Alibatizwa jinsi gani? Je, alinyunyiziwa maji?
Baada ya kubatizwa, Yesu alianza kufanya kazi ya pekee ambayo Mungu alimpa afanye duniani. Soma Luka 3:21-23 na Yohana 6:38, kisha mzungumzie swali hili:
Yesu alitanguliza kazi gani maishani baada ya kubatizwa?
5. Unaweza kufikia lengo la kubatizwa
Mwanzoni huenda ukawa na wasiwasi kuhusu kujiweka wakfu na kubatizwa. Hata hivyo, unaweza kufanya maendeleo hatua kwa hatua na mwishowe kupata ujasiri wa kufanya uamuzi huo muhimu. Ili uone baadhi ya watu waliofanya hivyo, onyesha VIDEO.
Soma Yohana 17:3 na Yakobo 1:5, kisha mzungumzie swali hili:
Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu ajitayarishe kwa ajili ya ubatizo?
Tunajiweka wakfu kwa kumwambia Yehova kwamba tunataka kumtumikia milele
Tunapobatizwa tunawaonyesha watazamaji kwamba tumejiweka wakfu kwa Mungu
6. Tunapobatizwa tunajiunga na familia ya Yehova
Tunapobatizwa tunajiunga na familia yenye umoja ya ulimwenguni pote. Ingawa tumetoka katika maeneo na malezi mbalimbali, sisi sote tunaamini mambo yaleyale na tunaishi kulingana na viwango vilevile vya maadili. Soma Zaburi 25:14 na 1 Petro 2:17, kisha mzungumzie swali hili:
Mtu anapobatizwa anakuwa na uhusiano gani na Yehova na watu wengine wanaomwabudu?
WATU FULANI HUSEMA: “Mimi siko tayari kubatizwa.”
Ikiwa wewe unahisi hivyo, je, bado unafikiri kwamba ubatizo ni lengo muhimu?
MUHTASARI
Yesu alifundisha kwamba ni lazima Wakristo wabatizwe. Ili kufikia lengo hilo, mtu anapaswa kujenga imani yenye nguvu kwa Yehova, kuishi kulingana na viwango vyake, na kujiweka wakfu kwake.
Ungejibuje?
Ubatizo ni nini, na kwa nini ni muhimu kubatizwa?
Kuna uhusiano gani kati ya kujiweka wakfu na kubatizwa?
Ni hatua gani ambazo mtu anapaswa kuchukua kabla ya kujiweka wakfu na kubatizwa?
CHUNGUZA ZAIDI
Jifunze ukweli kuhusu ubatizo.
Chunguza hatua ambazo mtu anapaswa kuchukua ili kufikia ubatizo.
“Upendo na Uthamini Wetu kwa Yehova Hutuchochea Kubatizwa” (Mnara wa Mlinzi, Machi 2020)
Soma uone kwa nini mwanamume fulani hakuongozwa tu na hisia alipoamua kubatizwa.
“Walitaka Nijithibitishie Ukweli” (Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 2013)
Chunguza kwa nini ubatizo ni lengo muhimu na jinsi unavyoweza kujitayarisha ili ubatizwe.
“Nibatizwe?” (Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, sura ya 37)
a Ikiwa mwanzoni mtu alibatizwa katika dini nyingine, anahitaji kubatizwa tena. Kwa nini? Kwa sababu dini hiyo haikufundisha ukweli ulio katika Biblia.—Ona Matendo 19:1-5 na Somo la 13.
-