-
Sala za Kurudia-Rudia-au za Kutoka Moyoni?Amkeni!—1996 | Juni 8
-
-
“Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi.”a (Mathayo 6:7) Tafsiri nyinginezo huonyesha hivi: “Katika sala zenu msipayuke-payuke kama wapagani.” (NE) “Katika kusali kwenu msijaze maneno matupu kama wafanyavyo wasio Wayahudi.”—Revised Standard Version.
Watu wengine hufikiri kwamba kutumia maneno mengi ndiko kumcha Mungu, kusema kwa ufasaha kuwa ndio ujitoaji, kurudia-rudia maneno na kutoa sala ndefu kuwa ndiko kupata itikio hakika. Hata hivyo, Mungu hapimi thamani ya sala kwa yadi au meta. Ni wazi, Yesu hakutaka wafuasi wake watumie sala zisizobadilika au kukariri sala. Kwa sababu hiyo, rosari, vitabu vya sala, au magurudumu ya sala ni yenye thamani gani ya kudumu?
Baada ya kusema yaliyoko juu, Yesu aliwapa wanafunzi wake sala ya kielelezo—ile Sala ya Bwana ijulikanayo sana. (Mathayo 6:9-13) Je, alikusudia watamke maneno hayo kwa kurudia kama kasuku? La hasha. Kwa kweli alipoyasema tena maneno hayo, zaidi ya mwaka mmoja baadaye, hata Yesu mwenyewe hakutumia maneno yaleyale. (Luka 11:2-4) Je, kuna rekodi yoyote ya Wakristo wa mapema kufanya hivyo au kurudia-rudia sala nyinginezo za kikawaida? Tena, la.
Je, hiyo yamaanisha kwamba hatuwezi kutaja jambo lilelile au kuomba mara nyingi? Hasha, kwa sababu Yesu pia alisema: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata.” (Mathayo 7:7, NW) Mara nyingi ni lazima kwetu kufanya ombi lilelile mara nyingi. Kwa hiyo Yehova huona jinsi juhudi zetu zilivyo katika maombi yetu na jinsi hisia zetu za ndani zilivyo kuhusu mambo yetu.
-