-
Inamaanisha Nini Kutounga Mkono Upande WowoteFurahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 45
Inamaanisha Nini Kutounga Mkono Upande Wowote?
Yesu aliwafundisha wafuasi wake kwamba hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Hilo linahusisha kutounga mkono upande wowote katika vita au siasa za ulimwengu. Ukweli ni kwamba si rahisi sikuzote kutounga mkono upande wowote. Huenda watu wakatudhihaki kwa sababu ya msimamo wetu. Tunawezaje kuepuka kuunga mkono upande wowote na kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova Mungu?
1. Wakristo wa kweli wana maoni gani kuhusu serikali za wanadamu?
Wakristo wanaheshimu serikali. Tunatii maneno haya ya Yesu: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari.” Hilo linamaanisha tunatii sheria za nchi, kama vile kulipa kodi. (Marko 12:17) Biblia inafundisha kwamba serikali za wanadamu zinatawala kwa sababu Yehova ameruhusu ziwepo. (Waroma 13:1) Basi, tunaelewa kwamba serikali za wanadamu zina mamlaka ya kadiri au yenye mipaka. Tunaamini kwamba Mungu atatumia Ufalme wake wa mbinguni kuondoa matatizo ya wanadamu.
2. Tunawezaje kuonyesha kwamba hatuungi mkono upande wowote?
Kama Yesu, sisi pia hatujihusishi na siasa. Watu walipoona muujiza mmoja wa Yesu, walitaka kumfanya awe Mfalme wao duniani, lakini alikataa. (Yohana 6:15) Kwa nini alikataa? Kwa sababu baadaye alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Tukiwa wanafunzi wa Yesu, tunaonyesha kwa njia mbalimbali kwamba hatuungi mkono upande wowote. Kwa mfano, hatushiriki katika vita. (Soma Mika 4:3.) Tunaheshimu nembo za taifa kama vile bendera, lakini hatuziabudu. (1 Yohana 5:21) Na hatuungi mkono wala kupinga mgombeaji au chama chochote cha kisiasa. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kabisa kwa serikali ya Mungu, yaani, Ufalme wake.
CHIMBA ZAIDI
Chunguza hali ambazo zinaweza kufanya iwe vigumu kutounga mkono upande wowote na jinsi unavyoweza kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova.
3. Wakristo wa kweli hawaungi mkono upande wowote
Yesu na wafuasi wake walituwekea mfano. Soma Waroma 13:1, 5-7 na 1 Petro 2:13, 14. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.
Kwa nini tunapaswa kuheshimu serikali za wanadamu?
Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunajitiisha chini ya serikali hizo?
Wakati wa vita, huenda mataifa fulani yakadai kwamba hayaungi mkono upande wowote, lakini yanasaidia pande zote zinazozozana. Kutounga mkono upande wowote kunamaanisha nini hasa? Soma Yohana 17:16. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie swali linalofuata.
Inamaanisha nini kutounga mkono upande wowote?
Tunapaswa kufanya nini ikiwa serikali za wanadamu zinatuamuru tufanye jambo linalopingana na sheria ya Mungu? Soma Matendo 5:28, 29. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.
Sheria za wanadamu zinapopingana na sheria za Mungu, tunapaswa kutii sheria za nani?
Unafikiri ni katika hali gani Wakristo hawapaswi kutii serikali za wanadamu?
4. Onyesha kwamba huungi mkono upande wowote kupitia mawazo na matendo yako
Soma 1 Yohana 5:21. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.
Katika video hiyo, kwa nini Ayenge alikataa kujiunga na chama cha kisiasa au kushiriki katika sherehe za kitaifa, kama vile kupiga saluti mbele ya bendera?
Je, unafikiri alifanya uamuzi wa hekima?
Msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote unaweza kujaribiwa katika hali gani nyingine? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.
Tunawezaje kuonyesha kwamba hatuungi mkono upande wowote kunapokuwa na mashindano ya michezo kati ya mataifa mbalimbali?
Tunawezaje kuendelea kutounga mkono upande wowote, iwe maamuzi ya wanasiasa yatatunufaisha au kutuletea madhara?
Msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote unawezaje kuathiriwa na mambo tunayosikia katika vyombo vya habari au watu tunaoshirikiana nao?
Ni katika hali gani ambazo Mkristo anapaswa kudumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote kupitia mawazo na matendo yake?
HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini hupigi saluti mbele ya bendera au kuimba wimbo wa taifa?”
Wewe ungejibuje?
MUHTASARI
Wakristo hujitahidi sana kutounga mkono upande wowote wa kisiasa kwa mawazo, maneno, na matendo yao.
Ungejibuje?
Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu serikali za wanadamu?
Kwa nini hatuungi mkono upande wowote wa kisiasa?
Ni hali gani zinazoweza kufanya iwe vigumu kutounga mkono upande wowote?
CHUNGUZA ZAIDI
Huenda tukahitaji kudhabihu mambo gani ili tusiunge mkono upande wowote?
Familia zinaweza kufanya nini ili kujitayarisha mapema kwa ajili ya hali zinazoweza kujaribu msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote?
Dumisha Msimamo wa Kutounga Mkono Upande Wowote Katika Sherehe za Umma (4:25)
Kwa nini kutetea nchi sio heshima kubwa zaidi ambayo mtu anaweza kupata?
Chunguza jinsi ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu unapofanya maamuzi kuhusu kazi.
“Kila Mmoja Ataubeba Mzigo Wake Mwenyewe” (Mnara wa Mlinzi, Machi 15, 2006)
-
-
Unaweza Kuvumilia MatesoFurahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
Wakristo wote wanatarajia kwamba watakabili upinzani au hata mateso. Je, hilo linapaswa kutuogopesha?
1. Kwa nini tunatarajia kuteswa?
Biblia inasema hivi waziwazi: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Yesu aliteswa kwa sababu hakuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani. Sisi pia si sehemu ya ulimwengu, kwa hiyo hatushangai tunapoteswa na serikali za wanadamu au mashirika ya kidini.—Yohana 15:18, 19.
2. Tunawezaje kujitayarisha kwa ajili ya mateso?
Sasa ndio wakati wa kujifunza kumtegemea Yehova kabisa. Tenga muda kila siku ili kusali kwake na kusoma Neno lake. Hudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida. Kufanya mambo hayo kutakupatia nguvu unazohitaji ili ukabili mateso kwa ujasiri, hata kama yanatoka kwa watu wa familia yako. Mtume Paulo, ambaye aliteswa mara nyingi, aliandika hivi: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”—Waebrania 13:6.
Tunaweza pia kuimarisha ujasiri wetu kwa kuhubiri kwa ukawaida. Tunapohubiri tunajifunza kumtegemea Yehova na kuepuka mtego wa kuwaogopa wanadamu. (Methali 29:25) Ukisitawisha ujasiri wa kuhubiri sasa, utakuwa tayari kuendelea kuhubiri hata ikiwa serikali itajaribu kutuzuia kuhubiri.—1 Wathesalonike 2:2.
3. Tunanufaikaje tunapovumilia mateso?
Bila shaka, hatufurahi tunapoteswa, lakini tunapovumilia mateso, imani yetu inaimarika. Tunamkaribia Yehova kwa sababu tunajionea jinsi anavyotusaidia tunapohisi kwamba hatuna nguvu za kuendelea kuvumilia. (Soma Yakobo 1:2-4.) Yehova anaumia anapoona tukiteseka, lakini anafurahi kuona tukivumilia. Biblia inasema hivi: “Ikiwa mnavumilia mateso kwa sababu ya kufanya mema, jambo hilo linakubalika kwa Mungu.” (1 Petro 2:20) Tukiendelea kuvumilia kwa uaminifu, Yehova atatupatia thawabu ya kuishi milele katika ulimwengu ambao tutamwabudu bila upinzani wowote.—Mathayo 24:13.
CHIMBA ZAIDI
Jifunze jinsi tunavyoweza kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova hata tunapokabili mateso, na baraka ambazo tutapata kwa kufanya hivyo.
4. Unaweza kuvumilia upinzani kutoka kwa watu wa familia
Yesu alijua kwamba baadhi ya watu katika familia zetu watajaribu kutuzuia kumwabudu Yehova. Soma Mathayo 10:34-36, kisha mzungumzie swali hili:
Mtu anapoamua kumtumikia Yehova, watu wa familia yake wanaweza kumtendeaje?
Ili uone mfano wa jambo hilo, onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Utafanya nini ikiwa mtu wa familia au rafiki atajaribu kukuzuia kumtumikia Yehova?
Soma Zaburi 27:10 na Marko 10:29, 30. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:
Ahadi hii inawezaje kukusaidia unapokabili upinzani kutoka kwa watu wa familia au marafiki?
5. Endelea kumwabudu Yehova licha ya kuteswa
Tunahitaji ujasiri ili kumtumikia Yehova watu wengine wanapojaribu kutuzuia kumtumikia. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.
Mfano uliowekwa na akina ndugu na dada katika video hiyo unakuimarishaje?
Soma Matendo 5:27-29 na Waebrania 10:24, 25. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:
Kwa nini ni muhimu sana kuendelea kumwabudu Yehova hata ikiwa serikali inatuzuia kuhubiri au kuhudhuria mikutano?
6. Yehova atakusaidia uvumilie
Mashahidi wa Yehova wenye umri na malezi mbalimbali wameendelea kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu hata wanapoteswa. Ili uone jambo lililowasaidia, onyesha VIDEO. Kisha mzungumzie swali linalofuata.
Katika video hiyo, ni nini kilichowasaidia Mashahidi hao kuvumilia?
Soma Waroma 8:35, 37-39 na Wafilipi 4:13. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:
Andiko hili linakuhakikishiaje kwamba unaweza kuvumilia jaribu lolote?
Soma Mathayo 5:10-12, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini unaweza kuwa na furaha hata unapoteswa?
Mamilioni ya watumishi wa Yehova wameendelea kumtumikia kwa uaminifu licha ya upinzani. Wewe pia unaweza!
WATU FULANI HUSEMA: “Mimi siwezi kuvumilia mateso.”
Ni maandiko gani yanayoweza kuwasaidia watu hao kupata ujasiri?
MUHTASARI
Yehova anathamini jitihada zetu za kumtumikia licha ya mateso. Kwa msaada wake, tunaweza kufanikiwa kuvumilia!
Ungejibuje?
Kwa nini Wakristo wanapaswa kutarajia kwamba watateswa?
Unaweza kufanya nini sasa ili uwe tayari utakapokabili mateso?
Ni nini kinachoweza kukusaidia uwe na uhakika kwamba unaweza kuendelea kumtumikia Yehova hata unapokabili jaribu lolote?
CHUNGUZA ZAIDI
Ona ndugu kijana akieleza jinsi Yehova alivyomsaidia kuvumilia alipofungwa gerezani kwa sababu ya kutounga mkono upande wowote.
Ona jambo lililowasaidia wenzi fulani wa ndoa waendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi licha ya upinzani.
Jifunze jinsi unavyoweza kukabili mateso kwa ujasiri.
“Jitayarishe Sasa kwa Ajili ya Mateso” (Mnara wa Mlinzi, Julai 2019)
Tunapaswa kuonaje upinzani kutoka kwa watu wa familia, na tunawezaje kufanikiwa kukabiliana na hali hiyo?
“Kweli Huleta, ‘Si Amani, Bali Upanga’” (Mnara wa Mlinzi, Oktoba 2017)
-