Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Somo la 31. Yesu Kristo Mfalme aliye mbinguni akiwa mbele ya utukufu wa Yehova.

      SOMO LA 31

      Ufalme wa Mungu Ni Nini?

      Ufalme wa Mungu ndio ujumbe muhimu zaidi katika Biblia. Yehova atatumia Ufalme huo kutimiza kusudi lake la mwanzoni la kuifanya dunia iwe paradiso. Ufalme huo ni nini? Tunajuaje kwamba umeanza kutawala? Ufalme huo umetimiza mambo gani? Na utatimiza mambo gani wakati ujao? Maswali hayo yatajibiwa katika somo hili na masomo mawili yanayofuata.

      1. Ufalme wa Mungu ni nini, na Mfalme wake ni nani?

      Ufalme huo ni serikali iliyoanzishwa na Yehova Mungu mwenyewe. Mfalme wa Ufalme huo ni Yesu Kristo, na anatawala kutoka mbinguni. (Mathayo 4:17; Yohana 18:36) Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Atatawala akiwa Mfalme . . . milele.” (Luka 1:32, 33) Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yesu atatawala watu wote duniani.

      2. Ni nani wanaotawala pamoja na Yesu?

      Yesu anatawala pamoja na wengine. “Watu kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa . . . watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:9, 10) Ni watu wangapi watakaotawala pamoja na Kristo? Tangu Yesu alipokuja duniani, mamilioni ya watu wamekuwa wafuasi wake. Lakini watu 144,000 ndio tu wanaoenda mbinguni kutawala pamoja na Yesu. (Soma Ufunuo 14:1-4.) Wakristo wengine wote walio duniani watakuwa raia wa Ufalme huo.​—Zaburi 37:29.

      3. Kwa nini Ufalme wa Mungu ni bora kuliko serikali za wanadamu?

      Ingawa watawala wa serikali za wanadamu wanajitahidi kufanya mambo mazuri, hawana uwezo wa kufanya mambo yote wanayotaka. Baada ya kipindi chao cha kutawala kwisha, huenda watawala wengine wabinafsi wakaanza kutawala na hawawajali raia wao. Lakini kuhusu Yesu Mtawala wa Ufalme wa Mungu, hakuna mtawala mwingine atakayechukua nafasi yake. Mungu “[ameusimamisha] ufalme ambao hautaangamizwa kamwe.” (Danieli 2:44) Yesu atatawala dunia yote, na hatakuwa na ubaguzi. Yesu ni mwenye upendo, fadhili, na haki, naye atawafundisha watu kuwatendea wengine kwa njia hiyohiyo, yaani, kwa upendo, fadhili, na haki.​—Soma Isaya 11:9.

      CHIMBA ZAIDI

      Chunguza uone kwa nini Ufalme wa Mungu ni serikali bora kuliko serikali zote za wanadamu.

      Yesu Kristo akiitawala dunia akiwa kwenye kiti chake cha ufalme mbinguni. Watawala wenzake wameketi nyuma yake. Nuru ya Yehova inaangaza nyuma yao.

      4. Serikali yenye nguvu itaitawala dunia yote

      Yesu Kristo ana nguvu nyingi sana za kutawala kuliko mtawala yeyote katika historia. Soma Mathayo 28:18, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa nini Yesu ana mamlaka kubwa zaidi kuliko mtawala yeyote wa serikali za wanadamu?

      Serikali za wanadamu hubadilika-badilika, na kila serikali hutawala sehemu fulani ya dunia. Namna gani Ufalme wa Mungu? Soma Danieli 7:14, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Kwa nini inafurahisha kujua kwamba Ufalme wa Mungu “hautaangamizwa”?

      • Kwa nini tunafurahi kujua kwamba utaitawala dunia yote?

      5. Ni lazima serikali za wanadamu ziondolewe

      Kwa nini ni lazima Ufalme wa Mungu uondoe serikali za wanadamu? Onyesha video, kisha mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Ufalme wa Mungu Ni Nini?​—Kisehemu (1:41)

      • Utawala wa serikali za wanadamu umekuwa na matokeo gani?

      Soma Mhubiri 8:9, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Je, unafikiri Ufalme wa Mungu unapaswa kuondoa serikali za wanadamu? Kwa nini?

      6. Watawala wa Ufalme wa Mungu wanaelewa hali yetu

      Kwa kuwa Mfalme wetu, Yesu, aliwahi kuwa mwanadamu, anaweza ‘kuusikitikia udhaifu wetu.’ (Waebrania 4:15) Wanaume na wanawake waaminifu 144,000 ambao watatawala pamoja na Yesu wamechaguliwa na Yehova “kutoka katika kila kabila na lugha na watu na taifa.”​—Ufunuo 5:9.

      • Je, unafarijika kujua kwamba Yesu na watawala wenzake wanaelewa hali za wanadamu? Kwa nini?

      Wanaume na wanawake watiwa mafuta kutoka malezi mbalimbali ambao waliishi katika vipindi tofauti.

      Yehova amewachagua wanaume na wanawake kutoka katika malezi mbalimbali watawale pamoja na Yesu

      7. Sheria za Ufalme wa Mungu ni bora zaidi

      Serikali huweka sheria ambazo zimekusudiwa kuwanufaisha na kuwalinda raia wake. Ufalme wa Mungu pia una sheria ambazo zinapaswa kufuatwa na raia wake. Soma 1 Wakorintho 6:9-11, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Unafikiri ulimwengu utakuwaje kila mtu atakapofuata sheria za Mungu?a

      • Je, unafikiri Yehova ana haki ya kuwawekea sheria raia wa Ufalme wake? Kwa nini?

      • Ni nini kinachoonyesha kwamba watu ambao hawafuati sheria hizo wanaweza kubadilika?​—Ona mstari wa 11.

      Polisi akielekeza magari barabarani. Watu wenye umri mbalimbali wakivuka barabara.

      Serikali huweka sheria ili kuwalinda na kuwanufaisha raia wake. Ufalme wa Mungu una sheria bora zinazowalinda na kuwanufaisha raia wake

      HUENDA MTU AKAULIZA: “Ufalme wa Mungu ni nini?”

      • Unawezaje kujibu swali hilo?

      MUHTASARI

      Ufalme wa Mungu ni serikali halisi iliyo mbinguni ambayo itaitawala dunia yote.

      Ungejibuje?

      • Watawala wa Ufalme wa Mungu ni nani?

      • Kwa nini Ufalme wa Mungu ni bora kuliko serikali zote za wanadamu?

      • Yehova anatarajia raia wa Ufalme wake wafanye mambo gani?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Chunguza uone Yesu alisema utawala wa Mungu utatawala kutokea wapi.

      “Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanachagua kuwa washikamanifu kwa Ufalme wa Mungu badala ya serikali za wanadamu?

      Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu (1:43)

      Chunguza jinsi Biblia inavyofafanua wale 144,000 ambao wamechaguliwa na Yehova kutawala pamoja na Yesu.

      “Ni Nani Wanaoenda Mbinguni?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Ni nini kilichomsadikishia mwanamke aliyekuwa gerezani kwamba Mungu peke yake ndiye anayeweza kuleta ulimwengu wenye haki?

      “Jinsi Nilivyopata Suluhisho la Ukosefu wa Haki” (Amkeni!, Novemba 2011)

      a Baadhi ya sheria hizo zitazungumziwa katika Sehemu ya 3.

  • Inamaanisha Nini Kutounga Mkono Upande Wowote
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Somo la 45. Dada kijana akiwa amesimama kwa heshima wanafunzi wenzake wanapoimba wimbo wa taifa lakini haimbi wala kuweka mkono kifuani kama wanafunzi wenzake.

      SOMO LA 45

      Inamaanisha Nini Kutounga Mkono Upande Wowote?

      Yesu aliwafundisha wafuasi wake kwamba hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Hilo linahusisha kutounga mkono upande wowote katika vita au siasa za ulimwengu. Ukweli ni kwamba si rahisi sikuzote kutounga mkono upande wowote. Huenda watu wakatudhihaki kwa sababu ya msimamo wetu. Tunawezaje kuepuka kuunga mkono upande wowote na kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova Mungu?

      1. Wakristo wa kweli wana maoni gani kuhusu serikali za wanadamu?

      Wakristo wanaheshimu serikali. Tunatii maneno haya ya Yesu: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari.” Hilo linamaanisha tunatii sheria za nchi, kama vile kulipa kodi. (Marko 12:17) Biblia inafundisha kwamba serikali za wanadamu zinatawala kwa sababu Yehova ameruhusu ziwepo. (Waroma 13:1) Basi, tunaelewa kwamba serikali za wanadamu zina mamlaka ya kadiri au yenye mipaka. Tunaamini kwamba Mungu atatumia Ufalme wake wa mbinguni kuondoa matatizo ya wanadamu.

      2. Tunawezaje kuonyesha kwamba hatuungi mkono upande wowote?

      Kama Yesu, sisi pia hatujihusishi na siasa. Watu walipoona muujiza mmoja wa Yesu, walitaka kumfanya awe Mfalme wao duniani, lakini alikataa. (Yohana 6:15) Kwa nini alikataa? Kwa sababu baadaye alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Tukiwa wanafunzi wa Yesu, tunaonyesha kwa njia mbalimbali kwamba hatuungi mkono upande wowote. Kwa mfano, hatushiriki katika vita. (Soma Mika 4:3.) Tunaheshimu nembo za taifa kama vile bendera, lakini hatuziabudu. (1 Yohana 5:21) Na hatuungi mkono wala kupinga mgombeaji au chama chochote cha kisiasa. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kabisa kwa serikali ya Mungu, yaani, Ufalme wake.

      CHIMBA ZAIDI

      Chunguza hali ambazo zinaweza kufanya iwe vigumu kutounga mkono upande wowote na jinsi unavyoweza kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova.

      Mwanamume ambaye haungi mkono upande wowote. Hasikilizi wagombeaji wa kisiasa wanaopingana wakizungumza na umati wa watu.

      3. Wakristo wa kweli hawaungi mkono upande wowote

      Yesu na wafuasi wake walituwekea mfano. Soma Waroma 13:1, 5-7 na 1 Petro 2:13, 14. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.

      VIDEO: Wakristo wa Kweli Hawaungi Mkono Upande Wowote​—Sehemu ya 1 (4:28)

      • Kwa nini tunapaswa kuheshimu serikali za wanadamu?

      • Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunajitiisha chini ya serikali hizo?

      Wakati wa vita, huenda mataifa fulani yakadai kwamba hayaungi mkono upande wowote, lakini yanasaidia pande zote zinazozozana. Kutounga mkono upande wowote kunamaanisha nini hasa? Soma Yohana 17:16. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Wakristo wa Kweli Hawaungi Mkono Upande Wowote​—Sehemu ya 2 (3:09)

      • Inamaanisha nini kutounga mkono upande wowote?

      Tunapaswa kufanya nini ikiwa serikali za wanadamu zinatuamuru tufanye jambo linalopingana na sheria ya Mungu? Soma Matendo 5:28, 29. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.

      VIDEO: Wakristo wa Kweli Hawaungi Mkono Upande Wowote​—Sehemu ya 3 (1:18)

      • Sheria za wanadamu zinapopingana na sheria za Mungu, tunapaswa kutii sheria za nani?

      • Unafikiri ni katika hali gani Wakristo hawapaswi kutii serikali za wanadamu?

      4. Onyesha kwamba huungi mkono upande wowote kupitia mawazo na matendo yako

      Soma 1 Yohana 5:21. Kisha, onyesha VIDEO na mzungumzie maswali yanayofuata.

      VIDEO: Wakristo wa Kweli Wanahitaji Ujasiri​—Ili Wasiunge Mkono Upande Wowote (2:50)

      • Katika video hiyo, kwa nini Ayenge alikataa kujiunga na chama cha kisiasa au kushiriki katika sherehe za kitaifa, kama vile kupiga saluti mbele ya bendera?

      • Je, unafikiri alifanya uamuzi wa hekima?

      Msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote unaweza kujaribiwa katika hali gani nyingine? Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.

      VIDEO: Masomo Kutoka kwa Mnara wa Mlinzi​—Usiunge Mkono Upande Wowote Katika Ulimwengu Huu Uliogawanyika (5:16)

      • Tunawezaje kuonyesha kwamba hatuungi mkono upande wowote kunapokuwa na mashindano ya michezo kati ya mataifa mbalimbali?

      • Tunawezaje kuendelea kutounga mkono upande wowote, iwe maamuzi ya wanasiasa yatatunufaisha au kutuletea madhara?

      • Msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote unawezaje kuathiriwa na mambo tunayosikia katika vyombo vya habari au watu tunaoshirikiana nao?

      Picha: 1. Kikundi cha watu wenye hasira walio na mabango wakiandamana. 2. Mwanamume akishangilia akiwa ameshika bendera wakati wa mashindano ya michezo. 3. Mwanafunzi anaimba wimbo wa taifa. 4. Mwanajeshi akiwa amebeba bunduki. 5. Wagombeaji wawili wa kisiasa wakifanya mjadala. 6. Mwanamke anaweka kura katika sanduku wakati wa kupiga kura.

      Ni katika hali gani ambazo Mkristo anapaswa kudumisha msimamo wa kutounga mkono upande wowote kupitia mawazo na matendo yake?

      HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini hupigi saluti mbele ya bendera au kuimba wimbo wa taifa?”

      • Wewe ungejibuje?

      MUHTASARI

      Wakristo hujitahidi sana kutounga mkono upande wowote wa kisiasa kwa mawazo, maneno, na matendo yao.

      Ungejibuje?

      • Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu serikali za wanadamu?

      • Kwa nini hatuungi mkono upande wowote wa kisiasa?

      • Ni hali gani zinazoweza kufanya iwe vigumu kutounga mkono upande wowote?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Huenda tukahitaji kudhabihu mambo gani ili tusiunge mkono upande wowote?

      Yehova Hajatuacha Kamwe (3:14)

      Familia zinaweza kufanya nini ili kujitayarisha mapema kwa ajili ya hali zinazoweza kujaribu msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote?

      Dumisha Msimamo wa Kutounga Mkono Upande Wowote Katika Sherehe za Umma (4:25)

      Kwa nini kutetea nchi sio heshima kubwa zaidi ambayo mtu anaweza kupata?

      “Mambo Yote Yanawezekana na Mungu” (5:19)

      Chunguza jinsi ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu unapofanya maamuzi kuhusu kazi.

      “Kila Mmoja Ataubeba Mzigo Wake Mwenyewe” (Mnara wa Mlinzi, Machi 15, 2006)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki