-
Matokeo ya Kuhubiri—“Mashamba . . . Ni Meupe kwa Ajili ya Kuvunwa”Ufalme wa Mungu Unatawala!
-
-
1, 2. (a) Kwa nini wanafunzi wanashangaa? (b) Yesu anazungumza kuhusu mavuno gani?
WANAFUNZI wanashangaa. Yesu amewaambia hivi: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” Wanatazama upande ambao Yesu anawaonyesha, lakini hawaoni mashamba meupe, bali ya kijani—rangi ya shayiri zilizoanza tu kumea. Labda wanajiuliza, ‘Anazungumzia mavuno gani?’ Kwani ‘itapita miezi kadhaa kabla ya mavuno kuanza.’—Yoh. 4: 35.
2 Hata hivyo, Yesu hazungumzi kuhusu mavuno halisi. Badala yake, anatumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi wake mambo mawili muhimu kuhusu mavuno ya kiroho, yaani, kuvuna watu. Ni mambo gani hayo? Ili kupata jibu la swali hilo, acheni tuchunguze simulizi hilo kwa kina zaidi.
Wachochewa Kutenda na Wanaahidiwa Shangwe
3. (a) Ni nini ambacho huenda kilimfanya Yesu aseme: “Mashamba . . . ni meupe kwa ajili ya kuvunwa”? (Ona maelezo ya chini.) (b) Yesu alifafanuaje maneno yake?
3 Mazungumzo ya Yesu na wanafunzi wake yalifanyika mwishoni mwa mwaka wa 30 W.K., karibu na mji wa Samaria ulioitwa Sikari. Wanafunzi wake walipokuwa katika mji huo, Yesu alibaki nyuma kwenye kisima fulani ambako alimweleza mwanamke mmoja kweli za kiroho, na mwanamke huyo alielewa mara moja umuhimu wa mafundisho ya Yesu. Wanafunzi wa Yesu waliporudi, mwanamke huyo alifanya haraka kwenda Sikari ili akawaambie jirani zake mambo yenye kustaajabisha aliyokuwa amejifunza. Ripoti yake iliamsha upendezi mkubwa, na majirani wake wengi walifanya haraka kwenda katika kisima hicho ili wakamwone Yesu. Huenda ni katika pindi hiyo—Yesu alipotazama mbali kwenye mashamba na kuona umati wa Wasamaria ukija—alisema: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.”a Kisha, ili kufafanua kwamba hakumaanisha mavuno halisi, bali mavuno ya kiroho, Yesu aliongezea hivi: ‘Mvunaji . . . anakusanya matunda kwa ajili ya uzima wa milele.’—Yoh. 4:5-30, 36.
4. (a) Yesu alifundisha mambo gani mawili kuhusu mavuno? (b) Tutachunguza maswali gani?
4 Yesu alifundisha mambo gani mawili muhimu kuhusu mavuno ya kiroho? Jambo la kwanza, kazi hiyo inapaswa kufanywa haraka. Maneno yake “mashamba . . . ni meupe kwa ajili ya kuvunwa” yalikusudiwa kuwachochea wafuasi wake kutenda. Ili kukazia kwamba wanafunzi wake wanapaswa kutenda kwa uharaka, Yesu aliongezea hivi: “Tayari mvunaji anapokea mshahara.” Naam, tayari mavuno yalikuwa yameanza na hakukuwa na wakati wa kukawia! Jambo la pili, wafanyakazi ni wenye shangwe. Yesu alisema wapandaji na wavunaji ‘watashangilia pamoja.’ (Yoh. 4:35b, 36) Kama vile Yesu alivyoshangilia alipoona kwamba “wengi wa Wasamaria . . . walimwamini,” ndivyo pia wanafunzi wake wangepata shangwe kubwa wakifanya kazi ya kuvuna kwa nafsi yote. (Yoh. 4:39-42) Kisa hicho kilichotokea katika karne ya kwanza kina umuhimu mkubwa sana kwetu kwa sababu kinaonyesha mambo yanayotokea leo wakati wa yale mavuno makubwa sana ya kiroho. Mavuno hayo ya siku za kisasa yalianza lini? Ni nani wanaoshiriki katika mavuno hayo? Kumekuwa na matokeo gani?
-
-
Matokeo ya Kuhubiri—“Mashamba . . . Ni Meupe kwa Ajili ya Kuvunwa”Ufalme wa Mungu Unatawala!
-
-
a Huenda maneno ya Yesu kuhusu ‘mashamba kuwa meupe’ yalirejelea kanzu nyeupe ambazo huenda zilivaliwa na umati wa Wasamaria ambao Yesu aliuona ukiwakaribia.
-