Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Wanadamu Wanateseka na Kupatwa na Mambo Mabaya?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Somo la 26. Wazazi wenye upendo wakiwa wamekaa hospitalini kando ya kitanda cha mwana wao ambaye amepatwa na jambo baya.

      SOMO LA 26

      Kwa Nini Wanadamu Wanateseka na Kupatwa na Mambo Mabaya?

      Jambo baya linapotokea watu hujiuliza, “Kwa nini jambo hili limetokea?” Tunafurahi sana kujua kwamba Biblia inajibu waziwazi swali hilo!

      1. Shetani alianzishaje uovu ulimwenguni?

      Shetani Ibilisi alimwasi Mungu. Shetani alitaka kuwatawala viumbe wengine, hivyo aliwashawishi wanadamu wa kwanza Adamu na Hawa wajiunge naye kuasi. Shetani alifanya hivyo alipomdanganya Hawa. (Mwanzo 3:1-5) Alimfanya afikiri kwamba Yehova alikuwa akimnyima jambo fulani zuri. Alidai kwamba wanadamu wangekuwa na furaha zaidi ikiwa hawangemtii Mungu. Shetani alisema uwongo wa kwanza kwa kumdanganya Hawa kwamba hangekufa. Hiyo ndiyo sababu Biblia inamwita Shetani kuwa “mwongo na ndiye baba ya uwongo.”​—Yohana 8:44.

      2. Adamu na Hawa waliamua kufanya nini?

      Yehova aliwaonyesha Adamu na Hawa ukarimu mwingi. Aliwaambia wangeweza kula matunda ya kila mti katika bustani ya Edeni isipokuwa mti mmoja. (Mwanzo 2:15-17) Hata hivyo, waliamua kula matunda ya mti waliokatazwa. Hawa alianza “kuchuma matunda ya mti huo na kula.” Baadaye, Adamu “akaanza kula.” (Mwanzo 3:6) Wote wawili hawakumtii Mungu. Kwa kuwa Adamu na Hawa walikuwa wakamilifu, walikuwa na uwezo wa kiasili wa kufanya mambo yaliyo sawa. Lakini kwa kutomtii Mungu kimakusudi, walitenda dhambi na kukataa utawala wake. Uamuzi huo uliwasababishia mateso mengi.​—Mwanzo 3:16-19.

      3. Uamuzi wa Adamu na Hawa umetuathirije?

      Baada ya Adamu na Hawa kutenda dhambi hawakuwa wakamilifu tena, hivyo wakapitisha hali ya kutokamilika kwa wazao wao wote. Biblia inasema hivi kumhusu Adamu: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote.”​—Waroma 5:12.

      Kuna sababu nyingi zinazofanya tuteseke. Wakati fulani tunateseka kwa sababu ya maamuzi mabaya tunayofanya, au kwa sababu ya maamuzi mabaya ya watu wengine. Na wakati mwingine tunateseka kwa sababu tunakuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.​—Soma Mhubiri 9:11.

      CHIMBA ZAIDI

      Chunguza sababu zinazoonyesha kwamba Mungu hasababishi uovu na kuteseka ulimwenguni leo, na jinsi anavyohisi tunapoteseka.

      4. Ni nani anayefanya wanadamu wateseke?

      Watu wengi wanaamini kwamba Mungu ndiye anayeutawala ulimwengu wote. Je, hilo ni kweli? Onyesha VIDEO.

      VIDEO: Ni Nani Anayeutawala Ulimwengu? (1:24)

      Soma Yakobo 1:13 na 1 Yohana 5:19, kisha mzungumzie swali hili:

      • Je, Mungu ndiye anayesababisha uovu na kuteseka?

      5. Utawala wa Shetani umekuwa na matokeo gani?

      Onyesha VIDEO.

      VIDEO: Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka?​—Kisehemu (3:07)

      Soma Mwanzo 3:1-6, kisha mzungumzie maswali haya:

      • Shetani alisema uwongo gani?​—Ona mstari wa 4 na 5.

      • Shetani alisema nini ili kudai kwamba Yehova anawanyima wanadamu jambo fulani zuri?

      • Kulingana na madai ya Shetani, je, wanadamu wanamhitaji Yehova awe Mtawala wao ili wawe na furaha?

      Soma Mhubiri 8:9, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa kuwa Yehova si Mtawala wa ulimwengu huu, hali zimekuwaje?

      Picha: Michoro inayoonyesha hali ya dunia tangu ilipoumbwa hadi wakati ujao itakapokuwa Paradiso. A. Dunia paradiso iliyo na mimea maridadi. B. Kwa karne nyingi utawala wa wanadamu umeijaza dunia dini za uwongo, migawanyiko, na uchafuzi. Baadhi ya serikali zenye nguvu zilizoonyeshwa ni Misri, China, Ugiriki, Roma, Uingereza, na Marekani. C. Watu wakiishi katika dunia iliyo Paradiso.
      1. Adamu na Hawa walikuwa wakamilifu na waliishi katika Paradiso. Lakini walimsikiliza Shetani wakamwasi Yehova

      2. Baada ya Adamu na Hawa kuasi, ulimwengu ulijaa dhambi, mateso, na kifo

      3. Yehova atakomesha dhambi, mateso, na kifo. Kwa mara nyingine, wanadamu watakuwa wakamilifu na kuishi katika Paradiso

      6. Yehova anajali tunapoteseka

      Je, Mungu anajali tunapoteseka? Ona mambo ambayo Mfalme Daudi na mtume Petro waliandika. Soma Zaburi 31:7 na 1 Petro 5:7, kisha mzungumzie swali hili:

      • Unahisije unapojua kwamba Yehova anaona na anajali tunapoteseka?

      7. Mungu atakomesha mateso yote yanayowapata wanadamu

      Soma Isaya 65:17 na Ufunuo 21:3, 4, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa nini inafariji kujua kwamba Yehova ataondoa madhara yote yanayowapata wanadamu?

      Je, wajua?

      Shetani aliposema uwongo wa kwanza alimchongea Yehova, yaani, alimharibia Yehova sifa kwa kudai kwamba ni Mtawala asiye na haki na upendo. Hivi karibuni, Yehova atalitakasa jina lake atakapoondoa mateso yanayowapata wanadamu. Hilo linamaanisha, atathibitisha kwamba utawala wake ndio utawala bora. Kutakaswa kwa jina la Yehova ndilo jambo muhimu zaidi ulimwenguni.​—Mathayo 6:9, 10.

      WATU FULANI HUSEMA: “Kuteseka ni mpango wa Mungu.”

      • Wewe ungesemaje?

      MUHTASARI

      Shetani Ibilisi na wanadamu wawili wa kwanza ndio waliosababisha uovu ulio ulimwenguni. Yehova anajali sana tunapoteseka na hivi karibuni ataondoa mateso.

      Ungejibuje?

      • Shetani Ibilisi alimwambia Hawa uwongo gani?

      • Uasi wa Adamu na Hawa unatuathirije sisi sote?

      • Tunajuaje kwamba Yehova anajali tunapoteseka?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Jifunze jinsi Biblia inavyofafanua maana ya dhambi.

      “Dhambi Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Soma mengi kuhusu suala ambalo Shetani Ibilisi alizusha katika bustani ya Edeni.

      “Kwa Nini Mungu Anaruhusu Watu Wateseke?” (Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 2014)

      Chunguza majibu yenye kuridhisha ya maswali fulani magumu.

      “Kwa Nini Wayahudi Wengi Waliuwawa? Kwa Nini Mungu Hakuzuia?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Ona jambo ambalo mwanamume fulani alijifunza kuhusu mateso aliyoona.

      Siko Peke Yangu Tena (5:09)

  • Kifo cha Yesu Kinawezaje Kutuokoa?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
    • Sisi hutenda dhambi, tunateseka, na tunakufa kwa sababu wanadamu wa kwanza Adamu na Hawa hawakumtii Mungu.a Lakini tuna tumaini. Yehova ameandaa njia ya kutuweka huru kutoka kwenye laana ya dhambi na kifo kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Biblia inafundisha kwamba Yesu alitoa fidia kupitia kifo chake. Fidia ni malipo yanayotolewa ili kumweka mtu huru. Yesu alilipa fidia kwa kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu. (Soma Mathayo 20:28.) Yesu alipodhabihu kwa hiari haki yake ya kuishi milele duniani, alitufungulia njia ya kupata tena uhai mkamilifu ambao Adamu na Hawa walipoteza. Pia, Yesu alionyesha kwamba yeye na Yehova wanatupenda sana. Somo hili litakusaidia kuthamini zaidi kifo cha Yesu.

      1. Kifo cha Yesu kinaweza kutunufaishaje leo?

      Kwa kuwa sisi ni watenda dhambi, tunafanya mambo mengi yasiyompendeza Yehova. Hata hivyo, ikiwa tunajuta sana kwa sababu ya dhambi tulizofanya na kumwomba Yehova kupitia Yesu Kristo atusamehe na kujitahidi kabisa kutorudia makosa hayo, tunaweza kufurahia urafiki wa karibu pamoja na Mungu. (1 Yohana 2:1) Biblia inasema hivi: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kwa ajili ya dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, ili awaongoze ninyi kwa Mungu.”​—1 Petro 3:18.

      2. Kifo cha Yesu kitatunufaishaje wakati ujao?

      Yehova alimtuma Yesu atoe uhai wake mkamilifu wa kibinadamu “ili kila mtu anayemwamini [Yesu] asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kupitia dhabihu ya Yesu, Yehova ataondoa madhara yote yaliyosababishwa na Adamu alipokosa kutii. Hilo linamaanisha kwamba tukionyesha imani katika dhabihu ya Yesu, tutapata nafasi ya kufurahia maisha milele katika dunia paradiso!​—Isaya 65:21-23.

      CHIMBA ZAIDI

      Jifunze mengi kuhusu sababu iliyofanya Yesu atoe uhai wake, na uchunguze jinsi unavyoweza kunufaika.

      3. Kifo cha Yesu kinatuweka huru kutoka kwenye dhambi na kifo

      Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Kwa Nini Yesu Alikufa?​—Sehemu ya 1 (2:01)

      • Adamu alipoteza fursa gani alipokosa kumtii Mungu?

      Soma Waroma 5:12, kisha mzungumzie swali hili:

      • Dhambi ambayo Adamu alifanya imeathirije maisha yako?

      Soma Yohana 3:16, kisha mzungumzie swali hili:

      • Kwa nini Yehova alimtuma Mwana wake duniani?

      A. Picha: 1. Adamu baada ya kukosa kumtii Mungu. 2. Waombolezaji wakiwa wamebeba jeneza. Picha: A. Adamu baada ya kukosa kumtii Mungu. B. Yesu Kristo. B. Picha: 1. Yesu Kristo. 2. Watu wa umri, jamii, tamaduni, na malezi mbalimbali.
      1. Adamu alikuwa mwanamume mkamilifu aliyekosa kumtii Mungu na hivyo akawasababishia wanadamu wote dhambi na kifo

      2. Yesu alikuwa mwanamume mkamilifu aliyemtii Mungu na kuwafungulia wanadamu njia ya kuwa wakamilifu na kupata uzima wa milele

      4. Kifo cha Yesu kinaweza kuwanufaisha watu wote

      Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

      VIDEO: Kwa Nini Yesu Alikufa?​—Sehemu ya 2 (2:00)

      • Kifo cha mtu mmoja kingewezaje kuwanufaisha watu wote?

      Soma 1 Timotheo 2:5, 6, kisha mzungumzie swali hili:

      • Adamu alikuwa mwanadamu mkamilifu ambaye aliwasababishia wanadamu wote dhambi na kifo. Yesu pia alikuwa mwanadamu mkamilifu. Yesu alitoa jinsi gani “fidia inayolingana” na uhai ambao Adamu alipoteza?

      5. Fidia ni zawadi ambayo Yehova amekupatia

      Rafiki za Yehova huona fidia kuwa zawadi waliyopewa kibinafsi. Kwa mfano, soma Wagalatia 2:20, kisha mzungumzie swali hili:

      • Mtume Paulo alionyeshaje kwamba aliona fidia kuwa zawadi aliyopewa kibinafsi?

      Adamu alipotenda dhambi, yeye na wazao wake wote walihukumiwa kifo. Lakini Yehova alimtuma Mwana wake afe, ili wewe upate nafasi ya kuishi milele.

      Unaposoma mistari ifuatayo, wazia jinsi Yehova alivyohisi alipomwona Mwana wake akiteseka. Soma Yohana 19:1-7, 16-18, kisha mzungumzie swali hili:

      • Unahisije kuhusu jambo ambalo Yehova na Yesu wamekufanyia?

      HUENDA MTU AKAULIZA: “Inawezekanaje mtu mmoja afe kwa ajili ya watu wote?”

      • Wewe ungejibuje swali hilo?

      MUHTASARI

      Kupitia kifo cha Yesu, Yehova anaweza kutusamehe dhambi zetu, na tunapata fursa ya kuishi milele.

      Ungejibuje?

      • Kwa nini Yesu alikufa?

      • Ni kwa njia gani uhai mkamilifu wa Yesu ulikuwa fidia inayolingana?

      • Kifo cha Yesu kinawezaje kukunufaisha?

      Lengo

      CHUNGUZA ZAIDI

      Jifunze kwa nini uhai mkamilifu wa Yesu unaitwa fidia.

      “Ni kwa Njia Gani Dhabihu ya Yesu Ilikuwa ‘Fidia kwa Ajili ya Wengi’?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Chunguza mambo tunayopaswa kufanya ili tuokolewe.

      “Yesu Huokoa​—Jinsi Gani?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      Je, Yehova anaweza kusamehe hata dhambi nzito?

      “Majibu ya Maswali ya Biblia” (Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 2013)

      Ona jinsi kujifunza kuhusu dhabihu ya Kristo kulivyomsaidia mwanamume kubadili utu wake.

      “Mimi Si Mtumwa wa Jeuri Tena” (Makala iliyo kwenye mtandao)

      a Dhambi haimaanishi tu kufanya jambo baya. Dhambi pia inarejelea madhara ambayo tumerithi kutoka kwa Adamu na Hawa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki