-
DhambiUfahamu wa Kina wa Maandiko
-
-
Ili awe msema-kweli, na vilevile kwa ajili ya faida ya familia yake nyingineyo ya ulimwengu wote mzima wote, Yehova Mungu hangeweza kukubaliana na mwendo huo wenye dhambi, ama ule wa viumbe vyake vya kibinadamu au wa mwana wa roho aliyegeuka kuwa mwasi. Akidumisha utakatifu wake, alipitisha kwa haki hukumu ya kifo juu yao wote. Kisha binadamu hao wawili walifukuzwa kwenye shamba la Mungu katika Edeni, kwa hiyo wakakatiziwa njia ya kuufikia ule mti mwingine uliotajwa na Mungu kuwa “mti wa uzima.”—Mwa 3:14-24.
Matokeo juu ya jamii ya wanadamu kwa ujumla. Waroma 5:12 lasema kwamba “kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Linganisha 1Yo 1:8-10.) Baadhi wameeleza kuwa hilo lamaanisha kuwa wazao wote wa Adamu wa wakati ujao walishiriki katika tendo la awali la dhambi ya Adamu, kwa sababu, yeye akiwa kichwa chao cha familia, aliwawakilisha na kwa hivyo, ikawa amewafanya kuwa washiriki katika dhambi yake. Hata hivyo, mtume anasema kifo ‘kilienea’ kwa wanadamu wote, jambo ambalo linadokeza ni matokeo ya hatua kwa hatua juu ya wazao wa Adamu wala si ya papo hapo.
Kuongezea hilo, mtume anaendelea kusema juu ya kifo kuwa kinatawala kama mfalme “tangu Adamu mpaka Musa, hata juu ya wale ambao hawakuwa wamefanya dhambi inayofanana na kosa la Adamu.” (Ro 5:14) Kwa kufaa dhambi ya Adamu inaitwa “kosa” kwa kuwa alipita nje ya sheria iliyotajwa wazi, amri ya moja kwa moja ambayo Mungu alimpa. Pia, wakati Adamu alipotenda dhambi, alifanya hivyo kwa hiari yake mwenyewe, akiwa binadamu aliye mkamilifu ambaye hakuwa na kasoro. Ni wazi kwamba wazao wake hawajapata kamwe kufurahia hali hiyo ya ukamilifu. Kwa hiyo, mambo hayapatani na maoni kwamba ‘wakati Adamu alipotenda dhambi, wote kati ya wazao wake ambao walikuwa hawajazaliwa walitenda dhambi pamoja naye.’ Ili wazao wote wa Adamu wahesabiwe kuwa na daraka la kuwa washiriki katika dhambi ya kibinafsi ya Adamu ingehitaji kuwe na wonyesho fulani upande wao wa kupenda yeye awe kichwa chao cha familia. Lakini kwa kweli hakuna yeyote wao aliyependa azaliwe naye, wao wakiwa walizaliwa katika nasaba ya Adamu kama tokeo la mapenzi ya kimwili ya wazazi wao.—Yoh 1:13.
Basi, uthibitisho waonyesha dhambi ilipitishwa kutoka kwa Adamu hadi kwa vizazi vilivyofuata likiwa ni tokeo la sheria ya urithi inayotambuliwa. Kwa wazi jambo hilo ndilo mtunga zaburi anarejezea anaposema hivi: “Nilizaliwa kwa maumivu nikiwa na kosa, na mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” (Zb 51:5) Dhambi, pamoja na matokeo yake, iliingia na kuenea kwa jamii yote ya kibinadamu si kwa sababu tu Adamu alikuwa ndiye kichwa cha familia cha jamii hiyo bali pia kwa sababu yeye, wala si Hawa, alikuwa ndiye mwasisi wake, au chanzo cha uhai wa kibinadamu. Kutokana naye, vilevile kutokana na Hawa, kwa lazima uzao wake ungerithi si tabia za kimwili tu bali pia tabia za kiutu, kutia ndani mwelekeo wa dhambi.—Linganisha 1Ko 15:22, 48, 49.
-
-
DhambiUfahamu wa Kina wa Maandiko
-
-
Ugonjwa, maumivu, na kuzeeka. Kwa kuwa kwa ujumla katika binadamu kifo kinahusianishwa na maradhi au hatua ya kuzeeka, basi mambo hayo huandamana na dhambi. Chini ya agano la Sheria ya Musa pamoja na Israeli, sheria zilizoongoza dhabihu za dhambi zilitia ndani upatanisho kwa ajili ya wale waliokuwa wameathiriwa na tauni ya ukoma. (Law 14:2, 19) Wale wenye kugusa maiti ya binadamu au hata kuingia ndani ya hema alilokufa mtu walikuwa najisi na walihitaji kutakaswa kisherehe. (Hes 19:11-19; linganisha Hes 31:19, 20.) Pia, Yesu alihusianisha maradhi na dhambi (Mt 9:2-7; Yoh 5:5-15), ijapokuwa alionyesha kwamba si lazima mateso hususa yawe matokeo ya matendo fulani hususa yenye dhambi. (Yoh 9:2, 3) Maandiko mengine yanaonyesha matokeo yenye faida ya uadilifu (mwendo ambao ni kinyume cha kutenda dhambi) juu ya afya ya mtu. (Met 3:7, 8; 4:20-22; 14:30) Wakati wa utawala wa Kristo, kuondolewa kwa kifo, ambacho hutawala pamoja na dhambi (Ro 5:21), kutaambatana na mwisho wa maumivu.—1Ko 15:25, 26; Ufu 21:4.
Dhambi na Sheria. Mtume Yohana anaandika kwamba “kila mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi anazoea pia kufanya uasi-sheria, na kwa hiyo dhambi ni uasi-sheria” (1Yo 3:4); pia kwamba “ukosefu wote wa uadilifu ni dhambi.” (1Yo 5:17) Kwa upande mwingine, mtume Paulo anasema juu ya ‘wale waliofanya dhambi bila sheria.’ Pia anaendelea kutaja kwamba “kabla ya Sheria [iliyopeanwa kupitia Musa] kuwako dhambi ilikuwa katika ulimwengu, lakini mtu yeyote hahesabiwi dhambi wakati hakuna sheria. Hata hivyo, kifo kilitawala kama mfalme tangu Adamu mpaka Musa, hata juu ya wale ambao hawakuwa wamefanya dhambi inayofanana na kosa la Adamu.” (Ro 2:12; 5:13, 14) Maneno ya Paulo yanafaa kueleweka kulingana na muktadha; taarifa zake za mapema zaidi katika barua hii kwa Waroma zaonyesha kwamba alikuwa akilinganisha wale walio chini ya agano la Sheria na wale walio nje ya agano hilo, na hivyo hawakuwa chini ya orodha hiyo ya sheria, huku akidhihirisha kwamba jamii zote mbili zilikuwa zenye dhambi.—Ro 3:9.
Wakati wa ile miaka 2,500 hivi kati ya mkengeuko wa Adamu na kutolewa kwa agano la Sheria katika 1513 K.W.K., Mungu hakuwa amewapa jamii ya wanadamu mfumo wowote kamili au kuipanga sheria katika utaratibu uliofafanua dhambi na ikiwa na vipengee tata na katika miundo yake yote. Ni kweli, yeye alikuwa ametoa amri fulani, kama zile alizopewa Noa baada ya Gharika ya dunia yote (Mwa 9:1-7) vilevile lile agano la tohara alilopewa Abrahamu na watu wa nyumba yake, kutia ndani watumwa wake wa kigeni. (Mwa 17:9-14) Lakini kuhusiana na Israeli mtunga zaburi angeweza kusema kwamba Mungu “anamtangazia Yakobo neno lake, na Israeli masharti yake na maamuzi yake ya hukumu. Hajafanya hivyo kwa taifa lingine lolote; nao hawajajua maamuzi yake ya hukumu.” (Zb 147:19, 20; linganisha Kut 19:5, 6; Kum 4:8; 7:6, 11.) Kuhusiana na agano la Sheria lililopewa Israeli ingeweza kusemwa hivi, “Mtu ambaye amefanya uadilifu wa Sheria ataishi kwa huo,” kwa maana kushikilia na kujipatanisha na Sheria hiyo kikamilifu kungeweza kutimizwa tu na mwanadamu asiye na dhambi, kama alivyokuwa Kristo Yesu. (Ro 10:5; Mt 5:17; Yoh 8:46; Ebr 4:15; 7:26; 1Pe 2:22) Hapana sheria nyingine kama hiyo iliyopata kutolewa tangu wakati wa Adamu hadi kutolewa kwa agano la Sheria.
‘Kufanya kwa asili mambo ya sheria.’ Hilo halikumaanisha kwamba, kwa vile hakukuwa na mfumo kamili wa sheria ya kupimia mwenendo wao, wanadamu wakati wa kipindi hicho kati ya Adamu na Musa walikuwa huru kutokana na dhambi. Kwenye Waroma 2:14, 15, Paulo anataja hivi: “Kwa maana wakati watu wa mataifa wasio na sheria wanapofanya kwa asili mambo ya sheria, watu hawa, ijapokuwa hawana sheria, wao ni sheria kwao wenyewe. Wao ndio wanaoonyesha kuwa yaliyomo katika sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao, huku dhamiri yao ikiwatolea ushahidi na, katikati ya fikira zao wenyewe, wanashtakiwa au hata kutetewa.” Kwa kuwa awali alifanywa katika mfano na sura ya Mungu, mwanadamu ana asili yenye adili, ambayo hutokeza uwezo wa kuwa na dhamiri. Hata wanadamu wasiokamilika, wenye dhambi huendelea kuwa na kiwango fulani cha hiyo, kama yanavyoonyesha maneno ya Paulo. (Ona CONSCIENCE.) Kwa kuwa kimsingi sheria ni ‘kiwango cha kujiendeshea,’ asili hii ya adili hutenda moyoni mwao kama sheria. Hata hivyo, kinyume cha sheria hii ya asili yao ya kiadili kuna sheria nyingine iliyorithiwa, ‘sheria ya dhambi,’ ambayo hupigana na mielekeo ya uadilifu, ikiwafanya kuwa watumwa wale wasioipinga isiwatawale.—Ro 6:12; 7:22, 23.
Asili hii ya adili na dhamiri yenye kushirikishwa inaonekana pia katika kisa cha Kaini. Japo Mungu hakuwa ametoa sheria yoyote kuhusiana na kuua binadamu, kupitia njia ambayo Kaini alijibu swali la Mungu, alionyesha kwamba dhamiri yake ilimhukumu baada ya kumuua Abeli. (Mwa 4:8, 9) Yosefu Mwebrania alionyesha ‘sheria ya Mungu ilikuwa ndani ya moyo wake’ alipojibu ombi la kutongoza la mke wa Potifa, na kusema hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” Ingawa Mungu alikuwa hajashutumu uzinzi kihususa, bado Yosefu aliutambua kuwa ni kosa, ni wenye kuvunja mapenzi ya Mungu kwa ajili ya binadamu kama ilivyosemwa katika Edeni.—Mwa 39:7-9; linganisha Mwa 2:24.
-