Adrián alianza kujifunza Biblia alipokuwa na umri wa miaka 16. Anasema hivi: “Nilipoendelea kujifunza Biblia, nilitambua uhitaji wa kubadili utu wangu.” Alihitaji kuondoa chuki na kuacha jeuri. Alinufaika sana na kile alichojifunza kwenye Waroma 12:17-19 kuhusu kutolipiza kisasi. Anasema: “Nilitambua kwamba Yehova atakomesha ukosefu wa haki kwa njia yake na kwa wakati wake. Hatua kwa hatua niliacha kuwa mjeuri.”
Siku moja jioni, Adrián alishambuliwa na kikundi cha wahalifu ambao zamani alipigana nao. Kiongozi wa kikundi hicho alipaaza sauti na kusema: “Jilinde!” Adrián anakiri hivi: “Nilitamani sana kulipiza kisasi.” Hata hivyo, badala ya kulipiza kisasi, alitoa sala fupi kwa Yehova na kuondoka eneo hilo.
Adrián anaendelea kusema: “Siku iliyofuata nilikutana na kiongozi wa genge hilo akiwa peke yake. Nilishikwa na hasira na nikataka kulipiza kisasi, lakini nilisali tena kimyakimya kwa Yehova anisaidie kujidhibiti. Jambo la kushangaza ni kwamba kijana huyo aliniomba msamaha kwa kusema: ‘Nisamehe kwa yaliyotokea usiku wa jana. Ukweli ni kwamba, ningependa kuwa kama wewe. Nataka kujifunza Biblia.’ Nilifurahi sana kwamba niliweza kudhibiti hasira yangu! Matokeo ni kwamba, tulianza kujifunza Biblia pamoja.”