-
Wakristo Wanapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Kileo?Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
Wakristo Wanapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Kileo?
Ulimwenguni pote, watu wana maoni mbalimbali kuhusu kileo. Baadhi ya watu hufurahia kunywa kileo wakiwa na marafiki. Wengine huamua kwamba hawatakunywa kileo kamwe. Na wengine hunywa kwa wingi mpaka wanalewa. Biblia inasema nini kuhusu kileo?
1. Je, ni kosa kunywa kileo?
Biblia haikatazi kunywa kileo. Badala yake, kati ya zawadi nyingi ambazo Mungu ametupatia, Biblia inataja “divai inayofanya moyo wa mwanadamu ushangilie.” (Zaburi 104:14, 15) Baadhi ya wanaume na wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia walikunywa kileo.—1 Timotheo 5:23.
2. Biblia inatoa ushauri gani kwa wale wanaoamua kunywa kileo?
Yehova anakataza ulevi na kunywa kileo kupita kiasi. (Wagalatia 5:21) Neno lake linasema hivi: “Usiwe miongoni mwa watu wanaokunywa divai nyingi mno.” (Methali 23:20) Hivyo, ikiwa tutaamua kunywa kileo, hata tukiwa faraghani, hatupaswi kunywa sana hivi kwamba tushindwe kufikiri vizuri, kudhibiti maneno na matendo yetu, au kujisababishia madhara ya kiafya. Ikiwa hatuwezi kudhibiti kiasi cha kileo tunachokunywa, tunapaswa kuamua kuacha kabisa kunywa kileo.
3. Tunawezaje kuheshimu uamuzi wa watu wengine kuhusu kileo?
Kila mtu anapaswa kujifanyia uamuzi inapohusu kunywa kileo. Hatupaswi kumhukumu mtu anayeamua kunywa kileo kwa kiasi, wala hatupaswi kumlazimisha mtu ambaye hataki kunywa kileo. (Waroma 14:10) Tunaamua kwamba hatutakunywa kileo ikiwa baada ya kunywa tutawasababishia wengine matatizo. (Soma Waroma 14:21.) Tunatafuta “si faida [yetu wenyewe], bali faida ya yule mtu mwingine.”—Soma 1 Wakorintho 10:23, 24.
CHIMBA ZAIDI
Chunguza kanuni za Biblia ambazo zitakusaidia kuamua ikiwa utakunywa kileo na kiasi ambacho utakunywa. Vilevile, chunguza jambo la kufanya ikiwa unapambana na tatizo la kunywa kupita kiasi.
4. Amua kama utakunywa kileo
Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu kunywa kileo? Ili upate jibu, chunguza muujiza wa kwanza aliofanya. Soma Yohana 2:1-11, kisha mzungumzie maswali haya:
Kutokana na muujiza huo, Yesu ana maoni gani kuhusu kileo na wale wanaokunywa kileo?
Kwa kuwa Yesu hakukataza kunywa kileo, Mkristo anapaswa kumwonaje mtu anayeamua kunywa kileo?
Hata hivyo, ingawa Mkristo yuko huru kunywa kileo, hilo halimaanishi kwamba sikuzote ni jambo la busara kufanya hivyo. Soma Methali 22:3, kisha uchunguze jinsi mambo yafuatayo yanavyoweza kukusaidia kuamua kama utakunywa kileo:
Ikiwa utaendesha gari au kutumia mashine.
Ikiwa wewe ni mjamzito.
Ikiwa daktari amekushauri usinywe kileo.
Ikiwa unashindwa kudhibiti kiasi unachokunywa.
Ikiwa sheria ya nchi haikuruhusu kunywa kileo.
Ukiwa pamoja na mtu ambaye ameamua hatakunywa kileo kwa sababu zamani alishindwa kudhibiti kiasi cha kileo alichokunywa.
Je, utaandaa kileo kwenye harusi au tafrija? Ili kuona jambo litakalokusaidia kuamua, onyesha VIDEO.
Soma Waroma 13:13 na 1 Wakorintho 10:31, 32. Baada ya kusoma kila andiko, zungumzieni swali hili:
Kutumia kanuni hii kunaweza kukusaidiaje kufanya uamuzi unaomfurahisha Yehova?
Kila Mkristo anapaswa kujifanyia uamuzi ikiwa atakunywa kileo au la. Hata ikiwa anaona ni sawa kunywa kileo, huenda wakati mwingine akaamua kutokunywa
5. Amua kiasi ambacho utakunywa
Ikiwa unaamua kunywa kileo, kumbuka jambo hili: Ingawa Yehova hakatazi kunywa kileo, anakataza kunywa kileo kupita kiasi. Kwa nini? Soma Hosea 4:11, 18, kisha mzungumzie swali hili:
Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa mtu atakunywa kileo kupita kiasi?
Tunawezaje kuepuka kunywa kileo kupita kiasi? Tunahitaji kuwa na sifa ya kiasi, na kutambua mipaka yetu. Soma Methali 11:2, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini ni vizuri kujiwekea kiasi hususa cha kileo ambacho utakunywa?
6. Jinsi ya kushinda zoea la kunywa kupita kiasi
Ona jambo lililomsaidia mwanamume fulani ashinde zoea la kunywa kileo kupita kiasi. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie maswali yanayofuata.
Katika video hiyo, Dmitry alitendaje baada ya kunywa kileo?
Je, ilikuwa rahisi kwake kuacha mara moja zoea hilo?
Mwishowe, nini kilichomsaidia kushinda uraibu wa kunywa kileo?
Soma 1 Wakorintho 6:10, 11, kisha mzungumzie maswali haya:
Kwa nini ulevi ni kosa zito?
Ni nini kinachoonyesha kwamba mtu aliye na zoea la kunywa kupita kiasi anaweza kubadilika?
Soma Mathayo 5:30, kisha mzungumzie swali hili:
Kukata mkono kunamaanisha kwamba mtu anapaswa kuacha tabia fulani ili amfurahishe Yehova. Unaweza kufanya nini ikiwa unapambana kushinda zoea la kunywa kileo kupita kiasi?a
Soma 1 Wakorintho 15:33, kisha mzungumzie swali hili:
Rafiki zako wanawezaje kufanya unywe kileo kupita kiasi?
HUENDA MTU AKAULIZA: “Je, ni vibaya kunywa pombe?”
Wewe ungejibuje swali hilo?
MUHTASARI
Yehova amewapa wanadamu kileo ili wafurahie. Lakini anakataza ulevi na kunywa kupita kiasi.
Ungejibuje?
Biblia inasema nini kuhusu kunywa kileo?
Kuna hatari gani ya kunywa kileo kupita kiasi?
Tunawezaje kuheshimu uamuzi wa watu wengine kuhusu kunywa kileo?
CHUNGUZA ZAIDI
Vijana wanawezaje kufanya maamuzi mazuri kuhusu kunywa kileo?
Chunguza hatua unazopaswa kuchukua ili ushinde zoea la kunywa kileo kupita kiasi.
“Mtazamo Unaofaa Kuhusu Pombe” (Mnara wa Mlinzi, Januari 1, 2010)
Je, Mkristo anaweza kushiriki kugonga glasi na kutakiana heri?
“Maswali Kutoka kwa Wasomaji” (Mnara wa Mlinzi, Februari 15, 2007)
Katika simulizi “Nilikuwa Mtungi wa Pombe Usiojaa,” ona jinsi mwanamume fulani alivyoshinda zoea la kunywa kileo kupita kiasi.
a Wale ambao ni waraibu wa kunywa kileo, wanahitaji kutafuta msaada wa wataalamu ili waache zoea hilo. Madaktari wengi wanapendekeza kwamba mtu aliyekuwa na tatizo la kunywa kileo kupita kiasi anapaswa kuacha kabisa kunywa kileo.
-
-
Kwa Nini Mavazi na Mwonekano Wetu Ni Muhimu?Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
-
-
SOMO LA 52
Kwa Nini Mavazi na Mwonekano Wetu Ni Muhimu?
Sisi sote tunapenda kuchagua mavazi tutakayovaa na jinsi tutakavyojipamba. Kuna kanuni za Biblia zinazoweza kutusaidia kuchagua mavazi na mapambo tunayopenda, na pia yatakayomfurahisha Yehova. Tutazungumzia baadhi ya kanuni hizo katika somo hili.
1. Tunapaswa kuongozwa na kanuni gani tunapochagua mavazi na mapambo?
Tunapaswa kuchagua “mavazi yanayofaa, kwa kiasi na utimamu wa akili,” na kudumisha mwonekano safi ambao unaonyesha kwamba ‘tunamtumikia Mungu.’ (1 Timotheo 2:9, 10) Fikiria kanuni hizi nne: (1) Tunapaswa kuvaa “mavazi yanayofaa.” Kama vile ambavyo umejionea katika mikutano ya kutaniko, watu wa Yehova wana mapendezi mbalimbali, lakini mavazi na mitindo yetu ya nywele huonyesha kwamba tunamheshimu Mungu tunayemwabudu. (2) Kuvalia “kwa kiasi” humaanisha kwamba mwonekano wetu haupaswi kuchochea hisia za ngono, wala hatupaswi kujielekezea fikira sana. (3) Tunaonyesha kwamba tuna “utimamu wa akili” kwa kuepuka kufuata kila mtindo wa mavazi au mapambo yanayopendwa na wengi. (4) Sikuzote mwonekano wetu unapaswa kuonyesha kwamba ‘tunamtumikia Mungu,’ ili iwe rahisi kwa wengine kuona kwamba tunamwabudu Mungu wa kweli.—1 Wakorintho 10:31.
2. Kwa nini tunapaswa kuwafikiria waabudu wenzetu tunapochagua mavazi?
Ingawa tuna uhuru wa kuchagua mavazi tutakayovaa, tunapaswa kufikiria jinsi mwonekano wetu utakavyowaathiri wengine. Tunajitahidi sana kuepuka kumkwaza mtu yeyote. Badala yake, ‘tunampendeza jirani yetu kwa mema ili kumjenga.’—Soma Waroma 15:1, 2.
3. Mwonekano wetu unawezaje kuwavutia watu kwenye ibada ya kweli?
Ingawa tunajitahidi kuvalia kwa njia inayofaa pindi zote, tunajitahidi hasa kuvalia vizuri tunapohudhuria mikutano ya kutaniko na tunaposhiriki katika huduma. Hatungependa kuwakengeusha watu wasikazie fikira ujumbe muhimu tunaowapelekea. Badala yake, mwonekano wetu unaweza kuwavutia watu kujifunza kweli na ‘kulipamba fundisho la Mwokozi wetu.’—Tito 2:10.
CHIMBA ZAIDI
Chunguza jinsi tunavyoweza kuhakikisha kwamba mavazi na mwonekano wetu unawasaidia wengine watambue sisi ni Wakristo.
Mwonekano wetu unaweza kuonyesha kwamba tunawaheshimu watu wenye mamlaka. Ingawa Yehova huona jinsi tulivyo moyoni, mwonekano wetu pia unapaswa kumheshimu
4. Mwonekano wetu mzuri unamheshimu Yehova
Ni sababu gani muhimu zaidi inayofanya tufikirie kwa makini mwonekano wetu? Soma Zaburi 47:2, kisha mzungumzie maswali haya:
Kwa kuwa tunamwakilisha Yehova, tunapaswa kuvalia kwa njia gani?
Je, unafikiri mwonekano wetu ni muhimu tunapohudhuria mikutano na tunaposhiriki katika huduma? Kwa nini?
5. Jinsi ya kufanya maamuzi mazuri kuhusu mavazi na mapambo
Iwe mavazi yetu ni ya bei ghali au bei rahisi, yanapaswa kuwa safi na yanayofaa hali hususa. Soma 1 Wakorintho 10:24 na 1 Timotheo 2:9, 10. Kisha mzungumzie kwa nini tunapaswa kuepuka kuvaa . . .
mavazi yasiyo safi na yasiyo nadhifu.
mavazi yanayobana sana, yanayoonyesha sehemu za mwili, au yanayochochea hisia za ngono.
Ingawa Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, Sheria hiyo inatusaidia kujua maoni ya Yehova. Soma Kumbukumbu la Torati 22:5, kisha mzungumzie swali hili:
Kwa nini tunapaswa kuepuka kuvaa na kujipamba kwa njia inayofanya mwanamume aonekane kama mwanamke au mwanamke kuonekana kama mwanamume?
Soma 1 Wakorintho 10:32, 33 na 1 Yohana 2:15, 16, kisha mzungumzie maswali haya:
Kwa nini tunapaswa kuepuka mwonekano unaoweza kuwaudhi wengine katika eneo tunaloishi au kutanikoni?
Ni mitindo gani ya mavazi na mapambo inayopendwa katika eneo unaloishi?
Je, unafikiri baadhi ya mitindo hiyo huenda isimfae Mkristo? Kwa nini?
Tunaweza kuvaa na kujipamba kwa njia mbalimbali na bado tukamfurahisha Yehova
WATU FULANI HUSEMA: “Nina haki ya kuvaa kwa njia yoyote ninayotaka.”
Je, unakubaliana na maoni hayo? Kwa nini?
MUHTASARI
Tunapofanya maamuzi mazuri kuhusu mwonekano wetu, tunaonyesha kwamba tunamheshimu Yehova na watu wengine.
Ungejibuje?
Kwa nini jinsi tunavyovalia na kujipamba ni muhimu kwa Yehova?
Ni kanuni gani zinazopaswa kutuongoza tunapofanya maamuzi kuhusu mwonekano wetu?
Mwonekano wetu unawezaje kuathiri maoni ya wengine kuhusu ibada ya kweli?
CHUNGUZA ZAIDI
Chunguza jinsi mavazi yako yanavyoweza kuathiri maoni ya wengine kukuhusu.
“Mwonekano Wangu Unanitambulishaje?” (Makala iliyo kwenye mtandao)
Jifunze kwa nini ni jambo la hekima kufikiria kwa makini kabla ya kuamua kujichanja chale, yaani, kuchora tattoo mwilini.
“Biblia Inasema Nini Kuhusu Kujichanja Chale?” (Makala iliyo kwenye mtandao)
Chunguza kanuni nyingine zinazopaswa kuongoza maamuzi yetu.
“Je, Mtindo Wako wa Mavazi Unamtukuza Mungu?” (Mnara wa Mlinzi, Septemba 2016)
Mwanamke fulani aliyetaka kumfurahisha Mungu alijifunza jinsi gani kuheshimu maoni ya wengine kuhusu mavazi?
“Mavazi na Mapambo Yalinizuia Kufanya Maendeleo” (Amkeni!, Desemba 22, 2003)
-