-
Pindua Kila Wazo Ambalo Ni Kinyume cha Ujuzi wa Mungu!Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2019 | Juni
-
-
‘FANYWA UPYA KATIKA NGUVU ZINAZOONGOZA AKILI YAKO’
7. Tunawezaje kubadili jinsi tulivyo kwa ndani?
7 Je, inawezekana kubadili mielekeo yetu ya asili au kubadili jinsi tulivyo hasa kwa ndani? Neno la Mungu linajibu hivi: “Mnapaswa kuendelea kufanywa upya katika nguvu zinazoongoza akili zenu, na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Efe. 4:23, 24) Ndiyo, inawezekana kubadili jinsi tulivyo kwa ndani, lakini si rahisi kufanya hivyo. Tunahitaji kufanya mengi zaidi kuliko tu kudhibiti tamaa na matendo yasiyofaa. Tunahitaji kubadili “nguvu zinazoongoza akili” yetu. Hilo linahusisha kubadili tamaa, mielekeo, na nia yetu. Kufanya hivyo kunahitaji jitihada za kuendelea.
8-9. Kisa cha ndugu mmoja kinakaziaje umuhimu wa kubadili jinsi tulivyo kwa ndani?
8 Acheni tuchunguze mfano wa ndugu mmoja ambaye hapo awali alikuwa mgomvi na alipenda kupigana. Alipoacha kunywa pombe na kupigana, alistahili kubatizwa, jambo lililotoa ushahidi mzuri sana katika ujirani alioishi. Lakini jioni moja, muda mfupi baada ya kubatizwa, alijaribiwa kwa njia ambayo hakutazamia. Mwanamume fulani mlevi alikuja nyumbani kwake na alitaka kupigana naye. Mwanzoni ndugu huyo alitamani kumpiga lakini alijizuia. Lakini mwanamume huyo alipolikufuru jina la Yehova, ndugu yetu aliyekuwa amebatizwa karibuni alishindwa kujizuia. Alitoka nje na kumpiga mwanamume huyo. Tatizo lilikuwa wapi? Ingawa kujifunza Biblia kulikuwa kumemsaidia kudhibiti mielekeo yake ya hasira, ndugu huyo hakuwa amebadili nguvu zinazoongoza akili yake. Kwa maneno mengine, hakuwa amebadili jinsi alivyo hasa kwa ndani.
9 Hata hivyo, ndugu yetu hakukata tamaa. (Met. 24:16) Kwa msaada wa wazee, aliendelea kufanya maendeleo. Hatimaye, alistahili kuwa mzee wa kutaniko. Kisha jioni moja, nje tu ya Jumba la Ufalme, alikabili moja kwa moja jaribu linalofanana na lile alilokuwa amekabili miaka kadhaa iliyopita. Mwanamume fulani mlevi alitaka kumpiga mzee mmoja wa kutaniko. Ndugu yetu alifanya nini? Kwa utulivu na upole, alizungumza na mwanamume huyo mlevi, akatuliza hali, na akamsaidia kufika nyumbani. Ni nini kilichomsaidia ndugu yetu kutenda kwa njia tofauti? Alikuwa amebadili nguvu zinazoongoza akili yake. Alikuwa amegeuza utu wake wa ndani kabisa akawa mpenda amani na mnyenyekevu, jambo lililomtukuza Yehova!
10. Ni nini kinachohusika ili tufanye mabadiliko yanayohitajika?
10 Mabadiliko hayo hayatendeki ghafla; wala hayatokei kimuujiza. Huenda tukahitaji ‘kujitahidi kabisa’ kwa kipindi cha miaka mingi. (2 Pet. 1:5) Mabadiliko hayo hayaji eti kwa kuwa tumekuwa “katika kweli” kwa muda mrefu. Tunahitaji kufanya yote tuwezayo ili kubadili jinsi tulivyo kwa ndani. Kuna hatua kadhaa za msingi zinazoweza kutusaidia kufanya mabadiliko hayo. Acheni tuchunguze baadhi ya hatua hizo.
JINSI TUNAVYOWEZA KUBADILI NGUVU ZINAZOONGOZA AKILI YETU
11. Sala hutusaidiaje kubadili nguvu zinazoongoza akili yetu?
11 Sala ndiyo hatua ya kwanza muhimu tunayopaswa kuchukua. Tunahitaji kusali kama mtunga zaburi alivyosali aliposema: “Umba moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na uweke roho mpya ndani yangu, iliyo imara.” (Zab. 51:10) Ni lazima tutambue kwamba tunahitaji kubadili nguvu zinazoongoza akili yetu na tumwombe Yehova atusaidie. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia tufanye mabadiliko yanayohitajika? Ahadi ya Yehova kuhusu Waisraeli waliokuwa na moyo mgumu inaweza kututia moyo. Alisema hivi: “Nitawapa moyo wenye umoja, nami nitatia roho mpya ndani yao . . . na kuwapa moyo wa nyama, [yaani, moyo ulio mwepesi kutii mwongozo wa Mungu].” (Eze. 11:19; maelezo ya chini) Yehova alikuwa tayari kuwasaidia Waisraeli hao wabadilike, na yuko tayari kutusaidia sisi pia.
12-13. (a) Kulingana na Zaburi 119:59, tunahitaji kutafakari kuhusu nini? (b) Unapaswa kujiuliza maswali gani?
12 Kutafakari ndiyo hatua ya pili muhimu. Tunapochunguza Neno la Mungu kila siku, tunahitaji kutenga wakati wa kutafakari, au kufikiria kwa kina ni mawazo na hisia gani tunazohitaji kubadili. (Soma Zaburi 119:59; Ebr. 4:12; Yak. 1:25) Ni lazima tutambue mawazo na hisia zozote tulizo nazo zinazotokana na falsafa za wanadamu. Tunahitaji kukubali kwa unyoofu kwamba tuna udhaifu fulani na kisha tujitahidi sana kuuondoa.
13 Kwa mfano, jiulize hivi: ‘Je, nina hisia zozote za wivu, hata kama ni kwa kiwango kidogo sana?’ (1 Pet. 2:1) ‘Je, nina hisia zozote za kujiona kuwa bora kuliko wengine kwa sababu ya malezi yangu, elimu, au uwezo wangu wa kifedha?’ (Met. 16:5) ‘Je, ninawadharau wengine kwa kuwa hawana vitu nilivyo navyo au kwa kuwa wametoka katika jamii tofauti na yangu?’ (Yak. 2:2-4) ‘Je, ninavutiwa na vitu vilivyo katika ulimwengu wa Shetani?’ (1 Yoh. 2:15-17) ‘Je, ninavutiwa na burudani zenye upotovu wa maadili na ukatili au jeuri?’ (Zab. 97:10; 101:3; Amo. 5:15) Kujiuliza maswali hayo kibinafsi kutakusaidia kuona mambo unayohitaji kurekebisha. Tutakapofanikiwa kushinda mawazo na hisia za moyo wetu zilizo kama “ngome zenye nguvu,” tutamfurahisha Baba yetu wa mbinguni.—Zab. 19:14.
14. Kwa nini ni muhimu sana kuchagua marafiki wazuri?
14 Kuchagua marafiki wazuri ndiyo hatua ya tatu muhimu tunayopaswa kuchukua. Iwe tunatambua au la, sisi huathiriwa sana na watu tunaoshirikiana nao. (Met. 13:20) Tunapokuwa kazini au shuleni, mara nyingi tumezungukwa na watu ambao hawawezi kutusaidia kusitawisha njia ya Mungu ya kufikiri. Hata hivyo, tunaweza kupata marafiki bora katika mikutano yetu ya Kikristo. Hapo ndipo tunapoweza kuchochewa au kuhimizwa, katika “upendo na matendo mazuri.”—Ebr. 10:24, 25, maelezo ya chini.
-