-
Kuwalea Watoto Katika Nidhamu ya MunguAmkeni!—2004 | Novemba 8
-
-
Nidhamu Ni Nini?
Biblia hueleza wazi daraka la wazazi kuhusu kutia nidhamu. Kwa mfano, Waefeso 6:4 husema hivi: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” Andiko hilo linaonyesha kwamba akina baba hasa ndio wanaopaswa kuongoza katika kuwatunza watoto wao. Bila shaka, mama pia hushirikiana na mume wake.
Kuhusu jambo hili kitabu The Interpreter’s Dictionary of the Bible kinasema: “Kwa upande mmoja, nidhamu inayotajwa katika Biblia inahusianishwa na kuzoeza, kufundisha, na ujuzi, na kwa upande ule mwingine inahusianishwa na kukaripia, kusahihisha, na kuadhibu. Kwa kawaida, nidhamu hutolewa ili kuwazoeza watoto.” Kwa hiyo, kutia nidhamu kunahusisha mengi zaidi ya kukemea; kunatia ndani mazoezi yote ambayo watoto wanahitaji ili kufaulu. Lakini wazazi wanawezaje kuepuka kuwakasirisha watoto wao?
Uwe na Hisia-Mwenzi
Ni nini humkasirisha mtoto? Ebu fikiria hali hii. Mfanyakazi mwenzako hukasirika upesi na hana subira. Yeye hakupendi naye huchambua kila kitu unachosema na kufanya. Mara nyingi yeye hupuuza kazi yako na kukufanya ujihisi kuwa hufai. Je, hilo halingekukasirisha na kukuvunja moyo?
Jambo kama hilo linaweza kumpata mtoto ikiwa wazazi wanamsumbua kila mara au kumsahihisha kwa ukali. Ni kweli kwamba mara kwa mara watoto wanahitaji kusahihishwa, nayo Biblia imewapa wazazi mamlaka ya kufanya hivyo. Hata hivyo, kumkasirisha mtoto kwa kumtendea kwa ukali na kwa njia isiyo na upendo kunaweza kumletea madhara ya kihisia, ya kiroho, na hata ya kimwili.
-
-
Kuwalea Watoto Katika Nidhamu ya MunguAmkeni!—2004 | Novemba 8
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]
“MWONGOZO WA AKILINI WA YEHOVA”
Waefeso 6:4 huzungumzia “mwongozo wa akilini wa Yehova.” Katika Biblia fulani, neno la awali la Kigiriki la taarifa hii “mwongozo wa akilini” hutafsiriwa kuwa “ufikirio,” “mashauri,” na “himizo.” Maneno haya yote yanaonyesha kwamba familia zinapaswa kufanya mengi zaidi ya kusoma tu Biblia au kumaliza tu kusoma kichapo fulani kinachozungumzia Biblia. Wazazi wanahitaji kuhakikisha kwamba watoto wao wanaelewa Neno la Mungu, umuhimu wa kutii, na jinsi Yehova anavyowapenda na kuwalinda.
Hilo linaweza kufanywaje? Judy, ambaye ni mama ya watoto watatu, aliona kwamba anahitaji kufanya mengi zaidi ya kuwakumbusha watoto wake kanuni za Mungu. “Niliona kwamba hawakufurahi niliporudia kusema mambo yaleyale katika njia ileile. Nilianza kutafuta njia tofauti za kuwafundisha. Njia moja ilikuwa kuchunguza makala za Amkeni! zinazozungumzia mambo hayo katika njia tofauti. Kwa hiyo, nilijifunza jinsi ya kuwakumbusha watoto wangu mambo fulani bila kuwakasirisha.”
Angelo, ambaye familia yake ilipatwa na hali ngumu, anaeleza jinsi alivyowafundisha binti zake kutafakari Neno la Mungu: “Tulisoma mistari ya Biblia pamoja, kisha nikachagua sehemu fulani za andiko na kuonyesha jinsi zinavyowahusu. Baadaye, walipokuwa wakijisomea Biblia, niliwaona wakifikiri sana, wakitafakari waone jinsi ya kutumia Neno la Mungu maishani mwao.”
-