-
“Mambo Yaliyofunuliwa Ni Yetu Sisi”Mnara wa Mlinzi—1986 | Mei 15
-
-
10. Ni nini uliokuwa mfereji mpya wa kupitishia mafunuo ya Yehova?
10 Mfereji huo mpya ulikuwa nini? Paulo aliutambulisha kwa Waefeso alipoandika kwamba ‘kwa njia ya kundi hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi ijulikane kwa kadiri ya kusudi la milele alilolikusudia katika Kristo Yesu Bwana wetu.’ (Waefeso 3:10, 11) Ndiyo, kundi la Kikristo, lililozaliwa katika Pentekoste mwaka 33 W.K., ndilo lililokabidhiwa “mambo yaliyofunuliwa” yaliyo mapya. Wakiwa kikundi, Wakristo wapakwa mafuta walitumikia wakiwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” aliyewekwa rasmi aandae chakula cha kiroho katika wakati unaofaa. (Mathayo 24:45) Sasa Wakristo walikuwa “mawakili wa siri [takatifu] za Mungu.”—1 Wakorintho 4:1.
11, 12. Ni nini yaliyokuwa baadhi ya mafunuo mazuri ajabu yaliyotolewa kupitia mfereji huo mpya?
11 Uhakika mkubwa wa hizo ‘siri takatifu’ mpya ulikuwa kwamba Yesu Kristo, ule Uzao ulioahidiwa, alikuwa ametokea. (Wagalatia 3:16) Yesu alikuwa ndiye “Shilo,” yule mwenye haki ya kutawala wanadamu, na Yehova alimweka rasmi awe Mfalme wa Ufalme ambao hatimaye ungerudisha Paradiso kwenye dunia hii. (Isaya 11:1-9; Luka 1:31-33) Yesu alikuwa pia ndiye Kuhani Mkuu aliyewekwa rasmi na Yehova, ambaye alitoa uhai wake mkamilifu usio na kidoa uwe ukombozi kwa ajili ya wanadamu, hayo yakiwa ni matumizi mazuri ajabu ya ile kanuni ya utakatifu wa damu. (Waebrania 7:26; 9:26) Tangu wakati huo, wanadamu wenye kuamini walikuwa na tumaini la kupata tena uhai mkamilifu wa kibinadamu uliopotezwa na Adamu.—1 Yohana 2:1, 2.
12 Huyo aliye Uzao ulioahidiwa alikuwa mpatanishi pia, mwenye kutendesha kazi kati ya wafuasi wake na Babaye wa kimbingu agano jipya lililochukua mahali pa lile agano la kale la Torati. (Waebrania 8:10-13; 9:15) Kwa kutegemea msingi wa agano jipya hili, kundi changa la Kikristo lilichukua mahali pa taifa la Israeli wa kimwili, likawa Israeli wa kiroho, ‘uzao wa Abrahamu’ wa kiroho pamoja na Yesu, na mawakili wa “mambo yaliyofunuliwa.” (Wagalatia 3:29; 6:16; 1 Petro 2:9) Zaidi ya hilo, watu wa mataifa walialikwa wawe sehemu ya Israeli huyo wa kiroho—jambo lisilowazika kwa Wayahudi! (Warumi 2:28, 29) Wakiwa pamoja, Waisraeli wa kiroho walio Wayahudi na wasio Wayahudi waliagizwa wafanye wanafunzi wa Yesu katika sehemu zote za dunia. (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, “mambo yaliyofunuliwa” yakawa yanahusu mataifa yote.
13. Hayo “mambo yaliyofunuliwa” mapya yalihifadhiwaje kwa ajili ya vizazi vya wakati ujao?
13 Baada ya muda, hayo “mambo yaliyofunuliwa” kupitia kundi la Kikristo yaliandikwa katika vile vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoikamilisha orodha ya vitabu vyenye roho ya Mungu katika Biblia. Lakini kwa mara nyingine, ndani ya vitabu hivyo yalikuwamo mambo mengi ya unabii kuhusu kusudi la Yehova ambayo yangeeleweka kwa ukamili baada ya karne nyingi tu. Kwa mara nyingine, waandikaji wa Maandiko walikuwa kwa kweli wakihudumia vizazi visivyokuwa vimezaliwa.
-
-
“Mambo Yaliyofunuliwa Ni Yetu Sisi”Mnara wa Mlinzi—1986 | Mei 15
-
-
16. Ni akina nani wamethibitika kuwa ndio mfereji wa kisasa wa Yehova?
16 Yesu alisema kwamba Ufalme wa Mungu ungeondolewa kwa Wayahudi na ‘kupewa taifa lingine lenye kuzaa matunda yake.’ (Mathayo 21:43) Katika karne ya kwanza, taifa hilo likawa ndilo lile kundi changa la Kikristo la Israeli wa kiroho. Leo, kuna kikundi kimoja tu kinachozaa matunda yanayofanana na yale ya kundi la kwanza. Waisraeli hao wa kiroho ndio washiriki wa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” wa Mathayo 24:45-47. Kama Wakristo wa kwanza, Wakristo hao wa siku hizi wamekuwa hawaogopi kuacha ‘nuru yao iangaze.’ (Mathayo 5:14-16) Kuanzia mwaka 1919, wao walijitwika kwa ushujaa ile kazi ya kuzihubiri habari njema za Ufalme katika ulimwengu wote kwa ushuhuda. (Mathayo 24:14) Kwa kuwa wamezaa matunda ya Ufalme wa Mungu, Yehova amewabariki sana kwa kuwafanya wawe na ujuzi wa kisasa katika “hekima ya Mungu iliyo ya namna nyingi.”—Waefeso 3:10.
17, 18. Ni ufahamu gani wenye kusonga mbele hatua kwa hatua ambao Yehova amewezesha kupitia mfereji wake wa kisasa?
17 Hivyo, katika mwaka 1923 unabii mkubwa wa Yesu juu ya kondoo na mbuzi ulieleweka vizuri, na ikatambuliwa kwamba ulimwengu mzima ulikuwa chini ya hukumu. (Mathayo 25:31-46) Katika mwaka 1925 watumishi wa Mungu wa kidunia wakawa ndio wenye ufahamu sahihi wa Ufunuo sura ya 12 na kutambua ni jambo gani hasa lilikuwa limetukia katika ule mwaka uliotiwa alama wa 1914. Katika mwaka 1932 ufahamu wao ulipata kina kirefu hata zaidi. Yehova alifunua kwamba mambo ya unabii juu ya kurudishwa kwa Wayahudi Yerusalemu hayakuhusu taifa la Israeli wa kimwili, lililokuwa limekosa uaminifu kwa muda mrefu na kutupiliwa mbali, bali yalihusu Israeli wa kiroho, kundi la Kikristo. (Warumi 2:28, 29) Halafu, katika mwaka 1935 ufahamu sahihi wa njozi ya Yohana ya “mkutano mkubwa” katika Ufunuo sura ya 7 ikafungua macho ya wapakwa mafuta waione ile kazi kubwa sana ya kukusanya iliyokuwa ingali mbele yao.—Ufunuo 7:9-17.
18 Jambo hilo lilichochea mwendo wa haraka katika kazi ya kuhubiri duniani pote, kwa kuwa mwishowe mkusanyo wa “vitu vya duniani” ulianza kusonga kwa bidii. (Waefeso 1:10) Katika mwaka 1939, mawingu ya vita yalipokusanyika juu ya Ulaya, suala la kutokuwamo lilieleweshwa wazi zaidi. Katika mwaka 1950 “wakuu” [“wana-wafalme,” NW ] walitambulishwa kwa ukamili zaidi. Katika mwaka 1962 utambulishi sahihi wa “mamlaka zilizo kuu” na uhusiano unaofaa kati ya Mkristo na mamlaka hizo ulifahamiwa waziwazi zaidi kutokana na “mambo yaliyofunuliwa.” (Warumi 13:1, 2) Na katika mwaka 1965 ukaja ufahamu wa wazi zaidi juu ya ufufuo wa kidunia na wale wanaoweza kufaidika kutokana nao.—Yohana 5:28, 29.
19. Jamii ya “mtumwa” wa Yehova leo imethibitikaje kuwa mtunzaji anayefaa wa Neno la Mungu?
19 Tena, kundi la Kikristo lililopakwa mafuta limekuwa katika karne hii ya 20 mtunzaji anayefaa wa Neno la Mungu, ule mkusanyo ulioandikwa wa “mambo yaliyofunuliwa.” Washiriki wenye kuwakilisha kundi hilo walijitwika kazi ya kufasiri Biblia katika Kiingereza cha kisasa, na, kufikia leo, Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures imetokea katika lugha 11, nakala zilizochapwa zikiwa ni milioni 40. Jamii ya “mtumwa” ya Wakristo waliopakwa mafuta ndiyo inayoongoza pia shughuli za kimataifa za kufundisha na kuchapisha vitabu vya masomo na magazeti vinavyoitegemea Biblia. Inasimamia mikutano ya kila juma, makusanyiko ya ukawaida, na shule mbali-mbali—yote hayo yakiwa yamekusudiwa kusaidia watafutaji ukweli wapate maarifa sahihi ya “mambo yaliyofunuliwa.” Kwa kweli, sasa “waadilifu” ‘wanang’aa kwa uangavu kama jua’ katika maana ya kiroho, wakithibitisha kuwa wanaustahili uwakili wao.—Mathayo 13:43.
-