Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Na Tuwe Namna Iliyo na Imani
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Desemba 15
    • 16, 17. (a) Paulo alipataje ujasiri kwa ajili ya huduma? (b) Tuchukue hatua zipi tukiona kwamba tunaogopeshwa na aina fulani ya huduma ya Kikristo?

      16 Paulo aliwaandikia Wakristo katika Thesalonike: “Baada ya sisi kuwa tumeteseka kwanza na kutendwa kwa ufidhuli (kama vile nyinyi mjuavyo) katika Filipi, tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu kusema nanyi habari njema ya Mungu kwa kushindana sana.” (1 Wathesalonike 2:2) Paulo na waandamani wake walikuwa ‘wametendwaje kwa ufidhuli’ wakiwa Filipi? Kulingana na wasomi fulani, neno la Kigiriki ambalo Paulo alitumia linamaanisha kutendwa kwa kutukanwa, kuaibishwa, au kwa jeuri. Wenye mamlaka katika Filipi walikuwa wamewapiga kwa fimbo, wakawafunga gerezani, na kuwafunga kwa mikatale. (Matendo 16:16-24) Mambo hayo yenye kuumiza yaliathirije Paulo? Je, watu katika jiji la Thesalonike, ambalo lilifuata katika safari yake ya mishonari, walimwona Paulo akirudi nyuma kwa hofu? La, yeye ‘alijipa ujasiri.’ Alishinda hofu, akaendelea kuhubiri kwa ujasiri.

      17 Paulo alitoa ujasiri wake wapi? Ndani yake mwenyewe? La, alisema alijipa ujasiri “kwa njia ya Mungu wetu.” Kitabu fulani cha marejezo cha watafsiri wa Biblia chasema kwamba taarifa hii yaweza kutafsiriwa “Mungu aliondoa hofu mioyoni mwetu.” Kwa hiyo ukiona kwamba huna ujasiri sana katika huduma yako, au ikiwa sehemu fulani ya huduma yako inaonekana hasa kuwa yenye kuogopesha, mbona usimwombe Yehova akufanyie hivyo pia? Mwombe akuondolee hofu hiyo moyoni mwako. Umwombe akusaidie kujipa ujasiri kwa ajili ya kazi hiyo. Kwa kuongezea, chukua hatua fulani halisi. Kwa mfano, fanya mpango wa kuhubiri na mtu ambaye ana ustadi katika aina hiyo ya kutoa ushahidi ambayo unaogopa kushiriki. Huenda ikahusu maeneo ya biashara, kuhubiri kivivi-hivi, au kutoa ushahidi kupitia simu. Labda mwenzako atakuwa tayari kuhubiri kwanza. Ikiwa hivyo, tazama na ujifunze. Lakini jipe ujasiri wa kuijaribu.

      18. Tunaweza kupata baraka zipi tukijipa ujasiri katika huduma yetu?

      18 Ukijipa ujasiri, fikiria matokeo ambayo huenda ukapata. Unapoendelea bila kuvunjika moyo, inaelekea utapata mambo mazuri yaliyoonwa unapowaeleza wengine ile kweli, mambo ambayo huenda hungeyapata. (Ona ukurasa wa 25.) Utaridhika kujua kwamba umempendeza Yehova kwa kufanya jambo ambalo ni gumu kwako. Utapata baraka zake na msaada wake ili kushinda hofu zako. Imani yako itaimarika. Kwa kweli, huwezi kujitahidi kujenga imani ya wengine bila kujenga imani yako mwenyewe wakati uo huo.—Yuda 20, 21.

  • Walijipa Ujasiri
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Desemba 15
    • Walijipa Ujasiri

      SI RAHISI wakati wote kujipa ujasiri wa kuhubiri. Hata mtume Paulo alisema kwamba pindi moja yeye alijipa ujasiri “kwa kushindana sana.” (1 Wathesalonike 2:2) Je, inastahili “kushindana sana” ili uweze kuhubiri? Si lazima tupate mambo yenye kutokeza, lakini mara nyingi watu wa Mungu hufurahi kwamba wamejipa ujasiri. Ebu fikiria vielelezo vichache.

      Tara, msichana mmoja mwenye umri wa miaka minane, alisikiliza kwa makini mwalimu wao alipokuwa akiambia darasa kwamba wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Wayahudi waliokuwa wamefungwa katika kambi za mateso walilazimishwa kuvalia ishara ya Star of David yenye rangi ya manjano kwa ajili ya utambulisho. Tara akajiuliza kama anapaswa kusema kwa ujasiri. “Nikasali macho yangu yakiwa wazi,” yeye akumbuka. Kisha akainua mkono, akasema kwamba Mashahidi wa Yehova pia walikuwa katika kambi hizo, na walilazimishwa kuvalia beji ya rangi ya zambarau yenye pembe tatu. Mwalimu alifurahi akamshukuru. Maelezo ya Tara yakatokeza mazungumzo zaidi pamoja na mwalimu huyo, ambaye baadaye hata alionyesha darasa lote ile vidio Jehovah’s Witnesses Stand Firm Against Nazi Assault.

      Nchini Guinea, Afrika Magharibi, Irène, mhubiri mchanga ambaye hakuwa amebatizwa alitaka kuboresha huduma yake. Mishonari aliyejifunza naye Biblia alimtia moyo ajaribu kuwaangushia wanafunzi wenzake shuleni magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Irène alisita kwa sababu wanadarasa wenzake hawakuwa wakimsikiliza. Lakini, akiwa ametiwa moyo na mishonari huyo, Irène aliamua kumwendea kwanza mwanafunzi ambaye alionekana kuwa mwenye upinzani zaidi. Irène alishangaa sana kwamba msichana huyo alisikiliza vizuri na kukubali kwa furaha magazeti hayo. Wanafunzi wengine pia waliyakubali. Irène aliangusha magazeti mengi sana mwezi huo kuliko jumla ya magazeti ambayo alikuwa ameangusha kwa miezi mitano iliyotangulia.

      Kule Trinidad mzee mmoja alisita sana kumwendea mkuu wa shule ili kumwonyesha jinsi gazeti la Amkeni! linavyoelimisha. Lakini akajipa ujasiri. Yeye asema: “Nilisali nilipokuwa nikiingia kwenye ua. Sikuamini wakati yule mkuu alipoonyesha furaha isivyo kawaida.” Alikubali gazeti la Amkeni! la “Vijana wa Leo Wana Tumaini Gani?” na hata akakubali litumiwe kufundisha darasa. Tangu wakati huo, amekubali magazeti 40 yanayozungumzia mambo mbalimbali.

      Akiwa kijana, Vaughn aliona kuhubiri kuwa jambo gumu. “Nilikuwa nashikwa na wasiwasi, natoka jasho mikononi, na kuzungumza haraka-haraka—singeweza kuzungumza polepole.” Hata hivyo, baadaye akawa mhudumu wa wakati wote. Na bado anapata ugumu wa kuzungumza. Pindi moja baada ya kuvunjika moyo akitafuta kazi, alitaka kumtolea mtu fulani ushahidi kwenye gari-moshi, “ili angalau apate mafanikio fulani kwenye siku hiyo mbaya.” Lakini aliwaogopa watu walioonekana kuwa wafanyabiashara mashuhuri waliokuwa katika gari-moshi la chini ya ardhi. Hatimaye, akajipa ujasiri wa kuzungumza na mzee mmoja aliyeketi kando yake. Wakawa na mazungumzo marefu. “Unauliza maswali mazuri sana ilhali wewe ni mchanga,” akasema mfanyabiashara huyo, akiuliza, “Je, wewe ni mwanatheolojia?” Vaughn akajibu, “La, mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” “Aha,” mtu huyo akasema akitabasamu. “Sasa nimeelewa.”

      Mashahidi hao wote—na wengine wengi—wamefurahi kwamba walijipa ujasiri wa kuhubiri. Je, wewe pia utajipa ujasiri?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki