-
Ni Upendo wa Aina Gani Unaoleta Furaha ya Kweli?Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2018 | Januari
-
-
2. Ni upendo gani usiofaa ambao watu waliojitenga na Mungu huonyesha? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)
2 Hata hivyo, Maandiko yaliyoongozwa na roho yalitabiri kwamba katika siku zetu watu waliojitenga na Mungu wangeonyesha upendo usiofaa—upendo wenye ubinafsi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Katika siku za mwisho . . . , watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Tim. 3:1-4) Upendo huo wenye ubinafsi haupatani hata kidogo na upendo wa Kikristo; ni tofauti kabisa na upendo huo. Watu wanaofuatilia malengo yenye ubinafsi hawawezi kupata furaha wanayotarajia. Kwa kweli, upendo wa aina hiyo hutokeza ulimwengu ambao ni ‘mgumu kushughulika nao.’
-
-
Ni Upendo wa Aina Gani Unaoleta Furaha ya Kweli?Mnara wa Mlinzi (Funzo)—2018 | Januari
-
-
UNAMPENDA MUNGU AU UNAJIPENDA MWENYEWE?
4. Kwa nini si vibaya kujipenda kwa kiwango kinachofaa?
4 Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo aliandika hivi: “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe.” Je, ni vibaya kujipenda? Hapana, ni jambo la kawaida na hata inafaa kujipenda kwa kiwango kinachofaa. Yehova alituumba hivyo. Yesu alisema hivi: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.” (Marko 12:31) Ikiwa hatujipendi, hatuwezi kuwapenda jirani zetu. Pia Maandiko yanasema, “Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Mwanamume anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.” (Efe. 5:28, 29) Hivyo, inafaa kujipenda kwa kiwango kinachofaa.
5. Unaweza kuwafafanuaje watu wanaojipenda wenyewe kupita kiasi?
5 Upendo unaotajwa kwenye 2 Timotheo 3:2 ni upendo usiofaa. Ni upendo uliopotoka, upendo wenye ubinafsi. Watu wanaojipenda wenyewe kupita kiasi hujifikiria kuliko ilivyo lazima. (Soma Waroma 12:3.) Jambo kuu maishani mwao ni wao wenyewe. Hawawajali wengine hata kidogo. Mambo yanapoenda kombo, wao huwa na mwelekeo wa kuwalaumu wengine badala ya kuwajibika kwa matendo yao. Kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinawalinganisha watu wanaojipenda wenyewe na ‘nungunungu ambaye hujikunja na kuwa kama mpira, akifurahia manyoya laini yenye joto upande wa ndani huku akielekeza nje miiba yake yenye ncha kali.’ Watu kama hao wenye ubinafsi hawana furaha ya kweli.
6. Kumpenda Mungu humfanya mtu awe na sifa zipi?
6 Mtume Paulo anataja kujipenda wenyewe kuwa jambo la kwanza katika orodha ya sifa zisizofaa ambazo zingeenea sana katika siku za mwisho. Wasomi wa Biblia wanadokeza kwamba sifa hiyo inatajwa ikiwa ya kwanza kwa sababu sifa zinazofuata hutokana nayo. Kinyume cha hilo, watu wanaompenda Mungu huonyesha sifa tofauti kabisa. Biblia huhusianisha upendo wa kimungu na shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia. (Gal. 5:22, 23) Mtunga zaburi aliandika hivi: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!” (Zab. 144:15) Yehova ni Mungu mwenye furaha, na watu wake huonyesha sifa hiyo. Zaidi ya hilo, tofauti na watu wanaojipenda wenyewe na wanaopenda tu kupokea, watumishi wa Yehova wanafurahia kujitoa kwa manufaa ya wengine.—Mdo. 20:35.
Tunaweza kuepukaje kuwa wenye kujipenda wenyewe? (Tazama fungu la 7)
7. Ni maswali gani yatakayotusaidia kuchanganua upendo wetu kwa Mungu?
7 Tunaweza kutambuaje ikiwa upendo wetu kwa Mungu umeanza kupungua na kwamba tumeanza kujipenda wenyewe zaidi? Fikiria himizo hili lililo katika Wafilipi 2:3, 4: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.” Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninatumia shauri hilo maishani? Je, ninataka kutoka moyoni kufanya mapenzi ya Mungu? Je, mimi hujitahidi kuwasaidia watu kutanikoni na katika huduma ya shambani?’ Si rahisi nyakati zote kujitoa kwa ajili ya wengine. Jitihada nyingi inahitajika na pia kujidhabihu. Lakini je, kuna jambo lingine lolote linaloweza kutupatia furaha zaidi kuliko kujua kwamba tuna kibali cha Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote?
8. Kumpenda Mungu kumewachochea wengine wafanye nini?
8 Kumpenda Mungu kumewachochea wengine waache kazi nzuri zenye mshahara mnono ili wamtumikie Yehova kikamili zaidi. Ericka, dada anayeishi Marekani ni daktari. Lakini badala ya kufuatilia cheo chenye umashuhuri katika taaluma ya kitiba, aliamua kuwa painia wa kawaida na ametumikia pamoja na mume wake katika nchi kadhaa. Anapokumbuka kipindi hicho, anasema hivi: “Mambo mengi ambayo tulijionea katika eneo la lugha ya kigeni, na marafiki wengi ambao tulipata, yameboresha maisha yetu kwelikweli. Bado mimi ni daktari, lakini ninapotumia muda mwingi zaidi na nguvu zangu kuwasaidia watu wapone kiroho na kuwasaidia ndugu na dada zangu kutanikoni, ninaridhika sana na kupata shangwe nyingi.”
JE, UNAJIWEKEA HAZINA MBINGUNI AU DUNIANI?
9. Kwa nini kupenda pesa hakuwezi kuleta furaha?
9 Paulo aliandika kwamba watu wangekuwa “wenye kupenda pesa.” Miaka kadhaa iliyopita, painia fulani nchini Ireland alizungumza na mwanamume mmoja kuhusu Mungu. Mwanamume huyo alichomoa noti ya pesa, akaiinua, na kumwambia hivi kwa kiburi: “Huyu ndiye mungu wangu!” Ingawa watu wengi hawawezi kusema hivyo waziwazi, ulimwengu huu umejaa watu wanaopenda pesa na vitu vinavyoweza kununuliwa na pesa hizo. Lakini Biblia inatuonya hivi: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.” (Mhu. 5:10) Watu kama hao hawawezi kamwe kuridhika na pesa, nao hujisababishia “maumivu mengi” kwa kujitahidi kujikusanyia pesa hizo.—1 Tim. 6:9, 10.
10. Aguri aliandika nini kuhusu utajiri na umaskini?
10 Bila shaka, sisi sote tunahitaji pesa. Kwa kadiri fulani, pesa ni ulinzi. (Mhu. 7:12) Lakini je, inawezekana mtu akawa na furaha ya kweli ikiwa ana pesa za kushughulikia mahitaji yake ya msingi tu? Ndiyo, inawezekana! (Soma Mhubiri 5:12.) Aguri mwana wa Yake aliandika hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile tu fungu langu la chakula.” Ni rahisi kuelewa kwa nini Aguri hakutaka kuwa maskini hohehahe. Alieleza kwamba hakutaka ashawishike kuiba kwa sababu wizi ungemvunjia Mungu heshima. Lakini kwa nini alisali kwamba asipate utajiri? Aliandika hivi: “Ili nisishibe na kukukana na kusema, ‘Yehova ni nani?’” (Met. 30:8, 9) Huenda unawajua watu wanaotumainia utajiri wao badala ya kumtumaini Mungu.
11. Yesu alitoa shauri gani kuhusu pesa?
11 Watu wanaopenda pesa hawawezi kumpendeza Mungu. Yesu alisema hivi: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” Alikuwa ametangulia kusema hivi: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula na ambako wezi huvunja na kuiba. Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni, ambako hazitaliwa na nondo wala kutu, na ambako wezi hawatavunja na kuiba.”—Mt. 6:19, 20, 24.
12. Kuishi maisha rahisi kunaweza kutusaidiaje kumtumikia Mungu? Toa mfano.
12 Watu wengi wametambua kwamba kuishi maisha rahisi huwafanya wawe na furaha zaidi na kuwapa muda mwingi zaidi wa kumtumikia Yehova. Jack, ndugu anayeishi Marekani, aliuza nyumba yake kubwa na biashara yake kwa sababu alijua kufanya hivyo kungemwezesha kufanya upainia pamoja na mke wake. Anakumbuka hivi: “Haikuwa rahisi kuuza nyumba yetu maridadi na ardhi tuliyomiliki. Hata hivyo, kwa miaka mingi ningerudi nyumbani nikiwa nimechoshwa na matatizo kazini. Mke wangu, ambaye alikuwa painia wa kawaida, alikuwa na furaha sikuzote. Alikuwa akisema hivi, ‘Mimi ninamtumikia mwajiri bora zaidi!’ Kwa kuwa sasa mimi pia ni painia, sote tunamfanyia kazi mwajiri yuleyule, Yehova.”
Tunaweza kuepukaje kuwa wenye kupenda pesa? (Tazama fungu la 13)
13. Tunaweza kufanya nini ili kuchanganua maoni yetu kuhusu pesa?
13 Ili kuchanganua maoni yetu kuhusu pesa, tunaweza kuchunguza kwa unyoofu maoni yetu kuhusu maswali haya: ‘Je, ninaamini kabisa yale ambayo Biblia inasema kuhusu pesa na, je, ninaishi kupatana na maoni hayo? Je, jambo kuu maishani mwangu ni kutafuta pesa? Je, ninathamini zaidi vitu vya kimwili kuliko uhusiano wangu pamoja na Yehova au na watu wengine? Je, kweli ninaamini kwamba Yehova ataniandalia mahitaji yangu?’ Tunaweza kuwa na uhakika kwamba hatawatamausha kamwe wale wanaomtumaini.—Mt. 6:33.
-