-
Kuisikiliza Dhamiri YakoMnara wa Mlinzi—2007 | Oktoba 15
-
-
Kuisikiliza Dhamiri Yako
“Vitu vyote ni safi kwa watu safi. Lakini kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi.” —TITO 1:15.
1. Paulo alijihusisha jinsi gani na makutaniko ya Krete?
BAADA ya mtume Paulo kumaliza safari tatu za umishonari, alikamatwa na mwishowe akapelekwa Roma, ambako alifungwa gerezani kwa miaka miwili. Alifanya nini alipowekwa huru? Wakati fulani, Paulo alitembelea kisiwa cha Krete akiwa pamoja na Tito, naye akamwandikia Tito hivi: “Nilikuacha wewe Krete, ili uyarekebishe mambo yaliyokuwa na kasoro na uweke rasmi wanaume wazee.” (Tito 1:5) Mgawo wa Tito ulihusu suala la dhamiri.
2. Tito alipaswa kushughulikia tatizo gani katika kisiwa cha Krete?
2 Paulo alimshauri Tito kuhusu sifa za kustahili za wazee wa kutaniko, kisha akaonyesha kwamba kuna “watu wengi watundu, wanaoongea maneno yasiyo na faida, na wanaodanganya akili za watu.” Watu hao walikuwa ‘wakiharibu nyumba nzima-nzima kwa kufundisha mambo ambayo hawakupaswa kufundisha.’ Tito alipaswa ‘kuendelea kuwakaripia.’ (Tito 1:10-14; 1 Timotheo 4:7) Paulo alisema kwamba akili na dhamiri za watu hao zilikuwa ‘zimetiwa unajisi,’ akitumia maneno hayo katika maana ya kutia doa, kama vile nguo nzuri inavyoweza kutiwa doa na rangi. (Tito 1:15) Huenda wengine kati ya watu hao walikuwa na malezi ya Kiyahudi, kwa kuwa ‘walishikamana na tohara.’ Leo makutaniko hayapotoshwi na watu walio na maoni kama hayo. Hata hivyo, tunaweza kujifunza mengi kuhusu dhamiri kutokana na mashauri ambayo Paulo alimpa Tito.
Wale Walio na Dhamiri Iliyotiwa Unajisi
3. Paulo alimwandikia Tito nini kuhusu dhamiri?
3 Ona ni katika hali gani Paulo alitaja neno dhamiri. “Vitu vyote ni safi kwa watu safi. Lakini kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi, bali akili zao na pia dhamiri zao zimetiwa unajisi. Wao hutangaza hadharani kwamba wanamjua Mungu, lakini humkana kwa matendo yao.” Kwa wazi, watu fulani walioishi wakati huo walihitaji kufanya mabadiliko ili “wawe na afya katika imani.” (Tito 1:13, 15, 16) Walikuwa na tatizo la kutofautisha kati ya mambo yaliyokuwa safi na yale ambayo hayakuwa safi, na hilo lilihusisha dhamiri yao.
4, 5. Ni kasoro gani ambazo watu wengine walikuwa nazo katika makutaniko, na hilo lilikuwa na matokeo gani juu yao?
4 Zaidi ya miaka kumi mapema, baraza linaloongoza la Kikristo lilifikia uamuzi wa kwamba waabudu wa kweli hawakuwa tena chini ya takwa la kutahiriwa, na wakayajulisha makutaniko uamuzi huo. (Matendo 15:1, 2, 19-29) Hata hivyo, watu wengine huko Krete walikuwa bado ‘wanashikamana na tohara.’ Walipinga waziwazi maamuzi ya baraza linaloongoza, ‘wakifundisha mambo ambayo hawakupaswa kufundisha.’ (Tito 1:10, 11) Wakiwa na maoni yaliyopotoka, huenda walitetea masharti ya Sheria ya Musa kuhusu vyakula na usafi wa kidesturi. Na huenda hata waliongezea yale ambayo Sheria ilisema, kama walivyofanya watangulizi wao katika siku za Yesu, na pia walitetea hadithi zisizo za kweli za Wayahudi na amri za wanadamu.—Marko 7:2, 3, 5, 15; 1 Timotheo 4:3.
5 Maoni hayo yalikuwa na matokeo mabaya juu ya maamuzi yao na ufahamu wao wa maadili, yaani, dhamiri yao. Paulo aliandika hivi: “Kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi.” Dhamiri zao zilipotoshwa sana hivi kwamba hazingeweza tena kutegemeka katika kuwaongoza kutenda na kuchanganua mambo. Zaidi ya hayo, waliwahukumu Wakristo wenzao katika mambo ya kibinafsi, mambo ambayo Mkristo angeweza kufanya uamuzi unaotofautiana na wa mwingine. Kuhusiana na hilo, Wakrete hao walikuwa wakiona mambo yaliyo safi kuwa najisi. (Waroma 14:17; Wakolosai 2:16) Walidai kwamba wanamjua Mungu, lakini matendo yao yalionyesha kwamba hawakumjua.—Tito 1:16.
“Safi kwa Watu Safi”
6. Paulo alitaja vikundi gani viwili vya watu?
6 Tunaweza kufaidika jinsi gani na yale ambayo Paulo alimwandikia Tito? Ona tofauti iliyopo katika maneno haya: “Vitu vyote ni safi kwa watu safi. Lakini kwa watu waliotiwa unajisi na wasio na imani hakuna kitu chochote kilicho safi, bali akili zao na pia dhamiri zao zimetiwa unajisi.” (Tito 1:15) Bila shaka, Paulo hakuwa akisema kwamba kwa Mkristo aliye safi kiadili, kila kitu ni safi na kinaruhusiwa. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu hilo kwa sababu Paulo alionyesha wazi katika barua nyingine kwamba mtu anayefanya uasherati, kuabudu sanamu, kuwasiliana na pepo, na kadhalika ‘hataurithi ufalme wa Mungu.’ (Wagalatia 5:19-21) Hivyo, tunapaswa kukata kauli kwamba Paulo alikuwa akizungumzia kweli ya ujumla kuhusu vikundi viwili vya watu, wale ambao ni safi kiadili na kiroho na wale ambao si safi.
-
-
Kuisikiliza Dhamiri YakoMnara wa Mlinzi—2007 | Oktoba 15
-
-
Sauti Mbalimbali, Maamuzi Mbalimbali
9. Ikiwa “vitu vyote ni safi,” kazi ya dhamiri ni nini?
9 Lakini Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba “vitu vyote ni safi kwa watu safi”? Paulo alikuwa akizungumza kuhusu Wakristo ambao walikuwa wamepatanisha maoni na ufahamu wao wa kiadili na viwango vya Mungu ambavyo vinapatikana katika Neno lake lililoongozwa na roho. Wakristo kama hao wanatambua kwamba inapohusu mambo mengi yasiyokatazwa moja kwa moja na Mungu, waamini wanaweza kuwa na maamuzi yanayotofautiana. Badala ya kuwahukumu wengine, wanaviona kuwa “safi” vitu ambavyo Mungu hashutumu. Hawatazamii kwamba watu wengine wote watakuwa na maoni kama yao kuhusu mambo fulani maishani ambayo Biblia haitoi mwongozo hususa. Acheni tufikirie mifano fulani.
-