Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Unaweza Kuvumilia Hadi Mwisho
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Oktoba 1
    • 10 Ni nani walio watazamaji katika shindano la mbio la kupata uhai ambalo Wakristo wameingia? Baada ya kuorodhesha mashahidi waaminifu wa Yehova wa kabla ya Ukristo, kama ilivyorekodiwa katika sura ya 11 ya kitabu cha Waebrania, Paulo aliandika: “Basi, kwa sababu tuna wingu kubwa hivyo la mashahidi likituzingira, . . . acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 12:1) Kwa kutumia mfano wa wingu, Paulo hakutumia neno la Kigiriki lifafanualo wingu lenye umbo na ukubwa fulani hususa. Badala yake, alitumia neno ambalo kwa mujibu wa mwandishi mmoja wa kamusi W. E. Vine, “ladokeza wingu lisilo na umbo hususa linalotanda na kufunika anga.” Ni dhahiri kwamba Paulo alikuwa akifikiria halaiki kubwa ya mashahidi—wengi sana hivi kwamba walikuwa kama wingu lisilo na umbo hususa.

      11, 12. (a) Mashahidi waaminifu wa kabla ya Ukristo waweza kutushangiliaje, kusema kitamathali, tuendelee kukimbia katika shindano la mbio kwa uvumilivu? (b) Twaweza kunufaikaje kikamili zaidi kutokana na ‘wingu kubwa la mashahidi’?

      11 Je, mashahidi waaminifu wa kabla ya Ukristo wanaweza kuwa watazamaji halisi siku hizi? Bila shaka, la. Wote wamelala katika kifo, wakingoja ufufuo. Hata hivyo, wao wenyewe walikuwa wakimbiaji wenye mafanikio walipokuwa hai, na vielelezo vyao bado vimo katika rekodi ya Biblia. Tunapojifunza Maandiko, waaminifu hawa wanaweza kudhihirika akilini mwetu na wanaweza kutushangilia, kusema kitamathali, ili tuendelee kukimbia katika shindano la mbio hadi mwisho.—Waroma 15:4.a

      12 Kwa mfano, mambo ya kilimwengu yakitushawishi, je, kuchunguza jinsi Musa alivyokataa utukufu wa Misri hakutuchochei tudumu mwendoni? Ikiwa jaribu linalotukabili laonekana kuwa kali, kukumbuka jaribu kali lililomkabili Abrahamu alipoambiwa amdhabihu mwanaye Isaka, kwa hakika kungetutia moyo tusiache shindano la imani. Kiwango ambacho ‘wingu hili kubwa’ la mashahidi hutuchochea katika mbio hizo hutegemea jinsi wanavyodhihirika waziwazi katika macho yetu ya uelewevu.

      13. Mashahidi wa Yehova wa siku hizi hutuchocheaje tuendelee na shindano la mbio la kupata uhai?

      13 Tunazungukwa pia na Mashahidi wa Yehova wengi sana siku hizi. Ni vielelezo vilivyoje vya imani ambavyo vimewekwa na Wakristo watiwa-mafuta na vilevile wanaume na wanawake wa “umati mkubwa”! (Ufunuo 7:9) Mara kwa mara twaweza kusoma masimulizi ya maisha yao katika gazeti hili na vichapo vingine vya Watch Tower.b Tufikiriapo imani yao, tunatiwa moyo kuvumilia hadi mwisho. Na ni jambo zuri kama nini kupata utegemezo wa rafiki wa karibu na watu wa jamaa ambao wenyewe wanamtumikia Yehova kwa uaminifu! Naam, tuna watu wengi wa kutuchochea kuendelea na shindano la mbio la kupata uhai.

      Pima Mwendo Wako kwa Hekima

      14, 15. (a) Kwa nini ni muhimu kupima mwendo wetu kwa hekima? (b) Kwa nini yatupasa kuwa wenye kusababu tuwekapo miradi?

      14 Mkimbiaji anapokimbia katika shindano la mbio ndefu, kama vile marathoni, ni lazima apime mwendo wake kwa hekima. “Kuanza mbio kwa kasi sana kwaweza kufanya ushindwe,” lasema gazeti la New York Runner. “Yaelekea matokeo yatakuwa kung’ang’ana sana katika kilometa za mwisho au kuacha kukimbia.” Mkimbiaji mmoja wa mbio za marathoni akumbuka: “Msemaji kwenye hotuba niliyohudhuria ili kujitayarisha kwa ajili ya shindano la mbio la marathoni alionya hivi waziwazi: ‘Usijaribu kushindana na wakimbiaji wanaokimbia kwa kasi. Kimbia kwa mwendo wako mwenyewe. La sivyo, utachoka na huenda ukalazimika kuacha kukimbia.’ Kutii shauri hilo kulinisaidia kumaliza shindano hilo la mbio.”

      15 Ni lazima watumishi wa Mungu wajikakamue kisulubu katika shindano la mbio la kupata uhai. (Luka 13:24) Hata hivyo, mwanafunzi Yakobo aliandika: “Hekima ya kutoka juu kwanza kabisa ni . . . yenye kukubali sababu.” (Yakobo 3:17) Ingawa kielelezo kizuri cha wengine chaweza kututia moyo tufanye mengi zaidi, kuwa wenye kusababu kutatusaidia kuweka miradi tuwezayo kutimiza kulingana na uwezo wetu na hali zetu. Maandiko yatukumbusha: “Acheni kila mmoja athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, na ndipo atakuwa na sababu ya mchachawo kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine. Kwa maana kila mmoja atachukua mzigo wake mwenyewe.”—Wagalatia 6:4, 5.

      16. Kiasi hutusaidiaje kupima mwendo wetu?

      16 Kwenye Mika 6:8, tunaulizwa swali hili lenye kuamsha fikira: “BWANA anataka nini kwako, ila . . . kwenda kwa unyenyekevu [“kiasi,” NW] na Mungu wako!” Kiasi chatia ndani kufahamu udhaifu wetu mbalimbali. Je, afya mbaya au uzee zinapunguza yale tuwezayo kufanya katika utumishi wa Mungu? Tusivunjike moyo. Yehova hukubali jitihada na dhabihu zetu ‘kulingana na tulicho nacho, si kulingana na kile ambacho hatuna.’—2 Wakorintho 8:12; linganisha Luka 21:1-4.

  • Unaweza Kuvumilia Hadi Mwisho
    Mnara wa Mlinzi—1999 | Oktoba 1
    • Mwisho Ukaribiapo

      20. Shindano la mbio la kupata uhai lawezaje kuwa gumu zaidi mwisho ukaribiapo zaidi?

      20 Katika shindano la mbio la kupata uhai, ni lazima tushindane na adui yetu mkuu, Shetani Ibilisi. Tukaribiapo mwisho, yeye anajaribu sana kutufanya tujikwae au kutufanya tupunguze mwendo. (Ufunuo 12:12, 17) Na si jambo rahisi kuendelea kuwa wahubiri wa Ufalme waliojiweka wakfu na walio waaminifu tunapofikiria vita, njaa kuu, magonjwa ya kuambukiza, na shida nyingine zinazoashiria “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4; Mathayo 24:3-14; Luka 21:11; 2 Timotheo 3:1-5) Isitoshe, huenda mara nyingine mwisho ukaonekana ukiwa mbali sana kuliko vile tulivyotarajia, hasa ikiwa tuliingia katika shindano la mbio miongo kadhaa iliyopita. Hata hivyo, Neno la Mungu hutuhakikishia kwamba mwisho utakuja. Yehova asema hautachelewa. Mwisho umekaribia.—Habakuki 2:3; 2 Petro 3:9, 10.

      21. (a) Ni nini kitakachotuimarisha tuendeleapo katika shindano la mbio la kupata uhai? (b) Tunapaswa kuazimia nini mwisho ukaribiapo?

      21 Basi, ili kufaulu katika shindano la mbio la kupata uhai, ni lazima tupate nguvu kutokana na kile ambacho Yehova ametuandalia kwa upendo ili tupate lishe kiroho. Twahitaji pia kitia moyo tuwezacho kupata kutokana na ushirika wetu na waamini wenzetu, ambao pia wanakimbia katika shindano hili la mbio. Hata ikiwa mnyanyaso mkali na matukio yasiyotarajiwa yanayotupata njiani yatafanya shindano letu la mbio liwe gumu zaidi, twaweza kuvumilia hadi mwisho kwa sababu Yehova huandaa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Inatia moyo kama nini kujua kwamba Yehova hutaka tumalize mwendo kwa ushindi! Kwa azimio thabiti, “acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu,” tukiwa na uhakika kwamba “katika majira yapasayo tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Waebrania 12:1 Wagalatia 6:9.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki