-
Lile Takwa Gumu la Kufuata Katika Hatua za Nyayo ZakeMnara wa Mlinzi—1988 | Mei 1
-
-
Lile Takwa Gumu la Kufuata Katika Hatua za Nyayo Zake
“Kwa maana Kristo aliteseka kwa ajili yenu ninyi na akawaachia ninyi kielelezo cha kibinafsi, ili kwamba ninyi mweze kufuata katika hatua za nyayo zake.”—1 PETRO 2:21, Phillips.
1, 2. (a) Ni jambo gani linaloweza kuwa takwa gumu kweli kweli, na kwa sababu gani linafanya Wakristo wapendezwe na kuliangalia? (b) Ni maswali gani yanayotokezwa hapa?
JE! WEWE umepata kutembea kando-kando ya ufuo wa bahari wenye mchanga, au kupitia uwanja wenye udongo mwororo na kujikuta ukishangazwa sana na ule mfuatano-fuatano wa hatua za nyayo zilizoachwa na mtu fulani aliyetembea hapo kabla ya wewe? Je! labda wewe hata ulichagua fuatano moja la hatua za nyayo na kujaribu kuzifuata, huku ukijaribu kufanya hatua zako mwenyewe zilingane sana na hizo kwa kadiri ilivyowezekana? Ikiwa ndivyo, uligundua kwamba halikuwa jambo rahisi. Kwa uhakika, kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za mwingine—kihalisi au kitamathali—ni takwa gumu kweli kweli. Na bado, kwa kujiita Wakristo, sisi tumeonyesha tamaa yetu ya kufanya lilo hilo, kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Kristo.
2 Je! wewe una nia ya kutia jitihada inayohitajiwa kabisa ili kutimiza hilo takwa gumu kwa mafanikio? Zaidi ya hilo, je! wewe umepiga moyo konde kufanya hivyo, liwe lo lote liwalo? Ikiwa ndivyo, kuyaelewa kwa ukamili magumu ya kufuata katika hatua za nyayo halisi kutakufanya ufanikiwe zaidi kufuata katika hatua za nyayo za kitamathali za Kristo.
Jifunze Kujipatanisha
3. Kwa sababu gani kufuata katika hatua za nyayo za mtu fulani kunaonekana kuwa si jambo la asili hapo kwanza?
3 Kila mmoja ana njia yake ya kipekee ya kutembea. Mathalani, urefu wa mpigo wa hatua unatofautiana kwa mtu na mtu, kama ilivyo kuhusu jinsi mtu anavyokanyagisha chini nyayo zake. Huenda vidole vya nyayo zake vikalazwa kirefu-refu, au huenda vikapindwa kwa ndani au kwa nje vikitazama kando kidogo, labda kwa kujipinda zaidi katika wayo mmoja kuliko ilivyo katika ule mwingine. Je! wewe unalitambua lile takwa gumu? Ili ufuate kwa ukaribu hatua za nyayo za mwingine, ni lazima wewe upatanishe urefu wa mpigo wa hatua na msimamo wa wayo wako ili ulingane na wake. Hapo kwanza litaonekana kuwa jambo lisilo la kiasili, lakini ni lazima lifanywe. Hakuna njia nyingine.
4. Kwa sababu gani kufuata katika hatua za nyayo za Yesu ni takwa gumu la pekee?
4 Njia ya Kristo ya kutembea, ikisemwa kitamathali, haikuwa na kifani, kwa kuwa miongoni mwa marika wake yeye peke yake ndiye aliyekuwa mwanadamu mkamilifu, “mmoja ambaye hakutenda dhambi.” (2 Wakorintho 5:21, NW) Kwa kuwa kwa asili wanadamu ni watenda dhambi wasiokamilika, kutembea katika hatua za nyayo za Yesu siyo njia yao ya kikawaida ya kutembea. Paulo alikumbusha Wakristo katika Korintho juu ya jambo hilo, akisema: “Kwa maana ninyi bado ni wa kimnofu. Kwa maana hali kuna wivu na ugomvi miongoni mwenu ninyi, je! ninyi si wa kimnofu na je! ninyi hamuwi mnatembea kama wanadamu wanavyofanya?” Maelekeo ya wivu na ugomvi, “kazi za mnofu,” ni ya kikawaida kwa watu wasiokamilika, lakini Yesu alitembea kwa kufuata ile njia ya upendo, na “upendo si wenye wivu, . . . hauwi wenye kuchokozeka.” Kwa hiyo kutembea katika hatua za nyayo za Kristo kunatokeza takwa gumu lililo kubwa kuliko kama sisi tungeombwa tufuate tu katika hatua za nyayo za mtu asiyekamilika.—1 Wakorintho 3:3; 13:4, 5; Wagalatia 5:19, 20; ona pia Waefeso 5:2, 8, NW.
5, 6. (a) Kwa sababu gani watu wengi wameshindwa kufuata katika hatua za nyayo za Kristo, hiyo ikiongoza Paulo kutoa shauri gani? (b) Ni jinsi gani watu wanavyotiwa moyo watembee katika hatua za nyayo za Kristo leo, tokeo likiwa nini kwao?
5 Kando na kutokamilika, ujinga wa kutojua mapenzi ya Mungu unaweza pia kuzuia mtu asitembee katika hatua za nyayo za Kristo. Hivyo Paulo aliwaonya kwa upole Wakristo Waefeso ‘wasiendelee kutembea sawa na vile mataifa pia yanatembea katika [mambo] yasiyo na faida ya akili zao, huku wakiwa wametiwa akili zao giza, na kutengwa na uhai ulio wa Mungu, kwa sababu ya ujinga wa kutojua ulio ndani yao, kwa sababu ya kutoweza kuhisi kwa mioyo yao.”—Waefeso 4:17, 18, NW.
6 Kupitia kazi ya kuhubiri Ufalme, leo watu wanahimizwa waache kutembea katika njia yao ya kikawaida, katika ujinga wa kutojua makusudi ya Mungu, katika giza la kiakili, wakisukumwa na mioyo isiyoweza kuhisi, ambayo inatafuta miradi isiyoweza kuleta faida. Wao wanatiwa moyo wajipatanishe na kile kielelezo kikamilifu cha Kristo, ‘wakitembea katika muungano pamoja naye,’ hivyo ‘wakileta kila fikira ndani ya utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.’ (Wakolosai 2:6, 7; 2 Wakorintho 10:5, NW) Watu wenye nia ya kutimiza hili takwa gumu wanatiwa uthabiti katika imani yao. Wanapozoea kutembea kwa kufuata njia aliyoitembea Kristo, inaendelea-endelea kuwa rahisi zaidi kwao.
7. Ni uhakikisho gani ambao sisi tunao kwamba, ingawa mara nyingi ni takwa gumu, inawezekana kufuata katika hatua za nyayo za Yesu?
7 Hata hivyo, mara nyingi hilo ni takwa gumu. Utofautiano ulio kati ya kiumbe aliyekamilika na asiyekamilika ni mkubwa. Kwa hiyo ni lazima viumbe wasiokamilika wafanye mabadiliko makubwa ili wajaribu kufuata kielelezo kikamilifu. Watu fulani wanatatizwa zaidi ya wengine kujipatanisha na njia ya maisha ya Kikristo, labda kwa sababu ya urithi au mazingira. Lakini Yehova anatuhakikishia kwamba mtu ye yote aliye kweli kweli na nia ya kujikaza anaweza kufanikiwa. “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” akasema mtume Paulo. (Wafilipi 4:13; ona pia 2 Wakorintho 4:7; 12:9.) Hiyo ni kweli pia kwa Wakristo wote.
Fanya Uangalifu
8, 9. (a) Kwa sababu gani fikira zisizogawanyika na mkazio mwingi wa fikira unahitajiwa kabisa wakati wa kufuata katika hatua za nyayo za mtu fulani? (b) Ni kufuata shauri gani la Kibiblia kutatusaidia tusitange-tange tutoke kwenye hatua za nyayo za Yesu?
8 Sisi hatuwezi kufuata hatua za nyayo halisi bila kuangalia kwa ukaribu ni wapi tunapokanyaga. Macho yetu yakitanga-tanga—yakikazwa juu ya mambo yanayoendelea kutuzunguka au juu ya vitu vingine—pasipo shaka sisi tutakanyaga kando tu punde si punde. Sisi tusipofanya uangalifu usiogawanyika na kukaza fikira kwa wingi sana, tutakengeuka kutoka hatua za nyayo tunazopaswa kuwa tukifuata. Hivyo, sikuzote kuna uhitaji wa kuwa macho, hasa wakati ambapo makelele ya ghafula au viondosha-fikira visivyotazamiwa huenda vikaondoa akili zetu kwenye jukumu tulilo nalo.—Linganisha Ayubu 18:10, 11.
9 Kwa njia ya kitamathali, hiyo ni kweli pia juu ya wale ambao wanafuata katika hatua za nyayo za Yesu. Yesu alionya wafuasi wake wafanye uangalifu wa ukaribu kwao wenyewe, mioyo yao isije “ikalemewa na kula kupita kiasi na kunywa kupita kiasi na masumbufu ya maisha.” (Luka 21:34, NW) Shetani anatumia viondosha-fikira hivi vya kila siku kusababisha sisi tuondoe macho yetu kwenye hatua za nyayo za Yesu. Yeye ana haraka ya kutushika bila kuwa macho, kwa kutumia kwa faida yake hali zisizotazamiwa, kama vile upinzani, ugonjwa, au vipingamizi vya kipesa. Ili kuhakikisha ‘hatupati kamwe kupeperukia mbali,’ ni lazima sisi ‘tufanye uangalifu ulio zaidi wa ule wa kawaida kwenye mambo yaliyosikiwa,’ ndiyo kusema, tuendelee kukaza macho yetu kwa ukaribu zaidi juu ya hatua za nyayo za Kristo kuliko wakati mwinginewo wote.—Waebrania 2:1; ona pia 1 Yohana 2:15-17, NW.
Usiache Njia
10. (a) Ni hatari gani inayokuwako wakati mifuatano ya alama za nyayo tofauti-tofauti inapopitana-pitana? (b) Katika maana ya kiroho, kwa sababu gani matokeo ya kufuata hatua za nyayo zisizofaa ni jambo zito?
10 Katika ufuo wa bahari uliosongamana watu, huenda kukawa na mifuatano kadhaa ya alama za nyayo katika ule mchanga wenye maji-maji, na alama za nyayo fulani huenda zikapitana-pitana na zile ambazo sisi tunafuata. Mifuatano mingi ya alama za nyayo huenda ikaonekana inafanana, angalau kwa kutazamwa kijuu-juu. Ni jambo muhimu kama nini kuhakikisha kwamba sisi tunafuata ile iliyo sahihi! Ama sivyo huenda tukadanganyika kwenda upande usiofaa. Katika maana ya kiroho, jambo hilo lingeweza kuwa na matokeo mazito. Hatari ya kufuata hatua za nyayo ambazo huenda zikaonekana kuwa sawa na kumbe si sawa inaonyeshwa katika mithali inayoonya hivi: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; lakini mwisho wake ni njia za mauti.”—Mithali 16:25.
11. Ni onyo gani ambalo Paulo aliwapa Wakristo wa kwanza, hiyo ikiwekea nani leo kielelezo?
11 Kwa sababu ya hatari hiyo iliyo halisi sana, Paulo alihisi akishurutika kuonya ndugu zake katika lile kundi la Kikristo la mapema hivi: “Mimi nastaajabu kwamba ninyi mnaondolewa kwa haraka sana kutoka kwa Yule ambaye aliita ninyi kwa fadhili zisizostahiliwa za Kristo mje kwa namna nyingine ya habari njema. . . . Kuna watu fulani ambao wanawasababishia ninyi matata na kutaka kupotosha zile habari njema juu ya Kristo. . . .Awaye yote ambaye anawatangazia ninyi kuwa habari njema jambo fulani linalozidi lile ambalo ninyi mlikubaliana nalo, acheni huyo awe mlaaniwa.” (Wagalatia 1:6-9, NW) Kwa kupatana na kielelezo cha Paulo, leo Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linatuonya juu ya waasi-imani na ndugu wa bandia ambao inaweza kusemwa, wanalaza chini alama za nyayo zilizo za kudanganya. Wakristo wa kweli hawataki kuacha kijia ambacho Kristo ameweka mbele yao kwa mwelekezo wa Mungu.—Zaburi 44:18, NW.
12. (a) Ni jinsi gani 2 Timotheo 1:13 inavyoweza kutusaidia tuepuke kuongozwa vibaya tufuate hatua za nyayo zilizo za kudanganya? (b) Ni mambo gani yanayoonyesha jinsi zilivyo namna nyinginezo za habari njema?
12 Kwa kufanya uangalifu wa ukaribu kwenye alama zinazotambulisha hatua za nyayo za Kristo, sisi tunaepuka kuongozwa vibaya. Maarifa sahihi juu ya Yesu, juu ya mafundisho yake na juu ya njia ambayo kundi la Kikristo linaendesha mambo yanatusaidia tutambue “kigezo cha maneno yenye afya” ambacho kinatuhami kutokana na wale ‘wanaopotosha zile habari njema juu ya Kristo.’ (2 Timotheo 1:13, NW) Namna nyinginezo za zinazoitwa habari njema eti—ambazo kwa kweli ni alama za nyayo zilizo za kudanganya—zinashindwa kuingia vizuri katika kigezo hicho cha ukweli. Zinakipotosha, zikifanya sura ya kigezo hicho ionekane kombokombo. Badala ya kuelewesha wazi kweli na kanuni za Biblia zilizo za msingi, zinazipinganisha. Badala ya kututia moyo tusonge kwenye utendaji mkubwa zaidi katika utumishi wa Yehova, zinatoa hoja za kupendelea upunguzaji mwendo. Ujumbe wazo si wa mwelekeo chanya, nao hautukuzi jina na tengenezo la Yehova; ni wa mwelekeo hasi, ni wa kutafuta-tafuta kasoro, na kuchambua-chambua. Kwa uhakika kabisa, hizo sizo hatua za nyayo tunazotaka kufuata.
Endeleza Mwendo Unaofaa
13. Mwendo unahusika jinsi gani wakati sisi tunapofuata katika hatua za nyayo za mtu mwingine?
13 Sisi tunapotembea, kwa sehemu fulani urefu wa mpigo wa hatua zetu unaamuliwa na wepesi wa kutembea kwetu. Kwa ujumla, kadiri tunavyozidi kutembea kasi ndivyo mpigo wa hatua zetu unavyozidi kurefuka; kadiri tunavyozidi kutembea pole, ndivyo unavyozidi kufupika. Hivyo, itakuwa rahisi zaidi kwetu kufuata katika hatua za nyayo halisi za mtu mwingine tukirekebisha mwendo wetu uafikiane na wake. Hali kadhalika, ili tutembee kwa mafanikio katika hatua za nyayo za kitamathali za Kiongozi wetu, Yesu Kristo, ni lazima sisi tudumishe mwendo wake.
14. (a) Ni katika njia gani mbalimbali huenda sisi tusiendeleze mwendo mmoja na Yesu? (b) Kwa sababu gani ni jambo la upumbavu kujaribu kwenda kasi kuliko “mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu”?
14 Kutoendeleza mwendo mmoja na Kristo kungemaanisha moja la mambo mawili. Ama sisi tunajaribu kwenda kasi zaidi, tukikimbia mbele ya “mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu” ambaye Yesu anatumia kutimiza kusudi la Yehova, ama tunajikokota kwa kubaki nyuma katika kufuata mwelekezo wa “mtumwa” huyo. (Mathayo 24:45-47, NW) Kama kielelezo cha lile jambo la kwanza, nyakati zilizopita Wakristo fulani wamekosa saburi juu ya mabadiliko au mitakatisho ya kimafundisho au kitengenezo ambayo wao walihisi ilihitajiwa kabisa na ilikuwa imekawia sana. Kwa kutotosheka kwa sababu walihisi mambo hayakuwa yakisonga mbele haraka vya kutosha, wao walijiondoa kati ya watu wa Yehova. Ni upumbavu na ni kukosa kama nini kufikiria mambo ya mbele! Mara nyingi jambo lile lile lililowaudhi lilibadilishwa baadaye—katika wakati wa Yehova.—Mithali 19:2; Mhubiri 7:8, 9.
15. Ni jinsi gani Mfalme Daudi na Yesu walikuwa vielelezo vyema vya kudumisha mwendo unaofaa?
15 Mwendo wa hekima ni kungojea Yehova afanye kitendo badala ya kujaribu kuamrisha mwendo ambao mambo yanapasa kutukia. Mfalme Daudi wa kale aliweka kielelezo kinachofaa. Yeye alikataa kupanga hila dhidi ya Mfalme Sauli katika jaribio la kudai umaliki kabla haujafika wakati wa Yehova kumpa. (1 Samweli 24:1-15) Hali kadhalika, “Mwana wa Daudi,” Yesu, aling’amua kwamba angelazimika kungoja ndio aingie kwa ukamili katika umaliki wake wa kimbingu. Yeye alijua lile tamko la kiunabii lililomhusu: “Keti kwenye mkono wa kuume wangu mpaka mimi niweke adui zako kama kibago kwa ajili ya nyayo zako.” Kwa hiyo wakati kikundi cha Wayahudi kilipotaka ‘kumbamba na kumfanya mfalme,’ Yesu alijiondoa kwa haraka. (Mathayo 21:9; Zaburi 110:1; Yohana 6:15, NW) Yapata miaka 30 baadaye, kulingana na Waebrania 10:12, 13, Yesu alikuwa bado akingojea umaliki wake. Kwa kweli, yeye alingoja kwa karne kama 19 kabla ya kusimamishwa akiwa Mfalme mwenye kuufaa Ufalme wa Mungu, wakati uliposimamishwa thabiti katika 1914.
16. (a) Toa kielezi juu ya jinsi huenda sisi tukasonga mbele polepole zaidi ya inavyotupasa. (b) Ni nini kusudi la saburi ya Yehova, na ni jinsi gani inatupasa sisi tuepuke kutumia vibaya saburi hiyo?
16 Hata hivyo, kushindwa kuendeleza mwendo unaofaa kungeweza pia kumaanisha kupunguza mwendo, kujikokota kwa kubaki nyuma. Hivyo, wakati Neno la Mungu linapoonyesha kwamba ni lazima mabadiliko yafanywe katika maisha zetu, je! sisi tunatenda bila kukawia? Au sisi tunatoa ubishi kwamba kwa kuwa Mungu ni mwenye saburi, tunaweza kuahirisha kufanya mabadiliko hayo mpaka wakati wa baadaye, tukitumainia kwamba huenda ikawa rahisi zaidi wakati huo? Ni kweli, Yehova ni mwenye saburi. Lakini hayuko hivyo ili sisi tuwe wazembe kwa kutofanya marekebisho yanayohitajiwa. Bali, “ana saburi na ninyi kwa sababu yeye hatamani watu wo wote waharibiwe bali atamani wote wafike kwenye toba.” (2 Petro 3:9, 15, NW) Ni afadhali kama nini, basi, kuiga mtunga zaburi aliyesema: “Mimi nilifanya haraka, nami sikukawia kushika amri zako.”—Zaburi 119:60, NW.
17. Kuendeleza mwendo unaofaa kunahusiana jinsi gani na kuhubiri Ufalme, hiyo ikituongoza tujiulize wenyewe swali gani?
17 Kujikokota kwa kubaki nyuma kungeweza kuhusisha ndani pia kuhubiri Ufalme. Kulingana na Mathayo 25, sasa Yesu anahukumu aina ya binadamu, akitenga “kondoo” kutoka kwenye “mbuzi.” Sana-sana jambo hili linatimizwa kupitia kuhubiriwa kwa “habari njema hizi za ufalme.” (Mathayo 24:14; 25:31-33; Ufunuo 14:6, 7, NW) Wakati uliogawiwa utimizaji wa kazi hii ya kutenganisha ni wenye mipaka. (Mathayo 24:34) Kadiri wakati unaopatikana ukaribiavyo kikomo, sisi tunaweza kutazamia Yesu aiharakishe kazi. Katika kufanya hivyo, yeye anatenda akiwa chombo cha Mungu, ambaye, akinena juu ya ile kazi ya kukusanya ndani, anaahidi hivi: “Mimi mwenyewe, Yehova, nitaiharakisha katika wakati wayo yenyewe.” (Isaya 60:22, NW) Sisi tulio wafanyakazi wenzi wa Mungu wenye kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Mwana wake, je! tunaharakisha mwendo wa kuhubiri kwetu Ufalme kufikie kadiri ambayo hali yetu ya kimwili na madaraka ya Kimaandiko yana ruhusu? Ripoti za utumishi wa shambani zinaonyesha kwamba mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo!
Epuka Uhakika wa Kupita Kiasi, Pambana na Mvunjiko wa Moyo
18. Kwa sababu gani huenda mtu akawa mwenye uhakika wa kupita kiasi, na ni jinsi gani Biblia inaonya juu ya hatari hii?
18 Kadiri tunavyovumilia kwa muda mrefu zaidi kufuata katika hatua za nyayo za mtu mwingine, ndivyo tutakavyozidi kuzoelea njia yake ya kutembea. Ingawa hivyo, tukiwa na ukinaifu, punde si punde tutakanyaga pasipofaa. Hivyo, wakati tunapofuata katika hatua za nyayo za Yesu za kitamathali, lazima tutambue ile hatari ya kuwa na uhakika wa kupita kiasi, kutegemea kizembe imara yetu wenyewe na majaliwa yetu, kuhisi kwamba sisi tumekwisha kumudu njia yake kamilifu ya kutembelea. Jambo lililopata Petro, lililoandikwa kwenye Luka 22:54-62, linatumikia kuwa onyo la wakati unaofaa. Pia linakazia ukweli wa 1 Wakorintho 10:12, ambayo inasema: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”
19. (a) Ni jambo gani linalopata kila Mkristo mara kwa mara? (Yakobo 3:2) (b) Inatupasa sisi tuone maneno ya Paulo kwenye Warumi 7:19, 24 jinsi gani?
19 Kwa sababu ya kutokamilika, kila Mkristo atapiga hatua ya kukanyaga pasipofaa mara kwa mara. Huenda huo mtoko wa njiani ukawa mdogo, usioonwa sana na wengine. Au huenda ukawa ni mkoseo wa kulenga shabaha ulio wazi, hivi kwamba utaonwa na wote. Vyo vyote iwavyo, inafariji kama nini kukumbuka ukiri huu wa haki wa Paulo: “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Ole wangu, maskini mimi!” (Warumi 7:19, 24) Bila shaka, maneno haya si ya kuonwa kuwa udhuru wa kutenda yasiyofaa. Bali, hayo ni kitia-moyo kwa Wakristo waliojitoa ambao wanamenyana na makosa ya kutokamilika, yakiwasaidia wawe na udumifu katika jitihada yao ya kutimiza lile takwa gumu la kutembea katika hatua za nyayo za Yesu zilizo kamilifu.
20. (a) Mithali 24:16 inatusaidia jinsi gani katika mbio yetu ya kutafuta uhai? (b) Inatupasa sisi tupige moyo konde kufanya nini?
20 “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, na yeye kwa uhakika atainuka,” inasema Mithali 24:16, NW. Katika mbio yetu ya kutafuta uhai, hakuna mmoja anayepaswa kuhisi akikazika kujiuzulu. Mbio hii ni kama mbio ya marathoni, mbio ya uvumilivu, si kama ule mfyatuko mfupi wa meta mia moja. Inaelekea sana kwamba mfyatukaji atashindwa mbio hiyo akikanyaga hatua moja tu mahali pasipofaa. Lakini mkimbiaji wa marathoni, hata kama anajikwaa, ana wakati wa kupata nafuu na kumaliza mwendo. Kwa hiyo wakati hatua fulani ya kibinafsi ya kukanyaga mahali pasipofaa inapokufanya wewe upaaze sauti ya kulia, “Ole wangu, maskini mimi!” kumbuka kwamba bado una wakati wa kupata nafuu. Bado wewe una fursa ya kurudisha hatua iwe pamoja na Kiongozi wako, Yesu Kristo. Hakuna sababu ya kutamauka! Hakuna sababu ya kuchoka na kuacha! Piga moyo konde ili, kwa msaada wa kimungu, utimize kwa mafanikio lile takwa gumu la ‘kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Yesu.’—1 Petro 2:21, NW.
-
-
Jamii ya Watu Wanaotembea Katika Hatua za Nyayo za YesuMnara wa Mlinzi—1988 | Mei 1
-
-
Jamii ya Watu Wanaotembea Katika Hatua za Nyayo za Yesu
“Sisi tulitembea katika roho ile ile, sivyo? Katika hatua za nyayo zile zile, sivyo?”—2 WAKORINTHO 12:18, NW.
1. Kwa sababu gani mara nyingi si vigumu kutambua mmoja wa Mashahidi wa Yehova?
“WAKIWA kikundi, wao ni waungwana, wenye kujali madaraka yao, na wanafanya vizuri shuleni. Hiyo haiwezi kusemwa juu ya vikundi vingine.” Ndivyo alivyosema mkuu wa shule moja ya msingi katika United States. Yeye alikuwa akinena juu ya nani? Watoto wa Mashahidi wa Yehova waliokuwa wanafunzi katika shule yake. Kweli kweli, watu wengi wameona kwamba Mashahidi wa Yehova, kutia ndani watoto wao, wanalandana mara nyingi katika njia fulani. Muda wa miaka iliyopita imezidi kuonekana wazi kwamba wao wana umoja wa ajabu kwa habari ya itikadi na mwenendo. Kwa hiyo si vigumu kuwatambua Mashahidi.
2. Ni nini iliyokuwa sifa yenye kuonyesha jinsi lilivyokuwa kundi la Kikristo la mapema, na Paulo alisema nini juu ya hilo?
2 Umoja wa Mashahidi wa Yehova ni jambo lisilo la kawaida katika ulimwengu huu usio na umoja. Lakini si vigumu kuelewa jambo hilo tukikumbuka kwamba wote wanajitahidi kutembea katika hatua za nyayo za Yesu. (1 Petro 2:21) Umoja huo ulionyesha pia hali ya Wakristo wa karne ya kwanza. Katika pindi moja, Paulo alilionya kwa upole hivi kundi lililokuwa Korintho: “Sasa mimi natia moyo ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana yetu Yesu Kristo kwamba imepasa ninyi nyote kusema kwa mwafaka, na kwamba imepasa kusiwe migawanyiko miongoni mwenu ninyi, bali kwamba ninyi mpate kuunganika kwa kufaa katika akili moja na katika mstari mmoja wa fikira.” (1 Wakorintho 1:10, NW) Pia Paulo alitoa mashauri yenye kuvuviwa na Mungu juu ya jinsi ya kushughulika na watu wasio na nia ya kudumisha umoja wa Kikristo.—Ona Warumi 16:17; 2 Wathesalonike 3:6, NW.
3, 4. Paulo alieleza jinsi gani juu ya umoja uliokuwa: kati yake mwenyewe na Tito, na ni nini uliokuwa msingi wa umoja huu?
3 Wapata mwaka 55 W.K., Paulo alituma Tito Korintho akasaidie katika kufanya changizo fulani kwa ajili ya ndugu wenye uhitaji katika Yudea, na inawezekana akaone jinsi kundi lilivyokuwa likitenda kwa kujibiza shauri la Paulo. Baadaye alipokuwa akiwaandikia Wakorintho, Paulo alirejeza kwenye ziara ya Tito ya hivi majuzi na akauliza: “Tito hakuwatumia nini hata kidogo kwa faida yake, sivyo? Sisi tulitembea katika roho ile ile, sivyo? Katika hatua za nyayo zile zile, sivyo?” (2 Wakorintho 12:18, NW) Paulo alimaanisha nini kwa kusema walitembea “katika roho ile ile” na “katika hatua za nyayo zile zile”?
4 Yeye alikuwa akieleza umoja uliokuwa kati yake na Tito. Tito alikuwa mwandamani wa Paulo mwenye kusafiri naye pindi kwa pindi, na bila shaka yeye alijifunza mengi kutokana na Paulo kwa njia hiyo. Lakini umoja uliokuwa kati ya wao wawili ulitegemea msingi wa kitu fulani chenye imara zaidi. Ulitegemea msingi wa uhusiano wao mzuri sana pamoja na Yehova na juu ya uhakika wa kwamba wote wawili walikuwa wafuasi wa hatua za nyayo za Kristo. Tito aliiga Paulo kama vile Paulo alivyoiga Kristo. (Luka 6:40; 1 Wakorintho 11:1, NW) Kwa hiyo wao walikuwa wakitembea katika roho ya Yesu na katika hatua za nyayo zake.
5. Ni jambo gani linaloweza kutazamiwa juu ya watu ambao leo wanaiga Paulo na Tito wanapotembea “katika roho ile ile” na “katika hatua za nyayo zile zile”?
5 Basi, si ajabu kwamba Wakristo wa karne hii ya 20, wanaotembea “katika roho ile ile” na “katika hatua za nyayo zile zile” kama Paul na Tito, wanashangilia umoja usio na ulinganifu. Kwa uhakika, ukosefu wa umoja wa Wakristo wa jina tu unawaonyesha wazi kuwa ni Wakristo wa kudanganya, wasiotembea katika hatua za nyayo za Kiongozi ambaye wao wanadai kumfuata. (Luka 11:17) Hiyo tofauti kubwa sana kati ya Wakristo wa kweli na wale wa jina tu inaweza kufanyiwa kielezi katika njia mbalimbali. Acheni tutaje nne.
Utakatifu wa Damu
6, 7. (a) Ni maoni gani sahihi juu ya damu yanayohusika katika kutembea katika hatua za nyayo za Yesu? (b) Ni nini tofauti kati ya Mashahidi wa Yehova na wengine leo ambao wanakataa kutiwa damu mishipani?
6 Wapata mwaka 49 W.K., baraza lenye kuongoza la kundi la karne ya kwanza lilipeleka barua iliyojibu swali hili: Je! Wakristo wasio Wayahudi wanapaswa kutii ile Sheria ya Musa? Barua hiyo ilisema hivi: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu ninyi, isipokuwa mambo haya yanayohitajiwa kabisa, kuendelea kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vinavyonyongwa na wa uasherati.” (Matendo 15:28, 29, NW) Angalia kwamba kushika mwiko wa damu kulikuwa miongoni mwa ‘mambo yanayohitajiwa kabisa.’ Kutembea katika hatua za nyayo za Yesu kungemaanisha kutoingiza damu katika mwili, ama kupitia mdomoni ama katika njia nyingineyo yote.
7 Kanuni hii imevunjwa kwa kutojali kabisa katika Jumuiya ya Wakristo na lile zoea la kutia damu mishipani. Ni kweli, katika miaka ya majuzi watu kadhaa mmoja mmoja wamepata kujua hatari za kiafya za kutiwa damu mishipani na wamekataa kutiwa damu kwa sababu za kitiba. Hususa hiyo ni kweli kwa kuwa wengi wamejipatia UKIMWI kutokana na dawa waliyotiwa. Lakini ni nani wanaotegemeza utakatifu wa damu kwa sababu ya kuheshimu sheria ya Mungu, wakifanya hivyo wakiwa kikundi? Wakati mgonjwa anapokataa kutiwa damu mishipani, moja kwa moja daktari anafikiri yeye ni nani? Je! kwa kawaida daktari hasemi hivi: ‘Bila shaka wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova’?
8. Shahidi mmoja katika Italia alibarikiwa jinsi gani kwa kupiga moyo konde ashike sheria ya Mungu katika jambo hili?
8 Antonietta anaishi Italia. Yapata miaka minane iliyopita, mwanamke huyu alikuwa mgonjwa sana, na kipimo cha damu yake kilikuwa chini sana hata madaktari wakasisitiza kwamba alihitaji kutiwa-tiwa damu ili kuokoa uhai wake. Yeye alikataa na akapingwa na madaktari hata watu wa ukoo. Hata vivulana wake wawili walimwomba hivi kwa kujitetea: “Mama, ikiwa wewe unatupenda kweli kweli, kubali damu.” Lakini Antonietta alipiga moyo konde kubaki mwaminifu, na jambo la kufurahisha ni kwamba yeye hakufa. Bado, hali yake ilikuwa mahututi mpaka daktari akasema: “Sisi hatuwezi kueleza ni kwa nini yeye angali hai.” Lakini mara tu namna ya matibabu yasiyokatalika yalipoanza, yeye alifanya maendeleo ya haraka sana mpaka daktari mwingine akasema: “Ni ajabu sana—wewe usingaliweza kupata nafuu kwa muda mfupi hivyo, hata kama sisi tungalikuwa tumekushindilia damu mchana kutwa.” Sasa, yeye ni painia wa kawaida, na wanaye wawili, ambao sasa wana miaka 12 na 14, wanafanya maendeleo mazuri sana katika ukweli. Antonietta alishika kwa ushujaa lile ‘jambo linalohitajiwa kabisa,’ utakatifu wa damu. Mashahidi wa Yehova wote wanashikilia maoni hayo hayo wanapotembea katika hatua za nyayo za Yesu.
Tabia Njema za Kiadili
9. Ni jambo gani jingine ‘linalohitajiwa kabisa’ ambalo linahusika ndani ya kufuata katika hatua za nyayo za Yesu, na ni jambo gani linalotukia kwa wale wanaoshindwa kulishika?
9 Jingine ambalo ni ‘jambo linalohitajiwa kabisa’ lililokaziwa katika ile barua iliyotoka kwa baraza lenye kuongoza la karne ya kwanza lilikuwa ‘kuendelea kushika mwiko wa uasherati.’ Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo alipanua jambo hilo, akisema: “Wala waasherati, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaotunzwa kwa makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume . . . hawatarithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10, NW) Wakristo wanasaidia watu ambao wanataka kutumikia Yehova wajiondolee mbali mazoea haya yasiyo safi. Hata washiriki wa kundi wanaotegwa nayo wanasaidiwa wajitakatishe wenyewe ikiwa wanageuka na kutubu. (Yakobo 5:13-15) Lakini Mkristo ye yote akianguka ndani ya mazoea hayo machafu na kukataa kutubu, kawaida moja ya Biblia yenye kutaja mambo moja kwa moja inatumika. Paulo alivuviwa na Mungu kusema: “Acheni kuchangamana katika uandamani pamoja na mtu ye yote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati. . . . Ondoeni yule mtu mwovu kutoka miongoni mwenu wenyewe.”—1 Wakorintho 5:11, 13, NW.
10, 11. (a) Ni nani ambao lazima wachukue lawama kwa viwango vya kiadili vilivyoshuka katika Jumuiya ya Wakristo, na kwa sababu gani? (b) Ni jinsi gani jambo lililoonwa na mwanamume mmoja katika Ufilipino linaonyesha kwamba, wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova wanadumisha viwango vya juu vya kiadili?
10 Lijapokuwako fundisho hili la wazi, Jumuiya ya Wakristo imetatanika katika ukosefu wa adili. Viongozi wa kidini wanaopunguza uzito wa viwango vya kimungu ni wa kulaumika kwa hali hii, kama wale wanaotaja-taja viwango vya Biblia kwa mdomo tu lakini wanashindwa kuvifikiliza kwa ushujaa katika makundi yao. Hata hivyo, katika jambo hili, pia, Mashahidi wa Yehova wakiwa jamii ya watu wanatembea katika hatua za nyayo za Yesu.
11 Fikiria Jose, kutoka Ufilipino. Akiwa na umri wa 17 alikuwa tayari mtokeza-matata na mcheza-kamari. Mara nyingi alilewa, alikuwa anaishi maisha ya ukosefu wa adili, na mara kwa mara alijikuta jela kwa sababu ya kuiba. Ndipo yeye alipokutana na Mashahidi wa Yehova. “Funzo la Biblia lilibadili kabisa maisha yangu,” yeye anasema. “Sasa mimi sinywi wala sivuti tena, nami nimejifunza kudhibiti tabia yangu ya moyoni. Sasa mimi nina dhamiri safi, nikiwa na mke mmoja tu. Pia nimepata staha ya jirani zangu, waliokuwa wakiniita ‘Jose, yule jamaa mwenye sifa mbaya’ na ‘Jose, lile jini.’ Sasa wao wananiita ‘Jose, yule Shahidi wa Yehova.’ Mwanangu na mpwa wangu wa kiume ni watumishi wa huduma katika kundi ambamo sasa mimi natumikia nikiwa mzee na painia wa kawaida.” Jose na mamilioni ya mashahidi wengine wa Kikristo wa Yehova wanatembea katika hatua za nyayo za Yesu wakiwa Wakristo safi kiadili.
Kutokuwamo
12. Ni mwelekeo gani wa Wakristo halisi ambao Yesu alikazia katika sala yake iliyoandikwa katika Yohana sura ya 17?
12 Katika ile sala ndefu ambayo Yesu alitoa jioni ya mwisho ya kuwa pamoja na wanafunzi wake, yeye alitaja njia nyingine ambayo wafuasi wake ‘wangetembea katika hatua za nyayo zake.’ Akinena juu ya wanafunzi wake, yeye alisema: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi nisivyo sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:16, NW) Hiyo inamaanisha kwamba Wakristo ni wasiokuwamo. Badala ya kuwa na sehemu katika siasa au mahitilafiano ya kitaifa, wao wanaambia wengine juu ya Ufalme wa Mungu, ule utatuzi mmoja tu kwa matatizo ya ulimwengu huu.—Mathayo 6:9, 10; Yohana 18:36.
13, 14. (a) Ni jinsi gani Jumuiya ya Wakristo inavyotofautiana na Mashahidi wa Yehova katika kutokuwamo? (b) Ni jinsi gani kudumisha kutokuwamo kwa kisiasa kwa upande wa Shahidi mmoja katika Japani kuliuletea manufaa udugu mzima?
13 Kanuni hii ya kutokuwamo imesahauliwa na walio wengi wa washiriki wa Jumuiya ya Wakristo, ambao kwa kawaida wanachukua asili zao za kitaifa kuwa za maana kuliko mahusiano yao ya kidini. Mike Royko, aliye mchangia safu za magazeti mbalimbali, anaonyesha kwamba “Wakristo” wamekuwa hawajapata kamwe ‘kujichunga sana wasifanye vita juu ya Wakristo wengine,” akiongezea hivi: “Kama wangalikuwa wamefanya hivyo, vilivyo vingi vya vita vyenye kuwaka sana moto katika Ulaya visingalitukia kamwe.” Kwamba Mashahidi wa Yehova wanadumu wakifuatilia sana kutokuwamo kwa Kikristo nyakati za vita ni uhakika unaojulikana vizuri. Lakini wakiwa ni wafuasi wa hatua za nyayo za Yesu, wao ni wasiokuwamo pia kuhusiana na masuala ya kijamii na kisiasa. Hivyo, hakuna jambo lo lote linalosumbua umoja wao wa ulimwenguni pote ulio wa kustaajabisha sana.—1 Petro 2:17.
14 Nyakati fulani kutokuwamo kwao kunaleta matokeo yasiyotazamiwa. Mathalani, katika wilaya ya Tsugaru ya kaskazini mwa Japani, uchaguzi unachukuliwa kwa uzito sana. Lakini Toshio, msaidizi wa meneja katika Idara ya Pesa ya afisi ya kwao ya kiserikali, alikataa kwa sababu za dhamiri kujihusisha katika kampeni ya kuchagua meya upya. Hiyo ilitokeza kushushwa cheo awe katika Idara ya Uondoaji Kinyesi. Hata hivyo, mwaka mmoja baadaye meya alikamatwa na kulazimishwa kujiuzulu kwa sababu ya mazoea ya ufisadi. Meya mpya alichaguliwa. Aliposikia juu ya kushushwa cheo kwa Toshio, yeye alimrudisha kwenye cheo cha juu cha usimamizi, na hiyo ikawaletea mibaraka ndugu Wakristo wa Toshio. Jinsi gani? Toshio anaeleza kwamba ni vigumu sana kupata ruhusa ya kutumia majumba ya mazoezi ya mwili kwa ajili ya vikusanyiko visivyo vya uanariadha. Lakini akiwa katika cheo chake cha sasa, “Yehova ameweza kunitumia mimi”—tukinukuu maneno ya Toshio mwenyewe—“kupata utumizi wa hayo majumba ya mazoezi ya mwili kwa ajili ya mikusanyiko ya wilaya mitatu na makusanyiko ya mizunguko manne.” Yeye anakata shauri hivi: “Mradi sisi tunabaki tukiwa waaminifu, Yehova atafungua njia zisizowazika za kututumia.”
Katika Maskani Zetu
15. Ni jinsi gani Yesu aliwaachia kigezo wafuasi wa hatua za nyayo zake kwa habari ya mahusiano ya kijamaa?
15 Sehemu nyingi ambamo Wakristo ‘wanafuata katika hatua za nyayo za Yesu’ ni katika maskani zao. Biblia inakisimamisha thabiti kielelezo cha Yesu kuwa ndicho kigezo cha kufuata kwa ajili ya mahusiano ya kinyumbani wakati inaposema: “Mwe wenye kujitiisha kwa mtu na mwenzake katika hofu ya Kristo. Acheni wake wawe wenye kujitiisha kwa waume wao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kundi . . . Kwa uhakika, kama vile kundi lilivyo katika hali ya kujitiisha kwa Kristo, acheni wake wawe hivyo kwa waume wao katika kila jambo. Waume, endeleeni kupenda wake zenu, sawa na vile Kristo pia alivyopenda kundi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yalo.”—Waefeso 5:21-25, NW.
16, 17. (a) Ni hali gani mbaya iliyo katika Jumuiya ya Wakristo kuhusu mahusiano ya kinyumbani? (b) Ni jinsi gani tu mahusiano ya kinyumbani yanaweza kufanyiwa maendeleo, kama inavyoonyeshwa na jambo lililoonwa na mume na mke waliofunga ndoa katika Brazili?
16 Leo Jumuiya ya Wakristo inapuuza shauri hili kwa sehemu kubwa na hivyo imejawa na jamaa zilizovunjika-vunjika kabisa. Jamaa zilizovunjika ni jambo la kawaida, na mara nyingi mahitilafiano kati ya mzazi na mtoto yanakuwa yenye kina kirefu sana. “Jamaa inabomoka-bomoka,” alionelea profesa mmoja wa saikolojia miaka kadhaa iliyopita. Wanasaikolojia wa watoto, washauri wa ndoa, na madaktari wa akili wanafanikiwa kidogo tu katika kudumisha upamoja wa jamaa zilizohatarika. Lakini Mashahidi wa Yehova wanajaribu sana kutumia kanuni za Biblia na wanajulikana sana kwa kuwa na mahusiano ya kijamaa yanayozidi wastani ule wa kawaida.
17 Mathalani, Aldemar alikuwa luteni katika polisi wa kijeshi katika Brazili na alikuwa na matatizo ya kijamaa. Mke wake alimwacha na kutafuta mtengano halali. Mwanamume huyo alianza kunywa kupindukia, na hata akajaribu kujiua. Baadaye, watu wa ukoo wake, ambao ni Mashahidi wa Yehova, walinena naye juu ya Biblia. Yeye alipenda mambo aliyosikia na kuanza kujifunza. Kwa kutaka kupatanisha maisha yake na msimamo wa kutokuwamo ambao unafanya Mashahidi wa Yehova wajulikane, yeye aliomba kufutwa kazi jeshini. Aldemar na mke wake walitatua tofauti zao za ndoa kwa kutumia kanuni za Biblia ambazo Aldemar alikuwa anajifunza. Leo, wao wanafuata pamoja katika hatua za nyayo za Yesu, wakitumikia Yehova pamoja wakiwa mapainia wa kawaida.
Wenye Utii kwa Sababu ya Upendo
18. (a) Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanabarikiwa kiroho leo? (b) Ni jinsi gani Isaya 2:2-4 inavyoendelea kutimizwa sasa?
18 Kuna ithibati ya kwamba Mashahidi wa Yehova wanatembea kwa umoja katika roho na katika hatua za nyayo za Kristo Yesu. Wakiwa watu mmoja mmoja na wakiwa kikundi, wao wanabarikiwa kiroho kwa kufanya hivyo. (Zaburi 133:1-3) Ithibati zilizo wazi za baraka ya kimungu juu yao zimesukuma umati wa watu wenye mioyo ya kufuata haki watende kupatana na unabii ulio kwenye Isaya 2:2-4. Katika miaka mitano tu iliyopita, watu 987,828 wamechukua hatua zinazohitajiwa kabisa kwa ajili ya wakfu na ndipo wakajitokeza kwa ajili ya ubatizo katika maji. Kwa upendo, Yehova hakuweka kikomo kilichoamrishwa kabisa juu ya hesabu ya watu ambao wanaweza kufanya hivyo kabla ya “ile dhiki kubwa” kudhurubu!—Ufunuo 7:9, 14, NW.
19. (a) Ni manufaa gani zenye kuonekana wazi ambazo huenda zikatokana na kutumikia Yehova, nazo zinapasa kuonwa jinsi gani? (b) Ni nini sababu yetu ya msingi ya kutii amri za Yehova?
19 Kama vile maono yaliyo juu yanavyoonyesha, mara nyingi baraka za kiroho zinazoshangiliwa na watu wa Mungu zinaandamana na manufaa zenye kuonekana wazi. Mathalani, kwa kushika mwiko wa kuvuta tumbako, kwa kuishi maisha za adili, na kwa kuheshimu utakatifu wa damu, wao wanaweza kuepuka kuwa majeruhi wa magonjwa fulani. Au kwa sababu ya kuishi kupatana na ukweli, wao wanaweza kunufaika kwa njia ya kiuchumi, kijamii, au ya kinyumbani. Zo zote za manufaa hizo zenye kuonekana wazi zinaonwa kuwa baraka kutoka kwa Yehova, nao wanathibitisha kwamba sheria za Yehova zina mafaa. Lakini uwezekano wa kupata faida hizo zenye mafaa sio wenyewe hasa ulio sababu ya kutii sheria za Mungu. Wakristo wa kweli wanatii Yehova kwa sababu wanampenda, kwa sababu yeye anastahili ibada yao, na kwa sababu kufanya mapenzi yake ndilo jambo la pekee lilio sawa. (1 Yohana 5:2, 3; Ufunuo 4:11) Shetani ndiye anayeshindania kwamba watu wanatumikia Mungu kwa ajili ya manufaa za ubinafsi tu.—Ona Ayubu 1:9-11; 2:4, 5.
20. Mashahidi wa Yehova wa leo wanatembea jinsi gani katika roho ile ile kama wale mashahidi waaminifu watatu wa Kiebrania wa nyakati za kale?
20 Mashahidi wa Yehova wa kisasa wanatembea katika roho ile ile kama wale mashahidi waaminifu watatu wa Kiebrania wa siku ya Danieli. Walipotishwa kukupushwa ndani ya tanuri yenye kuwaka moto, hawa walisema: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo [ndiyo kusema, hata ikiwa yeye anaacha tufe], ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.” (Danieli 3:17, 18) Kuwe au kusiwe na manufaa au matokeo yenye kuonekana wazi mara hiyo, Mashahidi wa Yehova wataendelea kufuata kwa ukaribu katika hatua za nyayo za Yesu, wakijua kwamba uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu umeahidiwa! Wakiwa jamii ya watu wenye umoja wao wataendelea kutembea “katika roho ile ile” na “katika hatua za nyayo zile zile,” liwe lo lote liwalo!
-