-
Mtwikeni Yehova Hangaiko Lenu LoteMnara wa Mlinzi—1994 | Novemba 15
-
-
8, 9. Ni faraja gani iwezayo kupatikana kwenye 1 Petro 5:6-11?
8 Petro aliongezea: “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote [“hangaiko lenu lote,” NW], kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu. Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani. Na Mungu wa neema yote, aliyewaita kuingia katika utukufu wake wa milele katika Kristo, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu. Uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”—1 Petro 5:6-11.
-
-
Mtwikeni Yehova Hangaiko Lenu LoteMnara wa Mlinzi—1994 | Novemba 15
-
-
10. Petro wa Kwanza 5:6, 7 yarejezea sifa zipi tatu ziwezazo kuondoa hangaiko?
10 Petro wa Kwanza 5:6, 7 yarejezea sifa tatu zinazoweza kutusaidia kukabiliana na hangaiko. Moja ni unyenyekevu, au “hali ya akili ya kujishusha.” Mstari 6 wamalizia kwa maneno “kwa wakati wake,” jambo lidokezalo uhitaji wa saburi. Mstari 7 waonyesha kwamba twaweza kumtwika Mungu hangaiko letu lote tukiwa na uhakika ‘kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yetu,’ na maneno hayo yatia moyo kumtumaini Yehova kabisa. Kwa hiyo ebu tuone jinsi unyenyekevu, saburi, na kumtumaini Mungu kabisa kuwezavyo kusaidia kuondoa hangaiko.
Jinsi Unyenyekevu Uwezavyo Kusaidia
11. Unyenyekevu waweza kutusaidiaje kukabiliana na hangaiko?
11 Tukiwa wanyenyekevu, tutakiri kwamba fikira za Mungu zashinda zetu kwa mbali sana. (Isaya 55:8, 9) Unyenyekevu hutusaidia kutambua uwezo wetu mdogo wa kiakili kwa kulinganishwa na akili ya Yehova inayojua mambo yote. Yeye huona mambo ambayo sisi hatutambui, kama ionyeshwavyo na kisa cha mwanamume mwadilifu Ayubu. (Ayubu 1:7-12; 2:1-6) Kwa kujinyenyekeza “chini ya mkono wa Mungu ulio hodari,” tunakiri hali yetu ya chini kwa kulinganisha na Mwenye Enzi Kuu aliye Mkuu Zaidi. Hilo nalo latusaidia kukabiliana na hali anazoruhusu. Mioyo yetu yaweza kutamani kupata faraja ya mara hiyo, lakini kwa kuwa sifa za Yehova zimesawazika kikamilifu, yeye ajua barabara wakati na jinsi ya kutenda kwa niaba yetu. Basi, kama watoto wachanga na tushike kwa unyenyekevu mkono wa Yehova ulio hodari, tukiwa na hakika kwamba yeye atatusaidia kukabiliana na mahangaiko yetu.—Isaya 41:8-13.
12. Hangaiko juu ya usalama wa mali laweza kupatwa na nini tukitumia kwa unyenyekevu maneno ya Waebrania 13:5?
12 Unyenyekevu watia ndani kuwa tayari kutumia shauri litokanalo na Neno la Mungu, ambalo mara nyingi laweza kuondoa hangaiko. Kwa mfano, ikiwa hangaiko letu limetokana na kujiingiza mno katika kufuatia mambo ya kimwili, ingekuwa vizuri kufikiria shauri hili la Paulo: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa [Mungu] mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Waebrania 13:5) Kwa kutumia shauri hilo kwa unyenyekevu, wengi wameacha kuwa na hangaiko kubwa sana kuhusu usalama wa vitu vya kimwili. Ingawa hali yao ya kifedha huenda isiweze kuwa bora zaidi, hawafikirii sana jambo hilo kiasi cha kutokeza madhara ya kiroho.
Fungu la Saburi
13, 14. (a) Kwa habari ya uvumilivu wenye saburi, mwanamume Ayubu alituandalia kielelezo gani? (b) Kumngoja Yehova kwa saburi waweza kutufanyia nini?
13 Maneno “kwa wakati wake” yaliyo katika 1 Petro 5:6 yadokeza uhitaji wa uvumilivu wenye saburi. Nyakati nyingine tatizo hudumu kwa muda mrefu, na hilo laweza kuongeza hangaiko. Wakati huo hasa ndipo tunapohitaji kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira [“uvumilivu,” NW] yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.” (Yakobo 5:11) Ayubu alipatwa na uharibifu wa kiuchumi, akapoteza watoto kumi katika kifo, akaugua maradhi yenye kukirihisha, naye alishutumiwa kwa uongo na wafariji bandia. Angalau hangaiko la kadiri fulani lingekuwa sawa katika hali hizo.
14 Kwa vyovyote vile, Ayubu alikuwa mwenye kielelezo chema katika uvumilivu wenye saburi. Ikiwa twapitia mtihani mgumu sana wa imani, huenda tukalazimika kungojea kupata faraja, kama alivyofanya. Lakini Mungu alitenda kwa niaba yake, hatimaye akimwondolea Ayubu mateseko yake na kumthawabisha kwa wingi sana. (Ayubu 42:10-17) Kumngoja Yehova kwa saburi husitawisha uvumilivu wetu na kufunua kina cha ujitoaji wetu kwake.—Yakobo 1:2-4.
-