-
Yesu KristoUfahamu wa Kina wa Maandiko
-
-
Hekima yapewa utu. Yaliyoandikwa katika Maandiko kumhusu yule Neno yanafaana sana na maelezo yaliyotolewa kwenye Methali 8:22-31. Hapo hekima inapewa utu, ikiwakilishwa kana kwamba inaweza kusema na kutenda. (Met 8:1) Waandikaji wengi waliodai kuwa Wakristo wa karne za mapema za Wakati wa Kawaida walielewa kisehemu hiki kuwa kinarejezea kwa njia ya mfano Mwana wa Mungu katika hali yake kabla ya kuwa binadamu. Kwa kuangalia maandiko ambayo tayari yamefikiriwa, hakuna shaka kwamba Mwana huyo ‘alitokezwa’ na Yehova ‘akiwa mwanzo wa njia yake, akiwa wa mapema zaidi kati ya kazi zake za zamani za kale,’ na kwamba huyo Mwana alikuwa ‘kando ya Yehova akiwa stadi wa kazi’ wakati wa uumbaji wa dunia, kama inavyosimuliwa katika mistari hii ya Methali. Ni kweli kwamba katika Kiebrania, ambacho huambatisha jinsia kwenye nomino zake (kama zinavyofanya lugha nyingine nyingi), neno linalotafsiriwa kuwa “hekima” sikuzote linakuwa na jinsia ya kike. Ndivyo ilivyo katika kisa hiki hata ijapokuwa hekima imepewa utu na basi isingezuia hekima kutumiwa kitamathali kumwakilisha Mwana wa Mungu aliye mzaliwa wa kwanza. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “upendo” katika usemi “Mungu ni upendo” (1Yo 4:8) limo pia katika jinsia ya kike lakini hilo halimfanyi Mungu kuwa wa kike. Sulemani, mwandikaji mkuu wa Methali (Met 1:1), alikitumia cheo qo·he′leth (mkutanishaji) kujihusu yeye mwenyewe (Mhu 1:1) na neno hilo pia limo katika jinsia ya kike.
-
-
UpendoUfahamu wa Kina wa Maandiko
-
-
Mungu. Mtume Yohana aliandika: “Mungu ni upendo.” (1Yo 4:8) Yeye ndiye mfano bora zaidi wa kuonyesha upendo, ndio sifa yake kuu zaidi. Hata hivyo, haiwezi kusemwa kwamba ‘upendo (sifa isiyo na uhai) ni Mungu.’ Anajitambulisha katika Biblia kama Mtu na kwa njia ya mfano anasema kwamba ana “macho,” “mikono,” “moyo,” “nafsi,” na kadhalika. Pia ana sifa nyingine, kama vile haki, nguvu, na hekima. (Kum 32:4; Ayu 36:22; Ufu 7:12) Zaidi ya hayo, ana uwezo wa kuchukia, sifa iliyo kinyume kabisa na upendo. Kwa sababu anapenda uadilifu anachukia uovu. (Kum 12:31; Met 6:16) Upendo unahusisha hisia na kuonyesha shauku nyororo, hisia ambayo ni mtu tu anayeweza kuwa nayo, au kuonyeshwa mtu mwingine. Ni kweli kwamba Mwana wa Mungu Yesu Kristo si sifa tu isiyo na uhai; alisema kwamba alikuwa na Baba yake, alifanya kazi naye, alimpendeza, na alimsikiliza, pia alisema kwamba malaika wanaona uso wa Baba yake, mambo ambayo hayawezi kufanywa na sifa isiyo na uhai.—Mt 10:32; 18:10; Yoh 5:17; 6:46; 8:28, 29, 40; 17:5.
Uthibitisho wa upendo wake. Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba Yehova Muumba na Mungu wa ulimwengu wote ni upendo. Uthibitisho huo unaonekana katika uumbaji wenyewe. Dunia yote imeumbwa kwa makini sana ili mwanadamu awe na afya, furaha, na maisha mazuri. Mwanadamu hakuumbwa ili tu aishi bali afurahie chakula, rangi na uumbaji maridadi, wanyama, na vilevile, kushirikiana na wanadamu wenzake, na kufurahia mambo mengine mengi yanayoleta furaha maishani. (Zab 139:14, 17, 18) Lakini Yehova ameonyesha hata zaidi upendo wake kwa mwanadamu kwa kumuumba kwa mfano na sura yake (Mwa 1:26, 27), akiwa na uwezo wa kupenda na uhitaji wa kiroho, naye amejifunua kwa wanadamu kupitia Neno lake na roho yake takatifu.—1Ko 2:12, 13.
Upendo wa Yehova kwa wanadamu ni kama ule wa Baba kwa watoto wake. (Mt 5:45) Hawanyimi chochote kinachowafaa, hata ikiwa ni kwa hasara yake mwenyewe; upendo wake unapita hisia zozote tunazoweza kuhisi au kuonyesha. (Efe 2:4-7; Isa 55:8; Ro 11:33) Aliwaonyesha wanadamu upendo mkubwa zaidi kwa kuwafanyia jambo la upendo zaidi ambalo mzazi anaweza kufanya. Alifanya hivyo kwa kutoa uhai wa Mwana wake mwaminifu, mzaliwa pekee. (Yoh 3:16) Mtume Yohana aliandika hivi: “Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.” (1Yoh 4:19) Kwa hiyo, yeye ndiye Chanzo cha upendo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa maana ni vigumu kwa yeyote kufa kwa ajili ya mtu mwadilifu; hata hivyo labda mtu anaweza kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu mwema. Lakini Mungu hupendekeza upendo wake kwetu kwa kuwa tulipokuwa bado watenda dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.”—Ro 5:7, 8; 1Yo 4:10.
Upendo wa Mungu unaodumu milele. Upendo wa Yehova kwa watumishi wake waaminifu ni wa milele; haushindwi wala kufifia, hata watumishi wake wawe katika hali nzuri au mbaya, au hata wakipatwa na matatizo makubwa au madogo. Mtume Paulo alisema: “Kwa maana nimesadiki kwamba wala kifo wala uzima wala malaika wala serikali wala mambo yaliyopo sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala uumbaji mwingine wowote havitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Ro 8:38, 39.
Enzi kuu ya Mungu inaongozwa na upendo. Yehova hufurahia kwamba enzi ya yake kuu inaongozwa na upendo na viumbe wake wanaiunga mkono wakichochewa na upendo. Anawapenda wale tu wanaopenda enzi yake kuu kwa sababu ya sifa zake nzuri na kwa sababu ya uadilifu wa enzi yake, wale wanaochagua enzi yake badala ya utawala mwingine wowote. (1Ko 2:9) Wanachagua kutumikia chini ya enzi yake badala ya kujitegemea—kwa sababu wana ujuzi kumhusu yeye na upendo, haki, na hekima yake, na wanatambua anawazidi kwa mbali katika kuonyesha sifa hizo. (Zb 84:10, 11) Ibilisi hakujitiisha kwa enzi hiyo kuu, alitaka kujitegemea, Adamu na Hawa walifanya hivyo pia. Ibilisi hata alipinga njia ya Mungu ya kutawala, ni kana kwamba alisema Mungu hana upendo na si mwadilifu (Mwa 3:1-5), na kwamba viumbe wa Mungu hawamtumikii kwa kuchochewa na upendo, bali kwa sababu ya ubinafsi.—Ayu 1:8-12; 2:3-5.
Yehova Mungu alimruhusu Ibilisi aishi na awashawishi watumishi wake, kutia ndani Mwana wake mzaliwa pekee, hadi kufikia kifo. Mungu alitabiri kwamba Yesu Kristo angekuwa mwaminifu. (Isa 53) Kwa nini alikuwa na uhakika huo kumhusu Mwana wake? Kwa sababu ya upendo. Yehova alimfahamu Mwana wake na upendo ambao Mwana wake alikuwa nao kumwelekea na jinsi alivyopenda uadilifu. (Ebr 1:9) Alimfahamu Mwana wake vizuri sana kwa undani. (Mt 11:27) Alikuwa na hakika kabisa kwamba Mwana wake angebaki mwaminifu. Zaidi ya hilo, “upendo . . . ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol 3:14) Ndio kifungo chenye nguvu zaidi ulimwenguni pote, upendo mkamilifu unawaunganisha kabisa Mwana na Baba. Akiwa na sababu hizohizo, Mungu ana imani na tengenezo la watumishi wake, akijua kwamba upendo unawaunganisha kabisa wengi wao kwake hata wanapojaribiwa na kwamba tengenezo la viumbe wake hawatamwacha.—Zb 110:3.
-