-
Kristo Analiongoza Kutaniko LakeMnara wa Mlinzi—2002 | Machi 15
-
-
5, 6. (a) Katika maono ambayo mtume Yohana aliona, “vinara saba vya taa vya dhahabu” na “zile nyota saba” zinafananisha nini? (b) Ni nini kinachoonyeshwa na kuwepo kwa “zile nyota saba” katika mkono wa kuume wa Yesu?
5 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chaonyesha kwamba mtumwa mwaminifu na mwenye busara anaongozwa moja kwa moja na Yesu Kristo. Katika maono juu ya “siku ya Bwana,” mtume Yohana aliona “vinara saba vya taa vya dhahabu, na katikati ya vinara vya taa mtu fulani kama mwana wa binadamu” ambaye “katika mkono wake wa kuume alikuwa na nyota saba.” Yesu alisema hivi alipomweleza Yohana maono hayo: “Kwa habari ya siri takatifu ya zile nyota saba ulizoona juu ya mkono wangu wa kuume, na ya vile vinara saba vya taa vya dhahabu: Zile nyota saba zamaanisha wale malaika wa makutaniko saba, na vile vinara saba vya taa vyamaanisha makutaniko saba.”—Ufunuo 1:1, 10-20.
6 Vile “vinara saba vya taa vya dhahabu” vinafananisha makutaniko yote ya Wakristo wa kweli yaliyopo katika “siku ya Bwana,” iliyoanza mwaka wa 1914. Namna gani “zile nyota saba?” Mwanzoni, zilifananisha waangalizi wote watiwa-mafuta, waliozaliwa kwa roho, ambao walisimamia makutaniko ya karne ya kwanza.a Waangalizi hao walikuwa katika mkono wa kuume wa Yesu—chini ya uthibiti na mwongozo wake. Naam, Kristo Yesu aliongoza jamii ya mtumwa. Hata hivyo, leo waangalizi watiwa-mafuta ni wachache. Kristo anayaongozaje makutaniko zaidi ya 93,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni?
7. (a) Yesu hulitumiaje Baraza Linaloongoza kutoa uongozi katika makutaniko duniani pote? (b) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba waangalizi Wakristo wanawekwa rasmi na roho takatifu?
7 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, sasa kikundi kidogo cha wanaume wanaostahili ambao wanateuliwa kutoka miongoni mwa waangalizi waliotiwa mafuta wanatumikia wakiwa Baraza Linaloongoza. Baraza hilo linawakilisha jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Kiongozi wetu hutumia Baraza hilo Linaloongoza kuweka rasmi wanaume wanaostahili—wawe watiwa-mafuta kwa roho au la—kuwa wazee katika makutaniko ya kwao. Kuhusiana na hilo, roho takatifu, ambayo Yehova amempa Yesu mamlaka ya kuitumia, inatimiza jukumu muhimu sana. (Matendo 2:32, 33) Kwanza kabisa, lazima waangalizi hao watimize matakwa yanayoonyeshwa katika Neno la Mungu lililopuliziwa kwa roho takatifu. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9; 2 Petro 1:20, 21) Kupendekezwa na kuwekwa rasmi hufanywa baada ya sala na chini ya uongozi wa roho takatifu. Isitoshe, watu waliowekwa rasmi wanadhihirisha matunda ya roho hiyo. (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo, ushauri huu wa Paulo unawahusu wazee wote, wawe watiwa-mafuta au la: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwalo roho takatifu imewaweka nyinyi rasmi kuwa waangalizi.” (Matendo 20:28) Wanaume hao waliowekwa rasmi hupokea mwongozo kutoka kwa Baraza Linaloongoza, nao hulichunga kutaniko kwa moyo wa kupenda. Kwa njia hiyo, Kristo yuko pamoja nasi sasa na analiongoza kutaniko.
-
-
Kristo Analiongoza Kutaniko LakeMnara wa Mlinzi—2002 | Machi 15
-
-
a Hapa “nyota” hazifananishi malaika halisi. Yesu hangetumia mwanadamu kuandika habari kwa ajili ya viumbe wa roho wasioonekana. Kwa hiyo, lazima “nyota” hizi ziwe zinafananisha waangalizi wa kibinadamu au wazee katika makutaniko, wanaoonwa kuwa wajumbe wa Yesu. Nyota hizo ni saba, idadi inayoonyesha ukamilifu kupatana na kiwango cha Mungu.
-