Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ona Baraka za Umoja wa Ufalme!
    Mnara wa Mlinzi—1984 | Oktoba 15
    • utengenezaji wa Biblia, vitabu vya Biblia na magazeti ukaongezeka sana. Hesabu zenye kuongozeka za watumishi wa Mungu walio wakfu na kubatizwa wanajitoa kwa moyo wa kupenda watumikie wakiwa mapainia wa kawaida na wasaidizi, wakitumia wakati kila siku katika utumishi wa lazima wa kupanda ukweli wa Ufalme katika mioyo ya wengi. Watangazaji wa Ufalme katika karibu makundi yote wanajitahidi kuongeza huduma yao, wakifanya hivyo kwa kuthamini sana baraka ambazo tayari amewamiminia.

      17. Ni jambo gani la pekee sana juu ya Mashahidi wa Yehova na kazi yao katika siku zetu?

      17 Ni Mashahidi wa Yehova peke yao wanaoshiriki katika kazi hiyo ya kutoa uzima kwa niaba ya serikali ya Ufalme wa Mungu. Ni wao peke yao wanaofurahia mavuno ambayo hata sasa yanaonekana. Pia, mbegu ambayo Yehova anatoa kwa wafanyi kazi wake wa shambani wenye nia imekaguliwa vizuri sana na kuchaguliwa vizuri sana! Vifaa vyetu vya funzo la Biblia vimetayarishwa vikiwa na kusudi la kuchochea mioyo ya wengi ambao wangali wavunwe na kuletwa katika tengenezo lenye amani la Yehova, kundi la Kikristo, ambalo katika Mathayo 13:30 linafananishwa na ‘ghala’ la Mwanaye.

      18. Kwa sababu gani twapaswa kuazimia kuendelea mbele katika utumishi wetu wa Ufalme tukiwa na uradhi na furaha?

      18 Kweli kweli, tumo katika siku ya Yehova, siku ya kuona utimizo wa “ahadi kubwa mno, za thamani” kwa watu wake waliojitoa. (2 Petro 1:4) Amani na umoja zinasitawi kati yetu. Tumepewa ufahamu ulio wazi wa makusudi ya Mungu wetu. Tuna amani ya akili katikati ya watu wa ulimwengu wenye hofu na wasiwasi. Wakati ujao wenye kujawa na baraka kubwa zaidi unatungojea. Je! hatuna furaha nyingi sana kuwa wapokeaji wa baraka hizo zote za umoja wa Ufalme? Na je, si tumeazimia kusonga mbele na kazi yetu ya Ufalme imletee sifa Yehova milele?​—Kutoka w5/15/84.

      Jibu Lako Ni Nini?

      ◻ Nia ya watumishi wa Yehova inatofautianaje na ile ya waliomo katika Jumuiya ya Wakristo?

      ◻ Kumiminwa kwa roho takatifu ya Mungu kumetokeza nini?

      ◻ Kupatana na Isaya 32:17, 18, watu wa Yehova wanafurahia baraka gani sasa?

      ◻ Tuna uthibitisho gani kwamba Yehova anabariki mashahidi wake wa Ufalme?

  • Heshimu Yehova, Kitabu cha Hesabu Kinasihi
    Mnara wa Mlinzi—1984 | Oktoba 15
    • Heshimu Yehova, Kitabu cha Hesabu Kinasihi

      YEHOVA MUNGU anastahili heshima ya moyo wote ya waabudu wake. Ni lazima wamtii yeye na kushirikiana kwa ushikamanifu na watumishi wake waliowekwa. Jambo hilo linakaziwa vizuri kama nini katika kitabu cha Biblia cha Hesabu!

      Msingi wa jina la kitabu hicho ni kule kuhesabiwa kwa Waisraeli mara mbili, ambako kumeandikiwa katika sura za 1 mpaka 4 na 26. Hesabu kiliandikwa na Musa kwenye nyanda za Moabu mwaka wa 1473 K.W.K. na kwa msingi kinazungumza juu ya kipindi cha miaka 38 na miezi 9, kuanzia nyuma mwaka wa 1512 K.W.K.​—Hesabu 1:1; Kumbukumbu la Torati 1:3.

      Mambo ambayo yameandikwa katika visehemu vitatu vya Hesabu ni matukio ya Mlima Sinai (1:1–10:10), baadaye katika jangwa (10:11–21:35) na juu ya nyanda za Moabu (22:1–36:13). Lakini visa hivyo vyaweza kutufundisha nini? Je! kuna kanuni katika Hesabu zinazoweza kuwafaidi Mashahidi wa Yehova leo?

      Mambo Yaliyomo Yanatia Moyo Kumheshimu Mungu

      Waisraeli wamekuwa kwenye sehemu ya chini ya Mlima Sinai kwa mwaka mmoja hivi Yehova anapomwamuru Musa ahesabu watu. Isipokuwa Walawi, watu wote wa kiume wenye miaka 20 kwenda juu wanaandikishwa, na hesabu yao ni 603,550. Mahali pa mzaliwa wa kwanza, Mungu achukua Walawi kwa ajili ya utumishi kwenye hema. Maagizo yanatolewa juu ya jinsi watakavyofuatana katika kufunga safari. Katika safari hiyo Yuda, kabila lenye watu wengi zaidi, ndilo linaloongoza. Kwa amri ya Mungu, nao Walawi wanaandikishwa na kupewa migawo ya kazi takatifu.​—Hesabu 1:1–4:49.

      Amri za Yehova kuhusu karantini zinafuatwa na sheria anazotoa kama zile zinazohusu visa vya wivu kuhusiana na uaminifu wa mke na nadhiri zenye kufanywa na Wanaziri. Kisha maelezo fulani ya kirefu yanatolewa kuhusiana na utumishi kwenye hema. Kwenye ujenzi wa hema na kuwekwa wakfu kwa madhabahu, wakuu wa kikabila walikuwa wametoa matoleo yenye thamani. Kwa kufuatisha aliyotoa Yehova kupitia njozi, Musa alitengenezesha kinara cha taa. Taa zake zilipowashwa na Walawi wakatakaswa, wangeweza kuanza kutumikia.​—Hesabu 5:1–8:26.

      Maagizo kuhusu Kupitwa yanarudiwa upya. Kupiga kambi na kung’oa kambi kunaelekezwa na wingu la kimuujiza lililo juu ya hema. Watu wanapiga kambi na kung’oa kambi ‘kwa amri ya Yehova.’ Ili kukutanisha kusanyiko na makusudi mengine, zile tarumbeta mbili za fedha zinatumiwa.​—Hesabu 9:1–10:10.

      Katika siku ya 20 ya mwezi wa pili katika mwaka wa pili baada ya kutoka Misri, wingu lililo juu ya hema linaanza kusonga na Israeli wanafunga safari. Vinatokea visa vya kunung’unika isivyo haki. Kimojawapo ni kilio cha kutaka nyama, lakini pupa inaonekana Yehova anapotoa kware. Miriamu na Haruni wanung’unika juu ya ndugu yao Musa, na kwa kuadhibiwa Miriamu anapigwa kwa ukoma kwa muda. Jambo hilo lapasa kutusukuma tuheshimu mamlaka iliyowekwa na Mungu kama nini!​—Hesabu 10:11–12:16.

      Wapelelezi 12 wanapelekwa kwenye Nchi ya Ahadi na kurudi wakiwa na matunda manono-manono siku 40 baadaye. Lakini wapelelezi 10 wanakazia sana ukubwa wa wakaaji hao na juu ya miji yao yenye maboma hata Waisraeli waliovunjika moyo wakataka kurudi Misri. Bila kufanikiwa wapelelezi waaminifu Yoshua na Kalebu wanawasihi wamwamini Yehova. Watu wanasema juu ya kupiga mawe Musa, Haruni, Yoshua na Kalebu, Mungu anasema atapiga na kufukuzia mbali taifa zima. Lakini Musa amsihi Yehova asifanye hivyo na Yehova anaamuru kwamba watu hao watatanga-tanga jangwani kwa miaka 40, mpaka wale wote wenye miaka 20 na zaidi wafe, isipokuwa tu Yoshua, Kalebu na kabila la Lawi. Halafu, Waisraeli wajaribu kuvamia Nchi ya Ahadi, nao wakashindwa kiasi cha kuvunjwa moyo.​—Hesabu 13:1–14:45.

      Sheria mbalimbali zinazohusu sadaka, kuvunja Sabato na vishada katika ncha za nguo zinatolewa halafu. Kisha Kora, Dathani, Abiramu, Oni na wakuu 250 wasema kwa kumpinga Musa na Haruni. Matokeo ya utovu huo wa heshima yanakuwa nini? Yehova amharibu Kora na wale 250 kwa moto, na waasi wale wengine wanaangamia wakati ardhi inapofunguka, na kuwameza pamoja na jamaa zao na mali zao. Siku iyo hiyo inayofuata Waisraeli wanung’unika juu ya Musa na Haruni, na kwa ajili ya ukosefu huo wa heshima 14,700 wanauawa na tauni inayoletwa na Yehova. Ili akomeshe kunung’unika huko na kuonyesha kwamba amechagua Haruni wa kabila la Lawi, Mungu anafanya kijiti cha Haruni kiote maua. Hilo linafuatishwa kwa maagizo yanayohusu kazi za makuhani na Walawi na kutakaswa kwa watu kutokana na unajisi.​—Hesabu 15:1–19:22.

      Katika Kadeshi kuna kilio cha kutaka maji. Kwa sababu Musa na Haruni hawamtakasi Yehova kwa kutoa maji kimuujiza, wanaambiwa kwamba hawataingia katika Nchi ya Ahadi. Wanapoondoka Kadeshi, watu hao wanafika kwenye Mlima Hori, ambako Haruni anakufa na mwanaye Eleazari anafanywa kuhani mkuu. Kisha Waisraeli wanamshinda mfalme wa Aradi. Baadaye, wanasema kwa kupinga Mungu na Musa, na pindi hiyo Yehova anapeleka nyoka wenye sumu kati yao kwa kuwaadhibu. Wenye kuumwa wanaponeshwa kwa kutazama tu nyoka wa shaba ambaye Mungu anamwambia Musa atengeneze na kumweka juu ya mti. Baada ya hapo, Israeli wanashinda Mfalme Sihoni Mwamori na Ogu mfalme wa Bashani, na kutwaa nchi zao.​—Hesabu 20:1–21:35.

      Kisha matukio kwenye nyanda za Moabu yanasimuliwa. Mfalme Balaki Mmoabi anamlipa Balaamu ili awalaani Waisraeli, lakini badala yake anawabariki mara tatu. Balaamu ndiye anasababisha wanawake wenye kumwabudu Baali waongoze Israeli kwenye mwenendo usio na adili wa kufanya ngono na kuabudu sanamu. Yehova anaharibu wakosaji 24,000 kabla Fineasi hajakomesha tauni hiyo kwa kuua mwanamume Mwisraeli mwenye mwenendo usio na adili na mwanamke Mmidiani.​—Hesabu 22:1–25:18; 31:15, 16.

      Baada ya watu kuhesabiwa tena na kielelezo kuwekwa kuhusu haki za urithi za mabinti, Musa anaitazama Nchi ya Ahadi na kumwagiza Yoshua awe mwenye kuchukua mahali pake. Maagizo yanatolewa kuhusu sadaka za kila siku, kila juma, kila mwezi na kila mwaka, na pia kuhusu kufanya nadhiri. Halafu Wamidiani wanalipwa kisasi kwa ajili ya sehemu yao katika kusababisha Waisraeli wamtende Mungu dhambi.​—Hesabu 26:1–31:54.

      Kabila za Reubeni, Gadi na Manase zinapewa urithi upande wa mashariki wa Yordani lakini ikiwa tu watashiriki katika kutiisha nchi iliyo magharibi mwa mto huo. Halafu, kuna orodha ya kambi nyingi za Israeli kutoka Misri mpaka nyanda za Moabu. Kisha Waisraeli wanapewa amri zinazohusu kukaa katika Nchi ya Ahadi. Kati ya mambo mengine, wanapaswa kuangamiza masalio ya dini ya uongo na kuwafukuzia mbali wakaaji wake. Mipaka ya nchi hiyo inawekwa, wakuu wanawekwa ili kumsaidia Yoshua na Eleazari kuigawa, na miji 48 inagawiwa Walawi. Miji ya makimbilio sita inawekwa kando na maagizo yanatolewa juu ya kushughulikia visa vya kumuua mtu bila kukusudia na kumuua mtu makusudi. Mwishowe, sheria zinatolewa juu ya ndoa ya mrithi wa kike.​—Hesabu 32:1–36:13.

      Unaposoma Hesabu, huenda ukavutiwa na mkazo wake juu ya kuheshimu Yehova na wale waliowekwa rasmi wawe na daraka kati ya watu wake. Lakini huenda ukawa na maswali juu ya mambo fulani. Kwa hiyo maswali na majibu yafuatayo huenda yakawa yenye kupendeza.

      Matukio Kwenye Mlima Sinai

      • 5:11-31​—Kwa kweli ilikuwaje kwa mke aliyepatikana na hatia ya kufanya uzinzi?

      Hakuna taabu iliyoletwa na maji yenyewe. Lakini yalinywewa mbele za Yehova, ambaye alijua kama mwanamke alikuwa na hatia ya uzinzi. Kama ndiyo, angefanya tumbo lake livimbe na paja lake lipooze. Kwa wazi paja linatumiwa hapa kufananisha viungo vya uzazi. (Linganisha Mwanzo 46:26.) ‘Kupooza’ kunadokeza kwamba viungo hivyo vingekwisha nguvu, na kufanya asiweze kuchukua mimba. Jambo hilo lingepatana na uhakika wa kwamba kama mwanamke huyo angekuwa bila hatia mume wake angemtunga mimba.

      • 8:25, 26​—Je! kanuni ya sheria juu ya kuacha kutumika inahusu watu wa Yehova leo?

      Makuhani walisaidiwa na watu wote wa kiume wenye kustahili wa jamaa tatu kubwa za Walawi. Baada ya muda, Walawi wangekuwa wengi, lakini hesabu ya nafasi za utumishi kwenye patakatifu zilikuwa chache. Basi, bila shaka, kwa sababu ya kuwahurumia wenye umri mkubwa na kuzuia kusiwe kusongamana kwa vyeo hivyo, Yehova aliagiza kwamba Walawi wa kiume wenye kufika miaka 50 wangeachishwa utumishi wa lazima, ingawa bado wangeweza kusaidia wakipenda. Lakini, jambo hilo haliwekei Waisraeli wa kiroho na wenzi wao amri yo yote kwa sababu hawako chini ya Torati. (Warumi 6:14; Waefeso 2:11-16) Iwapo umri mkubwa unamdhoofisha Mkristo asiweze kubeba daraka fulani, anaweza kuhamishwa kwenye namna fulani ya utumishi anaoweza. Kwa Mashahidi wa Yehova hakuna cha kustaafu kuhubiri habari njema za Ufalme.

      Kutanga-tanga Huku na Huku

      • 12:1​—Ni kwa nini Miriamu na Haruni walimnenea Musa mabaya kwa sababu ya mkeye Mkushi?

      Kufanya hivyo kulikuwa zaidi ya kukataa mkeye Musa. Nia yenyewe ilikuwa tamaa ya kuwa na uwezo zaidi, hasa kwa habari ya Miriamu. Mkeye Musa, Sipora, alikuwa amekuwa mbali lakini sasa alikuwa amejiunga naye, na Miriamu aliogopa mahali pake pa kuwa mwanamke wa kwanza kwa umaarufu katika kambi pangechukuliwa naye. (Kutoka 1.8:1-5) Kwa hiyo akamfanya Haruni ajiunge naye kumlaumu Musa kwa ajili ya kuoa Mkushi na kubisha juu ya cheo chake cha kipekee mbele za Mungu. Kwa sababu ya hilo, Yehova alikaripia vikali Miriamu na Haruni, lakini uhakika wa kwamba ni Miriamu tu alipigwa kwa ukoma huenda unadokeza kwamba yeye ndiye aliyekuwa mchochezi. Nia inayofaa ya Haruni ilionyeshwa alipoungama kosa na kusihi kwa ajili ya Miriamu mwenye ukoma. (Hesabu 12:10-13) Sipora naye alikuwa bintiye Reueli Mmidiani. (Mwanzo 25:1, 2; Hesabu 10:29) Katika Habakuki 3:7 “nchi ya Midiani” inalinganishwa na Kushani, ambalo kwa wazi ni jina jingine la Midiani au linahusu nchi jirani. Zaidi ya hayo, makabila fulani ya Kiaraibu yaliitwa Kusi au Kushimu. Kwa hiyo inaelekea kwamba “Mkushi” ni neno ambalo halikutumiwa tu kwa wazao wa Hamu kupitia Kushi lakini pia lilitumiwa kuhusu wakaaji fulani wa Midiani. Kwa hiyo, Sipora angeweza kuitwa Mkushi.

      • 21:14, 15​—“Chuo [kitabu] cha vita vya Yehova” kilikuwa nini?

      Bila shaka, hayo yalikuwa maandishi ya kihistoria yenye kutegemeka ya vita vya watu wa Yehova. Huenda yakawa yalianza wakati wa tendo la ushindi la Abrahamu juu ya wafalme wanne waliokuwa wamemteka Lutu na jamaa yake. (Mwanzo 14:1-16) Maandiko yanataja maandishi mbalimbali ambayo hayakuongozwa na Mungu, mengine ambayo yalitumiwa kuwa chanzo cha habari za waandikaji wa Biblia walioongozwa na Mungu.​—Yoshua 10:12, 13; 1 Wafalme 11:41; 14:19, 29.

      Kwenye Nyanda za Moabu

      • 22:20-22​—Kwa kuwa Yehova alimwambia Balaamu aende pamoja na watu wa Balaki, kwa sababu gani Yeye alikasirika wakati nabii huyo alipoenda pamoja nao?

      Yehova alimwambia Balaamu kwamba hangeweza kuwalaani Waisraeli, lakini nabii huyo mwenye pupa alienda akiwa na kusudi la kufanya hivyo ili athawabishwe na Mfalme Balaki wa Moabu. (2 Petro 2:15, 16; Yuda 11) Kwa sababu hiyo hasira ya Yehova ikawaka juu ya Balaamu. Bila shaka, Yehova hakukubali Israeli walaaniwe kwa vyo vyote. Lakini Balaamu, kama Kaini, alikuwa mkaidi na kupuuza mapenzi ya Mungu. (Mwanzo 4:6-8) Baada ya Yehova kubadili kila laana iliyokusudiwa na kuifanya iwe baraka, ukosefu wa adili wa Balaamu ulimsukuma adokeze kwamba Balaki atumie wanawake wa Moabu na Midiani kuwatongoza Waisraeli na kuwahusisha katika ibada ya Baali. (Kumbukumbu la Torati 23:5; Hesabu 31:15,16; Ufunuo 2:14) Jambo hilo lilileta hasira kali ya Mungu juu ya Israeli na kutokeza kifo cha watu 24,000. Baadaye, Balaamu mwenye pupa aliuawa na wale aliotaka kulaani. (Hesabu 25:1-9; 31:8) Lo! hilo ni onyo lenye kutuonya tuepuke pupa kama nini!

      • 25:10-13​—Ahadi hii kuhusu ukuhani ilitimizwaje?

      Inaonekana ukuhani mkuu uliendelea katika nasaba ya Fineasi mpaka wakati wa Kuhani Mkuu Eli, mzao wa Ithamari. Badiliko hilo labda lilifanywa kwa sababu ya kutostahili kwa muda kwa nasaba ya Fineasi. Lakini Mfalme Sulemani alimweka Kuhani Sadoki, ambaye alikuwa mzao wa Fineasi mahali pa mzao wa Ithamari, Abiathari. (1 Wafalme 1:1-14; 2:26, 27, 35) Kwa kadiri ile ambayo maandishi ya kihistoria yanaonyesha, inaelekea nasaba ya Fineasi iliendelea baada ya hapo kuwa katika cheo cha ukuhani mkuu kwa miaka mingi.

      • 30:6-8​—Je! mume wa mwanamke Mkristo anaweza kumfungua kutoka kwa nadhiri zake?

      La, kwa maana wafuasi wa Yesu hawako chini ya Torati. Yehova anashughulika na watu mmoja mmoja kuhusiana na nadhiri, na mume Mkristo hana mamlaka ya kuzibatilisha wala kuzitangua. Bila shaka, mke Mkristo hapaswi kufanya nadhiri zinazopingana na Neno la Mungu wala na madaraka yake ya Kimaandiko kumwelekea mume wake.​—Mhubiri 5:2-6.

      Ni Chenye Thamani Kubwa Kwetu

      Kiunganishi chenye thamani katika maandishi yanayoongoza kwenye kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu kinatolewa na kitabu cha Hesabu. Pia kinaelekeza kwa Yesu Kristo. Kwa mfano, dhabihu za wanyama na matumizi ya majivu ya ng’ombe-mke mwekundu ni mambo yaliyoelekeza kwenye uandalizi mkubwa zaidi wa kutakasa kupitia dhabihu ya Yesu. (Hesabu 19:2-9; Waebrania 9:13, 14) Kile kisa kilichohusu nyoka wa shaba kilitangulia kufananisha uandalizi mkubwa wa Yehova wa kuwa na uzima wa milele kupitia Kristo.​—Hesabu 21:8, 9; Yohana 3:14, 15.

      Kitabu cha Hesabu kinaweza kutusaidia tuepuke ibada ya sanamu na kufanya ngono zisizo na adili. Kinatuonyesha wazi hatari ya kunung’unika juu ya Mungu, watu alioweka rasmi na maandalizi yake. Na hakika masimulizi hayo yenye kusisimua yapasa kutuchochea tumheshimu kabisa kabisa Mungu wetu Yehova mwenye upendo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki