-
Mchungaji Mwema na “Zizi Hili” LakeMnara wa Mlinzi—1984 | Julai 15
-
-
Mchungaji Mwema na “Zizi Hili” Lake
1, 2. (a) Mfalme Daudi alimweleza Yehova jinsi gani katika Zaburi 23:1? (b) Kwa sababu gani ilifaa kumfananisha Yehova na mchungaji na Israeli kama kondoo wake?
“[YEHOVA] ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, kando ya maji ya utulivu huniongoza.” Mvulana mmoja aliyekuwa mchungaji wakati mmoja na pia mpiga-kinubi, na baadaye akawa mfalme wa taifa la Israeli, alitumia maneno hayo kuanza mmoja wa nyimbo zake zenye kupendwa sana.—Zaburi 23:1, 2.
2 Ni taifa la kale la Israeli tu ambalo mtunga zaburi mwingine angeweza kuandikia maneno ya Zaburi 95:6, 7: “Njoni, tuabudu, tusujudu, tupige magoti mbele za [Yehova] aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, na sisi tu watu wa malisho yake, na kondoo za mkono wake.” Ingawa mfalme wa kibinadamu wa taifa la Israeli angeweza kufananishwa na mchungaji, taifa hilo lilikuwa na mchungaji aliye juu zaidi, yaani Yehova Mungu. Ndiye Mchungaji aliye mzuri kabisa ambaye anaweza kuigwa na wanaume wanaotumikia wakiwa wachungaji kwa usemi wa mfano katika kundi la watu walio wakf wa Yehova.
3. Kumtaja Yehova kuwa Mchungaji kulifaaje hata kuhusiana na Yesu?
3 Mfalme Daudi alitangulia kuwa kivuli cha Yesu Kristo, isipokuwa Yesu Kristo ni mkubwa kuliko Daudi wa zamani, ambaye alikuwa babu yake wa kifalme. Kwa kufaa sana, basi, angeweza kutumia na kutaja maneno ya Daudi: ‘Yehova ndiye mchungaji wangu.’ Je! mtangulizi wake, Yohana Mbatizaji, hakuelekeza kidole kwa Yesu Kristo aliyekuwa akikaribia kwa kuwaambia wasikilizaji waliokuwa karibu naye hivi: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu”? (Yohana 1:29, 36) Kwa kumsema Yesu kuwa Mwana-kondoo, wa jamaa ya kondoo, huenda ikawa Yohana alikuwa akiyafikiria maneno ya Isaya 53:7: ‘Alipelekwa kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni.’ Na katika kitabu kile cha mwisho kabisa cha Biblia, kuanzia Ufunuo 5:6 na kuendelea, Yesu aliyetukuzwa anatajwa mara 28 kuwa Mwana-Kondoo wa mfano.
4. Ni kwa jinsi gani Yesu alikuwa kama kondoo katika zizi la kondoo na hilo zizi la kondoo lilikuwa nini?
4 Kwa kuzaliwa kimwujiza duniani alikuwa amezaliwa ndani ya taifa la Israeli, mwaka wa 2 K.W.K. Hivyo akaja chini ya agano la Torati ambalo Yehova, yule Mchungaji wa Israeli, alikuwa amefanya pamoja na watu wake wachaguliwa. Hilo agano la Torati, pamoja na Amri Kumi zalo, lilikuwa limepatanishwa kwa ajili ya taifa la Israeli na nabii Musa. (Wagalatia 4:4, 5) Na Yesu, akiwa mshiriki wa hao watu wachaguliwa, alikuwa mmoja wa kondoo wa mfano ambao Yehova ndiye alikuwa Mchungaji Mkubwa Kabisa wao. Hivyo Yesu alikuwa katika zizi la kondoo la mfano, yaani, kuwa na uhusiano wenye upendeleo pamoja na Mchungaji wa Kimungu akiwa amelindwa na agano la Torati ya Musa lililokuwa kama ukuta wa ulinzi.
5. Ni nini sababu ya kuwa na maoni tofauti juu ya zizi la kondoo la Yohana 10:1?
5 Je! hapa tunamaanisha kwamba lile “zizi” la kondoo linalotajwa katika Yohana sura ya 10, mstari wa 1, ni mpango wa agano la Torati ya Musa? Hasa-a! Yaliyokuwa maelezo ya hapo mbele ya zizi la kondoo kuwa ni agano la Kiabrahamu msingi wake ulikuwa ni yale maoni ya kwamba Yohana sura ya 10 ilitaja moja kwa moja zizi moja tu, na kama ingekuwa hivyo, basi kwa kufaa agano la Kiabrahamu ndilo lingekuwa maana yake. Hata hivyo, kujifunza zaidi sura hiyo kulionyesha kwamba kwa kweli Yesu alizungumza juu ya zizi zaidi ya moja. Kwa hiyo, kama tutakavyoona, ikafaa rekebisho la ufahamu lifanywe.
6. Unaonaje juu ya marekebisho hayo ya ufahamu wa mambo ya Kibiblia?
6 Mara kwa mara marekebisho hayo yanakuwa ya lazima, kwa maana Mithali 4:18 inatuambia kwamba “njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” Oh, ndiyo, wapinzani wa ile kweli wenye kuasi imani ‘wanasagia meno’ mafunuo hayo yanayokuja hatua kwa hatua, lakini sisi hatuhangaishwi nao. (Matendo 7:54) Bali, sisi tunamshukuru Yehova kwamba “nuru imemzukia mwenye haki, na furaha wanyofu wa moyo.” (Zaburi 97:11) Sisi tuna uhakika kwamba mtafurahi sana kujua maana yenyewe hasa ambayo mfano wa Yesu wa yale mazizi ya kondoo unayo kwenu na kwa Mashahidi wa Yehova wengine wote leo.
Zizi la Kondoo la Mapema, Chini ya Torati
7. Kuhusiana na zizi la kondoo la Kiisraeli, Yesu alichukuaje daraka jipya mwaka 29 W.K.?
7 Namna gani, basi, juu ya hilo zizi la kondoo la agano la Torati ya Musa? Baada ya Yesu kuwa amebatizwa na Yohana Mbatizaji, na akawa amepakwa mafuta kwa roho takatifu ya Yehova na akawa amemaliza siku 40 za kujaribiwa katika jangwa la Yudea, Yesu Kristo alikuja kwenye zizi la kondoo la Kiisraeli akiwa Mchungaji wa kiroho katika mwaka wa 29 W.K. Yesu Kristo alisema kwamba yeye alikuwa ametumwa hasa kwenye “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 10:6; 15:24) Kufikia wakati huo yeye alikuwa amekuwa mmoja tu wa Waisraeli wa kimwili wenye kuishi ndani ya mpango wa zizi la kondoo wa agano la Torati ya Musa. Lakini sasa, baada ya kupakwa mafuta na kuzaliwa kwa roho ya Yehova, Yesu Kristo angeweza kuja kwenye hilo zizi la kondoo akiwa katika daraka lake mpya la kuwa “mchungaji mwema.”—Yohana 10:11.
8. Ni nani aliyekuwa bawabu wa mfano wa Yohana 10:3, na jinsi gani hivyo?
8 Yohana Mbatizaji ndiye aliyekuwa wa kwanza kumtambua Yesu kuwa yule Mchungaji wa Kweli aliyewekwa na Mchungaji Mkubwa wa Wote, Yehova Mungu. Yesu hakuja kufanya unyang’anyi katika zizi la kondoo bali alikuja kufanya shughuli halali. Kwa njia yenye kuheshimika angeweza kujitokeza akubaliwe aingie katika zizi la kondoo la taifa la Israeli. Kwa kupatana na unabii wa Malaki 4:5 (linganisha Mathayo 11:12-14; Luka 1:13-17), Yohana alikuwa amepewa na yule Mchungaji Mkubwa wa Wote mgawo wa kuwa “bawabu” wa lile zizi la kondoo la Kiisraeli. (Yohana 1:15, 17, 19-28; 10:3) Yohana alitambua vithibitisho vya Yesu Kristo vya kuwa Mchungaji mdogo wa Yehova Mungu na pasipo kukawia akawa tayari kumwacha aingie, kumtambulisha kuwa Mchungaji wa Kimasihi ambaye angeita kondoo zake kwa majina na kuwaongoza malishoni.
9, 10. Yesu alifaaje maelezo yake mwenyewe juu ya mchungaji, na wachungaji Waisraeli walishughulikaje na kondoo zao?
9 Yesu alitimiza maelezo yake mwenyewe juu ya Mchungaji wa Kweli na Mwema, kama yanavyotajwa katika maneno haya kwenye Yohana 10:1-5: “Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang’anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo. Bawabu humfungulia huyo, na kondoo humsikia sauti yake; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. Naye awatoapo nje kondoo wake wote, huwatangulia; na wale kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake. Mgeni hawatamfuata kabisa, bali watamkimbia; kwa maana hawazijui sauti za wageni.”
10 Mchungaji wa kale wa Kiisraeli alizoeana sana na kondoo zake. Alikuwa akitoa mwito wa sauti isiyoweza kupatana na ya mwingine, naye aliitumia kuita kondoo zake wakusanyike pamoja wapokee uangalizi wake binafsi. Zaidi ya hilo, yeye alimpa kila mmoja wa kondoo zake jina lake mwenyewe. Kila kondoo angetii na kuitikia wakati jina lake mwenyewe liliitwa. Kondoo walijua uzito na mvumo wa sauti ya mchungaji wao mwenyewe na kwa hiyo hawangeitikia sauti ya mgeni asiyekuwa mwangalizi wao.
11. Sisi binafsi twapaswa tuoneje juu ya daraka la Yesu akiwa Mchungaji?
11 Kulingana na hilo, ni faraja kama nini kwetu kuwa tumehakikishiwa kwamba Mchungaji wetu wa kiroho anajua kila mmoja wetu kwa jina na anaweza kumpa kila mmoja wetu uangalizi na utunzaji wa kibinafsi! Sisi tusiwe kama wengi wa wasikilizaji wa siku za Yesu ambao hawakuuelewa ufananishi wenye maana sana aliowaeleza. Kwenye Yohana 10:6 imeandikwa hivi ili maneno haya yawe mfano wa kutuonya: “Mithali hiyo Yesu aliwaambia; lakini wao hawakuelewa na mambo hayo aliyowaambia.”
12. “Wageni” ambao Yesu alizungumza juu yao ni nani, na walikuwaje hivyo?
12 Waisraeli wale wengine waliokuja wakadai kuwa wao ndio Masihi, au Kristo aliyeahidiwa, ndio ambao Yesu aliwabandika jina la kuwa wageni. Hawakutambulishwa kuwa wao ni Mchungaji wa Kimasihi wa Yehova na yule “bawabu” wake aliyewekwa, ambaye alikuwa Yohana, yule ambaye Yesu mwenyewe alimjia ili abatizwe. Kwa kufanya hivyo Yesu hakukosea. (Mathayo 3:1-7; Marko 1:1-7; Luka 3:1-9) Ilikuwa ni kwa kusudi la kuwalinda watu kwamba Yesu akaona ni vizuri ajijulishe kwa watu kuwa Ndiye Yehova alikuwa akiwapelekea awe mchungaji wa kiroho wao. Pia kusudi lilikuwa kuwafunua wazi wachungaji wadanganyifu.
Zizi Jipya Chini ya Mchungaji Mwema
13. Mungu alifanya badiliko gani kwa habari ya zizi la kondoo lake?
13 Jambo la maana ni mtu aingie katika zizi la kondoo linalofaa, siku za huko nyuma na hata leo. Je! hilo linadokeza kwamba kungekuwako badiliko la mazizi ya kondoo yenye kukubaliwa na Yehova Mungu? Ndiyo. Yale ambayo Yesu aliendelea kusema katika Yohana sura ya 10 na yale yanayoonyeshwa na mambo ya uhakika ya historia—hayo yote mawili yanaonyesha kwamba Mungu angeweka zizi jipya mahali pa zizi la kondoo la Kiisraeli chini ya Torati. Angalia hilo tunapoendelea na maneno ya Yesu.
14, 15. Kwa sababu gani ni wazi kwamba katika Yohana 10:7-10 Yesu alisema juu ya zizi la kondoo jipya?
14 “Basi Yesu aliwaambia tena,” kwenye Yohana 10:7-10, “Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Wote walionitangulia ni wevi na wanyang’anyi; lakini kondoo hawakuwasikia. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho. Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.”
15 Angalia katika kifungu hicho Yesu anajisema yeye mwenyewe kuwa mlango wa zizi la kondoo analolitaja sasa, mlango wa kuingia katika hili zizi la kondoo la Mchungaji Mkubwa wa Wote, Yehova Mungu. Yesu siye aliyekuwa mlango wa mfano wa kuingia ndani ya zizi la kondoo la Israeli wa kimwili, kwa maana yeye mwenyewe alikuwa amezaliwa katika taifa hilo kwa uzazi wa kibikira kutokana na Mariamu bikira Myahudi. Yesu siye aliyekuwa mpatanishi aliye kama mlango wa agano la Torati ambalo kupitia hilo taifa la Israeli lilikuwa limeingizwa ndani ya uhusiano wa pekee kabisa pamoja na Yehova Mungu. Ilikuwa zamani sana kabla ya Yesu kuzaliwa duniani Yehova Mungu alipoliambia taifa la Israeli hivi: “Ni ninyi tu niliowajua katika jamaa zote zilizo duniani.” (Amosi 3:2) Mchungaji mdogo wa kweli wa Yehova Mungu angewaita kondoo wa kwanza wa kundi lake watoke katika zizi la kondoo la Kiyahudi lililo la mfano kisha awaongoze waingie ndani ya malisho ya pekee ya kiroho. Kwa hiyo lazima iwe sasa Yesu alikuwa ameanza kuzungumza juu ya zizi la kondoo jipya ambalo yeye, Mchungaji Mwema, alikuwa mlango walo katika maana nyingine.
16. (a) Kulikuwa kumekuwa kidokezi gani cha mapema kwamba Yehova angekuwa na zizi la kondoo jipya? (b) Yesu alionyeshaje kwamba hilo zizi la kondoo jipya lilikuwa karibu kutokea?
16 Wayahudi waliokataa kuwa wanafunzi wake wenye mfano wa kondoo walijisikia kwamba lao tu ndilo lililokuwa zizi la kondoo ambalo Yehova Mungu alilifikiria na kwamba lingeendelea kuwako mpaka wakati ujao usiojulikana. Wao hawakulifikiria lile “agano jipya” ambalo Yehova Mungu alikuwa ameahidi kuanzisha kulingana na unabii wa Yeremia 31:31-34. Hiyo ilimaanisha kungekuwa na uhusiano mpya pamoja na Yehova Mungu na, kwa hiyo, kungekuwa na zizi la kondoo la mfano lililo jipya. Yesu Kristo siye aliyekuwa mlango wa kuingia ndani ya zizi la kondoo ambalo lingefutiliwa mbali, liwe halina tena ukuta wa ulinzi wa Yehova. (Waebrania 8:7-13) Katika usiku alioadhimisha sikukuu yake ya mwisho ya Kupitwa akiwa pamoja na wanafunzi wake Wayahudi, Yesu alisema maneno yenye maana kubwa alipokuwa akiwapa divai ya Kupitwa. Aliipa divai hiyo maana ya mfano, akisema: “Kikombe hiki kinamaanisha lile agano jipya kwa uwezo wa damu yangu, ambayo itamwagwa chini kwa ajili yenu.”—Luka 22:20, NW; Mathayo 26:27-29.
17, 18. (a) Hilo zizi la kondoo jipya ambalo Yesu ni Mchungaji Mwema walo lilikuwa nini? (b) Yeye pia angeweza kufananishwaje na mlango wa zizi hilo jipya?
17 Yesu Kristo angekuwa ndiye mlango wa kuingia kwenye zizi la kondoo lenye kudumu, zizi ambalo lingechukua mahali pa lile zizi la kwanza la kondoo la Wayahudi waliotahiriwa waliokuwa chini ya agano la Torati ya Musa. Wakati Yesu alipowaacha nyuma duniani wanafunzi wake kisha akapaa mbinguni siku 40 baada ya kufufuliwa kwake kati ya wafu, alipaa akiwa bado ana haki yake ya kuwa na uzima mkamilifu wa kibinadamu. Yeye hakuwa ameipoteza haki hiyo kwa kutenda dhambi yo yote katika mwili. (Isaya 53:3-12; Matendo 8:30-35) Kwa hiyo, alikuwa na utayari wa kutumikia kuwa mpatanishi na kutumia haki ya uzima hiyo, iliyofananishwa na damu yake, ili atie muhuri agano jipya lililo zuri zaidi kwa ajili ya wanafunzi wake duniani. Alifanya hivyo si baada ya siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. wakati ambao roho takatifu ilimiminwa juu ya wanafunzi watiifu wa Kiyahudi waliokuwa wakingoja Yerusalemu.
18 Hivyo wanafunzi hao wakaingizwa ndani ya lile agano jipya, kukawa na zizi jipya la kondoo, zizi la kuwa na uhusiano pamoja na Yehova Mungu kwa kulitegemea agano jipya lililotiwa muhuri na damu ya Yesu Kristo. Kondoo wa mfano wa hili zizi jipya walizaliwa kwa roho ya Yehova na wakapakwa mafuta kwa roho hiyo. Yesu Kristo ndiye aliyekuwa mlango wa kuingia kwenye zizi hilo na pia ndiye aliyekuwa Mchungaji Mwema aliyewekwa na Yehova atunze kondoo walio ndani ya zizi.
19. Unabii katika Zekaria 13:7 ulitimizwa kwa njia gani?
19 Wakati wa zile sehemu za siku tatu ambazo Yesu alikuwa amekamatwa na akawa mfu katika kaburi, alikuwa amelazimika kumpokeza kabisa yule Mchungaji Mkubwa wa Wote, Yehova Mungu, uangalizi na utunzaji wa wanafunzi wake waliokuwa mfano wa kondoo. Hapo ndipo uneni wa Yehova kwenye Zekaria 13:7 ulipotimizwa, yaani: “Mpige mchungaji, nao kondoo watatawanyika; nami nitaugeuza mkono wangu juu ya wadogo.” Mkono wa yule Mchungaji Mweza Yote, Yehova, uligeuzwa ukawa juu ya wanafunzi hao wadogo, mpaka wakaja kurudishwa tena kwa Mchungaji mdogo wake aliyefufuliwa, Yesu Kristo.—Mathayo 26:31, 32.
20. Ni kwa njia gani andiko la Yohana 10:16 linaelekeza kwenye tazamio la zizi jingine bado litokee, na kwa sababu gani hilo lapasa kuwa jambo la kushughulikiwa nasi?
20 Lakini akiwa anafikiria hili zizi la kondoo jipya chini ya Mchungaji Mwema, angalia kwamba katika Yohana 10:16 Yesu alisema: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao imenipasa kuwaleta.” Je! hilo halionyeshi kwamba yeye angekuwa na zizi jingine, la pili, ambalo angekuwa Mchungaji Mwema walo? Ikiwa ndivyo, lingetokea wakati gani na ni nani wangekuwa kondoo ndani yalo? Hayo ni maswali yenye kufaa sana wakati huu, na majibu yayo yanaweza kuhusu moja kwa moja tumaini lako na mataraja ya milele. Basi na tuchunguze jambo hilo.
-
-
Zizi la Karibuni kwa Ajili ya “Kondoo Wengine”Mnara wa Mlinzi—1984 | Julai 15
-
-
Zizi la Karibuni kwa Ajili ya “Kondoo Wengine”
“Kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.”—YOHANA 10:16.
1. Ni nani walioongezwa katika zizi la kondoo la Israeli wa kiroho mwaka wa 36 W.K.?
ZIZI la kondoo jipya lilipoanzwa katika Pentekoste ya 33 W.K., lile zizi la kondoo la kwanza la Wayahudi wa kimwili waliokuwa chini ya agano la Torati ya Musa lilipitilia mbali likawa limekwisha kutimiza kusudi lake. Miaka mitatu na nusu baadaye akida Mroma Kornelio na jamaa yake na rafiki zake wenye kuamini katika Kaisaria waliongolewa, wakabatizwa na kupakwa roho. Kwa njia hiyo Mataifa wasiotahiriwa, wasiogeuzwa kuwa Wayahudi waliingizwa ndani ya zizi la kondoo ambalo Yesu Kristo ndiye “mlango.” (Matendo, sura ya 10) Zizi hilo linatia ndani “Israeli wa Mungu,” Waisraeli kulingana na roho, au Waisraeli wa kiroho. Je! ingeweza kusemwa juu ya wo wote wa hawa—Myahudi au Mtaifa—kwamba wao “si wa zizi hili,” zizi lililokusanywa kulingana na mpango wa agano jipya? Hata kidogo!—Wagalatia 6:16; Yohana 10:16.
2. Ni kwa jinsi gani Yesu angali akitumikia akiwa Mchungaji Mwema wa wale waliomo katika agano jipya?
2 Katika wakati huu ambao siku zimepita sana, mabaki ya huyu Israeli wa Mungu wangali duniani, na jambo hilo linahakikisha kwamba Yesu Kristo, aliye Mpatanishi wa lile agano jipya, amekuwa Mchungaji Mwaminifu na Mwema. Kwa hiyo hata leo, baada ya karne 19 za wakati, Yesu Kristo aliyetukuzwa anaweza kusema kwa haki, bila maringo ya bure, maneno aliyoyasema kabla ya kufa na kufufuliwa. Tunayasoma kwenye Yohana 10:14, 15: “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi; kama vile Baba [Mchungaji Mkubwa wa Wote] anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo.”
3, 4. Kwa sababu gani “kondoo wengine” watofautishwe na “kundi dogo”?
3 Kufikia hapo Yesu aliendelea kusema usemi wa ajabu lakini wenye shauku ya huruma: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Alikuwa akitaja nani hapo kuwa “kondoo wengine”?
4 Kwa kuwa hao “kondoo wengine” hawakuwa wa “zizi hili,” hawangetiwa kati ya Israeli wa Mungu, ambaye washiriki wake ni wenye urithi wa kiroho au wa kimbingu. Hao warithi wa Ufalme wangekuwa “kundi dogo” tu, kwa maana Yesu aliwaambia wanafunzi wake waliokuwa katika mwelekeo wa kumiminiwa roho takatifu siku ya Pentekoste hivi: “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa Baba yenu ameona vema kuwapa ule ufalme.” (Luka 12:32) Kundi dogo la kondoo ambao watapewa Ufalme wa kimbingu na ambao watatawala pamoja na yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, katika Ufalme huo, litakuwa na hesabu ya Waisraeli wa kiroho 144,000 tu.—Ufunuo 7:1-8; 14:1-5.
5. Ungewezaje kutumia Ufunuo 14:4 kuonyesha kwamba kwa kufaa kondoo wengine wana tumaini tofauti na lile la kundi dogo?
5 Ufunuo 14:4 unasema: “Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.” Hao Waisraeli wa kiroho 144,000 wangewezaje kuwa ni malimbuko (matunda ya kwanza) kutoka kwa wanadamu ikiwa hakungekuwa na matunda mengine, matunda ya baadaye? Basi ni jambo lililo wazi kabisa kwamba kando na wale Waisraeli wa kiroho 144,000 walio kundi dogo la kondoo wa kifalme katika agano jipya, kuna kondoo wengine wanaopaswa kukusanywa baadaye. Na je! si hivyo ndivyo mambo yamekuwa?
6, 7. Ufunuo 22:17 unatimizwaje, na ni nani wasiopewa ukaribishaji wa kuambiwa “njoo”?
6 Kwenye Ufunuo 22:17 ilitabiriwa kwamba “[roho] na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” Bibi-arusi wa kiroho wa Kristo hajipatii yeye mwenyewe ukaribishaji wa kujiambia “Njoo!” Yaani, haambii maneno hayo wale ambao Yehova Mungu bado anawahitaji wajaze jamii ya Bibi-arusi, ili kuifanya iwe na washiriki 144,000 barabara. Ni wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo” ulioanza mwaka wa 1914 W.K. tunaposikia ukaribishaji ukitolewa na “Bibi-arusi,” kwa kushirikiana na roho takatifu ya yule Mchungaji Mkubwa wa Wote. (Mathayo 24:3, NW)
7 Maneno hayo ya ukaribishaji yanatolewa kwa wanadamu walio hapa duniani, wanaotaka kufikia uzima mkamilifu wa kibinadamu wawe na sura na mfano wa Mungu katika Paradiso ambayo Ufalme wa Mungu kupitia Kristo utarudisha duniani. Leo, wakati wa huu umalizio wa mfumo wa mambo, wakaribishwa hao ni “kondoo wengine” wa unabii wa Yesu wenye kuchukua muda mrefu ulio kwenye Yohana 10:16. Wao si wa “zizi hili” ambalo Mchungaji Mwema Yesu alitaja hapo. Lakini wanaupata mwaliko kupitia baki la “kondoo” waliomo katika “zizi hili,” na wao wameshirikiana na baki la kiroho katika kutolea wengine mwaliko huo kufikia ukomo wa umalizio wa mfumo huu wa mambo.
8. Katika mwaka 1905 kulikuwako maoni gani juu ya kondoo wengine?
8 Katika toleo la Machi 15, 1905 la Mnara wa Mlinzi wa Sayuni (Kiingereza), makala ilichapishwa yenye kichwa “Mchungaji wa Kweli, Kondoo wa Kweli, Zizi la Kweli.” Ilitofautisha kondoo wa “zizi hili” na wale wanaoitwa “kondoo wengine.” Ilikazia kwamba “zizi hili” linahusu kundi la Wakristo wakati wa kile kilichoitwa “hiki kipindi cha Injili.” Kufuatia vichwa vidogo vinavyosema “Kondoo Wengine wa Kundi Jingine” na “Warithi-Wenzi wa Ahadi Ile Ile” (kurasa 89, 90) ilisemwa hivi:
“Kundi ambalo Bwana alikuwa akijikusanyia mwenyewe wakati wa mfano huo halikuwa Israeli wa kimwili, bali Israeli wa kiroho. . . . Kwa hiyo maoni ambayo wengine wamekuwa nayo kwamba sisi ambao ni watu wa Mataifa au ‘kondoo wengine’ wanaotajwa sasa tunakusanywa katika lile zizi moja si sahihi. . . . Kwa wazi hawa ‘kondoo wengine’ wanaotajwa katika mfano huu ni wale watakaokuwa kondoo wa Bwana baada ya ‘kundi dogo’ kukamilika.”
9, 10. (a) Kwa sababu gani mfano wa kondoo na mbuzi hauwezi kuhusu wakati wa Mileani? (b) Kondoo wengine wangekusanywa wakati gani?
9 Katika fungu la baadaye la makala hiyo wale “kondoo wengine” wanalinganishwa na “kondoo” wanaosimuliwa katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, kama ulivyoandikwa katika Mathayo 25:31-46. Katika mwaka wa 1905 ilidhaniwa kwamba mfano huo ungehusu wakati wa Utawala wa Mileani wa Kristo baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye uwanja wa pigano wa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14-16) Hata hivyo, lazima tukumbuke kwamba mfano wa kondoo na mbuzi ulikuwa sehemu ya mwisho ya jibu la Yesu kwa ulizo la wanafunzi wake juu ya ni nini ingekuwa ishara ya ‘kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo.’ (Mathayo 24:3, NW) Kwa hiyo lazima utimizo wa mfano huu uwe wakati wa huu umalizio wa mfumo wa mambo ulioanza mwaka wa 1914.
10 Kwa hiyo inathaminiwa kwamba Mchungaji Mwema Yesu Kristo hakuanza kuwakusanya wale “kondoo wengine” wa Yohana 10:16 katika karne ya kwanza wakati Wasamaria waliotahiriwa walipoanza kuongolewa kwenye Ukristo. Wala yeye hakufanya hivyo wakati akida Mroma, yule Mtaifa asiyetahiriwa, Kornelio, alipoongolewa mwaka wa 36 W.K. hivi. Basi, ni wakati gani Mchungaji Mwema alianza kukusanya kondoo wengine wake? Karne nyingi baadaye, ndiyo, katika karne hii ya 20, kulingana na mambo ya hakika ya kisa hiki.—Matendo 8:4-17; 10:9-48.
11. Kufikia mwaka 1935 Waisraeli wa kiroho walikuwa wakikaza fikira juu ya nini?
11 Tunaona kwamba mpaka masika ya mwaka wa 1935 mabaki ya Waisraeli wa kiroho walio ndani ya “zizi hili” walikuwa wakijishughulisha sana kukusanya katika zizi hilo wale wa mwisho waliohitajiwa ili kufanyiza ushirika kamili wa Waisraeli wa kiroho 144,000. Hao ndio wangekuwa wa mwisho kuletwa chini ya agano jipya lililopatanishwa na Mchungaji Mwema, aliyekufa akiwa Mwana-kondoo wa Mungu ili aitoe “damu ya agano la milele.” (Waebrania 13:20; Zaburi 50:5) Basi, ni jambo gani lililotukia mwaka wa 1935?
12. Ni jambo gani lisilo la kawaida lililotokea kwa kukamatana na kusanyiko mwaka 1935?
12 Kusanyiko kuu la Mashahidi wa Yehova lilipangwa wakusanyike pamoja kwenye mji mkuu wa United States ya Amerika, Washington, D.C., ambalo Wanafunzi wa Biblia wenye kumcha Mungu waliofanana na yule Yonadabu asiyekuwa Mwisraeli walikaribishwa kwa njia ya pekee walihudhurie. Katika siku ya pili ya kusanyiko, Mei 31, msimamizi wa wakati huo wa Sosaiti alisisimua wakusanyikaji kwa hotuba yake iliyohusu Ufunuo 7:9-17, kuhusiana na ule “umati mkubwa” (Ufunuo 7:9, Habari Njema kwa Watu Wote) Alieleza kwamba huo “umati mkubwa” uliotabiriwa ungekuwa wa watu walio “kondoo wengine,” wale waliotangulia kufananishwa na Yonadabu, au Yehonadabu, yule mwanamume asiye Mwisraeli aliyeambatana na Yehu, mfalme wa Israeli katika wonyesho wa juhudi yake kwa ajili ya Yehova na kwa kupambana na waabudu wa yule mungu wa uongo Baali. (2 Wafalme 10:15-28; Yeremia 35:6-19) Hivyo Yehu hakuonyesha “uachiliaji wa ushindani wo wote kuelekea Yehova,” (NW) au, kulingana na tafsiri ya Authorized Version, alionyesha “juhudi kwa ajili ya BWANA.”—2 Wafalme 10:16.
13, 14. (a) Ni nani wakaja kuwa Wayonadabu wa kisasa? (b) Lilikuwa jambo la kufaa wafanye nini, na kwa sababu gani?
13 Mamia ya wale waliotaka kuwa kama Yonadabu na kuwa kati ya “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema waliitikia ukaribishaji uliotangazwa kisha wakahudhuria kusanyiko la Washington. Ili wawe akina Yonadabu wa kisasa waliofananishwa, kulingana na Maandiko ilikuwa lazima wajitoe wakf kikamili kwa Yehova Mungu kupitia Mchungaji Mwema wake na kuonyesha wakf huo kwa kuzamishwa kabisa katika maji, kama vile kondoo wa “zizi hili” wamefanya. Basi ikawa kwamba, Jumamosi, Juni 1, 1935, wakusanyikaji 840 walibatizwa katika maji. Ubatizo huo ulifanana na ule wa watu wengi uliofanywa siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. huko Yerusalemu. Hiyo ilikuwa njia yenye kuvutia na pia yenye kipindi cha matukio ya maana kama nini kwa Mchungaji Mwema, alipoonyesha kwamba sasa alikuwa amekusudia kuwaleta chini ya uchungaji wake wale kondoo wengine ambao wangesikiliza sauti yake kwa kupendelea awe Mchungaji wao! Hakika jambo hilo lilimfurahisha sana! Baada ya kusanyiko la Washington la mwaka wa 1935 ile hotuba kuu yenye kueleza Ufunuo 7:9-17 ilichapishwa katika safu za gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), katika matoleo ya Agosti 1 na 15, 1935, chini ya kichwa “Ule Umati Mkubwa” (Sehemu ya 1 na ya 2).
14 Maelfu kwa maelfu ya wasomaji waliona wakati huo pendeleo lao la kuwa kondoo wengine wa Mchungaji Mwema na la kupewa mgawo kwenye zizi lililowafaa. Basi walibatizwa mapema kadiri walivyoweza ili waonyeshe uamuzi wao unaofaa wa kujiweka wakf kwa yule Mchungaji Mkubwa wa Wote kupitia Mchungaji mdogo wake, Yesu Kristo. Kwa kuwa wanatambua kwamba Mchungaji mdogo wa Yehova alitoa nafsi yake ya kibinadamu kwa ajili ya kondoo wote, wao nao “wamefua mavazi yao” ya kitambulisho katika “damu” ya huyu “Mwana-kondoo wa Mungu” na “kuyafanya meupe” ili wafaulu ukaguzi wa kimungu.—Ufunuo 7:14.
15. Kondoo wengine wamekuwa wengi jinsi gani, na hilo linatoa ushuhuda zaidi juu ya nini?
15 Umalizio wa mfumo wa mambo, ulioanza mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914, haukumalizika mwaka wa 1935 kwa sababu ya Mchungaji Mwema kugeuza fikira zake za kuokoa uhai ziwaelekee wale kondoo wengine. Bali umeendelea mpaka mwaka huu wa 1984. Mwisho ungali utafika baada ya kutimizwa kwa mahubiri kamili juu ya Ufalme. Tayari wale wanaojionyesha kuwa wamo katika zizi la wale kondoo wengine kwenye miadhimisho ya Chakula cha Jioni cha Bwana ni mamilioni, na bado wengine wengi sana wako njiani wakija kuingia zizi hilo. Tayari wameipita kwa wingi sana ile hesabu iliyotangulia kuwekwa ya 144,000, ambayo ni hesabu yenye kikomo waliyowekewa wale walioingizwa ndani ya “zizi hili” lililowekwa akiba kwa ajili ya Waisraeli wa kiroho, wale wenye kurithi pamoja na Mchungaji Mwema katika Ufalme wake wa kimbingu. Jambo hilo la hakika linatoa ushuhuda zaidi kwamba hao hawamo katika “zizi hili” la “kundi dogo” la Mchungaji Mwema.—Luka 12:32.
16, 17. (a) Uhusiano ni nini kati ya kondoo wengine na kundi dogo? (b) Maneno ya Yesu juu ya kuwa “kundi moja” yamekuwa na utimizo gani?
16 Je! utofautiano wa matumaini, yaani, tumaini la kuishi mbinguni la kondoo wa “zizi hili” na tumaini la kuishi duniani la wale kondoo wengine walio wa zizi lile jingine lililotokezwa majuzi, umewafanya watengane waache kushirikiana, kama kwamba hawana ushirika katika jambo lo lote? Matukio ya tangu mwaka wa 1935 yanajibu Kwa Mkazo, Hapana! Yesu, yule Mchungaji Mwema, alitabiri kwamba hawangetengana, kwa maana aliendelea kusema: “Kisha kutakuwako kundi moja.” (Yohana 10:16) Hapo tunaona kwamba hakusema, “kundi moja katika zizi moja.” Lakini ingawa kungekuwa na mazizi mbali mbali, kulipasa kuwe “mchungaji mmoja” tu, na huyo ndiye Mfalme-Mchungaji ambaye amekuwa akitawala katika mbingu tangu kumalizika kwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914 W.K. Kulingana na uhakika huo, “kondoo” hao wana ile kazi moja wanayopaswa kutimiza wakiwa pamoja, yaani, ‘kuzihubiri habari njema hizi za Ufalme katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote,’ kabla ya mwisho wa huu mfumo wa mambo ya ulimwengu wa kale.—Mathayo 24:14, NW.
17 Wale kondoo wengine hawajisikii kwa njia yo yote kuwa wanafanyiwa ubaguzi wa kutengwa na lile kundi dogo. Wote pamoja wanakuwa kundi moja la kondoo za Mchungaji Mwema. Wale kondoo wengine wanafurahia sana kushirikiana kwa urafiki mkubwa pamoja na lile kundi dogo. Wanalihesabu kuwa pendeleo kubwa kutumikia kwa majira fulani katika mwili pamoja na hao watakaokuwa wafalme na makuhani wakati ujao, nao wawe raia zao wakati wa Ufalme wa Mileani.
18. (a) Itakuwaje wakati ujao kwa agano jipya na kondoo wapakwa mafuta katika “zizi hili”? (b) Kondoo wengine wana taraja gani?
18 Katika wakati wake Mungu, mabaki ya Waisraeli wa kiroho watakapomaliza mwendo wao wa kidunia na kuondoka katika dunia wakaingie katika thawabu yao ya kimbingu, lile agano jipya lililotegemezwa juu ya damu ya Mpatanishi, yule Mchungaji Mwema Yesu Kristo, litaacha kutumika, kwa maana litakuwa limefanikiwa kutimiza kusudi lake. Hapo ndipo mwadhimisho wa Chakula cha Jioni cha Bwana siku ya Kupitwa ya kila mwaka utakapokoma. Hapo pia ndipo “zizi hili” la kundi la Waisraeli wa kiroho litakapoacha kuwako. Kondoo wengine waliojiweka wakf na kubatizwa watabaki duniani waingie katika baraka ambazo Ufalme wenye kufanyizwa na yule Mchungaji Mwema Yesu Kristo na makuhani walio wafalme wenzake 144,000 utawamiminia. “Kundi” litakaloachwa juu ya dunia safi litakuwa la “kondoo wengine” wenye mwungano peke yao. Wao wataendelea kuisikiliza sauti ya Mfalme-Mchungaji wao, na kufanya hivyo kutawaongoza wapate uzima wa milele katika ukamilifu wa kibinadamu wakiwa juu ya dunia iliyo Paradiso.—Kutoka w2/15/84.
Je! Wewe Unaweza Kueleza?
◻ Ni nini kinachoonyesha kwamba kondoo wengine ni tofauti na wale waliomo katika kundi dogo?
◻ Ufunuo 22:17 unatimizwaje leo?
◻ Ni wakati gani na ni wapi kondoo wengine walianza kujitokeza wazi?
◻ Kwa kuwa kondoo wengine wamo ndani ya zizi tofauti na wapakwa mafuta, wao ni kundi moja jinsi gani?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Makala “Umati Mkubwa,” iliyochapishwa mwaka 1935, ilisaidia kutambulisha “kondoo wengine”
[Picha katika ukurasa wa 17]
Wito wa “kundi dogo” uliposogelea mwisho, Yesu alikusanya umati wa “kondoo wengine”
-
-
Njoni Kwenye “Ongezeko la Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya ya 1984!Mnara wa Mlinzi—1984 | Julai 15
-
-
Njoni Kwenye “Ongezeko la Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya ya 1984!
HAKUNA mtu anayefahamu vizuri zaidi ya Yehova Mungu mwenyewe, juu ya uhitaji wa watumishi wake duniani kukutana katika makusanyiko makubwa. Hiyo ndiyo sababu yeye alipanga watu wake wa kale Israeli wawe wakikutana mara tatu kila mwaka katika mahali
-